Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • mwbr18 Oktoba kur. 1-6
  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha
  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha—2018
  • Vichwa vidogo
  • OKTOBA 1-7
  • OKTOBA 8-14
  • OKTOBA 15-21
  • OKTOBA 22-28
  • OKTOBA 29–NOVEMBA 4
Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha—2018
mwbr18 Oktoba kur. 1-6

Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha

OKTOBA 1-7

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOHANA 9-10

nwtsty picha

Zizi la kondoo

Zizi la kondoo lilikuwa uzio uliotengenezwa ili kuwalinda kondoo kutokana na wezi na wanyama wawindaji. Wachungaji waliingiza makundi yao ndani ya zizi wakati wa usiku ili wawe salama. Katika nyakati za Biblia, mazizi ya kondoo hayakuwa na paa na yalikuwa na miundo na ukubwa mbalimbali, mara nyingi yalijengwa kwa mawe na yalikuwa na mlango mmoja tu. (Hes 32:16; 1Sa 24:3; Sef 2:6) Yohana anazungumza kuhusu kuingia kwenye zizi la kondoo “kupitia mlango,” ambao ulilindwa na “mlinzi wa mlango.” (Yoh 10:1, 3) Katika zizi linalotumiwa kuhifadhi kondoo wa wachungaji mbalimbali, makundi mengi ya kondoo yalilala pamoja wakati wa usiku, na mlinzi wa mlango aliendelea kukaa macho ili kuwalinda. Wakati wa asubuhi, mlinzi wa mlango angefungua mlango kwa ajili ya wachungaji. Kila mchungaji angekusanya kundi lake kwa kuwaita kondoo nje, na kondoo wangeweza kutambua sauti ya mchungaji wao na kutoka nje. (Yoh 10:3-5) Yesu alirejelea zoea hilo ili kuonyesha jinsi anavyowatunza wanafunzi wake.—Yoh 10:7-14.

nwtsty habari za utafiti kwenye Yoh 10:16

nitawaleta: Au “kuwaongoza.” Kitenzi cha Kigiriki aʹgo kilichotumiwa hapa kinaweza kumaanisha “kuwaleta” au “kuwaongoza,” ikitegemea na muktadha. Hati moja ya zamani ya Kigiriki iliyoandikwa karibu mwaka wa 200 W.K. ilitumia neno la kigiriki (sy·naʹgo) linalofanana na kitenzi hiki ambalo mara nyingi hutafsiriwa “kukusanya.” Akiwa Mchungaji Mwema, Yesu anawakusanya, anawaongoza, anawalinda, na kuwalisha kondoo wa zizi hili (pia wanarejelewa kuwa “kundi dogo” kwenye Lu 12:32) na kondoo wengine. Hawa watakuwa kundi moja wakiongozwa na mchungaji mmoja. Maneno hayo yanakazia umoja ambao wafuasi wa Yesu wangefurahia.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti kwenye Yoh 9:38

akamsujudia: Au “akamwinamia; akaanguka kifudifudi; akatoa heshima.” Kitenzi cha Kigiriki pro·sky·neʹo kinapotumiwa kurejelea ibada kwa mungu, kinatafsiriwa “kuabudu.” (Mt 4:10; Lu 4:8) Hata hivyo, katika muktadha huu, mwanamume aliyeponywa, ambaye alikuwa kipofu tangu kuzaliwa, alimtambua Yesu kuwa mwakilishi wa Mungu na akamsujudia. Hakumwona kuwa Mungu lakini alimwona kama ilivyotabiriwa kuwa “Mwana wa binadamu,” Masihi aliye na mamlaka kutoka kwa Mungu. (Yoh 9:35) Alipomsujudia Yesu, kwa wazi mwanamume huyo alifanya kama watu walioelezwa kwenye Maandiko ya Kiebrania walivyokuwa wakifanya. Walianguka kifudifudi walipokutana na manabii, wafalme, au wawakilishi wengine wa Mungu. (1Sa 25:23, 24; 2Sa 14:4-7; 1Fa 1:16; 2Fa 4:36, 37) Katika visa vingi, watu walipomsujudia Yesu walionyesha shukrani zao kwa ufunuo kutoka kwa Mungu au kushuhudia baraka kutoka kwa Mungu.—Ona habari za utafiti kwenye Mt 2:2; 8:2; 14:33; 15:25.

nwtsty habari za utafiti kwenye Yoh 10:22

Sherehe ya Wakfu: Jina la Kiebrania la sherehe hii ni Hanuka (chanuk·kahʹ), linalomaanisha “kuzinduliwa; kuwekwa wakfu.” Ilifanywa kwa siku nane, kuanzia siku ya 25 ya mwezi wa Kislevu, karibu na majira ya baridi kali, (ona habari ya utafiti kuhusu majira ya baridi kali katika sura hii na nyongeza B15) ili kukumbuka kuwekwa wakfu tena kwa hekalu la Yerusalemu kulikofanyika mwaka wa 165 K.W.K. Mfalme wa Siria Antioko wa Nne Epifane alikuwa amemdharau Yehova, Mungu wa Wayahudi, kwa kunajisi hekalu Lake. Kwa mfano, alijenga madhabahu juu ya ile madhabahu kuu, ambapo matoleo ya kila siku ya dhabihu yalikuwa yakitolewa. Katika mwezi wa Kislevu siku ya 25, 168 K.W.K, ili kulinajisi kabisa hekalu la Yehova, Antioko alitoa dhabihu ya nguruwe kwenye madhabahu na alimwaga mchuzi wa nguruwe katika kila sehemu ya hekalu. Alichoma malango ya hekalu, akabomoa chumba cha makuhani, na akachukua madhabahu ya dhahabu, meza ya mikate ya wonyesho, na kinara cha taa cha dhahabu. Kisha akaliweka wakfu hekalu la Yehova kwa mungu wa kipagani anayeitwa Zeu wa Olympus. Miaka miwili baadaye, Yudasi Makabayo aliliteka tena jiji na hekalu. Baada ya hekalu kutakaswa, kuwekwa wakfu tena kulifanywa siku ya 25 ya mwezi wa Kislevu, mwaka wa 165 K.W.K., miaka mitatu kamili tangu Antioko alipokuwa ametoa dhabihu yenye kuchukiza juu ya madhabahu kwa Zeu. Dhabihu za kila siku zilianza tena kutolewa kwa Yehova. Hakuna maelezo hususa katika Maandiko yanayoonyesha kwamba Yehova alimpa ushindi Yudasi Makabayo na kumwongoza arudishe hekalu. Hata hivyo, Yehova alikuwa ametumia wanaume wa mataifa ya kigeni, kama vile, Koreshi wa Uajemi, kutimiza makusudi fulani kuhusiana na ibada Yake. (Isa 45:1) Hivyo, inapatana na akili kufikia mkataa kwamba Yehova angeweza kumtumia mwanamume kutoka kati ya watu wake waliowekwa wakfu ili atimize kusudi Lake. Maandiko yanaonyesha kwamba hekalu lilipaswa kuwepo na kuendelea kufanya kazi ili unabii kuhusu Masihi, huduma yake, na dhabihu aliyotoa upate kutimizwa. Pia, dhabihu za Walawi zilipaswa kuendelea kutolewa mpaka wakati ambapo Masihi angetoa dhabihu kubwa zaidi, uhai wake kwa ajili ya wanadamu. (Da 9:27; Yoh 2:17; Ebr 9:11-14) Wafuasi wa Kristo hawakuagizwa waadhimishe Sherehe ya Wakfu. (Kol 2:16, 17) Hata hivyo, hakuna rekodi yoyote inayoonyesha kwamba Yesu au wanafunzi wake walishutumu kusherehekea sherehe hiyo.

OKTOBA 8-14

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOHANA 11-12

“Iga Huruma ya Yesu”

nwtsty habari za utafiti kwenye Yoh 11:24, 25

Ninajua atafufuka: Martha alifikiri Yesu alikuwa akizungumza kuhusu ufufuo wa wakati ujao, katika siku ya mwisho. (Ona habari ya utafiti kwenye Yoh 6:39.) Imani yake kuhusiana na fundisho hilo inapendeza sana. Ingawa hilo ni fundisho linaloelezwa waziwazi katika Maandiko yaliyoongozwa na roho, viongozi wa kidini wa siku zake, walioitwa Masadukayo, walipinga kwamba kutakuwa na ufufuo. (Da 12:13; Mk 12:18) Kwa upande mwingine, Mafarisayo waliamini kutokufa kwa nafsi. Hata hivyo, Martha alijua kwamba Yesu alifundisha kuhusu tumaini la ufufuo na hata alifanya miujiza ya ufufuo, hata ingawa hakuwa amewafufua watu ambao walikuwa wamekufa kwa muda mrefu kama Lazaro.

Mimi ndiye ufufuo na uzima: Kifo cha Yesu na ufufuo wake vilifungua njia kwa ajili ya wafu kurudishwa kwenye uhai. Baada ya Yesu kufufuliwa, Yehova alimpa nguvu za kuwafufua wafu na pia kuwawezesha wapate uzima wa milele. (Ona habari za utafiti kwenye Yoh 5:26.) Katika Ufu 1:18, Yesu anajiita “aliye hai,” ambaye ana “funguo za kifo na za Kaburi.” Kwa hiyo, Yesu ndiye tumaini kwa walio hai na wafu. Aliahidi kufungua makaburi na kuwapa uhai wafu, ili waende mbinguni wakatawale pamoja naye au waishi duniani wakitawaliwa na serikali yake ya mbinguni.—Yoh 5:28, 29; 2Pe 3:13.

nwtsty habari za utafiti kwenye Yoh 11:33-35

akilia: Au “kilio.” Neno la Kigiriki lililotafsiriwa kuwa “akilia” mara nyingi linarejelea kulia kwa sauti kubwa. Yesu alitumia kitenzi hichohicho alipokuwa akitabiri kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu.—Lu 19:41.

akaugua . . . na kutaabika: Kutumiwa kwa maneno haya mawili ya lugha ya awali kunafafanua hisia kali ambazo Yesu alikuwa nazo katika kisa hiki. Kitenzi cha Kigiriki kilichotafsiriwa “kuugua” (em·bri·maʹo·mai) kwa kawaida humaanisha hisia kali, lakini katika muktadha huu kinaonyesha kwamba hisia za Yesu ziliguswa sana kiasi cha kuugua. Neno la Kigiriki “kutaabika” (ta·rasʹso) kihalisi linarejelea kufadhaika. Kulingana na msomi mmoja, katika muktadha huu neno hilo linamaanisha “kujisababishia ghasia ndani yako; kuathiriwa na maumivu makali au huzuni.” Kitenzi hichohicho kilichotumiwa kwenye Yoh 13:21 kinafafanua Yesu alivyotenda alipofikiria kuhusu kusalitiwa na Yuda.—Ona habari za utafiti kwenye Yoh 11:35.

moyoni: Tnn., “rohoni.” Neno la Kigiriki pneuʹma linalotumiwa hapa linatuonyesha nguvu inayochochewa na moyo wa mfano wa mtu ambayo inasababisha aseme na kufanya mambo kwa njia fulani.—Ona Kamusi, “Roho.”

akatokwa na machozi: Neno linalotumiwa hapa (da·kryʹo) ni aina ya kitenzi cha nomino ya Kigiriki inayowakilisha neno “machozi” linalotumiwa katika maandiko mengine kama vile Lu 7: 38; Mdo 20:19, 31; Ebr 5:7; Ufu 7:17; 21:4. Mkazo unaelekezwa kwenye machozi yanayotoka wala si kilio kinachosikika. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kitenzi hiki cha Kigiriki kilitumiwa tu katika mstari huu, na ni tofauti na kile kilichotumiwa katika Yoh 11:33 (ona habari za utafiti) kuelezea kilio cha Maria na Wayahudi. Yesu alijua kwamba angemfufua Lazaro, lakini alihuzunika sana alipoona rafiki zake wapendwa wakiomboleza. Akichochewa na upendo na huruma kwa marafiki wake, alitokwa na machozi hadharani. Simulizi hilo linatufundisha kwamba Yesu anawahurumia wale wanaopoteza wapendwa wao kutokana na kifo kilichosabishwa na Adamu.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti kwenye Yoh 11:49

kuhani mkuu: Taifa la Israeli lilipokuwa likijitawala lenyewe, kuhani mkuu angedumisha cheo chake kwa muda wote aliokuwa hai. (Hes 35:25) Hata hivyo, wakati Waroma walipotawala Israeli, watawala waliochaguliwa na Roma walikuwa na mamlaka ya kumweka na kumwondoa kuhani mkuu. (Ona Kamusi, “Kuhani Mkuu.”) Kayafa, aliyewekwa na Waroma, alikuwa na ujuzi wa kushughulika na watu ambaye alidumu katika cheo hicho kwa muda mrefu kuliko makuhani wengine waliotangulia. Aliwekwa kuwa kuhani mkuu mwaka wa 18 W.K. na aliendelea katika cheo hicho mpaka mwaka wa 36 W.K. Kwa kusema kwamba Kayafa alikuwa kuhani mkuu mwaka huo, yaani, mwaka wa 33 W.K., Yohana alimaanisha waziwazi kwamba kipindi cha Kayafa akiwa kuhani mkuu kilitia ndani mwaka muhimu sana ambao Yesu aliuawa.—Ona Nyongeza B12 kuona eneo ambalo huenda kulikuwa na nyumba ya Kayafa.

nwtsty habari za utafiti—Yoh 12:42

watawala: Inaonekana kwamba neno la Kigiriki “watawala” linalotumiwa hapa linarejelea washiriki wa mahakama kuu ya Kiyahudi, Sanhedrini. Neno hilo linatumiwa katika Yoh 3:1 kumrejelea Nikodemo, mshiriki wa mahakama hiyo.—Ona habari za utafiti kwenye Yoh 3:1.

kufukuzwa katika sinagogi: Au “kutengwa; kupigwa marufuku asishiriki katika sinagogi.” Kielezi cha Kigiriki a·po·sy·naʹgo·gos kinatumiwa tu hapa na katika Yoh 12:42 na 16:2. Mtu aliyefukuzwa angeepukwa na kudharauliwa na kila mtu kama mtu asiyetakiwa katika jamii. Kutengwa kwa njia hiyo na Wayahudi wenzake kungekuwa na matokeo mabaya ya kiuchumi kwa familia. Masinagogi, ambayo hasa yalitumiwa kwa ajili ya kutoa elimu, kwa kiwango fulani pia yalikuwa yakitumiwa kama mahamaka ambazo zilikuwa na mamlaka ya kutoa hukumu ya kupigwa mijeledi na kutengwa.—Ona habari za utafiti—Mt 10:17.

OKTOBA 15-21

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOHANA 13-14

nwtsty habari za utafiti—Yoh 13:5

kuiosha miguu ya wanafunzi: Katika Israeli la kale, mara nyingi watu walivaa viatu vya wazi. Vilikuwa na soli na mikanda ambayo ilifungwa kwenye kifundo cha mguu, hivyo miguu ya msafiri ilichafuka alipotembea kwenye barabara na mashamba yenye vumbi au matope. Kwa hiyo, ilikuwa ni kawaida kwa mtu kuvua viatu vyake alipoingia ndani ya nyumba, na mwenye nyumba mkarimu angehakikisha kwamba wageni wake wanaoshwa miguu. Biblia ina marejeo mengi sana yanayoonyesha desturi hii. (Mwa 18:4, 5; 24:32; 1Sa 25:41; Lu 7:37, 38, 44) Yesu alipoosha miguu ya wanafunzi wake, alitumia desturi hii kuwafundisha somo la unyenyekevu na kutumikiana.

nwtsty habari za utafiti—Yoh 13:12-14

mnapaswa: Au “mnawajibu wa.” Kitenzi cha Kigiriki kilichotumiwa hapa mara nyingi kilitumiwa katika mambo ya kiuchumi, kihalisi kilimaanisha “kudaiwa na mtu fulani; kuwa na deni.” (Mt 18:28, 30, 34; Lu 16:5, 7) Katika mstari huu na katika muktadha mwingine, neno hili lina maana pana ya kuwajibika au kuwa na wajibu wa kufanya jambo fulani.—1Yo 3:16; 4:11; 3Yo 8.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Yoh 14:6

Mimi ndiye njia na kweli na uzima: Yesu ndiye njia kwa sababu ni kupitia kwake tu tunaweza kumfikia Mungu kwa sala. Pia, yeye ndiye “njia” ya wanadamu kupatanishwa na Mungu. (Yoh 16:23; Ro 5:8) Yesu ndiye kweli kwa sababu alizungumza na kuishi kupatana na kweli. Pia, alitimiza unabii mwingi unaoonyesha daraka lake kuu katika kutimiza kusudi la Mungu. (Yoh 1:14; Ufu 19:10) Unabii huo wote umekuwa “‘ndiyo’ [au ulitimizwa] kupitia yeye.” (2Ko 1:20) Yesu ndiye uzima kwa sababu kupitia fidia, alifanya wanadamu waweze kupata “uzima ulio wa kweli,” yaani, “uzima wa milele.” (1Ti 6:12, 19; Efe 1:7; 1Yo 1:7) Pia, atathibitika kuwa “uzima” kwa mamilioni ya watu watakaofufuliwa wakiwa na tarajio la kuishi katika Paradiso milele.—Yoh 5:28, 29.

nwtsty habari za utafiti—Yoh 14:12

kazi kubwa kuliko hizi: Yesu hakumaanisha kwamba miujiza ambayo wanafunzi wake wangefanya ingekuwa mikubwa kuliko ile aliyofanya. Badala yake, kwa unyenyekevu alitambua kwamba wangefanya kazi kubwa ya kuhubiri na kufundisha kuliko ile aliyofanya. Wafuasi wake wangehubiri eneo kubwa, wangewafikia watu wengi zaidi, na wangehubiri kwa muda mrefu kuliko alivyofanya. Maneno hayo ya Yesu yanaonyesha wazi kwamba alitarajia wafuasi wake waendeleze kazi yake.

OKTOBA 22-28

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOHANA 15-17

nwtsty habari za utafiti—Yoh 15:19

ulimwengu: Katika muktadha huu, neno la Kigiriki koʹsmos linarejelea ulimwengu wa wanadamu ambao ni jamii ya wanadamu wasio waadilifu waliojitenga na Mungu. Wanadamu hao hawatii ndani watumishi wa Mungu. Yohana ndiye mwandishi pekee wa Injili anayenukuu maneno ya Yesu aliposema wafuasi wake si sehemu ya ulimwengu au si mali ya ulimwengu. Wazo hilo linarudiwa mara mbili katika sala ya mwisho ya Yesu akiwa pamoja na mitume wake waaminifu.—Yoh 17:14, 16.

nwtsty habari za utafiti—Yoh 15:21

kwa ajili ya jina langu: Katika Biblia, wakati mwingine neno “jina” linawakilisha mtu mwenye jina, sifa yake, na kila kitu anachowakilisha. (Ona habari za utafiti—Mt 6:9.) Katika kisa cha jina la Yesu, linawakilisha mamlaka na cheo alichopewa na Baba yake. (Mt 28:18; Flp 2:9, 10; Ebr 1:3, 4) Hapa Yesu anafafanua kwa nini watu wa ulimwengu wangefanya mambo ya kuwapinga wafuasi wake: kwa sababu hawamjui Yule aliyemtuma. Kumjua Mungu kungewasaidia waelewe na kukubali kile kinachowakilishwa na jina la Yesu. (Mdo 4:12) Hilo lingetia ndani cheo cha Yesu akiwa Mtawala aliyechaguliwa na Mungu, Mfalme wa wafalme, ambaye kwake watu wote wanapaswa kumwinamia kwa heshima ili wapate uzima.—Yoh 17:3; Ufu 19:11-16; linganisha Zb 2:7-12.

it-1 516

Ujasiri

Wakristo wanahitaji ujasiri ili wasichafuliwe na mtazamo na mwenendo wa ulimwengu wenye uadui na Yehova Mungu na waendelee kuwa washikamanifu Kwake licha ya kukabiliana na chuki ya ulimwengu. Yesu Kristo aliwaambia wafuasi wake hivi: “Ulimwenguni mtapata dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yoh 16:33) Mwana wa Mungu hakufinyangwa na mtazamo wa ulimwengu bali aliushinda ulimwengu kwa kutouiga hata kidogo. Mfano bora wa Yesu Kristo akiwa mshindi na matokeo ya mwenendo wake usio na makosa unaweza kumpa mtu ujasiri anaohitaji ili kumwiga Yesu kwa kuendelea kujitenga na kutochafuliwa na ulimwengu.—Yoh 17:16.

utafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Yoh 17:21-23

kimoja: Au “katika muungano.” Yesu alisali kwamba wafuasi wake wa kweli wangekuwa kitu “kimoja” wakifanya kazi kwa umoja kwa ajili ya kutimiza kusudi lilelile, kama Yesu na Baba yake walivyo kitu “kimoja”, wakionyesha wanashirikiana na wana mawazo yanayofanana. (Yoh 17:22) Katika 1Ko 3:6-9, Paulo anafafanua aina hii ya umoja miongoni mwa wahudumu Wakristo wanaposhirikiana kufanya kazi na wanaposhirikiana pamoja na Mungu.—Ona 1Ko 3:8 na habari za utafiti—Yoh 10:30; 17:11.

wakamilishwe wawe kitu kimoja: Au “waunganishwe kikamili.” Katika mstari huu, Yesu anahusianisha muungano kamili na kupendwa na Baba. Jambo hili linapatana na Kol 3:14, linalosema: “Upendo . . . ni kifungo kikamilifu cha muungano.” Inaposema muungano huo ni mkamilifu haimaanishi kwamba tofauti zote za utu kama vile uwezo wa mtu binafsi, mazoea yake, na dhamiri yake zinaondolewa. Inamaanisha kwamba wafuasi wa Yesu wana umoja katika matendo, imani, na mafundisho.—Ro 15:5, 6; 1Ko 1:10; Efe 4:3; Flp 1:27.

nwtsty habari za utafiti—Yoh 17:24

msingi wa ulimwengu: Neno la Kigiriki “msingi” linarejelea “kuzaliwa” katika Ebr 11:11, ambapo neno “uzao” linatumiwa. Maneno “msingi wa ulimwengu” yanayotumiwa hapa, kwa wazi yanarejelea kuzaliwa kwa watoto wa Adamu na Hawa. Yesu anahusianisha “msingi wa ulimwengu” na Abeli, ambaye kwa wazi ndiye mwanadamu wa kwanza kukombolewa na ndiye wa kwanza ambaye jina lake “[limeandikwa] katika kitabu cha kukunjwa cha uzima tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.” (Lu 11:50, 51; Ufu 17:8) Maneno haya ambayo Yesu alisema katika sala aliyotoa kwa Baba yake yanathibitisha pia kwamba tangu zamani—kabla ya Adamu na Hawa kupata watoto—Mungu alimpenda Mwana wake mzaliwa pekee.

OKTOBA 29–NOVEMBA 4

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOHANA 18-19

nwtsty habari za utafiti—Yoh 18:37

nitoe ushahidi kuhusu: Kama yanavyotumiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa “kutoa ushahidi” (mar·ty·reʹo) na “ushahidi” (mar·ty·riʹa; marʹtys) yana maana pana. Maneno yote hayo yalitumiwa katika maana ya kutoa uthibitisho unaotegemea mambo ambayo mtu alijionea au kutokana na ujuzi wa kibinafsi, lakini pia yanaweza kutia ndani “kutangaza; kuthibitisha; kusifu.” Si kwamba tu Yesu alishuhudia na kutangaza kweli ambazo alisadiki bali pia aliishi kwa njia ambayo iliunga mkono kweli zilizotolewa katika neno la kinabii la Baba yake na ahadi zake. (2Ko 1:20) Habari hususa zilikuwa zimetabiriwa kuhusu kusudi la Mungu kuelekea Ufalme na Utawala wa Kimasihi. Maisha yote ya Yesu akiwa duniani, kutia ndani kifo chake cha kidhabihu, kulitimiza unabii wote uliotabiriwa kumhusu. Hilo linatia ndani vivuli, au matukio, yaliyo kwenye agano la Sheria. (Kol 2:16, 17; Ebr 10:1) Hivyo, kwa maneno na matendo, inaweza kusemwa kwamba Yesu ‘alitoa ushahidi kuhusu kweli.’

kweli: Yesu hakuwa akirejelea kweli kwa ujumla bali alikuwa akirejelea kweli kuhusu kusudi la Mungu. Jambo kuu katika kusudi la Mungu ni kwamba Yesu, “mwana wa Daudi,” angetumikia akiwa Kuhani Mkuu na Mfalme wa Ufalme wa Mungu. (Mt 1:1) Yesu alieleza kwamba sababu kuu ya kuja katika ulimwengu wa wanadamu, maisha yake duniani, na huduma yake ilikuwa kutangaza kweli kuhusu Ufalme huo. Malaika walitangaza ujumbe kama huo kabla Yesu hajazaliwa na wakati alipozaliwa katika Bethlehemu ya Yudea, jiji ambalo Daudi alizaliwa.—Lu 1:32, 33; 2:10-14.

nwtsty habari za utafiti—Yoh 18:38a

Kweli ni nini?: Inaonekana kwamba swali la Pilato linarejelea kweli kwa ujumla, si ile “kweli” ambayo Yesu alikuwa akizungumzia. (Yoh 18:37) Lingekuwa swali la unyoofu, bila shaka Yesu angelijibu. Lakini inawezekana Pilato aliuliza swali lisilohitaji jibu akiwa na mtazamo usiofaa au wa kutoamini, ni kama alikuwa akisema, “Kweli? Kweli ni nini? Hakuna kitu kama hicho!” Kwa kweli, Pilato hata hakusubiri jibu bali alitoka na kwenda nje kwa Wayahudi.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Yoh 19:31

siku hiyo ya Sabato ilikuwa kuu: Kwa kawaida Nisani 15, siku moja baada ya Pasaka, ilikuwa sabato, haidhuru iliangukia siku gani. (Law 23:5-7) Sabato hiyo ya pekee ilipoangukia siku ileile ya Sabato ya kawaida (siku ya saba ya Juma la Kiyahudi iliyoanza Ijumaa baada ya jua kutua hadi Jumamosi jua lilipotua), ingekuwa Sabato “kuu.” Sabato hiyo ilitanguliwa na siku ya kifo cha Yesu, ambacho kilitukia siku ya Ijumaa. Katika kipindi cha miaka kuanzia 29 W.K. hadi 35 W.K., mwaka pekee ambapo Nisani 14 iliangukia siku ya Ijumaa ilikuwa mwaka wa 33 W.K. Kwa hiyo, uthibitisho huu unatuhakikishia kwamba Nisani 14, 33 W.K., ndiyo siku ambayo Yesu alikufa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki