Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
APRILI 2-8
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 26
“Pasaka na Ukumbusho—Zina Ulinganifu Gani? Zinatofautianaje?”
nwtsty picha
Mlo wa Pasaka
Vitu muhimu katika mlo wa Pasaka vilikuwa: nyama ya kondoo dume iliyochomwa (mifupa ya mnyama huyo haikupaswa kuvunjwa) (1); mikate isiyo na chachu (2); na mboga chungu za majani (3). (Kut 12:5, 8; Hes 9:11) Kulingana na Mishna inawezekana mboga hizo chungu za majani zilikuwa saladi, chicory, pepperwort, endive, au dandelion, ambazo ziliwakumbusha Waisraeli kuhusu uchungu wa utumwa wa Misri. Yesu alitumia mkate usio na chachu kuwakilisha mwili wake wa kibinadamu ulio mkamilifu. (Mt 26:26) Na mtume Paulo alimwita Yesu “mwanakondoo wetu wa Pasaka.” (1Ko 5:7) Kufikia karne ya kwanza, divai (4) ilikuwa ikitumika kama sehemu ya mlo wa Pasaka. Yesu alitumia divai kuwakilisha damu yake, ambayo ingemwagwa kama dhabihu.—Mt 26:27, 28.
nwtsty habari za utafiti—Mt 26:26
unamaanisha: Neno la Kigiriki e·stinʹ (linamaanisha “ni”) linaleta wazo la “kuonyesha; kuashiria; kuwakilisha.” Mitume wa Yesu walielewa maana ya neno hilo, kwa kuwa katika kisa hiki walimwona Yesu mwenye mwili mkamilifu akiwa mbele yao, na walikuwa wakitarajia kula mkate usio na chachu na si kula mwili halisi wa Yesu. Kwa hiyo, mkate huo usingeweza kuwa mwili halisi wa Yesu. Ni vizuri kutambua kwamba neno hili e·stinʹ la Kigiriki lilitumiwa pia katika Mt 12:7, na tafsiri nyingi za Biblia zimetafsiri neno hilo kuwa “unamaanisha.”
nwtsty habari za utafiti—Mt 26:28
damu . . . ya agano: Agano jipya kati ya Yesu na Wakristo watiwa-mafuta, lilifanywa kupitia dhabihu ya Yesu. (Ebr 8:10) Hapa Yesu anatumia maneno yaleyale yaliyotumiwa na Musa alipokuwa mpatanishi wa taifa la Israeli na kuanzisha agano la Sheria kwenye Mlima Sinai. (Kut 24:8; Ebr 9:19-21) Kama damu ya ng’ombe na mbuzi ilivyohalalisha agano la Sheria kati ya Mungu na taifa la Israeli, ndivyo damu ya Yesu ilivyohalalisha agano jipya ambalo Yehova angefanya na Israeli la kiroho. Agano hilo lilianza kufanya kazi katika Pentekoste 33 W.K.—Ebr 9:14, 15.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mt 26:17
Siku ya kwanza ya Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu: Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu ilianza Nisani 15, siku moja baada ya Pasaka (Nisani 14), na ilifanywa kwa siku saba. (Ona Nyongeza B15.) Hata hivyo, katika siku za Yesu, Pasaka ilihusianishwa sana na sherehe hiyo hivi kwamba nyakati nyingine siku hizo nane, kutia ndani Nisani 14, zilirejelewa kuwa “Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu.” (Lu 22:1) Katika muktadha huu, maneno “Siku ya kwanza ya” yanaweza kurejelea “Siku moja kabla.” (Linganisha na Yoh 1:15, 30, ambapo neno la Kigiriki “kabla”, lililo na muundo uleule, limetumiwa badala ya neno “kwanza” [proʹtos] na hivyo mstari huo unasema “alikuwapo kabla [proʹtos] yangu.”) Kwa hiyo, neno la awali la Kigiriki, pamoja na desturi za Kiyahudi, zilifanya wanafunzi wa Yesu wamuulize jambo la kufanya siku ya Nisani 13. Wakati wa mchana wa Nisani 13, wanafunzi walifanya matayarisho kwa ajili ya Pasaka, ambayo walisherehekea baadaye “ilipofika jioni” mwanzoni mwa Nisani 14.—Mk 14:16, 17.
nwtsty habari za utafiti—Mt 26:39
niondolee kikombe hiki: Katika Biblia, mara nyingi “kikombe” kilitumiwa kuwakilisha mapenzi ya Mungu, au “mgawo” wa mtu. (Ona habari za utafiti—Mt 20:22.) Hapana shaka kwamba Yesu alihangaikia sana jinsi ambavyo kifo chake akiwa amehukumiwa kuwa mtu aliyekufuru na mchochezi wa uasi kingemletea Mungu suto na hilo lilimchochea kusali kwamba “kikombe” hicho kiondolewe.
APRILI 9-15
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 27-28
“Nendeni Mkafanye Wanafunzi—Kwa Nini, Wapi, na Jinsi Gani?”
nwtsty habari za utafiti—Mt 28:19
mkafanye wanafunzi: Kitenzi cha Kigiriki ma·the·teuʹo kinaweza kurejelea “fundisha” ukiwa na kusudi la kufanya wanafunzi. (Linganisha na neno lililotumiwa katika Mt 13:52, ambapo limetafsiriwa “anapofundishwa.”) Vitenzi “kubatiza” na “kufundisha” vinaonyesha mambo yanayohusika katika amri ya ‘kufanya wanafunzi.’
watu wa mataifa yote: Tafsiri ya neno kwa neno inasema “mataifa yote,” lakini muktadha unaonyesha kwamba maneno hayo yanarejelea watu kutoka katika mataifa yote, kwa kuwa kiwakilishi cha Kigiriki “wao” katika neno mkiwabatiza kimeandikwa kwa jinsia ya kiume na kinarejelea watu, si “mataifa” kwa kuwa neno “mataifa” halina jinsia katika Kigiriki. Amri hiyo ya kuwafikia “watu wa mataifa yote” ilikuwa mpya. Kabla ya Yesu kuanza huduma yake, Maandiko yanaonyesha kwamba Watu wa Mataifa walikaribishwa kwenda Israeli ikiwa walitaka kumtumikia Yehova. (1Fa 8:41-43) Hata hivyo, kwa kutoa amri hii Yesu aliwaagiza wanafunzi wake wapanue kazi ya kuhubiri kwa kuwafikia watu wengine mbali na Wayahudi, na hivyo akakazia kwamba kazi ya Kikristo ya kufanya wanafunzi inapaswa kufanywa duniani pote.—Mt 10:1, 5-7; Ufu 7:9; ona habari za utafiti—Mt 24:14.
nwtsty habari za utafiti—Mt 28:20
kuwafundisha: Neno la Kigiriki linalorejelea “kufundisha” linahusisha kutoa maagizo, kufafanua, kuonyesha vitu kwa hoja, na kutoa uthibitisho. (Ona habari za utafiti—Mt 3:1; 4:23.) Kuwafundisha kushika mambo yote ambayo Yesu aliamuru kungekuwa jambo la kuendelea, ambalo lingehusisha kufundisha alichofundisha, kutumia mafundisho yake maishani, na kufuata mfano wake.—Yoh 13:17; Efe 4:21; 1Pe 2:21.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mt 27:51
pazia: Pazia hilo maridadi lililotiwa nakshi lilitenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi katika hekalu. Mapokeo ya Kiyahudi yanaonyesha kwamba pazia hilo zito lilikuwa na urefu wa mita 18, upana wa mita 9, na unene wa sentimita 7.4. Mbali tu na kuonyesha hasira yake kwa wale waliomuua Mwana wake, Yehova alipopasua pazia hilo vipande viwili alikuwa pia akionyesha kwamba njia ya kuingia mbinguni ilikuwa imefunguliwa.—Ebr 10:19, 20; ona Kamusi.
patakatifu: Neno la Kigiriki na·osʹ linalotumiwa hapa linarejelea sehemu ya katikati iliyokuwa na Patakatifu na Patakatifu Zaidi.
nwtsty habari za utafiti—Mt 28:7
mkawaambie wanafunzi wake kwamba alifufuliwa: Mbali tu na kuwa wanafunzi wa kwanza kuambiwa kuhusu ufufuo wa Yesu, wanawake hao waliagizwa pia wakawajulishe wanafunzi wale wengine. (Mt 28:2, 5, 7) Kulingana na mapokeo ya Kiyahudi yasiyo ya kimaandiko, ushahidi wa mwanamke hakukubaliwa mahakamani. Tofauti na hilo, malaika wa Yehova aliwaheshimu wanawake hao kwa kuwapa mgawo huo wenye shangwe.
APRILI 16-22
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MARKO 1-2
“Umesamehewa Dhambi Zako”
nwtsty habari za utafiti—Mk 2:9
Ni jambo gani rahisi zaidi: Inaweza kuwa rahisi kwa mtu kusema kwamba anaweza kusamehe dhambi, kwa sababu hakuna uthibitisho wowote unaoonekana ambao ungehitajika ili kuthibitisha madai yake. Lakini kusema Simama . . . utembee, muujiza ungehitajika ili kuonyesha kwamba Yesu alikuwa na mamlaka ya kusamehe dhambi. Simulizi hili na andiko la Isaya 33:24 yanaonyesha kwamba magonjwa yanatokana na hali yetu ya dhambi.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mk 1:11
Sauti ikasikika kutoka mbinguni: Mara ya kwanza kati ya mara tatu ambazo Yehova anaripotiwa kuzungumza moja kwa moja na wanadamu katika masimulizi ya Injili.—Ona habari za utafiti—Mk 9:7; Yoh 12:28.
Wewe ni Mwanangu: Akiwa kiumbe wa roho, Yesu alikuwa Mwana wa Mungu. (Yoh 3:16) Tangu alipozaliwa akiwa mwanadamu, Yesu alikuwa “mwana wa Mungu” kama Adamu alivyokuwa alipokuwa mwanadamu mkamilifu. (Lu 1:35; 3:38) Hata hivyo, tunaweza kusema kwamba maneno ya Mungu hapa yanaashiria mengi zaidi ya kumtambulisha tu. Kupitia tangazo hili ambalo lilitia ndani kumiminwa kwa roho takatifu, Mungu alionyesha kwamba mwanadamu Yesu alikuwa Mwana Wake mpendwa wa kiroho, ‘aliyezaliwa tena’ akiwa na tumaini la kurudi mbinguni na kwamba alikuwa ametiwa mafuta kwa roho awe Mfalme aliyewekwa rasmi na Kuhani Mkuu.—Linganisha Yoh 3:3-6; 6:51; Lu 1:31-33; Ebr 2:17; 5:1, 4-10; 7:1-3.
nimekukubali: Au “Ninapendezwa sana nawe; Ninafurahishwa sana nawe.” Neno kama hilo lilitumiwa kwenye Mt 12:18, ambalo ni nukuu kutoka katika Isa 42:1 kuhusu Masihi aliyeahidiwa, au Kristo. Kumiminwa kwa roho takatifu na tangazo la Mungu kuhusu mwana wake ulikuwa uthibitisho wa wazi kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa.—Ona habari za utafiti—Mt 3:17; 12:18.
nwtsty habari za utafiti—Mk 2:28
Bwana wa Sabato: Yesu alisema maneno hayo kujihusu yeye mwenyewe (Mt 12:8; Lu 6:5), akionyesha kwamba angeweza kuitumia siku ya Sabato kufanya kazi aliyoagizwa na Baba yake wa mbinguni. (Linganisha Yoh 5:19; 10:37, 38.) Yesu alifanya miujiza ya pekee sana katika siku ya Sabato, kutia ndani kuwaponya wagonjwa. (Lu 13:10-13; Yoh 5:5-9; 9:1-14) Ni wazi kwamba kufanya hivyo kulionyesha kitulizo atakacholeta wakati ambapo Ufalme wake utatawala, ambao utakuwa kama pumziko la sabato.—Ebr 10:1.
APRILI 23-29
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MARKO 3-4
“Kuponya Katika Siku ya Sabato”
nwtsty habari za utafiti—Mk 3:5
kwa hasira na kuhuzunika sana: Ni Marko peke yake anayeeleza hisia za Yesu alipotambua ugumu wa mioyo ya viongozi wa kidini katika pindi hii. (Mt 12:13; Lu 6:10) Inawezekana kwamba Petro ndiye aliyekuwa chanzo cha ufafanuzi huo wa wazi kuhusu hisia za Yesu, kwa kuwa Petro alikuwa mtu mwenye hisia nyingi.—Tazama “Utangulizi wa Marko.”
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mk 3:29
anayekufuru roho takatifu: Kukufuru ni kuchongea, kusema maneno yenye kuumiza au matukano dhidi ya Mungu au dhidi ya mambo matakatifu. Kwa kuwa Mungu ndiye chanzo cha roho takatifu, kupinga kimakusudi roho takatifu au utendaji wake ni kumkufuru Mungu. Kama inavyoonyeshwa kwenye Mt 12:24, 28 na Mk 3:22, viongozi wa dini ya Kiyahudi waliona roho ya Mungu ikitenda kazi kupitia Yesu alipofanya miujiza; lakini walidai kwamba nguvu hizo zilitoka kwa Shetani Ibilisi.
atakuwa na hatia ya dhambi ya milele: Inaonekana inarejelea dhambi iliyofanywa kimakusudi ambayo ina madhara ya milele; hakuna dhabihu inayoweza kufunika dhambi kama hiyo.—Ona habari ya utafiti yenye kichwa anayekufuru roho takatifu kuhusu mstari huu na habari ya utafiti katika simulizi linalopatana na hili kwenye Mt 12:31.
MAISHA YA MKRISTO
“Yule Aliye na Masikio ya Kusikiliza, na Asikilize”
nwtsty habari za utafiti—Mk 4:9
Yule aliye na masikio ya kusikiliza, na asikilize: Kabla ya kusimulia mfano wa mpandaji, Yesu alisema: “Sikilizeni.” (Mk 4:3) Alimalizia mfano huo kwa himizo hilo, akikazia jinsi ilivyo muhimu kwa wafuasi wake kutii ushauri wake kwa uangalifu. Himizo kama hilo linaweza kupatikana katika Mt 11:15; 13:9, 43; Mk 4:23; Lu 8:8; 14:35; Ufu 2:7, 11, 17, 29; 3:6, 13, 22; 13:9.
APRILI 30–MEI 6
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MARKO 5-6
“Yesu Ana Nguvu za Kuwafufua Wapendwa Wetu Waliokufa”
nwtsty habari za utafiti—Mk 5:39
hajafa bali amelala usingizi: Mara nyingi Biblia inafananisha kifo na usingizi. (Zb 13:3; Yoh 11:11-14; Mdo 7:60; 1Ko 7:39; 15:51; 1Th 4:13) Yesu alikuwa karibu kumfufua msichana huyo, kwa hiyo alisema hivyo kwa sababu alikuwa karibu kuonyesha kwamba kama tu watu wanavyoweza kuamshwa kutoka katika usingizi mzito, ndivyo wanavyoweza kuamshwa kutoka katika kifo. Nguvu za Yesu za kumfufua msichana huyo zilitoka kwa Baba yake, “anayewafanya wafu kuwa hai na kuyaita mambo yasiyokuwako kana kwamba yako.”—Ro 4:17.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mk 5:19
ukawaambie: Tofauti na maagizo ya kawaida ya Yesu ya kutotangaza miujiza yake (Mk 1:44; 3:12; 7:36), Yesu alimwagiza mwanamume huyo akawaeleze ndugu zake wa ukoo kile kilichokuwa kimetokea. Inawezekana Yesu alifanya hivyo kwa sababu aliombwa aondoke katika eneo hilo na hangeweza kutoa ushahidi yeye mwenyewe; pia kufanya hivyo huenda kungezuia kuenea kwa habari zisizofaa kuhusu nguruwe waliokuwa wamekufa.
nwtsty habari za utafiti—Mk 6:11
kung’uteni mavumbi yaliyo kwenye miguu yenu: Ishara hiyo ilionyesha kwamba wanafunzi hawangekuwa na hatia ya hukumu ambayo ingetoka kwa Mungu. Msemo kama huo unaonekana pia katika Mt 10:14; Lu 9:5. Marko na Luka wanaongezea maneno ili kuwa ushahidi [au, “dhidi”] kwao. Paulo na Barnaba walitumia agizo hilo walipokuwa Antiokia ya Pisidia. (Mdo 13:51) Paulo alipofanya jambo kama hilo alipokuwa Korintho kwa kukung’uta mavazi yake, aliongezea kusema hivi: “Damu yenu na iwe juu ya vichwa vyenu wenyewe. Mimi ni safi.” (Mdo 18:6) Huenda tayari wanafunzi walifahamu ishara kama hizo; Wayahudi waliojiona kuwa watu wa kidini wangekung’uta kile walichoona kuwa mavumbi yasiyo safi kabla ya kuingia tena katika nchi ya Kiyahudi ikiwa walikuwa wamesafiri kupitia nchi za Watu wa Mataifa. Hata hivyo, Yesu alikuwa akifikiria jambo tofauti alipowapa wanafunzi wake maagizo haya.