Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
MEI 3-9
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | HESABU 27-29
Hazina za Kiroho
it-2 528 ¶5
Matoleo
Matoleo ya kinywaji. Matoleo ya kinywaji yalitolewa pamoja na matoleo mengine mengi, hasa baada ya Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi. (Hes 15:2, 5, 8-10) Toleo hilo lilikuwa divai (“kileo”) na ilimiminwa juu ya madhabahu. (Hes 28:7, 14; linganisha Kut 30:9; Hes 15:10.) Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo huko Filipi hivi: “Ikiwa ninamiminwa kama toleo la kinywaji juu ya dhabihu na utumishi mtakatifu ambao imani yenu imewaongoza, ninafurahi.” Hapo alitumia mfano wa toleo la kinywaji, kuelezea utayari wake wa kujitoa kwa ajili ya Wakristo wenzake. (Flp 2:17) Muda mfupi kabla ya kifo chake, alimwandikia Timotheo hivi: “Tayari ninamiminwa kama toleo la kinywaji, na wakati wangu wa kufunguliwa umekaribia sana.”—2Ti 4:6.
MEI 10-16
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | HESABU 30-31
“Timiza Nadhiri Zako”
it-2 1162
Nadhiri
Ilitolewa kwa Hiari, Lakini Ikitolewa Lazima Itimizwe. Nadhiri zilitolewa kwa hiari. Hata hivyo, mtu alipotoa nadhiri, ilikuwa lazima kuitimiza kulingana na sheria ya Mungu. Maneno yaliyotafsiriwa “kuweka nadhiri” kwenye Hesabu 30:2 katika Kiebrania, kihalisi yanatokeza wazo la ‘kujifunga wajibu juu ya nafsi,’ kumaanisha kwamba uhai wa mtu huyo ulitolewa kama dhamana ya kutimiza alichoapa. (Ona pia Ro 1:31, 32.) Kwa kuwa uhai ulihusika, inaeleweka kwa nini Maandiko yanamsihi mtu awe mwangalifu sana anapoweka nadhiri, akifikiria kwa uzito wajibu anaojichukulia. Sheria inasema hivi: “Ukiweka nadhiri kwa Yehova . . . Mungu wako kwa hakika atakudai; la sivyo, utakuwa umetenda dhambi. Lakini usipoweka nadhiri, hutakuwa na hatia ya dhambi.”—Kum 23:21, 22.
it-2 1162
Nadhiri
Ahadi nzito inayotolewa kwa Mungu kufanya tendo fulani, kutoa toleo au zawadi fulani, kuingia katika utumishi au hali fulani, au kuepuka vitu fulani ambavyo havina kasoro. Nadhiri ilikuwa tamko ambalo mtu alifanya kwa hiari yake mwenyewe. Kwa kuwa ni ahadi nzito, nadhiri ilionwa kuwa sawa na kiapo, na mara nyingi maneno hayo mawili hutumiwa pamoja katika Biblia. (Hes 30:2; Mt 5:33) “Nadhiri” hutolewa na mtu anayeonyesha tamaa ya kufanya jambo fulani, na “kiapo” ni ombi linalotolewa kwa mamlaka kubwa zaidi ili kuthibitisha ukweli wa tangazo fulani au kumwajibisha mtu kwa tangazo hilo. Mara nyingi kiapo huambatana na agano la kulithibitisha.—Mwa 26:28; 31:44, 53.
Hazina za Kiroho
it-2 28 ¶1
Yeftha
Watu wangeweza kutolewa kwa ajili ya utumishi wa Yehova katika hema la ibada. Ilikuwa haki ya wazazi kufanya uamuzi huo. Samweli ni mmoja kati ya watu hao. Kabla Samweli hajazaliwa, mama yake Hana aliapa na kutoa ahadi kwamba angemtoa atumikie katika hema la ibada. Elkana alikubali nadhiri hiyo. Mara tu Samweli alipoachishwa kunyonya, Hana alimtoa kwa ajili ya utumishi wa hema la ibada. Hana alipeleka pia mnyama ambaye angetolewa dhabihu. (1Sa 1:11, 22-28; 2:11) Samsoni ni mtoto mwingine ambaye alitolewa kwa ajili ya utumishi wa Yehova wa kuwa Mnadhiri.—Amu 13:2-5, 11-14; linganisha mamlaka ya baba juu ya binti yake kama inavyoonyeshwa kwenye Hes 30:3-5, 16.
MEI 17-23
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | HESABU 32-33
“Wafukuze Wakaaji Wote wa Nchi”
it-1 404 ¶2
Kanaani
Kwa hekima, “hakuna jambo lolote ambalo [Yoshua] hakufanya kati ya mambo yote ambayo Yehova alimwamuru Musa.” (Yos 11:15) Lakini taifa la Israeli halikufuata mfano wake mzuri na kuangamiza kabisa chanzo cha uchafuzi nchini. Kuwepo kwa Wakanaani miongoni mwao kuliwaathiri Waisraeli, na baada ya muda, kulitokeza vifo vingi zaidi kuliko idadi ya Wakanaani ambao wangekufa iwapo agizo la kuwaangamiza lingetekelezwa kwa uaminifu—bila kutaja uhalifu, ukosefu wa maadili, na ibada ya sanamu uliotokea. (Hes 33:55, 56; Amu 2:1-3, 11-23; Zb 106:34-43) Yehova alikuwa amewaonya Waisraeli kwamba haki yake na hukumu zake hazina upendeleo na kwamba ikiwa Waisraeli wangeanzisha mahusiano na Wakanaani, wafunge ndoa nao, washiriki katika ibada yao, na kukubali desturi zao za kidini na mazoea yao mapotovu, wangejiletea hukumu ileile ya maangamizi na hatimaye ‘nchi ingewatapika’ wao pia.—Kut 23:32, 33; 34:12-17; Law 18:26-30; Kum 7:2-5, 25, 26.
Hazina za Kiroho
it-1 359 ¶2
Mpaka
Baada ya kupiga kura kufahamu eneo la kijiografia la kila kabila, kungekuwa na uhitaji wa kutambua ukubwa wa eneo lake kwa msingi wa sababu ya pili: idadi ya watu katika kabila hilo. “Mtaigawanya nchi hiyo kwa kura na kuimiliki kulingana na familia zenu. Kundi kubwa litapokea urithi mkubwa zaidi na kikundi kidogo kitapokea urithi mdogo. Kila mtu atapokea urithi wake mahali ambapo kura yake itaangukia.” (Hes 33:54) Uamuzi wa kura kuhusu upande wa kijiografia haungebadilika, hata hivyo, badiliko lingeweza kufanywa kuhusiana na ukubwa wa urithi. Kwa hiyo, eneo la Yuda lilipoonekana kuwa kubwa sana, lilipunguzwa kwa kuwagawia watu wa kabila la Simeoni maeneo ndani ya ardhi hiyo.—Yos 19:9.
MEI 31–JUNI 6
MAISHA YA MKRISTO
Endelea Kuwa Tayari Katika Sehemu ya Mwisho ya “Siku za Mwisho”
nwtsty habari za utafiti Mt 24:8
Maneno hayo ya Kigiriki kihalisi yanarejelea maumivu makali ambayo mtu hupata wakati wa kuzaa. Ingawa hapa yametumiwa kurejelea mahangaiko, uchungu, na kuteseka kwa ujumla, huenda yakawa yanadokeza kwamba katika kipindi kinachotangulia dhiki kuu inayotajwa katika Mt 24:21, matatizo na mateso yataongezeka, yatakuwa makali zaidi, na yatakuwa ya muda mrefu zaidi kama tu maumivu ya kuzaa.
JUNI 7-13
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 3-4
“Sheria za Yehova Ni Zenye Hekima na Haki”
it-2 1140 ¶5
Uelewaji
Bidii ya kujifunza na kutumia Neno la Mungu na amri zilizomo inaweza kumsaidia mtu kuwa na ufahamu mwingi zaidi kuliko walimu wake na uelewaji mwingi zaidi kuliko wanaume wazee. (Zb 119:99, 100, 130; linganisha Lu 2:46, 47.) Hiyo ni kwa sababu hekima na uelewaji ni sehemu ya masharti safi ya Mungu na maamuzi yake ya hukumu; hivyo ikiwa Waisraeli wangefuata sheria hizo kwa uaminifu mataifa yanayowazunguka yangewaona kuwa watu wenye “hekima na uelewaji.” (Kum 4:5-8; Zb 111:7, 8, 10; linganisha 1Fa 2:3.) Mtu mwenye uelewaji anatambua Neno la Mungu haliwezi kukosolewa, na angependa kupatanisha njia yake na kile inachosema, hivyo anamwomba Mungu amsaidie kufanikiwa katika hilo. (Zb 119:169) Anaruhusu ujumbe wa Mungu uingie ndani kabisa (Mt 13:19-23), anauandika kwenye kibao cha moyo wake (Met 3:3-6; 7:1-4), na anasitawisha chuki kuelekea “kila njia ya uwongo” (Zb 119:104). Mwana wa Mungu alipokuwa duniani, alionyesha ana uelewaji huo, hata akakataa kuepuka kufa juu ya mti wa mateso kwa sababu Maandiko yalitabiri alipaswa kufa kwa njia hiyo.—Mt 26:51-54.
JUNI 28–JULAI 4
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 9-10
Hazina za Kiroho
it-1 103
Wazao wa Anaki
Jamii ya watu wakubwa isivyo kawaida walioishi katika maeneo ya milima ya Kanaani kutia ndani maeneo ya pwani, hasa Kusini ya Kanaani. Pindi moja wanaume watatu maarufu wa uzao wa Anaki, yaani, Ahimani, Sheshai, na Talmai, waliishi Hebroni. (Hes 13:22) Huko ndiko kwa mara ya kwanza wapelelezi 12 Waebrania waliowaona wazao wa Anaki, na kwa sababu hiyo 10 kati ya wapelelezi hao wakatoa ripoti zenye kuogopesha, wakidai kwamba wanaume hao walikuwa wazao wa Wanefili walioishi kabla ya Gharika na kwamba kwa kulinganishwa nao, Waebrania walikuwa kama “panzi.” (Hes 13:28-33; Kum 1:28) Ukubwa wao ulitumiwa kuwa kiwango cha kulinganisha na kuwafafanua wanaume wengine wakubwa, kama vile Waemi na Warefaimu. Inaonekana kwamba kwa sababu ya nguvu zao, watu walitunga methali iliyosema: “Ni nani anayeweza kuwashinda wana wa Anaki? ”—Kum 2:10, 11, 20, 21; 9:1-3.