Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • mwbr18 Novemba kur. 1-4
  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha
  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha—2018
  • Vichwa vidogo
  • NOVEMBA 5-11
  • NOVEMBA 12-18
  • NOVEMBA 19-25
Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha—2018
mwbr18 Novemba kur. 1-4

Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha

NOVEMBA 5-11

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOHANA 20-21

“Je, Unanipenda Kuliko Hawa?”

nwtsty habari za utafiti—Yoh 21:15, 17

Yesu akamuuliza Simoni Petro: Mazungumzo haya kati ya Yesu na Petro yalifanyika siku chache baada ya Petro kumkana Yesu mara tatu. Yesu alimuuliza Petro maswali matatu ya kutaka Petro aeleze hisia zake kumhusu kwa unyoofu mpaka “Petro akahuzunika.” (Yoh 21:17) Simulizi la Yohana lililorekodiwa kwenye Yoh 21:15-17 linatumia vitenzi viwili vya Kigiriki: a·ga·paʹo na phi·leʹo, ambavyo vyote viwili vimetafsiriwa kuwa upendo katika Kiswahili. Yesu alimuuliza Petro hivi mara tatu: “Je, unanipenda?” Na mara tatu Petro alijibu kwamba ‘anampenda.’ Mara zote Petro alimhakikishia upendo wake, na Yesu alikazia kwamba upendo ulipaswa kumchochea Petro kulisha na “kuchunga” wanafunzi wa Yesu kiroho, ambao hapa Yesu anawarejelea kama wanakondoo, au “kondoo wadogo.” (Yoh 21:16, 17; 1Pe 5:1-3) Yesu alimpa Petro nafasi ya kuthibitisha upendo wake mara tatu, kisha akampa wajibu wa kutunza kondoo wake. Kwa njia hiyo, Yesu alimthibitishia Petro kwamba alikuwa amemsamehe kwa kumkana mara tatu.

je, unanipenda kuliko hawa?: Kisarufi, maneno, “kuliko hawa” yanaweza kueleweka kwa njia zaidi ya moja. Baadhi ya wasomi wanapendekeza maana kama vile “je, unanipenda kuliko unavyowapenda wanafunzi hawa wengine?” au “je, unanipenda kuliko wanavyonipenda hawa wanafunzi wengine?” Hata hivyo, maana inayofaa zaidi ni “je, unanipenda kuliko vitu hivi?” yaani, samaki waliokuwa wamewavua au vitu mambo yanayohusiana na biashara ya uvuvi. Kwa hiyo, wazo kuu katika mstari linaonekana kuwa: ‘Je, unanipenda kuliko vitu vya kimwili au kufuatia vitu vya kimwili? Ikiwa ndivyo, lisha wanakondoo wangu.’ Swali hilo linafaa unapofikiria historia ya Petro. Ingawa Petro alikuwa mmoja kati ya wanafunzi wa kwanza wa Yesu (Yoh 1:35-42), mwanzoni hakumfuata Yesu kwa kuendelea. Badala yake, alirudia kazi yake ya uvuvi. Miezi kadhaa baadaye, Yesu alimwita Petro kutoka kwenye biashara hiyo muhimu ili awe ‘mvuvi wa watu.’ (Mt 4:18-20; Lu 5:1-11) Kwa mara nyingine tena, muda mfupi baada ya Yesu kufa, Petro alisema kwamba anaenda kuvua samaki, na mitume wengine walijiunga naye. (Yoh 21:2, 3) Kwa hiyo, inaonekana kwamba Yesu alikuwa akikazia kwa Petro kwamba kuna uhitaji wa kufanya uamuzi wa kukata maneno: Je, angetanguliza kazi yake ya kimwili ya biashara ya uvuvi, ambayo iliwakilishwa na rundo la samaki waliokuwa mbele yake, au angetanguliza kazi ya kiroho ya kulisha wanakondoo wa Yesu au wafuasi wake?—Yoh 21:4-8.

mara ya tatu: Petro alikuwa amemkana Bwana wake mara tatu; sasa Yesu anampa Petro nafasi ya kuthibitisha hisia zake mara tatu. Petro alipofanya hivyo, Yesu alimwambia aonyeshe upendo huo kwa kutanguliza utumishi mtakatifu badala ya vitu vingine vyote. Akishirikiana na ndugu wengine wanaotegemeka, Petro angelisha, kuimarisha, na kuchunga kundi la wafuasi waaminifu wa Kristo. Ingawa walikuwa watiwa-mafuta bado walihitaji kulishwa kiroho.—Lu 22:32.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Yoh 20:17

Acha kuning’ang’ania: Kitenzi cha Kigiriki haʹpto·mai kinaweza kumaanisha “kugusa” au “kung’ang’ania; kuning’inia.” Baadhi ya watafsiri walitafsiri maneno ya Yesu kuwa: “Usiniguse.” Hata hivyo, Yesu hakuwa akikataa kuguswa na Maria Magdalene, kwa kuwa, baada ya kufufuliwa hakuwazuia wanawake waliomwona ‘kumshika miguu.’ (Mt 28:9) Inaonekana Maria Magdalene alihofia kwamba Yesu alikuwa karibu kwenda mbinguni. Akichochewa na tamaa kubwa ya kuendelea kubaki na Bwana wake, alimshikilia Yesu na hakutaka amwache. Ili kumhakikishia kwamba bado hakuwa akiondoka, Yesu alimwagiza Maria aache kumng’ang’ania na badala yake aende kwa wanafunzi wake na kuwatangazia habari kuhusu ufufuo wake.

nwtsty habari za utafiti—Yoh 20:28

Bwana wangu na Mungu wangu!: Tnn., “Bwana wangu na Mungu [ho the·osʹ] wangu!” Baadhi ya wasomi wanaona maneno hayo kuwa mazungumzo ya mshangao yaliyoelekezwa kwa Yesu lakini kihalisi yalielekezwa kwa Mungu, Baba yake. Wengine wanadai kwamba Kigiriki cha awali kinataka maneno hayo yaonekane yalikuwa yakielekezwa kwa Yesu. Hata ikiwa hivyo, kusudi la maneno hayo “Bwana wangu na Mungu wangu” linaeleweka vizuri mtu anapozingatia muktadha wa Maandiko yote yaliyoongozwa na roho. Kwa kuwa rekodi zinaonyesha kwamba mwanzoni tayari Yesu alikuwa amewatumia wanafunzi wake ujumbe huu, “Ninapanda kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu na kwa Mungu wangu na Mungu wenu,” Tomasi hakuwa na sababu ya kuamini kwamba Yesu alikuwa Mungu mweza yote. (Ona habari za utafiti—Yoh 20:17.) Tomasi alikuwa amemsikia Yesu akisali kwa “Baba” yake, akimwita “Mungu wa pekee wa kweli.” (Yoh 17:1-3) Kwa hiyo, huenda Tomasi alimwita Yesu “Mungu wangu” kwa sababu zifuatazo: Alimwona Yesu kuwa “mungu” bali si Mungu mweza yote. (Ona habari za utafiti—Yoh 1:1.) Au inawezekana alikuwa akimtambulisha Yesu katika njia inayofanana na ile ambayo watumishi wa Mungu walitumia kuwatambulisha malaika waliokuwa wametumwa na Yehova, kama ilivyorekodiwa kwenye Maandiko ya Kiebrania. Tomasi aliyajua masimulizi yanayohusu watu, au wakati mwingine waandikaji wa masimulizi ya Biblia, walioitikia au kuzungumza kumhusu malaika kana kwamba alikuwa Yehova Mungu. (Linganisha na Mwa 16:7-11, 13; 18:1-5, 22-33; 32:24-30; Amu 6:11-15; 13:20-22.) Kwa hiyo, inawezekana Tomasi alimwita Yesu “Mungu wangu” katika maana hii, alimtambua Yesu kuwa mwakilishi na msemaji wa Mungu wa kweli.

Wengine wanadai kwamba kutumiwa kwa kibainishi-wazi cha Kigiriki kabla ya maneno “bwana” na “mungu” kunaonyesha kwamba maneno hayo yanarejelea Mungu mweza yote. Hata hivyo, katika muktadha huu kutumiwa kwa kibainishi hicho kunaweza tu kuwakilisha sarufi ya Kigiriki. Visa ambavyo nomino ya kiima yenye kibainishi-wazi inatumika katika Kigiriki kuonyesha kauli ya msemaji vinaweza kuonyeshwa katika tafsiri ya neno kwa neno ya maandiko kama vile Lu 12:32 (Tnn., “lile kundi dogo”) na Kol 3:18–4:1 (Tnn., “wale wake”; “wale waume”; “wale watoto”; “wale baba”; “wale watumwa”; “wale mabwana”). Vivyo hivyo, tafsiri ya neno kwa neno ya 1Pe 3:7 ingeweza kusomeka: “Wale waume.” Kwa hiyo, kibainishi katika mstari huu hakiwezi kutumiwa kuonyesha wazo ambalo Tomasi alikuwa nalo akilini aliposema maneno hayo.

NOVEMBA 12-18

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATENDO 1-3

“Roho Takatifu Yamiminwa Juu ya Kutaniko la Kikristo”

w86 12/1 29 ¶4-5, 7

Michango Inayoufurahisha Moyo

Katika siku ya kwanza ya kuzaliwa kwa kundi la Kikristo katika mwaka 33 W.K., ‘ushiriki wa mtu na mwenzake, kula vyakula, na kutoa sala’ ni mambo yaliyozoewa na waongofu wale 3,000 waliokuwa wamebatizwa karibuni. Kwa sababu gani nzuri? Ili kufanya iwezekane kuikaza imani yao changa ‘kwa kuwa wakidumu katika fundisho la mitume.’—Matendo 2:41, 42.

Wayahudi na wageni waliobadilika kufuata dini ya Wayahudi walikuwa wamekuja Yerusalemu wakipanga kukaa kwa kipindi cha Sikukuu ya Pentekoste tu. Lakini wale ambao walipata kuwa Wakristo walitamani kubaki kwa muda mrefu zaidi wajifunze mengi zaidi ili kuitia nguvu imani yao mpya. Jambo hilo lilitokeza tatizo la dharura la chakula na mahali pa kulala. Wengine wa watu hao wenye kuzuru hawakuwa na pesa za kuwatosha, hali wengine walikuwa na ziada. Kwa hiyo mchango wa muda ulifanywa na wenye uhitaji wakagawiwa vitu vya kimwili.—Matendo 2:43-47.

Kuuza shamba na majengo na kugawana vitu vyote hivyo na wengine kulikuwa jambo la mtu mwenyewe kujitolea. Hakuna mtu aliyeshurutishwa kuuza wala kutoa upaji; wala hiyo haikuwa njia ya kutia watu moyo wawe maskini. Wazo linaloonyeshwa si kwamba washiriki walio matajiri zaidi waliuza uwanja wao wote na hivyo wakawa maskini. Bali, kwa sababu ya kuhurumia waamini wenzao chini ya hali zilizokuwako wakati huo, wao waliuza uwanja na kuchanga pesa zote zilizopatikana ili waandae kilichohitajiwa kwa kusudi la kusogeza mbele faida za Ufalme.—Linganisha 2 Wakorintho 8:12-15.

Kutafuta Hazina za Kiroho

it-2 61 ¶1

Yesu Kristo

“Wakili Mkuu wa uzima.” Ili kuonyesha fadhili zisizostahiliwa za Baba yake, Yesu Kristo alitoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uwe dhabihu. Hilo liliwezesha kuwe na muungano kati ya Kristo na wafuasi wake waliochaguliwa kutawala naye kule mbinguni na pia likawezesha kuwe na mpango kwa ajili ya wale watakaokuwa hapa duniani wakiwa raia wa utawala wake wa Ufalme. (Mt 6:10; Yoh 3:16; Efe 1:7; Ebr 2:5; ona FIDIA.) Hivyo, akawa “Wakili Mkuu wa uzima” [“Mkuu wa uzima,” UV] kwa wanadamu wote. (Mdo 3:15) Neno la Kigiriki lililotumiwa hapa kihalisi linamaanisha “kiongozi mkuu,” kama lilivyotumiwa kumhusu Musa (Mdo 7:27, 35) akiwa “mtawala” katika Israeli.

BORESHA HUDUMA YAKO

it-1 p. 129

Mtume

Ni nani aliyechukua nafasi ya Yuda Iskariote na kuwa mtume wa 12?

Mitume 11 tu ndio waliobaki kwa sababu Yuda Iskariote aliasi na kufa akiwa si mwaminifu, na kwa siku 40 tangu Yesu afufuliwe hadi alipopaa kwenda mbinguni hakumchagua mwanafunzi yeyote achukue nafasi ya Yuda. Muda fulani kati ya siku kumi tangu Yesu apae kwenda mbinguni na siku ya Pentekoste ilionekana kwamba kulikuwa na umuhimu wa kuchagua mtu mwingine ili achukue nafasi ya Yuda, si kwa sababu alikufa, bali ni kwa sababu ya usaliti mbaya, kama Maandiko yaliyonukuliwa Petro yalivyoonyesha. (Mdo 1:15-22; Zb 69:25; 109:8; linganisha na Ufu 3:11) Tofauti na huyo, mtume mwaminifu Yakobo alipokufa, hakuna rekodi yoyote inayoonyesha kwamba walihangaika kuchagua mtu mwingine ili achukue nafasi yake akiwa mtume.—Mdo 12:2.

Maelezo ya Petro yanathibitisha kwamba mtu yeyote aliyefikiriwa kuchukua nafasi ya mtume wa Yesu Kristo alipaswa kuwa na sifa zifuatazo; alipaswa kuwa mtu aliyemfahamu Yesu, kushuhudia kazi zake, miujiza yake na hasa ufufuo wake. Kulingana na jambo hilo inaonekana kwamba baada ya muda isingewezekana kuchukua nafasi ya mtume, labda ikiwa Mungu angefanya mpango fulani ili kumstahilisha mtu aliyechaguliwa. Hata hivyo, wakati fulani kabla ya Pentekoste, kulikuwa na wanaume fulani waliofikia viwango hivyo, na wanaume wawili kati yao walifaa zaidi kuchukua nafasi ya Yuda aliyekosa kuwa mwaminifu. Bila shaka wakiwa na andiko la Methali 16:33 akilini, walipiga kura, na Mathia alichaguliwa na hatimaye “akahesabiwa pamoja na wale mitume 11.” (Mdo 1:23-26) Kwa hiyo, alikuwa miongoni mwa wale “kumi na wawili” ambao walisuluhisha tatizo lililohusu wanafunzi waliozungumza Kigiriki (Mdo 6:1, 2), na Paulo alimrejelea kati ya wale “kumi na wawili” alipokuwa akimzungumzia Yesu aliyefufuliwa alipowatokea kama inavyoelezwa kwenye 1 Wakorintho 15:4-8. Hivyo, Pentekoste ilipofika, kulikuwa na mitume 12 ambao walikuwa msingi wa Israeli la kiroho ambalo liliundwa baadaye.

NOVEMBA 19-25

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATENDO 4-5

“Waliendelea Kutangaza Neno la Mungu kwa Ujasiri”

it-1 128 ¶3

Mtume

Utendaji Katika Kutaniko la Kikristo. Mitume waliimarishwa sana walipomiminiwa roho ya Mungu wakati wa Pentekoste. Sura tano za kwanza za kitabu cha Matendo ya Mitume zinaonyesha wazi ujasiri mkubwa ambao mitume walikuwa nao wa kutangaza habari njema na kuhusu ufufuo wa Yesu licha ya kufungwa gerezani, kupigwa, na kutishwa kuuawa na watawala wao. Katika kipindi kilichofuata Pentekoste, uongozi wa mitume, chini ya nguvu za roho takatifu, ulifanya kuwe ongezeko lenye kustaajabisha katika kutaniko la Kikristo. (Mdo 2:41; 4:4) Mwanzoni, huduma yao ilielekezwa hasa Yerusalemu, kisha ikapanuka kufikia Samaria, na baadaye, katika ulimwengu wote uliojulikana wakati huo.—Mdo 5:42; 6:7; 8:5-17, 25; 1:8.

Kutafuta Hazina za Kiroho

it-1 514 ¶4

Jiwe la Pembeni

Zaburi 118:22 inaeleza kwamba jiwe lililokataliwa na wajenzi lingekuwa “jiwe kuu la pembeni” (Kiebrania, roʼsh pin·nahʹ). Yesu alinukuu na kuonyesha kwamba unabii huo ulimhusu yeye mwenyewe akiwa “jiwe kuu la pembeni” (Kigiriki, ke·pha·leʹ go·niʹas, kichwa cha pembeni). (Mt 21:42; Mk 12:10, 11; Lu 20:17) Kama jiwe la juu kabisa katika jengo linavyoonekana waziwazi, ndivyo Yesu Kristo alivyo jiwe tukufu katika kutaniko la Kikristo la watiwa-mafuta, ambalo linafananishwa na hekalu la kiroho. Petro pia alionyesha Zaburi 118:22 inamhusu Kristo, kuonyesha kwamba Kristo alikuwa ndiye “jiwe” lililokataliwa na wanadamu lakini lililochaguliwa na Mungu kuwa “jiwe kuu la pembeni.”—Mdo 4:8-12; ona pia 1Pe 2:4-7.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki