Je! Ye Yote Ameona Mungu?
ABRAHAMU mzee wa ukoo mwenye sifa kubwa, ambaye aliishi zaidi ya miaka 1900 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo, alionwa na Muumba wetu kwa maoni ya uchangamfu mwingi hata akaitwa “rafiki ya Mungu.” (Yakobo 2:23, Byington) Kama mtu ye yote angepewa pendeleo la kuona Mungu, kwa uhakika Abrahamu angekuwa ndiye mtu huyo. Basi, pindi fulani, wageni watatu walimjia wakiwa na ujumbe wa kimungu. Abrahamu alielekeza maneno yake kwa mmoja wao kama kwamba anaambia Yehova. Je! hiyo inamaanisha kwamba Abrahamu kwa kweli aliona Mungu?
Usimulizi huu unapatikana katika Mwanzo 18:1-3, NW. Humo tunasoma: “Yehova akamtokea miongoni mwa ile miti mikubwa ya Mamre, yeye akiwa ameketi kwenye mwingilio wa hema wapata wakati wa joto la siku. Yeye alipoinua macho yake, ndipo yeye akatazama na pale walikuwapo wanaume watatu wamesimama umbali fulani kutoka alipo. Wakati yeye alipopata kuwaona alianza kukimbia kuwalaki kutoka kwenye mwingilio wa hema na akaendelea na kuinama chini kwenye dunia. Ndipo yeye akasema: ‘Yehova, ikiwa, sasa, mimi nimepata upendeleo katika macho yako, tafadhali usipite kando ya mtumishi wako.’ “
Baadaye, wakati Abrahamu na wageni wake watatu walipokuwa wakitazama mandhari ya Sodoma wakiwa mahali palipoinuka, wawili waliondoka wakazuru jiji lile. Mstari 22 ndipo unaposema: “Lakini kwa habari ya Yehova, yeye alikuwa bado amesimama mbele ya Abrahamu.” Ingeonekana kutokana na hilo kwamba Mungu alikuwapo pamoja na Abrahamu akiwa amejivika mwili wa kimnofu. Hivyo ndivyo watu fulani wanavyokazania, ambao wanaitikadi kwamba Mungu na Yesu Kristo ni mtu yule yule mmoja.
Kwa habari ya Mwanzo 18:3, Melancthon W. Jacobus mwanachuo wa Biblia aliandika hivi: “Hapa Mungu anaonekana kwa mara ya kwanza iliyopata kuwa katika maandishi akiwa mwanadamu miongoni mwa wanadamu, ili kuonyesha uhakika wa Kuwako Kwake, na wa ufungamano Wake na wanadamu, na ili kwa kitendo hiki halisi amhakikishie yule mzee wa ukoo juu ya kuwako kwa ushirika na uenzi wa Kimungu.” Wale walio na maoni haya wangeweza kukata shauri kwamba Abrahamu aliona Yehova kikweli kwa macho yake ya kimwili na kwamba watu ambao waliona Yesu Kristo waliona Mungu pia. Lakini je! mkato huo wa shauri unapatana na Biblia?
Aliyosema Yesu
Badala ya kutangaza kwamba yeye alikuwa ndiye Mungu katika mnofu, Yesu Kristo alisema: “Mimi ni Mwana wa Mungu.” (Yohana 10:36, NW) Akiwa Mwakilishi mkamilifu wa Yehova Mungu, Yesu alisema hivi pia: “Mimi siwezi kufanya jambo hata moja la uanzilishi wangu mwenyewe; sawa na vile mimi nasikia, mimi nahukumu; na hukumu ambayo mimi natoa ni adilifu, kwa sababu mimi natafuta, si mapenzi yangu mwenyewe, bali mapenzi ya yeye ambaye alinituma mimi.” (Yohana 5:30, NW) Wakati Yesu alipokuwa juu ya mti wa mateso, yeye alimpelekea sala Muumba mkuu katika mbingu, akimtaja kuwa “Mungu wangu, Mungu wangu.” (Mathayo 27:46, NW) Baada ya ufufuo wake, Yesu alimwambia Mariamu Magdalene: “Mimi ninapaa kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu na kwa Mungu wangu na Mungu wenu.” (Yohana 20:1, 17, NW) Kwa kuwa Yesu Kristo hakuwa Mungu-mtu, hakuna mtu ambaye aliona Yesu angeweza kusema kwamba yeye alikuwa ameona Mungu kwa njia hiyo.
Yohana, mtume ambaye Yesu alipenda hasa, alitilia nguvu uhakika wa kwamba mitume hawakuwa wakiona Mungu wakati wao walipotazama Yesu. Akiwa chini ya uvuvio wa Mungu Yohana alisema: “Hakuna mwanadamu ameona Mungu wakati wo wote.” (Yohana 1:18, NW) Basi, ni nani ambaye Abrahamu alimwona? Ono la Musa linatusaidia kupata jibu.
Jinsi Musa Alivyoona Mungu
Wakati mmoja Musa alijieleza kuwa mwenye tamaa ya kuona Mungu. Kwenye Kutoka 33:18-20, NW, tunasoma hivi: “‘Sababisha mimi [Musa] nione, tafadhali, utukufu wako.’ Lakini yeye [Mungu] akasema: ‘Mimi mwenyewe nitasababisha wema wangu wote upite mbele ya uso wako, na mimi nitatangaza rasmi jina la Yehova mbele yako wewe; na mimi nitapendelea yule ambaye mimi nitapata kupendelea, na mimi nitaonyesha rehema kwa yule ambaye mimi nitapata kuonyesha rehema.’ Na yeye akaongezea: ‘Wewe huwezi kuona uso wangu, kwa sababu hakuna mwanadamu wa kupata kuniona mimi na bado awe hai.’ “
Kile ambacho Mungu aliruhusu Musa kuona kilikuwa utukufu Wake wenye kupita. Mistari 21-23 inataarifu hivi: “Na Yehova akasema zaidi hivi: ‘Hapa mimi nina mahali pamoja, na lazima wewe ujiweke mwenyewe juu ya ule mwamba. Na itapasa kutukia kwamba wakati utukufu wangu unapokuwa unapita ni lazima mimi nikuweke wewe katika shimo katika ule mwamba, na mimi lazima nitie kiganja changu juu yako wewe kiwe kisetiri mpaka mimi niwe nimepita. Baada ya hapo ni lazima mimi niondoe kiganja changu, na wewe utaona kweli kweli mgongo wangu. Lakini uso wangu si wa kupata kuonwa.’ “
Kupatana na yale ambayo Yehova alimwambia Musa na yale ambayo mtume Yohana alisema, Musa hakuona Mungu akijivika mwili wala hakuona umbo la kimwili la Mungu. Kile tu ambacho Musa aliona ni mwako wa baada ya kuwapo kwa kimungu, ukipitia hapo. Hata ilipokuwa hivyo ilikuwa lazima yeye apewe himaya ya kimungu. Kwa wazi, si Mungu mwenyewe ambaye alionwa na Musa.
Wakati Musa aliponena na Mungu “uso kwa uso,” kama inavyotaarifiwa kwenye Kutoka 33:11, NW, yeye hakuwa katika mawasiliano ya kuonana na Yehova. Usemi huo unaonyesha namna ambayo katika hiyo Musa aliwasiliana na Mungu, si kile ambacho yeye aliona. Kunena na Mungu “uso kwa uso” kunaonyesha maongezi kati ya watu wawili. Vivyo hivyo, mtu anaweza kuendesha maongezi kati yake na mwingine kwa simu, bila kuona mtu yule mwingine.
Musa alipoongea na Mungu na kupokea maagizo kutoka kwake, mawasiliano hayo hayakuwa kupitia njozi, kama ilivyokuwa mara nyingi kwa habari ya manabii wengine. Jambo hilo linaonwa kwenye Hesabu 12:6-8, ambapo sisi tunasoma: “Yeye aliendelea kusema: ‘Sikieni maneno yangu, tafadhali. Kama kungekuja kuwa na nabii wenu kwa ajili ya Yehova, ingekuwa ni katika njozi mimi ningejijulisha mwenyewe kwake. Katika ndoto mimi ningenena naye. Si hivyo Musa mtumishi wangu! Yeye anaitibarishwa nyumba yangu yote. Kinywa kwa kinywa mimi ninanena naye, hivyo nikimwonyesha yeye, wala si kwa vitendawili; na sura ya Yehova ndicho kitu ambacho yeye anaangalia.’” Ni katika maana gani Musa aliangalia “sura ya Yehova”?
Musa aliangalia “sura ya Yehova” wakati yeye, Haruni, na wanaume fulani wengine walipoenda juu ya Mlima Sinai. Kwenye Kutoka 24:10, NW, imeandikwa hivi: “Wao walipata kuona Mungu wa Israeli. Na chini ya nyayo zake palikuwa na kile kilichoelekea kuwa kama kazi ya mawe-mabamba ya yakuti samawi na kama zile mbingu zenyewe kwa utakato.” Lakini ni jinsi gani Musa na wale wanaume wengine walipata ‘kuona Mungu wa Israeli,’ kwa kuwa Mungu alikuwa amemwambia, “Hakuna mwanadamu wa kupata kuniona mimi na bado awe hai”? Mstari wa 11 unaeleza, kwa maana unasema: “Yeye hakutokeza mkono wake dhidi ya wale wanaume mashuhuri wa wana wa Israeli, lakini wao walipata njozi ya Mungu wa kweli na wakala na kunywa.” Kwa hiyo sura ya Mungu ambayo Musa na wengine waliona ilikuwa kwa njia ya njozi.
Wawakilishi wa Kimalaika
Haijahitajiwa kabisa Muumba mkuu wa ulimwengu wote mzima aje chini kutoka mahali pale palipotukuka katika mbingu ili awaletee wanadamu fulani ujumbe mbalimbali. Kando na vile visa vitatu vilivyo katika maandishi ambapo sauti ya Mungu mwenyewe ilisikiwa wakati Mwanaye alipokuwa duniani, sikuzote Yehova ametumia malaika kupitisha ujumbe Wake mbalimbali. (Mathayo 3:17; 17:5; Yohana 12:28) Hata ile Sheria ambayo Mungu alilipa taifa la Israeli kwenye Mlima Sinai ilipitishwa kwa njia ya malaika, ingawa Musa alionyeshwa kama kwamba akiongea moja kwa moja na Mungu mwenyewe. Kuhusu hilo, mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa nini, basi, Sheria? Hiyo iliongezwa ili kufanya mikiuko ya sheria idhihirike, mpaka awasili uzao ambaye ile ahadi ilikuwa imefanywa kwake; nayo ilipitishwa kupitia malaika kwa mkono wa mpatanishi.”—Wagalatia 3:19,NW.
Kwamba Musa kwa kweli alinena na malaika aliyekuwa anawakilisha Mungu kibinafsi inaonyeshwa pia kwenye Matendo 7:38 (NW), inayotaarifu hivi: “Huyu ndiye yule ambaye alikuja kuwa miongoni mwa lile kundi katika jangwa pamoja na malaika ambaye alinena naye juu ya Mlima Sinai na pamoja na baba zetu wa kwanza-kwanza.” Malaika huyo alikuwa mnenaji wa kibinafsi kwa ajili ya Yehova Mungu, Muumba, na kwa hiyo yeye alinena na Musa kama kwamba ni Mungu mwenyewe aliyekuwa akinena.
Malaika aliyeletea Musa ujumbe wa Mungu kwenye kichaka cha miiba chenye kuwaka moto alikuwa mnenaji pia. Yeye anatambulishwa kuwa malaika wa Yehova kwenye Kutoka 3:2, NW, ambapo tunaambiwa hivi: “Malaika wa Yehova alitokea kwake katika mwali wa moto katikati ya kichaka cha miiba.” Mstari wa 4 unasema: “Yehova alipoona kwamba yeye aligeukia kando kukagua, mara hiyo Mungu akamwita kutoka katikati ya kile kichaka cha miiba.” Katika mstari wa 6, mnenaji huyo wa kimalaika mwenye kunena kwa ajili ya Mungu alisema: “Mimi ndimi Mungu wa baba yako, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.” Kwa hiyo alipokuwa akinena na huyu mwakilishi wa kibinafsi wa Mungu, Musa alinena kama kwamba alikuwa akinena na Yehova mwenyewe.—Kutoka 4:10, NW.
Katika sura ya 6 ya Waamuzi, sisi tunapata kielelezo kingine cha mwanamume akinena na Mungu kupitia mwakilishi wa kimalaika. Mstari wa 11 (NW) unatambulisha mleta-ujumbe huyo kuwa “malaika wa Yehova.” Hapo tunasoma hivi: “Baadaye malaika wa Yehova akaja na kuketi chini ya ule mti mkubwa uliokuwa katika Ofra, uliokuwa wa Yoashi yule Mwabiezeri, wakati Gideoni mwana wake alipokuwa akipiga-piga ngano katika shinikizo-divai ili aiondoe haraka machoni pa Midiani.” Mjumbe huyu, “malaika wa Yehova,” anaonyeshwa baada ya hapo kama kwamba ndiye Yehova Mungu mwenyewe. Katika mistari 14 na 15, sisi tunasoma: “Hapo Yehova akaelekeana na [Gideoni] na kusema: ‘Nenda katika hii nguvu yako, na wewe kwa uhakika utaokoa Israeli kutoka katika kiganja cha Midiani. Je! kwani si mimi ninayekutuma wewe?’ Naye akamwambia: ‘Niwie radhi, Yehova. Mimi nitaokoa Israeli nikiwa na kitu gani?’ “Kwa hiyo malaika aliyejivika mwili ambaye alionwa na Gideoni, na ambaye alinena naye, anaonyeshwa katika usimulizi wa Kibiblia kama kwamba yeye alikuwa ndiye Mungu mwenyewe. Katika mstari wa 22, Gideoni anasema: “Mimi nimeona malaika wa Yehova uso kwa uso!” Malaika huyo alinena yale yale kabisa ambayo Mungu alimwambia anene. Basi, Gideoni alinena pamoja na Mungu kupitia mnenaji huyu wa kimalaika.
Fikiria, pia, kisa cha Manoa na mke wake, wazazi wa Samsoni. Usimulizi huu unanena pia juu ya yule mjumbe wa kimalaika kuwa “malaika wa Yehova” na “malaika wa Mungu wa kweli.” (Waamuzi 13:2-18, NW) Katika mstari wa 22, Manoa anaambia mke wake: “Sisi tutakufa hakika, kwa sababu ni Mungu ambaye sisi tumeona.” Ingawa yeye hakumwona Yehova Mungu kikweli, Manoa alihisi hivyo kwa sababu alikuwa ameona mnenaji wa Mungu binafsi, aliyejivika mwili.
“Hakuna Mwanadamu Ameona Mungu”
Sasa inawezekana kuelewa ni kwa nini Abrahamu alielekeza maneno kwa mnenaji wa Mungu wa kimalaika aliyejivika mwili kama kwamba alikuwa akiongea na Yehova Mungu mwenyewe. Kwa kuwa malaika huyu alinena yale yale kabisa ambayo Mungu alitaka amwambie Abrahamu, na alikuwa hapo akimwakilisha Yeye binafsi, maandishi ya Kibiblia yangeweza kusema kwamba “Yehova mwenyewe alitokea kwake.”—Mwanzo 18:1, NW.
Kumbuka kwamba mnenaji wa Mungu wa kimalaika angeweza kupitisha ujumbe Wake mbalimbali sawasawa kabisa na vile simu au redio inavyoweza kupitisha maneno yetu kwa mtu mwingine. Kwa sababu hiyo, inaweza kueleweka ni jinsi gani Abrahamu, Musa, Manoa, na wengine wangeweza kunena pamoja na malaika aliyejivika mwili kama kwamba walikuwa wanaongea na Mungu. Ingawa hao watu mmoja mmoja waliweza kuona malaika hawa na utukufu wa Yehova ulioonekana kupitia kwao, wao hawakuweza kuona Mungu. Basi, hiyo haipinganishi kwa vyo vyote ile taarifa ya mtume Yohana: “Hakuna mwanadamu ameona Mungu wakati wo wote.” (Yohana 1:18, NW) Kile ambacho wanaume hawa waliona kilikuwa wawakilishi wa kimalaika wala si Mungu mwenyewe.