SOMO LA 46
Mifano ya Hali za Kawaida
BILA SHAKA ni muhimu kutumia mifano ambayo inapatana na habari unayozungumzia. Lakini ili mifano hiyo iwe na matokeo, ni muhimu pia ifae wasikilizaji.
Wasikilizaji wanahusikaje na aina ya mifano unayotumia unapowahutubia? Yesu Kristo alifanya nini? Yesu alipokuwa akizungumza na umati wa watu au na wanafunzi wake hakutumia mifano ya mambo ambayo hayakujulikana katika Israeli. Watu hawangeelewa mifano kama hiyo. Kwa mfano, Yesu hakutaja maisha katika makao ya kifalme kule Misri wala matendo ya kidini katika India. Lakini alitumia mifano ambayo ilihusu utendaji wa kawaida wa watu katika nchi zote. Alizungumzia kushona nguo, kufanya biashara, kupoteza kitu chenye thamani, na kuhudhuria sherehe za arusi. Alifahamu jinsi ambavyo watu hutenda katika hali mbalimbali, na alitumia vizuri hali hizo katika mifano. (Mk. 2:21; Luka 14:7-11; 15:8, 9; 19:15-23) Kwa kuwa Yesu alifundisha Waisraeli hasa, mara nyingi mifano yake iligusia vitu na utendaji uliokuwa kawaida katika maisha yao. Kwa hiyo, alitaja mambo kama ukulima, jinsi kondoo wanavyomtii mchungaji, na kuhifadhi divai katika ngozi za wanyama. (Mk. 2:22; 4:2-9; Yn. 10:1-5) Pia alitaja mifano ya matukio ambayo watu walielewa kama vile uumbaji wa wanadamu wawili wa kwanza, Furiko la siku za Noa, kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora, kifo cha mke wa Loti, pamoja na mifano mingine. (Mt. 10:15; 19:4-6; 24:37-39; Luka 17:32) Unapochagua mifano ya kutumia, je, wewe pia hufikiria kwa makini mambo ambayo wasikilizaji hutenda kwa ukawaida na desturi zao?
Namna gani kama unazungumza na mtu mmoja au labda watu wachache badala ya watu wengi? Jaribu kuchagua mfano ambao hasa unafaa vizuri watu hao wachache. Yesu alipomhubiria yule mwanamke Msamaria kwenye kisima kimoja karibu na Sikari, alitaja “maji yaliyo hai,” ‘kutopata kiu hata kidogo,’ na “bubujiko la maji linalobubujika ili kutoa uhai udumuo milele”—hizo zote ni semi zinazohusu utendaji wa mwanamke huyo. (Yn. 4:7-15) Na Yesu alipozungumza na wanaume waliokuwa wakiosha nyavu zao, alitumia semi zinazohusu uvuvi. (Luka 5:2-11) Katika hali hizo mbili, Yesu angalitaja mambo ya ukulima kwa sababu watu hao waliishi katika eneo la ukulima, lakini mifano yake ilikuwa na matokeo zaidi kwa sababu alitaja utendaji wao binafsi ili waelewe mambo wazi. Je, unajitahidi kufanya hivyo?
Ingawa Yesu alikazia fikira “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli,” mtume Paulo hakutumwa kwa Israeli tu, bali pia kwa watu wa Mataifa. (Mt. 15:24; Mdo. 9:15) Je, jambo hilo lilibadili mazungumzo ya Paulo? Ndiyo. Katika barua aliyowaandikia Wakristo kule Korintho, alitaja mambo ambayo watu wa Mataifa walifahamu kama mashindano ya kukimbia, mazoea ya kula katika mahekalu ya sanamu, na maandamano ya kusherehekea ushindi.—1 Kor. 8:1-10; 9:24, 25; 2 Kor. 2:14-16.
Je, wewe huchagua kwa uangalifu mifano unayotumia kama Yesu na Paulo? Je, unafikiria desturi na utendaji wa kila siku wa wasikilizaji wako? Ni kweli kwamba ulimwengu umebadilika tangu karne ya kwanza. Watu wengi wanafahamu habari za ulimwengu kupitia televisheni. Mara nyingi wanafahamu hali katika nchi nyinginezo. Ikiwa ndivyo hali ilivyo, si vibaya kutumia habari hizo kama mifano. Hata hivyo, mambo yanayogusa sana mioyo ya watu ni yale yanayohusu maisha yao ya kawaida ya nyumbani, ya familia, kazini, ya chakula, na hali ya hewa.
Ukiona unahitaji kufafanua sana mfano wako, huenda ikawa unazungumzia jambo ambalo wasikilizaji hawalielewi. Mfano kama huo unaweza kufunika kwa urahisi jambo unalofundisha. Basi, wasikilizaji wanaweza kukumbuka mfano lakini wasiweze kukumbuka kweli ya Maandiko uliyokuwa ukijaribu kufundisha.
Yesu alitumia mambo rahisi ya kila siku badala ya kufanya ulinganifu unaotatanisha. Alitumia mambo madogo kufafanua mambo makubwa na mambo rahisi kufafanua mambo magumu. Yesu aliunganisha mambo ya kawaida na kweli za kiroho, akawasaidia watu kushika vizuri zaidi kweli hizo na kuzikumbuka. Huo ni mfano mzuri sana wa kuiga!