Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
JUNI 4-10
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MARKO 15-16
“Yesu alitimiza Unabii”
nwtsty habari za utafiti—Mk 15:24, 29
wakagawana mavazi yake: Simulizi kwenye Yoh 19:23, 24 linaongezea habari za ziada ambazo hazikutajwa na Mathayo, Marko, na Luka: Inaonekana kwamba askari Waroma walipigia kura mavazi yake ya nje na vazi la ndani; askari hao waligawanya mavazi yake ya nje “vipande vinne, kila askari kipande kimoja”; hawakutaka kurarua vazi la ndani, kwa hiyo, walilipigia kura; kwa kupigia kura vazi la Masihi walitimiza Zb 22:18. Inaonekana kwamba ilikuwa kawaida kwa askari waliotekeleza hukumu ya kifo kujiwekea mavazi ya aliyeuawa, kwa hiyo, wahalifu walivuliwa mavazi yao na mali nyingine kabla ya kuuawa. Hilo lilifanya kuuawa kwa njia hiyo kuwa jambo lenye kuaibisha hata zaidi.
wakitikisa vichwa vyao: Ishara hiyo ilionyesha dharau, kumshushia mtu heshima, au kumdhihaki, na kwa kawaida iliandamana na maneno ya dharau. Bila kujua wapita-njia hao walitimiza unabii unaopatikana kwenye Zb 22:7.
nwtsty habari za utafiti—Mk 15:43
Yosefu: Tofauti iliyopo kati ya waandikaji wa Injili inaonekana wazi kupitia habari walizoandika kumhusu Yosefu. Mathayo aliyekuwa mkusanya-kodi anasema kwamba alikuwa “tajiri”; Marko, ambaye aliandika hasa kwa ajili ya Waroma, anasema kwamba alikuwa “mshiriki wa Baraza aliyeheshimiwa” ambaye alikuwa akiungojea Ufalme wa Mungu; Luka, aliyekuwa daktari mwenye huruma, anasema kwamba “alikuwa mtu mwema na mwadilifu” ambaye hakupiga kura kuunga mkono tendo la Baraza la kumuua Yesu; Yohana peke yake ndiye anayeripoti kwamba alikuwa “mwanafunzi wa . . . siri kwa sababu aliwaogopa Wayahudi.”—Mt 27:57-60; Mk 15:43-46; Lu 23:50-53; Yoh 19:38-42.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mk 15:25
saa ya tatu: Yaani, karibu saa 3:00 asubuhi. Watu fulani wanatumia maneno hayo kuonyesha kwamba simulizi hili linapingana na Yoh 19:14-16, ambalo linasema Pilato alimkabidhi Yesu kwao “karibu saa sita” ili wamuue. Ingawa Maandiko hayaelezi kikamili sababu ya tofauti iliyopo, yafuatayo ni mambo fulani ya kuzingatia: Kwa ujumla, masimulizi yote ya Injili yanapatana kuhusu wakati wa matukio ya siku ya mwisho ya Yesu duniani. Masimulizi yote manne yanaonyesha kwamba makuhani na wazee walikutana kulipopambazuka kisha wakampeleka Yesu mbele ya Gavana Mroma Pontio Pilato. (Mt 27:1, 2; Mk 15:1; Lu 22:66–23:1; Yoh 18:28) Mathayo, Marko, na Luka wanaripoti kwamba Yesu alipokuwa tayari ametundikwa kwenye mti wa mateso, giza lilitokea katika nchi yote kuanzia “saa sita mpaka saa tisa.” (Mt 27:45, 46; Mk 15:33, 34; Lu 23:44) Tunaweza kuelewa wakati ambapo hukumu ya kifo ilianza kutekelezwa tunapozingatia hili: Watu fulani waliona kupigwa mijeledi kuwa sehemu ya utekelezaji wa hukumu ya kifo. Nyakati nyingine mtu alipigwa sana mijeledi hivi kwamba akafa. Yesu alipigwa sana mijeledi hivi kwamba ingawa alianza kubeba mti wa mateso, baada ya muda alihitaji msaada wa kubebewa mti huo. (Lu 23:26; Yoh 19:17) Ikiwa kupigwa mijeledi kulionwa kuwa mwanzo wa utekelezaji wa hukumu ya kifo, basi muda fulani ungepita kabla ya Yesu kutundikwa kwenye mti wa mateso. Ili kuunga mkono wazo hilo, kupigwa mijeledi na kuuawa kwa kutundikwa kwenye mti wa mateso kunatajwa pamoja kwenye Mt 27:26 na Mk 15:15. Hivyo, huenda watu wakawa na maoni yanayotofautiana kuhusu kutekelezwa kwa hukumu ya kifo kwa kutegemea wanafikiri hukumu hiyo ilianza kutekelezwa wakati gani. Huenda hilo likatusaidia kuelewa sababu iliyomfanya Pilato ashangae aliposikia kwamba Yesu alikufa upesi baada ya kutundikwa kwenye mti wa mateso. (Mk 15:44) Isitoshe, mara nyingi waandikaji wa Biblia hugawa siku katika sehemu nne zenye urefu wa saa tatu, kama usiku ulivyogawanywa. Kugawanya siku kwa njia hiyo kunatusaidia kuelewa kwa nini kuna marejeo mengi kuhusu saa tatu, saa sita, saa tisa, ambazo zilihesabiwa kuanzia saa 12:00 asubuhi. (Mt 20:1-5; Yoh 4:6; Mdo 2:15; 3:1; 10:3, 9, 30) Pia, kwa ujumla watu hawakuwa na saa zilizoonyesha wakati hususa, kwa hiyo, neno “karibu” lilitumiwa kukadiria saa kama tunavyoona kwenye Yoh 19:14. (Mt 27:46; Lu 23:44; Yoh 4:6; Mdo 10:3, 9) Kwa muhtasari: Inawezekana Marko alijumlisha kupigwa mijeledi na kutundikwa kwenye mti wa mateso, huku Yohana akirejelea tu wakati wa kutundikwa kwenye mti. Huenda waandikaji wote wawili walikadiria saa kwa kutumia kipindi cha saa tatu kilichokuwa karibu zaidi, na Yohana alitumia neno “karibu” alipozungumzia wakati ambapo Yesu alitundikwa. Mambo hayo yanaweza kutusaidia kuelewa tofauti ya wakati unaotajwa kwenye masimulizi hayo. Mwishowe, kwa kuwa Yohana aliandika miaka mingi sana baadaye, na kuonyesha wakati unaoonekana kutofautiana na ule ulioandikwa na Marko, tunapata uthibitisho kwamba Yohana hakunakili simulizi la Marko.
nwtsty habari za utafiti—Mk 16:8
kwa sababu waliogopa: Kulingana na hati za zamani zaidi zinazopatikana zinazoonyesha sehemu ya mwisho ya kitabu cha Marko, Injili hiyo inamalizia kwa maneno ya mstari wa 8. Watu fulani wanadai mstari huo unamalizia ghafla sana na haiwezekani kwamba maandishi ya awali ya kitabu hicho yalimalizia kwa njia hiyo. Hata hivyo, dai hilo halina msingi hasa ukizingatia kwamba Marko alitumia mtindo wa kuandika kwa muhtasari. Pia, Jerome na Eusebio, wasomi wa karne ya nne, wanaonyesha kwamba maandishi ya awali yanamalizia kwa maneno “kwa sababu waliogopa.”
Kuna hati kadhaa za Kigiriki na tafsiri za lugha nyingine zinazoongeza umalizio mrefu au umalizio mfupi baada ya mstari wa 8. Umalizio mrefu (ulio na mistari 12 ya ziada) unapatikana katika Kodeksi ya Alexandria, Kodeksi ya Efraemi Syri rescriptus, na Kodeksi ya Bezae Cantabrigiensis, zote za karne ya tano W.K. Umalizio huo mrefu unapatikana pia katika Vulgate ya Kilatini, Cureton ya Kisiria, na Peshitta ya Kisiria. Hata hivyo, haupatikani katika hati mbili za mapema zaidi za Kigiriki za karne ya nne, yaani, Kodeksi ya Sinai na Kodeksi ya Vatikani, au katika Kodeksi ya Kisiria ya Sinai ya karne ya nne au ya tano, au katika hati ya Marko ya awali zaidi ya Kikoptiki cha Kisahidi ya karne ya tano. Vivyo hivyo, hati za zamani zaidi za Marko katika Kiarmenia na Kigeorgia zinamalizia katika mstari wa 8.
Hati kadhaa za baadaye za Kigiriki na tafsiri za lugha fulani zina umalizio mfupi (unaotia ndani sentensi chache tu). Kodeksi ya Regius ya karne ya nane W.K. ina umalizio mrefu na mfupi. Inatoa maelezo machache kabla ya kila umalizio yanayosema kwamba masimulizi hayo yalitumiwa na wenye mamlaka au wataalamu fulani katika karne hiyo ya nane, ingawa inaonyesha kwamba hakuna yoyote kati yake ambayo yalikuwepo katika maandishi ya awali. UMALIZIO MFUPI
Umalizio mfupi baada ya Mk 16:8 si sehemu ya Maandiko yaliyoongozwa na roho. Umalizio huo unasema hivi:
Lakini mambo yote yaliyokuwa yameamriwa wakayasimulia kwa ufupi kwa wale waliomzunguka Petro. Tena, baada ya mambo hayo, Yesu mwenyewe akapeleka kupitia wao tangazo takatifu na lisiloweza kuharibika la wokovu wa milele kutoka mashariki mpaka magharibi.
UMALIZO MREFU
Umalizio mrefu baada ya Mk 16:8 si sehemu ya Maandiko yaliyoongozwa na roho. Umalizio huo unasema hivi:
9 Baada ya kufufuka mapema siku ya kwanza ya juma akamtokea kwanza Maria Magdalene, ambaye alikuwa amefukuza roho waovu saba kutoka kwake. 10 Maria Magdalene akaenda, akawaambia wale waliokuwa wamekuwa pamoja na Yesu, kwa maana walikuwa wakiomboleza na kulia. 11 Lakini wao, waliposikia alikuwa amefufuka na Maria Magdalene alikuwa amemwona, hawakuamini. 12 Tena, baada ya mambo hayo aliwatokea katika umbo lingine wawili kati yao wakitembea, walipokuwa wakienda mashambani; 13 nao wakarudi wakawaambia wale wengine. Wala hawakuwaamini. 14 Lakini baadaye akawatokea wale kumi na mmoja wenyewe walipokuwa wameketi mezani, naye akaushutumu ukosefu wao wa imani na ugumu wa moyo, kwa sababu hawakuwaamini wale waliokuwa wamemwona sasa akiwa amefufuka kutoka kwa wafu. 15 Naye akawaambia: “Nendeni, mkaingie katika ulimwengu wote na kuhubiri habari njema kwa uumbaji wote. 16 Yeye anayeamini na kubatizwa ataokolewa, lakini yule ambaye hataamini atahukumiwa adhabu. 17 Zaidi ya hayo, ishara hizi zitafuatana na wale wanaoamini: Kwa kutumia jina langu watatoa roho waovu, watasema kwa lugha, 18 nao watainua nyoka kwa mikono yao, na wakinywa kitu chochote chenye kuua hakitawaumiza hata kidogo. Wataweka mikono yao juu ya watu wagonjwa, nao watapona.”
19 Kwa hiyo, basi, Bwana Yesu, alipokuwa amekwisha kusema nao, akachukuliwa juu mpaka mbinguni na kuketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu. 20 Basi, wakatoka kwenda na kuhubiri kila mahali, huku Bwana akifanya kazi pamoja nao na kuutegemeza ujumbe huo kupitia ishara zenye kufuatana nao.
JUNI 11-17
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | LUKA 1
“Iga Unyenyekevu wa Maria”
nwtsty habari za utafiti—Lu 1:69
pembe ya wokovu: Au “mkombozi mwenye nguvu.” Katika Biblia, mara nyingi pembe za wanyama huwakilisha nguvu na ushindi. (1Sa 2:1; Zb 75:4, 5, 10; 148:14; maelezo ya chini) Pia, watawala na falme zinawakilishwa na pembe, iwe ni zenye uadilifu au la, na ushindi wao unalinganishwa na kusukuma kwa pembe. (Kum 33:17; Da 7:24; 8:2-10, 20-24) Katika muktadha huu, maneno “pembe ya wokovu” yanamrejelea Masihi kuwa yule aliye na nguvu za kuokoa, mkombozi mwenye nguvu.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Lu 1:76
utaenda mbele za Yehova: Yohana Mbatizaji ‘angeenda mbele za Yehova’ katika maana ya kwamba angemtangulia Yesu, ambaye angemwakilisha Baba yake na kuja katika jina la Baba yake.—Yoh 5:43; 8:29; ona pia habari za utafiti kuhusu Yehova katika mstari huu.
JUNI 18-24
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | LUKA 2-3
“Vijana—Je, Mnaendelea Kukua Kiroho?”
nwtsty habari za utafiti—Lu 2:41
Wazazi wake walikuwa na desturi: Sheria haikuwaamuru wanawake wahudhurie sherehe ya Pasaka. Hata hivyo, Maria alikuwa na desturi ya kuandamana na Yosefu kwenye safari ya kila mwaka hadi Yerusalemu kwa ajili ya sherehe hiyo. (Kut 23:17; 34:23) Kila mwaka, walisafiri umbali wa kilomita 300 hivi kwenda na kurudi pamoja na familia yao iliyokuwa ikiongezeka.
nwtsty habari za utafiti—Lu 2:46, 47
kuwauliza maswali: Kutokana na jinsi watu waliokuwa wakimsikiliza Yesu walivyoitikia, inaonekana kwamba maswali yake hayakuwa tu ya mvulana anayejaribu kutosheleza udadisi wake. (Lu 2:47) Katika muktadha fulani, neno la Kigiriki lililotafsiriwa ‘kuuliza maswali’ linaweza kurejelea aina ya maswali yanayoulizwa na kujibiwa kwa maswali mengine yanayotumiwa wakati wa kesi mahakamani. (Mt 27:11; Mk 14:60, 61; 15:2, 4; Mdo 5:27) Wanahistoria wanasema kwamba baadhi ya viongozi mashuhuri wa kidini walikuwa na desturi ya kubaki hekaluni baada ya sherehe na kufundisha kwenye mojawapo ya kumbi zilizokuwemo hekaluni. Watu wangeketi miguuni pa wanaume hao ili kuwasikiliza na kuuliza maswali.
walikuwa wakishangazwa: Kitenzi cha Kigiriki “kushangazwa” kinachotumiwa hapa kinaweza kurejelea mshangao wa kuendelea au wa kurudiwa-rudiwa.
nwtsty habari za utafiti—Lu 2:51, 52
akaendelea kuwatii: Au “akaendelea kujitiisha; akaendelea kuwa mtiifu.” Hali ya kuendelea ya kitenzi cha Kigiriki inaonyesha kwamba baada ya kuwashangaza walimu hekaluni na ujuzi wake wa Neno la Mungu, Yesu alirudi nyumbani na kwa unyenyekevu akajitiisha kwa wazazi wake. Utii huo ulikuwa muhimu kuliko ule wa mtoto mwingine yeyote; ulikuwa sehemu ya kutimiza Sheria ya Musa katika kila jambo.—Kut 20:12; Gal 4:4.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Lu 2:14
na amani duniani kwa watu wenye nia njema: Hati fulani zinasema “na amani duniani, nia njema kwa watu,” na maneno hayo yanapatikana katika tafsiri fulani za Biblia. Lakini maneno yanayotumiwa katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya yanapatana na hati nyingi zaidi. Tangazo hili la malaika halirejelei nia njema ya Mungu kuelekea watu wote licha ya mtazamo na matendo yao. Badala yake, linarejelea wale wanaopokea nia yake njema kwa sababu ya kuwa na imani ya kweli kwake na kuwa wafuasi wa Mwana wake.—Ona habari za utafiti kuhusu watu wenye nia njema katika mstari huu.
watu wenye nia njema: Ni wazi kwamba “nia njema” inayorejelewa katika tangazo hili la malaika inaonyeshwa na Mungu, si wanadamu. Neno la Kigiriki eu·do·kiʹa linaweza pia kutafsiriwa “kibali; upendeleo; kukubaliwa.” Kitenzi eu·do·keʹo kinachohusiana na neno hilo, kinatumiwa kwenye Mt 3:17; Mk 1:11; na Lu 3:22 (ona habari za utafiti—Mt 3:17; Mk 1:11), ambapo Mungu anazungumza na Mwana wake punde tu baada ya ubatizo wake. Kimsingi kitenzi hicho kinamaanisha, “kukubali; kufurahishwa na; kupendezwa na.” Kama yalivyotumiwa hapa, maneno “watu wa nia njema” (an·throʹpois eu·do·kiʹas) yanawakilisha watu ambao wana kibali cha Mungu na nia yake njema, na yanaweza pia kutafsiriwa “watu ambao anawakubali; watu ambao wanamfurahisha.” Kwa hiyo, tangazo hilo la malaika lilikuwa likirejelea nia njema ya Mungu, si kuelekea wanadamu kwa ujumla, bali kuelekea wale ambao wana imani ya kweli kwake na ambao wanakuwa wafuasi wa Mwana wake. Ingawa katika muktadha fulani neno la Kigiriki eu·do·kiʹa linaweza kurejelea nia njema ya wanadamu (Ro 10:1; Flp 1:15), mara nyingi linatumiwa kuhusu nia njema ya Mungu, au upendezi mwema, au njia inayokubaliwa naye (Mt 11:26; Lu 10:21; Efe 1:5, 9; Flp 2:13; 2Th 1:11). Kulingana na Septuajinti neno hilo linatumiwa kuhusu “nia njema” ya Mungu kwenye Zb 51:18 [50:20, LXX].
JUNI 25–JULAI 1
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | LUKA 4-5
“Pinga Vishawishi Kama Yesu Alivyofanya”
nwtsty video
Mnara wa Hekalu
Huenda Shetani alimsimamisha Yesu kihalisi juu ya “mnara wa [au “sehemu ya juu zaidi ya”] hekalu” na kumwambia ajitupe chini, lakini mahali hususa ambapo Yesu alisimama hapajulikani. Kwa kuwa neno “hekalu” linalotumiwa hapa linaweza kurejelea jengo lote la hekalu, huenda ikawa Yesu alisimama juu ya kona ya kusini-mashariki (1) ya eneo la hekalu. Au huenda ikawa alisimama juu ya kona nyingine ya hekalu. Ikiwa angeanguka kutoka juu ya eneo lolote kati ya hayo angekufa isipokuwa tu kama Yehova angemwokoa.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Lu 4:17
kitabu cha kukunjwa cha nabii Isaya: Kitabu cha Kukunjwa cha Bahari ya Chumvi cha Isaya kimefanyizwa kwa vipande 17 vya mafunjo vilivyounganishwa, na hivyo kufanyiza kitabu cha kukunjwa kilicho na urefu wa mita 7.3 kilicho na safu 54. Huenda kitabu cha kukunjwa kilichotumiwa katika sinagogi la Nazareti kilikuwa na urefu kama huo. Kwa kuwa katika karne ya kwanza vitabu vya Biblia havikuwa vimepangwa katika sura na mistari, Yesu alihitaji kutafuta simulizi hususa alilotaka kusoma. Lakini tunaona wazi kwamba Yesu alifahamu vizuri kabisa Neno la Mungu kwa kuwa alipata mahali ambapo maneno hayo ya kinabii yalikuwa yameandikwa.
nwtsty habari za utafiti—Lu 4:25
kwa miaka mitatu na miezi sita: Kulingana na 1Fa 18:1, Eliya alitangaza mwisho wa ukame “katika mwaka wa tatu.” Kwa sababu hiyo, baadhi ya watu wamedai kwamba Yesu anapinga simulizi la 1 Wafalme. Hata hivyo, simulizi kwenye Maandiko ya Kiebrania halidokezi kwamba ukame uliisha kabla ya miaka mitatu kwisha. Ni wazi kwamba maneno “katika mwaka wa tatu” yanahusu kipindi kilichoanza wakati ambapo kwa mara ya kwanza Eliya alimwambia Ahabu kwamba kutakuwa na ukame. (1Fa 17:1) Kuna uwezekano kwamba tangazo hilo lilitolewa katika majira ya kiangazi—ambayo kwa kawaida yaliendelea kwa miezi sita hivi lakini huenda yalikuwa yameendelea kwa muda mrefu kuliko kawaida. Isitoshe, ukame huo haukwisha mara moja baada ya Eliya kuzungumza na Ahabu, “katika mwaka wa tatu,” bali uliisha baada ya jaribio la moto kwenye Mlima Karmeli. (1Fa 18:18-45) Hivyo, kipindi cha wakati kinachotajwa na Yesu hapa, kutia ndani maneno kama hayo yaliyoandikwa na ndugu nusu ya Kristo kwenye Yak 5:17, kinapatana vizuri na kile cha 1Fa 18:1.