Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
DESEMBA 3-9
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATENDO 9-11
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mdo 10:6
Simoni, mtengenezaji wa ngozi: Mtengenezaji wa ngozi alishughulika na ngozi za wanyama, na alitumia kemikali fulani kuondoa manyoya, nyama, na mafuta yoyote yaliyosalia. Kisha alitumia kemikali nyingine kali ili kutayarisha ngozi hiyo kwa ajili ya kutengeneza bidhaa mbalimbali za ngozi. Shughuli yote ya kutengeneza ngozi ilitokeza harufu mbaya na ilihitaji maji mengi sana, huenda hilo likatusaidia kuelewa kwa nini Simoni aliishi kando ya bahari, huenda kandokando ya mji wa Yopa. Kulingana na Sheria ya Musa, mtu aliyefanya kazi ya kugusa mizoga hakuwa safi. (Law 5:2; 11:39) Kwa hiyo, Wayahudi wengi waliwadharau watengenezaji wa ngozi na wangesita kuishi katika nyumba ya mtu kama huyo. Hata baadaye Talmud ilisema kwamba kazi ya mtengenezaji wa ngozi ilikuwa duni kuliko ya mtu aliyeokota kinyesi. Hata hivyo, Petro hakuruhusu maoni hayo yamzuie kuishi na Simoni. Mtazamo huo mzuri wa Petro ulikuwa utangulizi mzuri wa mgawo uliofuata—kumtembelea Mtu wa Mataifa nyumbani kwake. Wasomi fulani wanasema kwamba neno la Kigiriki lililotafsiriwa “mtengenezaji wa ngozi” (byr·seusʹ) huenda likawa jina la pili la Simoni.
DESEMBA 10-16
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATENDO 12-14
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mdo 13:9
Sauli, aitwaye pia Paulo: Kuanzia hapa na kuendelea, Sauli anaitwa Paulo. Mtume huyo alizaliwa na wazazi Wayahudi na alikuwa na uraia wa Kiroma. (Mdo 22:27, 28; Flp 3:5) Hivyo, inawezekana kwamba tangu utotoni alikuwa na jina la Kiebrania Sauli na pia jina la Kiroma Paulo. Lilikuwa jambo la kawaida kwa Wayahudi wakati huo kuwa na majina mawili, hasa wale walioishi nje ya nchi ya Israeli. (Mdo 12:12; 13:1) Baadhi ya watu wa ukoo wa Paulo walikuwa na majina ya Kiroma na ya Kigiriki. (Ro 16:7, 21) Akiwa “mtume kwa mataifa,” Paulo alipewa mgawo wa kutangaza habari njema kwa watu wasio Wayahudi. (Ro 11:13) Inaonekana aliamua kutumia jina lake la Kiroma; huenda alihisi lingekubalika kwa urahisi zaidi. (Mdo 9:15; Gal 2:7, 8) Watu fulani wametoa wazo kwamba alianza kutumia jina lake la Kiroma ili kumheshimu Sergio Paulo, jambo ambalo halionekani kuwa kweli, kwa kuwa Paulo aliendelea kulitumia hata baada ya kuondoka Kipro. Wengine wamependekeza kwamba Paulo aliepuka kutumia jina lake la Kiebrania kwa kuwa lilipotamkwa katika Kigiriki lilikuwa sawa na neno la Kigiriki linalomrejelea mtu (au mnyama) aliyeyumbayumba alipotembea.—Ona habari za utafiti—Mdo 7:58.
Paulo: Katika tafsiri ya Kiswahili ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, jina Pauʹlos, linalotokana na neno la Kilatini Paulus ambalo linamaanisha “Mdogo,” limetumiwa mara 169 kumrejelea Paulo na mara moja kumrejelea liwali wa Kipro aliyeitwa Sergio Paulo.—Mdo 13:7.
DESEMBA 17-23
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATENDO 12-14
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mdo 16:37
sisi ni Waroma: Yaani, raia wa Roma. Inaonekana kwamba Paulo na huenda Sila pia walikuwa raia wa Roma. Sheria ya Roma ilisema kwamba raia alistahili kupewa nafasi ya kujitetea mahakamani na hakupaswa kuadhibiwa mbele ya watu kabla ya kuhukumiwa. Uraia wa Roma ulimwezesha mtu kupata haki na mapendeleo fulani popote alipoenda kwenye milki hiyo. Raia wa Roma alikuwa chini ya sheria za Roma, si sheria za majiji ya mikoa. Aliposhtakiwa, angeweza kukubali kushughulikiwa na sheria za eneo lake; lakini bado angedumisha haki ya kusikilizwa na mahakimu Waroma. Aliposhtakiwa kwa kosa linalostahili adhabu ya kifo, alikuwa na haki ya kukata rufaa kwa maliki. Mtume Paulo alihubiri katika maeneo mengi kotekote katika Milki ya Roma. Alitumia haki yake akiwa raia wa Roma mara tatu katika Biblia. Mara ya kwanza ni hapa katika jiji la Filipi alipowaambia mahakimu wa Filipi kwamba wamekiuka haki zake kwa kumpiga.—Ili uone mara hizo nyingine mbili, tazama habari za utafiti—Mdo 22:25; 25:11.
DESEMBA 24-30
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATENDO 17-18
“Mwige Mtume Paulo Unapohubiri na Kufundisha”
nwtsty habari za utafiti—Mdo 17:2, 3
akajadiliana: Paulo hakuwatangazia habari njema tu. Alifafanua na kutoa uthibitisho akitumia Maandiko, yaani, Maandiko ya Kiebrania yaliyoongozwa na roho. Hakusoma tu Maandiko; alijadiliana nao, na alibadili hoja alizotoa ili ziwafae wasikilizaji wake. Kitenzi cha Kigiriki di·a·leʹgo·mai kinafafanuliwa kuwa “kubadilishana mawazo; maongezi; kuzungumza.” Kinatokeza wazo la kuchangamana na watu. Neno hilo la Kigiriki linatumiwa pia katika Mdo 17:17; 18:4, 19; 19:8, 9; 20:7, 9.
kuthibitisha kwa marejeo: Neno hilo la Kigiriki linamaanisha “kuweka kando ya.” Hilo huenda likamaanisha kwamba Paulo alilinganisha kwa uangalifu unabii katika Maandiko ya Kiebrania na matukio katika maisha ya Yesu, na kuonyesha jinsi Yesu alivyotimiza unabii huo.
nwtsty habari za utafiti—Mdo 17:17
sokoni: Soko (Kigiriki, a·go·raʹ) la Athene lilikuwa Kaskazini Magharibi ya Akropoli, na lilikuwa na ukubwa wa ekari 12 hivi. Mambo mengi zaidi yalifanywa kwenye soko hilo mbali na kuuza na kununua. Lilikuwa kitovu cha kiuchumi, kisiasa, na kitamaduni cha jiji hilo. Waathene walifurahia kukutana hapo ili kujadili masuala mbalimbali ya kitaalamu.
nwtsty habari za utafiti—Mdo 17:22, 23
Kwa Mungu Asiyejulikana: Maneno ya Kigiriki A·gnoʹstoi the·oiʹ yalikuwa sehemu ya maneno yaliyokuwa kwenye madhabahu fulani huko Athene. Waathene walionyesha kwamba waliogopa miungu kwa kujenga mahekalu na madhabahu mengi, hata walitengeneza madhabahu kwa ajili ya miungu isiyo halisi kama vile, Umashuhuri, Kiasi, Nishati, Ushawishi, na Huruma. Labda wakiogopa kwamba watakosa kumtaja mungu fulani kisha awakasirikie, waliweka wakfu madhabahu kwa “Mungu Asiyejulikana.” Kupitia madhabahu hiyo, watu walikubali kwamba kuna Mungu ambaye hawamjui. Kwa ustadi, Paulo alitumia madhabahu hiyo kuwa msingi wa mahubiri yake kuwajulisha kumhusu Mungu—yule Mungu wa kweli—ambaye hawakuwa wamemfahamu kufikia wakati huo.
nwtsty habari za utafiti—Mdo 18:21
Yehova akipenda: Maneno hayo yanakazia uhitaji wa kutilia maanani mapenzi ya Mungu tunapofanya au kupanga kufanya chochote. Mtume Paulo alitumia kanuni hiyo sana. (1Ko 4:19; 16:7; Ebr 6:3) Mwanafunzi Yakobo pia aliwatia moyo wasomaji wake waseme: “Yehova akipenda, tutaishi na kufanya hili au lile.” (Yak 4:15) Maneno hayo hayapaswi kurudiwa-rudiwa ovyoovyo; yeyote anayesema kwa unyoofu “Yehova akipenda” anapaswa kujaribu kutenda kulingana na mapenzi ya Yehova. Si lazima maneno hayo yatamkwe, mara nyingi yanasemwa moyoni.—Tazama habari za utafiti—Mdo 21:14; 1Ko 4:19; Yak 4:15 na Nyongeza C.