Kwa Nini Inakupasa Ujue Ukweli Juu ya Abrahamu
ABRAHAMU—je! alikuwa shujaa wa kihadithi tu au mnabii wa kweli? Jibu la swali hilo ni la maana kadiri gani? Kulingana na orodha ya matukio ya Biblia, Abrahamu aliishi kama miaka 4,000 iliyopita. Kwa hiyo huenda wengine wakasababu kwamba, ‘Kuna tofauti gani hata kama ni kweli alikuwako au hakuwako?’
Ni kwamba, nusu ya wakaaji wa ulimwengu ni wa dini zinazodai kuamini katika Abrahamu. Kichapo 1988 Britannica Book of the Year kinaorodhesha asilimia 32.9 ya ulimwengu kuwa Wakristo, asilimia 17.2 kuwa Waislamu, na asilimia 0.4 kuwa Wayahudi, na Abrahamu ni mtu mashuhuri katika hizi dini zote tatu. Kwa uhakika, waamini wenye moyo mweupe kutoka imani hizi wanapaswa kutaka kuhakikisha kwamba mambo ambayo wamefunzwa juu ya Abrahamu ni ukweli. Hata wale walio wa dini nyinginezo au wale wasiodai kuwa na dini yoyote ile wanapaswa kupendezwa. Kwa nini?
Kwa sababu Biblia inasema kwamba Abrahamu alikuwa mnabii, (Mwanzo 20:7) Hilo ni neno la Kibiblia linalotumiwa kueleza juu ya mnenaji wa Mungu mwenye ujumbe kwa wanadamu wengine. Ikiwa Abrahamu alikuwa mnabii wa kweli, wote wana nafasi ya kunufaika. Kwa nini? Kwa sababu ujumbe aliopokea ulikuwa na habari njema kwa aina ya binadamu wote. (Wagalatia 3:8) Kulingana na Biblia, Mungu alimwahidi Abrahamu hivi: “Kwa uhakika jamaa zote za ardhi zitajibariki zenyewe kwa njia ya wewe.”—Mwanzo 12:3, NW.
Hiyo ni ahadi ya kushangaza sana, na Abrahamu aliisikia ikitamkwa katika angalau pindi nyingine mbili. (Mwanzo 18:18; 22:18) Ili kuitimiza, Mungu hata atawafufua kutoka kwa wafu wawakilishi wa jamaa ambazo zimekufa zikamalizika kabisa. Maisha yatakuwa baraka kweli kweli kwa wafufuliwa hao, kwa kuwa wengi wao watarudi kwenye hali ya kidunia inayofanana na Paradiso ambayo mwanadamu alipoteza hapo awali. Baada ya hapo, watafunzwa jinsi ya kupata baraka ya uhai wa milele.—Mwanzo 2:8, 9, 15-17; 3:17-23.
Kwa upande ule mwingine, ikiwa Abrahamu alikuwa mtu wa kihadithi tu, hakungekuwa na msingi wowote wa kuamini hiyo ahadi nzuri ajabu aliyoipokea. Tena, ikiwa ahadi za Biblia haziwezi kutegemewa, huenda watu fulani wakafanya ubishi wa kupendelea kujitolea kabisa ufuataji wa anasa za maisha ya sasa. Kama vile alivyoandika mmoja wa Wakristo wa mapema: “Wasipofufuliwa wafu, na tule, na tunywe, maana kesho tutakufa.”—1 Wakorintho 15:32.
Kwa hiyo, wewe una kila sababu ya kuchunguza swali hili, Je! Abrahamu alikuwa shujaa wa kihadithi tu au alikuwa mnabii wa kweli? Huenda ukashtuka kujua yale ambayo makasisi mashuhuri wa karne ya 19 wamesema juu ya jambo hili. Kwa wakati uliopo, wachimbuzi wa vitu vya kale wamegundua vitu vya kustaajabisha vinavyokinza maoni ya makasisi hao.