Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rs uku. 54-uku. 58
  • Dhambi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Dhambi
  • Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Dhambi ya Kwanza Ilikuwa Nini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Sababu Kwanini Tunazeeka na Tunakufa
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Yesu Huokoa—Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Dhambi
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
Pata Habari Zaidi
Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
rs uku. 54-uku. 58

Dhambi

Maana: Kulingana na maandishi ya Biblia ya Kiebrania na Kigiriki, dhambi ni kukosa alama. Mungu mwenyewe huweka “alama” ambayo viumbe wake wenye akili wanapaswa kufikia. Kukosa kufikia alama hiyo ni dhambi, ambayo pia ni ukosefu wa uadilifu, au uasi-sheria. (Rom. 3:23; 1 Yoh. 5:17; 3:4) Dhambi ni chochote ambacho hakipatani na utu wa Mungu, viwango vyake, njia, na mapenzi yake, ambayo yote ni matakatifu. Huenda ikatia ndani mwenendo mbaya, mtu kushindwa kufanya anayopaswa kufanya, maneno mabaya, mawazo machafu, au tamaa au nia ambazo ni za ubinafsi. Biblia inatofautisha kati ya dhambi iliyorithiwa na dhambi ya kukusudiwa, kati ya tendo la dhambi ambalo mtu anatubia na zoea la kutenda dhambi.

Iliwezekanaje Adamu afanye dhambi ikiwa alikuwa mkamilifu?

Kuhusu habari ya Adamu kuwa mkamilifu, soma Mwanzo 1:27, 31 na Kumbukumbu la Torati 32:4. Yehova Mungu alipotangaza uumbaji wake wa duniani, kutia ndani mwanamume na mwanamke, kuwa kitu “chema sana,” alimaanisha nini? Ili Mungu, ambaye kazi yake ni kamilifu, aseme kwamba kile alichoumba kilikuwa “chema sana,” ni lazima kilifikia viwango vyake vikamilifu.

Je, ukamilifu ulimaanisha kwamba Adamu na Hawa hawawezi kufanya kosa? Mtu anayetengeneza roboti huitarajia itende sawasawa na alivyoipangia kutenda. Lakini roboti kamilifu haiwezi kuwa mwanadamu mkamilifu. Sifa zinazoonwa kuwa za lazima hazifanani. Adamu na Hawa walikuwa wanadamu, si roboti. Mungu aliwapa wanadamu uwezo wa kuchagua kati ya mema na mabaya, kati ya kutii na kutotii, kufanya maamuzi ya kiadili. Kwa kuwa wanadamu waliumbwa hivyo, kutoweza kufanya maamuzi hayo (na si uamuzi usio wa hekima) ndiko kungeonyesha kutokamilika.—Linganisha na Kumbukumbu la Torati 30:19, 20; Yoshua 24:15.

Ili isemwe kwamba Adamu na Hawa waliumbwa wakamilifu, je, ni lazima maamuzi yao yote yawe sawa baada ya kuumbwa? Hilo lingemaanisha kwamba hawakuwa na uchaguzi. Lakini Mungu hakuwaumba kwa njia ya kwamba watii tu bila kutaka. Mungu aliwapa uwezo wa kuchagua, ili waweze kutii kwa sababu walimpenda. Au, wakiruhusu mioyo yao iwe na ubinafsi, wangekuwa wasiotii. Ni jambo gani la maana zaidi kwako—mtu anapokufanyia jambo fulani kwa sababu amelazimishwa kulifanya au kwa sababu anataka kulifanya?—Linganisha na Kumbukumbu la Torati 11:1; 1 Yohana 5:3.

Watu hao wakamilifu wangewezaje kuwa na ubinafsi, na kutenda dhambi? Ijapokuwa waliumbwa wakiwa wakamilifu, miili yao haingeendelea kutenda kazi kikamilifu ikiwa haingelishwa chakula kinachofaa. Vivyo hivyo, pia, ikiwa wangeruhusu akili zilishwe mawazo mabaya, hilo lingesababisha uharibifu wa kiadili, kutokuwa watakatifu. Andiko la Yakobo 1:14, 15 linasema hivi: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.” Kwa habari ya Hawa, tamaa mbaya zilianza kusitawi alipomsikiliza Shetani, aliyesema kwa kutumia nyoka. Adamu alimtii mke wake wakati alipomsihi ajiunge naye kula tunda lililokatazwa. Badala ya kuyakataa mawazo mabaya, watu hao wawili walisitawisha tamaa za ubinafsi. Dhambi ikatokea.—Mwa. 3:1-6.

Je, dhambi ya Adamu ilikuwa sehemu ya “mpango wa Mungu?”

Ona ukurasa wa 27, chini ya kichwa “Adamu na Hawa,” pia ukurasa wa 172, 173, chini ya kichwa “Majaliwa.”

Je, siku hizi kweli kuna “dhambi”?

Mfano: Mgonjwa akivunja kipima-joto, je, hilo linathibitisha kwamba yeye si mgonjwa? Mwizi akisema kwamba haamini yaliyoandikwa katika vitabu vya sheria, je, hilo litamfanya asiwe na hatia ya uhalifu? Hali kadhalika, uhakika wa kwamba watu wengi wanaamini kwamba si lazima kuishi kulingana na viwango vya Biblia haukomeshi dhambi.—Ona 1 Yohana 1:8.

Huenda watu fulani wakachagua kutenda yale ambayo Neno la Mungu linakataza. Lakini hilo halithibitishi kwamba Biblia ina makosa. Andiko la Wagalatia 6:7, 8 huonya hivi: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia; kwa sababu yeye anayepanda kwa mwili wake atavuna uharibifu kutokana na mwili wake.” Kuenea kwa magonjwa yanayotokana na ngono, familia zilizovunjika, na kadhalika, kunathibitisha ukweli wa yale ambayo Biblia inasema. Mungu alimuumba mwanadamu; Yeye anajua kitakachotuletea furaha yenye kudumu; Yeye anatuambia mambo hayo katika Biblia. Je, si jambo la busara kumsikiliza? (Ili kupata uthibitisho wa kuwako kwa Mungu, ona kichwa “Mungu.”)

Mambo mengi yanayoitwa dhambi, je, si mambo ya kawaida tu ambayo wanadamu hufanya?

Je, ngono ni dhambi? Je, Adamu na Hawa walitenda dhambi kwa kufanya ngono? Biblia haisemi hivyo. Andiko la Mwanzo 1:28 linasema kwamba Mungu mwenyewe aliwaambia Adamu na Hawa ‘wazae na kuwa wengi na kuijaza dunia.’ Ili kufanya hivyo, je, hawangekuwa na mahusiano ya ngono kati yao? Na andiko la Zaburi 127:3 linasema kwamba “wana ni urithi kutoka kwa Yehova,” kwamba wao ni “thawabu.” Kumbuka kwamba Hawa alikula kwanza tunda lililokatazwa na alifanya hivyo akiwa peke yake; ndipo baadaye akampa Adamu sehemu yake. (Mwa. 3:6) Kwa wazi, mti uliozaa lile tunda lililokatazwa ulikuwa mti halisi. Kile ambacho Biblia inakataza si mahusiano ya ngono ya kawaida kati ya mume na mke bali mambo kama vile uasherati, uzinzi, ngono kati ya watu wa jinsia moja, na ngono na mnyama. Matokeo mabaya ya matendo hayo yanaonyesha kwamba katazo hilo linathibitisha Yule anayejua jinsi tulivyoumbwa anatupenda.

Mwa. 1:27: “Mungu akamuumba mtu [Adamu] kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba.” (Kwa hiyo, jambo ambalo ni sawa kwa Adamu lilikuwa kuonyesha sifa takatifu za Mungu, kukubali na kuthamini mwelekezo wa Mungu. Kukosa kufanya hivyo kulikuwa ni kukosa kuifikia alama, kufanya dhambi. Ona Waroma 3:23, pia 1 Petro 1:14-16.)

Efe. 2:1-3: “Ninyi [Wakristo] ndio ambao Mungu alifanya kuwa hai ingawa mlikuwa wafu katika makosa na dhambi zenu, ambazo wakati fulani mlitembea ndani yake kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii. Ndiyo, wakati fulani sisi sote tulijiendesha katikati yao kupatana na tamaa za mwili wetu, tukifanya mambo yanayopendwa na mwili na fikira, nasi kiasili tulikuwa watoto wa ghadhabu sawa na wale wengine.” (Tukiwa wazao wa Adamu mtenda-dhambi, sisi tulizaliwa katika dhambi. Tangu kuzaliwa, moyo wetu una mwelekeo wa kutenda mabaya. Tusipozuia maelekeo hayo mabaya, huenda mwishowe tukaizoea njia hiyo ya maisha. Huenda hata ikaonekana kuwa “jambo la kawaida” kwa sababu wengine walio karibu nasi wanafanya mambo hayo. Lakini Biblia inatambulisha yaliyo mema na yaliyo mabaya kwa maoni ya Mungu, kwa sababu ya jinsi alivyomfanya mwanadamu na kusudi lake kwa wanadamu. Tukimsikiliza Muumba wetu na kumtii kwa upendo, maisha yatakuwa yenye maana sana kwa kadiri tusivyopata kujua, nasi tutakuwa na wakati ujao wa milele. Muumba wetu anatukaribisha kwa uchangamfu tuonje ili tuone jinsi maisha hayo yalivyo mazuri.—Zab. 34:8.)

Dhambi ina matokeo gani juu ya uhusiano wa mtu na Mungu?

1 Yoh. 3:4, 8: “Kila mtu aliye na mazoea ya kufanya dhambi anazoea pia kufanya uasi-sheria, na kwa hiyo dhambi ni uasi-sheria. Yeye ambaye huendelea kufanya dhambi hutokana na Ibilisi.” (Jambo hilo ni zito kama nini! Wale wanaochagua kimakusudi maisha ya dhambi, wakizoea kuitenda, Mungu anawaona kuwa wahalifu. Njia ambayo wamechagua ndiyo ile ambayo Shetani mwenyewe alichagua pale mwanzoni.)

Rom. 5:8, 10: “Tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu. . . . Tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake.” (Ona kwamba watenda-dhambi wanaitwa adui za Mungu. Basi, ni jambo la hekima kama nini kujifaidi wenyewe na uandalizi ambao Mungu amefanya ili tupatanishwe naye!)

1 Tim. 1:13: “Nilionyeshwa rehema [asema mtume Paulo], kwa sababu nilikosa ujuzi nami nilitenda kwa ukosefu wa imani.” (Lakini Bwana alipomwonyesha njia iliyo sawa, hakukataa kuifuata.)

2 Kor. 6:1, 2: “Tukifanya kazi pamoja naye, tunawasihi ninyi pia msipokee fadhili zisizostahiliwa za Mungu kisha mkose kusudi lake. Kwa maana anasema: ‘Katika wakati unaokubalika nilikusikia, na katika siku ya wokovu nilikusaidia.’ Tazama! Sasa ndio wakati unaokubalika hasa. Tazama! Sasa ndiyo siku ya wokovu.” (Sasa ndio wakati ambapo nafasi ya wokovu inapatikana. Mungu hatawaonyesha milele wanadamu wenye dhambi fadhili hizo zisizostahiliwa. Kwa hiyo, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusikose kusudi la fadhili hizo.)

Dhambi inaweza kuondolewaje?

Ona kichwa, “Fidia.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki