Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
JANUARI 6-12
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MWANZO 1-2
“Yehova Aumba Uhai Duniani”
it-1 527-528
Uumbaji
Mungu aliposema kwenye Siku ya Kwanza, “Kuwe na nuru,” mwangaza ulipenyeza kwenye mawingu, hata ingawa kufikia wakati huo chanzo cha mwangaza huo hakingeweza kuonekana kutokea duniani. Inaonekana kwamba jambo hilo lilitokea hatua kwa hatua, kama anavyosema mtafsiri J. W. Watts: “Na hatua kwa hatua kukawa na nuru.” (Mwa 1:3, A Distinctive Translation of Genesis) Mungu alitenganisha kati ya nuru na giza, akaita nuru Mchana na giza Usiku. Hilo linaonyesha kwamba dunia ilikuwa ikizunguka kwenye mhimili wake kuzunguka jua, hivi kwamba kungekuwa na vipindi vya nuru na giza katika vizio vya mashariki na magharibi.—Mwa 1:3, 4.
Siku ya Pili, Mungu alitokeza anga kwa kutenganisha “maji na maji.” Kiasi fulani cha maji kilibaki duniani, lakini kiasi kikubwa zaidi cha maji kikainuliwa juu ya uso wa dunia, na kati ya maji hayo kukawa na anga. Mungu aliita anga hilo Mbingu. Aliliita hivyo kwa kutegemea mahali lilipokuwa kuhusiana na dunia, kwa sababu haisemekeni kwamba maji yaliyoning’inia angani yalifunika nyota, sayari, na vitu vingine vilivyo katika mbingu.—Mwa 1:6-8; tazama ANGA.
Siku ya Tatu kupitia nguvu za Mungu za kimuujiza, maji yaliyo duniani yalikusanywa sehemu moja, kwa hiyo nchi kavu ikatokea, na Mungu akaiita Dunia. Vilevile katika siku hiyo, Mungu alitenda mwenyewe kwa kuweka uhai ndani ya atomu zilizo duniani, si kupitia mageuzi wala vitu havikujitokeza vyenyewe. Mungu alitokeza nyasi, majani, na miti ya matunda. Mimea iliyo katika makundi hayo matatu ilikuwa na uwezo wa kuzaa kulingana na “aina” zake.—Mwa 1:9-13.
it-1 528 ¶5-8
Uumbaji
Vilevile ni vizuri kutambua kwamba kitenzi cha Kiebrania ba·raʼʹ, kinachomaanisha “kuumba,” hakijatumiwa kwenye Mwanzo 1:16. Badala yake, kitenzi cha Kiebrania ʽa·sahʹ, kinachomaanisha “kufanyiza,” ndicho kimetumiwa. Kwa kuwa jua, mwezi, na nyota zinatiwa ndani ya neno “mbingu” kwenye Mwanzo 1:1, ziliumbwa muda mrefu kabla ya Siku ya Nne. Siku ya nne Mungu ‘alifanya’ vitu hivyo vilivyo mbinguni viwe na uhusiano mpya kuelekea uso wa dunia na anga lililo juu yake. Inaposema Mungu aliviweka “katika anga la mbingu ili kuangazia dunia,” hilo linaonyesha kwamba sasa vitu hivyo vingeweza kuonekana kutoka kwenye uso wa dunia, kana kwamba vilikuwa angani. Vilevile, vitu hivyo vinavyotokeza nuru vingekuwa “ishara ya kuonyesha majira na siku na miaka,” na hivyo baadaye vingemwongoza mwanadamu kwa njia mbalimbali.—Mwa 1:14.
Siku ya Tano, Mungu aliumba viumbe wenye nafsi ambao si binadamu. Mungu hakuumba kiumbe mmoja tu ambaye alikusudia apitie hatua za mageuzi na kutokeza viumbe wa aina nyingine, bali kupita nguvu za Mungu maelfu ya makundi ya viumbe walio hai yaliumbwa. Simulizi hilo linasema: “Mungu akaumba viumbe wakubwa wa baharini na viumbe wote walio hai waendao na waliojaa majini kulingana na aina zao na kila kiumbe mwenye mabawa anayeruka, kulingana na aina yake.” Mungu alifurahishwa na viumbe alioumba, akawabariki, na kuwaambia ‘wawe wengi,’ jambo ambalo lingewezekana, kwa sababu viumbe hao wa makundi mengi mbalimbali walikuwa wamepewa uwezo na Mungu wa kuzaana “kulingana na aina zao.”—Mwa 1:20-23.
Siku ya Sita “Mungu akaumba wanyama wa mwituni kulingana na aina zao na wanyama wa kufugwa kulingana na aina zao na wanyama wote wanaotambaa kulingana na aina zao,” na kazi hiyo ilikuwa nzuri, kama kazi za Mungu za uumbaji zilizotangulia.—Mwa 1:24, 25.
Kuelekea mwishoni mwa siku ya sita ya uumbaji, Mungu alitokeza kiumbe wa aina mpya kabisa, aliye bora kuliko wanyama, ingawa ni wa hali ya chini kuliko malaika. Alikuwa mwanamume, aliyeumbwa kulingana na mfano na sura ya Mungu. Ingawa andiko la Mwanzo 1:27 linasema kifupi kuhusu wanadamu, “mwanamume na mwanamke [Mungu] aliwaumba,” simulizi lingine kwenye Mwanzo 2:7-9 linaonyesha kwamba Mungu alimuumba mwanamume kutokana na mavumbi ya ardhi, kisha akapuliza kwenye mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, na mwanamume huyo akawa nafsi iliyo hai, ambaye aliandaliwa makao ya paradiso yaliyokuwa na chakula. Katika kisa hiki, Mungu alitumia vitu vilivyo duniani kuumba kisha, baada ya kumfanyiza mwanamume, akamuumba mwanamke akitumia ubavu mmoja wa Adamu. (Mwa 2:18-25) Baada ya mwanamke kuumbwa, sasa mwanamume alikuwa kamili akiwa kiumbe wa “aina yake.”—Mwa 5:1, 2.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 52
Yesu Kristo
Si Muumba-mwenza. Hata hivyo, kushiriki kwa huyo Mwana katika kazi za uumbaji, hakukumfanya awe Muumba-mwenza wa Baba yake. Nguvu za uumbaji zilitoka kwa Mungu kupitia roho takatifu, au nguvu ya utendaji yake. (Mwa 1:2; Zb 33:6) Na kwa kuwa Yehova ndiye Chanzo cha uhai wote, uumbaji wote ulio hai, unaoonekana na usioonekana, unapata uhai kutoka kwake. (Zb 36:9) Basi, badala ya kuwa Muumba-mwenza, huyo Mwana alikuwa wakala au chombo ambacho Yehova, Muumba, alitumia kufanya kazi. Yesu mwenyewe alisema kuwa Mungu ndiye aliyeumba, na Maandiko kwa ujumla yanaonyesha yeye ndiye Muumba.—Mt 19:4-6; ona UUMBAJI.
JANUARI 13-19
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MWANZO 3-5
“Matokeo Mabaya ya Uwongo wa Kwanza”
it-2 186
Maumivu ya Kuzaa
Huu ni uchungu unaohusiana na kuzaa. Baada ya mwanamke wa kwanza, Hawa, kufanya dhambi, Mungu alimwambia jinsi ambavyo angehisi wakati wa kuzaa watoto. Ikiwa angeendelea kuwa mtiifu, angeendelea kupata baraka za Mungu na kuzaa kungekuwa tukio lenye shangwe tu, kwa maana, “baraka ya Yehova ndiyo inayomtajirisha mtu, naye haichanganyi na maumivu.” (Met 10:22) Lakini sasa, kama sheria ya jumla, kutokamilika kwa mwili wake kungetokeza maumivu. Basi, Mungu akasema (mara nyingi mambo ambayo anaruhusu yanasemwa kuwa yeye ndiye anayefanya yatokee): “Nitazidisha sana uchungu wa mimba yako; utazaa watoto kwa uchungu.”—Mwa 3:16.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 192 ¶5
Lameki
Shairi ambalo Lameki aliwatungia wake zake (Mwa 4:23, 24) linaonyesha ujeuri uliokuwepo wakati huo. Shairi lake linasema: “Sikieni sauti yangu, enyi wake za Lameki; sikilizeni maneno yangu: Nimemuua mwanamume kwa sababu ya kunijeruhi, naam, mwanamume kijana kwa sababu ya kunipiga. Ikiwa Kaini atalipizwa kisasi mara 7, basi Lameki ni mara 77.” Inaonekana Lameki alikuwa akijitetea, akisisitiza kwamba hakuua kimakusudi, kama Kaini alivyofanya. Lameki alidai kwamba alikuwa akijilinda alipomuua mtu aliyemjeruhi. Kwa hiyo, shairi hili lilikuwa ishara ya kumkinga dhidi ya mtu yeyote ambaye angetamani kulipiza kisasi dhidi yake kwa sababu ya kumuua mtu aliyemshambulia.
it-1 338 ¶2
Kukufuru
“Kuliitia jina la Yehova” kunakotajwa katika nyakati za Enoshi katika kipindi cha kabla ya Gharika hakukufanywa kwa unyoofu na kwa njia inayofaa, kwa maana muda mrefu kabla ya hapo, Abeli bila shaka alikuwa akizungumza na Mungu akitumia jina lake. (Mwa 4:26; Ebr 11:4) Lakini, ikiwa kama wasomi fulani wanavyodai, kuliitia huko kwa jina la Mungu kulifanywa kwa njia ya kulitumia vibaya na kulihusianisha jina la Yehova na wanadamu au na sanamu, basi hicho kilikuwa kitendo cha kukufuru.—Tazama ENOSHI, ENOSI.
JANUARI 27–FEBRUARI 2
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MWANZO 9-11
“Dunia Yote Iliendelea Kuwa na Lugha Moja”
it-1 239
Babiloni Mkuu
Hali Iliyokuwa Katika Jiji la Kale la Babiloni. Kuanzishwa kwa jiji la Babiloni katika Eneo Tambarare la Shinari kulifanywa wakati uleule na ujenzi wa Mnara wa Babeli. (Mwa 11:2-9) Kusudi kuu lililofanya mnara huo na jiji hilo lijengwe halikuwa kulitukuza jina la Mungu, bali ni ili wajenzi ‘wajijengee jina maarufu.’ Minara ya ziggurat ambayo imevumbuliwa katika magofu ya Babiloni la kale na katika maeneo mengine ya Mesopotamia inathibitisha kwamba ule mnara wa awali ulijengwa kwa sababu za kidini, bila kuzingatia umbo au mtindo uliotumiwa kuujenga. Hatua madhubuti ambayo Yehova Mungu alichukua ya kuvuruga ujenzi wa hekalu hilo unaonyesha kwamba chanzo cha kazi hiyo kilikuwa dini ya uwongo. Ingawa jina la Kiebrania la jiji hilo, Babeli, linamaanisha “Mvurugo,” majina ya Kisumeri (Ka-dingir-ra) na Kiakadi (Bab-ilu) yanamaanisha “Lango la Mungu.” Basi wakaaji waliobaki katika jiji hilo walibadili kidogo jina hilo ili kuepuka matokeo mabaya ya hapo awali, ingawa bado jina hilo jipya lilihusianisha jiji hilo na dini.
it-2 202 ¶2
Lugha
Simulizi la Mwanzo linafafanua jinsi ambavyo baadhi ya familia za wanadamu ziliungana kipindi cha baada ya Gharika katika mradi uliopingana na mapenzi ya Mungu ambayo alikuwa amemfunulia Noa na wanawe. (Mwa 9:1) Badala ya kutawanyika na ‘kuijaza dunia,’ waliamua kuunganisha jamii ya wanadamu katika sehemu moja, na kuishi katika sehemu ambayo sasa inajulikana kama Eneo Tambarare la Shinari huko Mesopotamia. Inaonekana kwamba eneo hilo lingekuja kuwa kituo cha kidini, ambapo kungekuwa na mnara wa kidini.—Mwa 11:2-4.
it-2 202 ¶3
Lugha
Mungu Mweza-Yote alisitisha mradi huo wa kimbelembele kwa kuharibu umoja ulioendeleza kazi yao. Alifanya hivyo kwa kuvuruga lugha moja waliyotumia. Hilo lilifanya isiwezekane kuelekeza kazi mbalimbali katika mradi huo na hilo lilifanya watapakae katika sehemu mbalimbali za dunia. Kuvurugwa kwa lugha kungezuia au kufanya iwe vigumu kuanzisha mradi ambao ungeenda kinyume, au kukiuka mwongozo wa Mungu, kwa kuwa hilo lingepunguza uwezo wa wanadamu wa kuunganisha uwezo wa kiakili na wa kimwili katika miradi mikubwa na vilevile kufanya iwe vigumu kutumia ujuzi mwingi uliokusanywa kutoka katika vikundi mbalimbali vya lugha vilivyofanyizwa—kwa kweli, ujuzi huo haukutoka kwa Mungu, bali waliupata kutokana na shughuli na utafiti wa wanadamu. (Linganisha na Mhu 7:29; Kum 32:5.) Basi, ingawa hilo lilitokeza chanzo kikuu cha mtengano katika jamii ya kibinadamu, kuvurugwa kwa lugha ya wanadamu kuliifaidi jamii ya kibinadamu kwa kufanya iwe vigumu kutimiza miradi hatari ambayo ingewaumiza. (Mwa 11:5-9; linganisha na Isa 8:9, 10.) Ukichunguza baadhi ya mambo ambayo yamefanywa katika nyakati zetu, ambayo yamewezekana kwa sababu ya ujuzi wa kilimwengu ambao wanadamu wameutumia vibaya, unaweza kuelewa kwa nini Mungu alitambua kimbele jambo ambalo lingetokea ikiwa mradi ulioanzishwa huko Babeli ungeendelea bila kuvurugwa.
it-2 472
Mataifa
Kwa kuwa sasa kulikuwa na vizuzi vya lugha, kila kabila lingesitawisha utamaduni, sanaa, desturi, tabia, na dini yake—kila kikundi kikifanya mambo kwa njia yake. (Law 18:3) Vikiwa wamejitenga na Mungu, vikundi mbalimbali vya watu vilitengeneza sanamu zilizowakilisha miungu iliyokuwa katika hekaya zao.—Kum 12:30; 2Fa 17:29, 33.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 1023 ¶4
Hamu
Inawezekana kwamba Kanaani mwenyewe ndiye aliyehusika moja kwa moja katika tukio hilo na Hamu baba yake alikosa kumrekebisha. Au Noa, alizungumza kinabii kupitia mwongozo wa Mungu, na kutabiri kwamba mwelekeo mbaya wa Hamu, labda ambao tayari ulikuwa umeonekana katika Kanaani mwanaye, ungekuwa urithi wa wazao wa Kanaani. Laana hiyo ilitimizwa kwa sehemu wakati Waisraeli waliotokana na Shemu walipowatiisha Wakanaani. Wakanaani ambao hawakuangamizwa (kwa mfano, kabila la Wagibeoni [Yos 9]) walifanywa kuwa watumwa wa Israeli. Karne nyingi baadaye, laana hiyo ilitimizwa wakati wazao wa Kanaani mwana wa Hamu walipotawalia na serikali za ulimwengu zilizotokana na Yafethi, yaani, Umedi na Uajemi, Ugiriki, na Roma.
it-2 503
Nimrodi
Mwanzo wa ufalme wa Nimrodi ulitia ndani majiji ya Babeli, Ereki, Akadi, na Kalne, ambayo yote yalikuwa katika nchi ya Shinari. (Mwa 10:10) Basi inawezekana kwamba alitoa mwongozo kuhusu kuanza kujengwa kwa Babeli na mnara wake. Wazo hilo linapatana na maoni ya kale ya Wayahudi. Josephus aliandika hivi: “Hatua kwa hatua, [Nimrodi] alibadilisha mfumo wa utawala na kuwa wa kimabavu, akiamini kwamba njia pekee ya kuwafanya wanadamu waache kumwogopa Mungu ni kwa kuwafanya waendelee kutegemea nguvu zake mwenyewe. Alitishia kulipiza kisasi dhidi ya Mungu ikiwa angeiangamiza dunia tena; kwa maana angejenga mnara mrefu kuliko kimo cha maji na kulipiza kisasi kuuawa kwa mababu zake. Watu walikuwa tayari kufuata ushauri wake [Nimrodi], wakihisi kwamba kujitiisha chini ya Mungu ni utumwa; basi wakaanza kujenga mnara huo . . . na ulijengwa kwa kasi ya ajabu.”—Jewish Antiquities, I, 114, 115 (iv, 2, 3).