Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • mwbr18 Julai kur. 1-6
  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha
  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha—2018
  • Vichwa vidogo
  • JULAI 2-8
  • JULAI 9-15
  • JULAI 16-22
  • JULAI 23-29
  • JULAI 30–AGOSTI 5
Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha—2018
mwbr18 Julai kur. 1-6

Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha

JULAI 2-8

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | LUKA 6-7

“Wapimie Wengine kwa Ukarimu”

nwtsty habari za utafiti—Lu 6:37

Endeleeni kusamehe, nanyi mtasamehewa: Au “Endeleeni kuachilia, nanyi mtaachiliwa.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kusamehe” linamaanisha kihalisi “kuachilia huru; kufungulia (kwa mfano, mfungwa).” Katika muktadha huu, linapotumiwa kuonyesha kwa nini hatupaswi kuhukumu au kulaumu, linatokeza wazo la kuondolea mashtaka na kusamehe, hata ikiwa inaonekana kwamba adhabu au malipo yanapaswa kutolewa.

nwtsty habari za utafiti—Lu 6:38

Muwe na mazoea ya kuwapa watu: Au “Endeleeni kutoa.” Kitenzi cha Kigiriki kinachotumiwa hapa kinaweza kumaanisha “kutoa” na kinarejelea tendo linaloendelea.

nwtsty habari za utafiti—Lu 6:38

mfuko wa nguo zenu: Neno la Kigiriki linamaanisha kihalisi “kifua chenu,” lakini katika muktadha huu huenda linamaanisha mkunjo uliokuwa juu ya mshipi uliofanyizwa na sehemu inayoning’inia ya vazi la nje. Huenda ‘kumwaga kwenye mfuko wa nguo’ kukarejelea zoea la wafanyabiashara fulani la kujaza bidhaa zilizonunuliwa kwenye mkunjo huo wa nguo ya nje.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Lu 7:35

watoto wake: Au “matokeo yake.” Hapa hekima inazungumziwa kama mtu na inaonyeshwa kuwa ina watoto. Katika simulizi linalopatana na hili kwenye Mt 11:19, hekima inaonyeshwa ikiwa na “kazi.” Watoto wa hekima, au kazi—yaani, uthibitisho uliotolewa na Yohana Mbatizaji na Yesu—zinaonyesha wazi kwamba mashtaka dhidi yao yalikuwa ya uwongo. Ni kana kwamba Yesu anasema: ‘Angalieni kazi na mwenendo mzuri, nanyi mtajua kwamba mashtaka hayo ni ya uwongo.’

JULAI 9-15

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | LUKA 8-9

“Njoo, Uwe Mfuasi Wangu—Unahitaji Kufanya Nini?”

it-2 494

Kiota

Mwandishi fulani alipomwambia Yesu: “Mwalimu, nitakufuata popote utakapoenda,” Yesu alimwambia: “Mbweha wana mapango na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali pa kulaza kichwa chake.” (Mt 8:19, 20; Lu 9:57, 58) Hapa Yesu alikuwa akionyesha kwamba ili mtu huyo awe mfuasi wake angehitaji kuacha starehe na mambo mengine yanayofurahiwa na watu, na badala yake amtegemee Yehova kikamili. Kanuni hiyo inapatikana katika sala ya kielelezo aliyowafundisha wanafunzi wake: “Utupatie leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii,” na pia katika maneno haya yake: “Vivyo hivyo, kwa hakika yeyote kati yenu asipoaga mali zake zote hawezi kuwa mwanafunzi wangu.”—Mt 6:11; Lu 14:33.

nwtsty habari za utafiti—Lu 9:59, 60

nikamzike baba yangu: Huenda maneno hayo hayamaanishi kwamba baba ya mwanamume huyo alikuwa ametoka tu kufa na hivyo alikuwa akiomba akafanye mipango ya mazishi. Ikiwa ingalikuwa hivyo, haipatani na akili kwamba angalikuwa hapo akizungumza na Yesu. Katika nyakati za kale, kule Mashariki ya Kati, mtu katika familia alipokufa mazishi yalifanywa upesi sana, kwa kawaida siku ileile. Kwa hiyo, huenda baba ya mwanamume huyo alikuwa mgonjwa au amezeeka, lakini hakuwa amekufa. Pia, Yesu hangemwambia mwanamume huyo amwache mzazi wake ikiwa alikuwa mgonjwa na mwenye uhitaji, kwa hiyo, lazima kuwe kulikuwa na washiriki wengine wa familia ambao wangeshughulikia mahitaji hayo ya lazima. (Mk 7:9-13) Kwa maneno mengine, mwanamume huyo alikuwa akisema, ‘Nitakufuata, lakini si wakati ambapo baba yangu bado yuko hai. Subiri hadi baba atakapokufa halafu nimzike.’ Hata hivyo, kwa maoni ya Yesu, mwanamume huyo alikuwa akipoteza fursa ya kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani mwake.—Lu 9:60, 62.

Waache wafu wawazike wafu wao: Kama ilivyoonyeshwa katika habari za utafiti kuhusu Lu 9:59, inawezekana kwamba baba ya mwanamume ambaye Yesu alikuwa akizungumza naye alikuwa mgonjwa au amezeeka, lakini hakuwa amekufa. Hivyo, ni wazi kwamba Yesu alikuwa akisema: ‘Waache wale ambao wamekufa kiroho wawazike wafu wao,’ yaani, mwanamume huyo alipaswa kuwaacha watu wengine wa ukoo wake wamtunze baba yake hadi atakapokufa na kuzikwa. Kwa kumfuata Yesu, mtu huyo angekuwa katika njia ya uzima wa milele na si kati ya wale ambao wamekufa kiroho machoni pa Mungu. Katika jibu lake, Yesu anaonyesha kwamba kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani na kuutangaza kila mahali ni muhimu ili kuendelea kuwa hai kiroho.

nwtsty picha

Kulima kwa plau

Mara nyingi kulima kwa plau kulifanywa katika majira ya vuli wakati ambapo mvua zililegeza udongo uliokuwa umekaushwa na jua kali la majira ya kiangazi. (Ona Nyongeza B15.) Plau fulani zilifanyizwa na mbao iliyochongoka ambayo huenda ncha yake ilikuwa ya chuma, na ambayo iliunganishwa kwenye ubao uliovutwa na mnyama mmoja au zaidi. Baada ya udongo kulimwa, mbegu zilipandwa. Katika Maandiko ya Kiebrania, mara nyingi kazi ya kulima kwa jembe la plau ilitumiwa katika mifano mingi. (Amu 14:18; Isa 2:4; Yer 4:3; Mik 4:3) Yesu alipofundisha mambo muhimu, mara nyingi alitumia mifano ya utendaji wa kilimo. Kwa mfano, alizungumzia kuhusu kazi inayohusika katika kulima kwa jembe la ng’ombe ili kukazia umuhimu wa kuwa mwanafunzi aliyejitoa kwa moyo wote. (Lu 9:62) Mtu anayelima kwa jembe linalovutwa na ng’ombe akikengeushwa, anaweza kulima mistari iliyo kombo. Vivyo hivyo, mwanafunzi wa Kristo akikengeuka au kugeuka na kuacha kutimiza majukumu yake anaacha kustahili Ufalme wa Mungu.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Lu 8:3

waliokuwa wakiwahudumia: Au “walikuwa wakiwategemeza (kuwaandalia).” Neno la Kigiriki di·a·ko·neʹo linaweza kurejelea kushughulikia mahitaji ya wengine kwa kutafuta, kupika, na kuandaa chakula, na kadhalika. Linatumiwa kwa njia kama hiyo kwenye Lu 10:40 (“nishughulike”), Lu 12:37 (“kuwahudumia”), Lu 17:8 (“unihudumie”), na Mdo 6:2 (“kugawa chakula”), lakini linaweza pia kurejelea huduma nyingine ambazo mtu anafanyiwa. Hapa linafafanua jinsi ambavyo wanawake waliotajwa katika mstari wa 2 na 3 walivyomtegemeza Yesu na wanafunzi wake na kuwasaidia kukamilisha mgawo wao waliopewa na Mungu. Kwa kufanya hivyo, wanawake hao walimtukuza Mungu, naye alionyesha anawathamini kwa kuhifadhi katika Biblia matendo yao ya huruma na ukarimu ili vizazi vyote vya wakati ujao visome kuwahusu. (Met 19:17; Ebr 6:10) Neno hilohilo la Kigiriki linatumiwa kuwahusu wanawake kwenye Mt 27:55; Mk 15:41.

JULAI 16-22

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | LUKA 10-11

“Mfano wa Msamaria Mwema”

nwtsty video

Barabara Kutoka Yerusalemu Kwenda Yeriko

Huenda barabara (1) inayoonyeshwa katika video hii fupi ilipita kwenye njia kama hiyo ambayo huenda zamani iliunganisha Yerusalemu na Yeriko. Barabara hiyo ilikuwa na urefu wa zaidi ya kilomita 20 na mteremko mkali wa kilomita moja uliojipinda-pinda kutoka Yerusalemu hadi Yeriko. Mara nyingi sana watu walivamiwa na wahalifu katika barabara hiyo ya nyikani isiyokuwa na watu wengi hivi kwamba kikosi cha askari kiliwekwa hapo ili kuwalinda wasafiri. Jiji la Yeriko la Waroma (2) lilikuwa kwenye barabara iliyotoka kwenye nyika ya Yudea. Jiji la kale la Yeriko (3) lilikuwa kilomita 2 hivi kutoka kwenye jiji hilo la Waroma.

nwtsty habari za utafiti—Lu 10:33, 34

msamaria fulani: Kwa ujumla, Wayahudi waliwadharau Wasamaria na walikataa kushirikiana nao kwa njia yoyote. (Yoh 4:9) Hata Wayahudi fulani walitumia neno “Msamaria” kama neno la dharau au matusi. (Yoh 8:48) Rabi mmoja ananukuliwa kwenye Mishna akisema: “Mtu anayekula kipande cha mkate ambacho amepewa na Msamaria ni kama amekula nyama ya nguruwe.” (Shebith 8:10) Wayahudi wengi hawangeamini ushahidi wa Msamaria au kukubali huduma inayotolewa nao. Kwa kuwa Yesu alifahamu mtazamo wenye dharau ambao kwa kawaida Wayahudi walikuwa nao, alitoa hoja yenye nguvu katika mfano huu ambao mara nyingi unaitwa mfano wa Msamaria mwema, au mwenye ujirani.

akayamwagia majeraha yake mafuta na divai, kisha akayafunga: Tabibu Luka anarekodi mfano ambao Yesu alisimulia, akifafanua jinsi jeraha lilivyotibiwa kupatana na mbinu za siku hizo. Mafuta na divai zilitumiwa kwa ukawaida nyumbani kutibu majeraha. Nyakati nyingine mafuta yalitumiwa kulegeza majeraha (linganisha Isa 1:6), na divai ina uwezo wa kusafisha kidonda na kuua wadudu. Pia, Luka alifafanua jinsi majeraha yalivyofungwa na hivyo kuyazuia yasiathiriwe zaidi.

nyumba ya wageni: Neno la Kigiriki linamaanisha kihalisi “mahali ambapo watu wote walipokewa au kukaribishwa.” Wasafiri pamoja na wanyama wao wangeweza kupata mahali pa kulala katika nyumba hizo. Msimamizi wa nyumba hiyo aliwapa wasafiri maandalizi ya msingi, na ikiwa angelipwa, angewashughulikia watu alioachiwa awatunze.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Lu 10:18

Ninamwona Shetani akiwa tayari ameanguka kutoka mbinguni kama radi: Ni wazi kwamba Yesu anazungumza kwa njia ya kinabii, akiona Shetani akitupwa kutoka mbinguni kana kwamba tayari jambo hilo limetukia. Ufu 12:7-9 inafafanua vita vilivyotukia mbinguni na kuhusianisha kuanguka kwa Shetani na kuzaliwa kwa Ufalme wa Kimasihi. Yesu alikuwa hapa akikazia kushindwa kwa Shetani na roho waovu wakati wa vita hivyo vya wakati ujao, kwa kuwa Mungu alikuwa amewawezesha wanafunzi 70, ambao walikuwa wanadamu wasio wakamilifu, kufukuza roho waovu.—Lu 10:17.

nwtsty habari za utafiti—Lu 11:5-9

Rafiki, nikopeshe mikate mitatu: Katika desturi za Mashariki ya Kati, watu hupenda kufanya yote wawezayo ili kuonyesha ukarimu, kama mfano huu unavyoonyesha. Hata ingawa wageni walifika katikati ya usiku bila kutazamiwa, jambo ambalo linaonyesha kwamba usafiri wakati huo haukuwa wenye kutegemeka, mwenye nyumba alihisi kwamba ana jukumu kubwa la kumwandalia mgeni wake kitu cha kula. Hata alihisi ana wajibu wa kumsumbua jirani yake saa hizo ili tu kuomba chakula.

Acha kunisumbua: Jirani katika mfano huu hakutaka kumsaidia, si kwa sababu hakuwa mwenye urafiki, bali kwa sababu tayari alikuwa amelala. Mara nyingi nyumba za nyakati hizo, hasa za maskini, zilikuwa za chumba kimoja tu kikubwa. Ikiwa mwenye nyumba huyo angeamka, angeisumbua familia yote, kutia ndani watoto waliokuwa wamelala.

anaendelea kumwomba: Neno la Kigiriki linalotumiwa hapa linaweza kutafsiriwa kihalisi kuwa “bila kiasi” au “bila aibu.” Hata hivyo, katika muktadha huu, linamaanisha kudumu kwa ujasiri au kusisitiza. Mwanamume katika mfano wa Yesu haaibiki au kujizuia kuomba anachohitaji kwa kusisitiza, naye Yesu anawaambia wanafunzi wake kwamba wanapaswa kutoa sala zao kwa msisitizo kama huo.—Lu 11:9, 10.

JULAI 23-29

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | LUKA 12-13

“Ninyi Ni Wenye Thamani Kuliko Shore Wengi”

nwtsty habari za utafiti—Lu 12:6

shore: Neno la Kigiriki strou·thiʹon linaonyesha udogo na linamaanisha ndege mdogo wa aina yoyote, lakini mara nyingi lilitumiwa kuwarejelea shore, ndege wa bei ya chini zaidi ambaye aliuzwa kwa ajili ya chakula.

nwtsty habari za utafiti—Lu 12:7

hata nywele zote za vichwa vyenu zimehesabiwa: Inasemekana kwamba kichwa cha mwanadamu kina wastani wa nywele zaidi ya 100,000. Kwa Yehova kujua kihususa hata mambo madogo kadiri hiyo kunatuhakikishia kwamba anamjali sana kila mfuasi wa Kristo.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Lu 13:24

Jitahidini sana: Au “Endeleeni kupambana.” Himizo la Yesu linakazia uhitaji wa kutenda kwa moyo wote kuingia kupitia mlango mwembamba. Katika muktadha huu, vitabu fulani vya marejeo vimependekeza maneno hayo yatafsiriwe “Jitahidi kikamili; Fanya jitihada zote.” Neno la Kigiriki a·go·niʹzo·mai linahusiana na nomino ya Kigiriki a·gonʹ, ambayo mara nyingi ilitumiwa kurejelea mashindano ya riadha. Kwenye Ebr 12:1, nomino hiyo inatumiwa kwa njia ya mfano kuwakilisha “shindano la mbio” za uzima. Pia imetumiwa kwa njia pana zaidi kurejelea “pambano” (Flp 1:30; Kol 2:1) au “pigano” (1Ti 6:12; 2Ti 4:7). Kitenzi cha Kigiriki kinachotumiwa kwenye Lu 13:24 kinatafsiriwa kwa njia mbalimbali kama vile “[kushiriki] katika shindano” (1Ko 9:25), ‘kujikaza’ (Kol 1:29; 4:12; 1Ti 4:10), na “pigana” (1Ti 6:12). Kwa sababu neno hilo linahusiana sana na mashindano katika michezo ya mbio, watu fulani wamependekeza kwamba jitihada ambayo Yesu aliwatia watu moyo wafanye inaweza kulinganishwa na mwanariadha anayejitahidi sana kwa nguvu zake zote kushinda tuzo.

nwtsty habari za utafiti—Lu 13:33

haiwezekani: Au “haipatani na akili (ni jambo lisiloweza kuwaziwa).” Ingawa hakuna unabii wa Biblia unaosema waziwazi kwamba Masihi angekufa Yerusalemu, mkataa huo unaweza kufikiwa kutokana na Da 9:24-26. Isitoshe, ikiwa Wayahudi wangemuua nabii, na hasa Masihi, ingetazamiwa kwamba wangemuua katika jiji hilo. Mahakama kuu, yaani, Sanhedrini iliyokuwa na washiriki 71, ilikutania Yerusalemu, kwa hiyo kesi ya watu walioshtakiwa kuwa manabii wa uwongo ilifanyiwa huko. Huenda pia Yesu alikuwa akifikiria kwamba Yerusalemu ndiko dhabihu za kawaida zilitolewa kwa Mungu na mahali ambapo mwanakondoo wa Pasaka alichinjwa. Maneno ya Yesu yalithibitika kuwa ya kweli. Alifikishwa mbele ya Sanhedrini kule Yerusalemu na kuhukumiwa. Naye alikufa katika Yerusalemu, nje tu ya kuta za jiji, akiwa “mwanakondoo . . . wa Pasaka.”—1Ko 5:7.

JULAI 30–AGOSTI 5

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | LUKA 14-16

“Mfano wa Mwana Mpotevu”

nwtsty habari za utafiti—Lu 15:11-16

Mtu fulani alikuwa na wana wawili: Sehemu fulani za mfano wa mwana mpotevu ni za pekee. Ni mojawapo ya mifano mirefu zaidi ambayo Yesu aliwahi kutoa. Jambo lenye kutokeza la mfano huo ni mahusiano ya familia ambayo anaelezea. Katika mifano mingine, mara nyingi Yesu alitaja vitu visivyo na uhai, kama vile aina mbalimbali za mbegu au udongo, au uhusiano rasmi kati ya bwana na watumwa wake. (Mt 13:18-30; 25:14-30; Lu 19:12-27) Hata hivyo, katika mfano huu, Yesu anakazia uhusiano wa karibu kati ya baba na wana wake. Wengi ambao husikia simulizi hilo huenda hawakuwa na baba mwenye fadhili na upendo kama huyo. Mfano huo unaonyesha huruma na upendo mwingi ambao Baba yetu wa mbinguni huwaonyesha watoto wake duniani, wale wanaoendelea kukaa naye na wale ambao humrudia baada ya kupotea.

Yule mdogo: Kulingana na Sheria ya Musa, mzaliwa wa kwanza alipokea urithi maradufu. (Kum 21:17) Kwa hiyo, ikiwa mwana mkubwa katika mfano huo alikuwa ndiye mzaliwa wa kwanza, hilo lingemaanisha kwamba urithi wa yule mwana mdogo ulikuwa nusu ya ule wa ndugu yake mkubwa.

akatumia vibaya: Neno la Kigiriki linalotumiwa hapa linamaanisha kihalisi “kutawanya (kuelekea upande tofauti-tofauti).” (Lu 1:51; Mdo 5:37) Kwenye Mt 25:24, 26, limetafsiriwa “kupepeta.” Hapa limetumiwa katika maana ya kufuja, kutumia kwa upumbavu.

maisha ya anasa: Au “maisha ya upotevu (ya kutojali).” Neno la Kigiriki linalohusiana na hilo linatumiwa likiwa na maana sawa kwenye Efe 5:18; Tit 1:6; 1Pe 4:4. Kwa kuwa neno la Kigiriki linaweza kutia ndani wazo la kuishi maisha ya kutumia pesa bila mpango, au upotevu, tafsiri fulani za Biblia hutumia maneno “kuishi kama mpotevu.”

akalishe nguruwe: Wanyama hawa hawakuwa safi kulingana na Sheria, kwa hiyo kwa Myahudi kazi hiyo ilikuwa ya kudharaulika na yenye kuchukiza.—Law 11:7, 8.

maganda ya karuba: Tunda au maganda ya karuba yana koa linalong’aa la rangi yenye mchanganyiko wa zambarau na kahawia na, kupatana na maana halisi ya jina lake katika Kigiriki (ke·raʹti·on, “pembe ndogo”), yana umbo la pembe iliyojipinda. Maganda ya karuba yanatumiwa hadi leo kama chakula kwa ajili ya farasi, ng’ombe, na nguruwe. Tunaweza kuona jinsi kijana huyo alivyokuwa katika hali mbaya sana tunapozingatia kwamba alikuwa tayari kula chakula kinacholiwa na nguruwe.—Ona habari za utafiti—Lu 15:15.

nwtsty habari za utafiti—Lu 15:17-24

dhidi yako: Au “machoni pako.” Kihusishi cha Kigiriki e·noʹpi·on, kinachomaanisha kihalisi “mbele; machoni pa,” kimetumiwa kwa njia hiyo kwenye 1Sa 20:1 katika Septuajinti. Katika mstari huo, Daudi anamuuliza Yonathani: “Nimemtendea baba yako dhambi gani” [au “nimetenda dhambi gani dhidi ya baba yako?”]

wafanyakazi: Aliporudi nyumbani, yule mwana mdogo alikusudia kumwomba baba yake amkubali, si kama mwana, bali kama mfanyakazi. Mfanyakazi huyo hakuwa sehemu ya shamba hilo, kama walivyokuwa watumwa, bali alikuwa kibarua, mtu wa nje aliyekodiwa, mara nyingi kwa siku moja tu.—Mt 20:1, 2, 8.

kumbusu kwa wororo: Au “kumbusu kwa upendo.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kumbusu kwa wororo” linaeleweka kuwa aina ya kitenzi phi·leʹo kinachoonyesha msisitizo, na nyakati nyingine kinaweza kutafsiriwa “kubusu” (Mt 26:48; Mk 14:44; Lu 22:47) lakini mara nyingi kinamaanisha “kumpenda” mtu. (Yoh 5:20; 11:3; 16:27). Kwa kumsalimu kwa uchangamfu na kwa urafiki, baba katika mfano huo anaonyesha utayari wake wa kumkaribisha tena mwana wake aliyetubu.

kuitwa mwanao: Hati fulani zinaongezea: “Nifanye niwe mmoja wa wafanyakazi wako,” lakini maandishi ya tafsiri ya sasa yanapatana na hati fulani za mapema zaidi zinazoheshimika. Wasomi fulani wanafikiri kwamba maneno hayo ya ziada yaliongezwa ili kufanya mstari huo upatane na Lu 15:19.

kanzu . . . pete . . . viatu: Kanzu hiyo haikuwa tu nguo ya kawaida lakini ilikuwa bora zaidi—huenda ilikuwa aina ya vazi rasmi lililorembeshwa sana ambalo lilitolewa kwa mgeni mheshimiwa. Tendo la kumvisha mwana wake pete linaonyesha kibali na upendo ambao baba alikuwa nao kutia ndani heshima, staha, na cheo ambacho mwana huyo aliyerudi alikuwa akipewa. Haikuwa kawaida kwa watumwa kuvaa pete na makubazi (viatu). Hivyo, baba alikuwa akidhihirisha kwamba mwana wake alikuwa akikaribishwa arudi akiwa mshiriki kamili wa familia.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Lu 14:26

hamchukii: Katika Biblia, neno “chuki” lina maana kadhaa. Linaweza kumaanisha hisia ya uhasama inayochochewa na nia ya kudhuru, ikimchochea mtu kuwadhuru wengine. Au linaweza kurejelea hisia kali ya kutompenda au ya kuepuka mtu au kitu, na hivyo kumfanya mtu ajiepushe kabisa na mtu au kitu hicho. Au huenda neno hilo likarejelea kupenda kwa kadiri ndogo. Kwa mfano, Yakobo anaposemekana kuwa ‘alimchukia’ Lea na kumpenda Raheli, inamaanisha kwamba hakumpenda Lea kama alivyompenda Raheli (Mwa 29:31, maelezo ya chini; Kum 21:15, maelezo ya chini), na neno hilo linatumiwa katika njia hiyo katika vitabu vingine vya kale vya Kiyahudi. Hivyo, Yesu hakumaanisha kwamba wafuasi wake walipaswa kuwa na uhasama kuelekea familia zao na kujielekea, kwa kuwa hilo lingepingana na Maandiko mengine yote. (Linganisha Mk 12:29-31; Efe 5:28, 29, 33.) Katika muktadha huu, neno ‘chuki’ lingeweza kutafsiriwa “kuwapenda kwa kadiri ndogo zaidi.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki