Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
SEPTEMBA 6-12
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUMBUKUMBU LA TORATI 33-34
“Pata Kimbilio Katika ‘Mikono ya Yehova ya Milele’”
it-2 51
Yeshuruni
Ni jina la heshima la Israeli. Katika Septuajinti ya Kigiriki neno “Yeshuruni” linatafsiriwa kuwa neno linaloonyesha upendo wa dhati, neno linalotumiwa ni “mpendwa.” Jina hilo “Yeshuruni” lilipaswa kuwakumbusha Waisraeli kuhusu agano walilofanya na Yehova na hivyo walipaswa kuendelea kuwa wanyoofu. (Kum 33:5, 26; Isa 44:2) Kwenye Kumbukumbu la Torati 32:15, jina Yeshuruni limetumiwa kinyume. Badala ya kutenda kulingana na jina hilo, Yeshuruni, taifa la Israeli lilimwacha Muumba wao na kumdharau Mwokozi wao.
Hazina za Kiroho
it-2 439 ¶3
Musa
Musa alikuwa na umri wa miaka 120 alipokufa. Biblia inasema hivi waziwazi kuhusu nguvu zake za kimwili: “Macho yake hayakuwa yamedhoofika, na nguvu zake hazikuwa zimeisha.” Yehova alimzika mahali ambapo hapajulikani. (Kum 34:5-7) Inaelekea, Yehova alifanya hivyo ili kuwazuia Waisraeli wasinaswe na mtego wa ibada ya uwongo kwa kutengeneza kaburi lake kuwa madhabahu. Ni wazi kwamba Ibilisi alitamani kutumia mwili wa Musa kwa kusudi kama hilo, kwa sababu Yuda, mfuasi wa Yesu Kristo ambaye pia ni ndugu yake wa kambo aliandika hivi: “Mikaeli, yule malaika mkuu alipopingana na Ibilisi na kubishana naye kuhusu mwili wa Musa, hakuthubutu kumhukumu kwa kumtukana, bali alimwambia: ‘Yehova na akukemee.’” (Yuda 9) Waisraeli, wakiwa chini ya uongozi wa Yoshua, walimwombolezea Musa kwa siku 30 kabla ya kuingia katika nchi ya Kanaani.—Kum 34:8.
SEPTEMBA 20-26
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOSHUA 3-5
“Yehova Hubariki Matendo ya Imani”
it-2 105
Yordani
Kwa kawaida, sehemu ya Mto Yordani iliyo upande wa chini wa Bahari ya Galilaya ina kina cha mita 1 hadi 3 hivi na upana wa mita 27 hadi 30 hivi. Lakini wakati wa majira ya kuchipua Mto Yordani huvunja kingo zake na kuwa mpana na wenye kina zaidi. (Yos 3:15) Haingekuwa salama kwa taifa la Israeli lililokuwa na wanaume, wanawake, na watoto kuvuka Mto Yordani ukiwa umefurika, hasa karibu na Yeriko. Maji katika sehemu hiyo yana nguvu sana hivi kwamba katika nyakati za karibuni waogeleaji wamesombwa na maji hayo. Hata hivyo, Yehova aliyazuia kimuujiza maji ya Mto Yordani na hivyo Waisraeli wakavuka kwenye nchi kavu. (Yos 3:14-17) Karne nyingi baadaye, muujiza kama huo ulitokea tena Eliya alipokuwa na Elisha, halafu tena Elisha alipokuwa peke yake.—2Fa 2:7, 8, 13, 14.
OKTOBA 4-10
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOSHUA 8-9
“Masomo Tunayojifunza Kutokana na Simulizi la Wagibeoni”
it-1 930-931
Gibeoni
Walivyoshughulika na Yoshua. Katika siku za Yoshua Wahivi waliishi katika eneo la Gibeoni, ambalo lilikuwa moja kati ya mataifa saba ya Kanaani yaliyopaswa kuharibiwa. (Kum 7:1, 2; Yos 9:3-7) Wagibeoni waliitwa pia Waamori, kwa kuwa nyakati nyingine jina hilo lilitumiwa kuwarejelea Wakanaani wote. (2Sa 21:2; linganisha Mwa 10:15-18; 15:16.) Tofauti na Wakanaani wengine, Wagibeoni walitambua kwamba licha ya kuwa na jeshi kubwa na ukuu wa jiji lao, hawangefaulu kupigana na Waisraeli kwa sababu Yehova alikuwa akiwapigania. Kwa hiyo, baada ya kuharibiwa kwa Yeriko na Ai, wanaume wa Gibeoni, ambao inaonekana pia waliwakilisha majiji matatu ya Wahivi ya Kefira, Beerothi, na Kiriath-yearimu (Yos 9:17), waliwatuma wawakilishi kwa Yoshua huko Gilgali ili kufanya amani. Mabalozi hao wa Wagibeoni—waliokuwa wamevalia nguo na viatu vilivyochakaa, wakiwa na viriba vya divai vilivyochakaa, magunia yaliyochakaa, na mikate iliyokauka na kuvunjika-vunjika—walijitambulisha kuwa wametoka katika nchi ya mbali na hivyo hawangeweza kuwazuia Waisraeli kushinda maeneo ya Wakanaani. Walitaja jinsi mkono wa Yehova ulivyowashinda Wamisri na wafalme wa Waamori Sihoni na Ogu. Lakini kwa hekima hawakutaja kuhusu Yeriko na Ai, kwa kuwa ikiwa kwa kweli walitoka “nchi ya mbali sana,” basi habari hizo hazingekuwa zimewafikia kabla ya kuondoka kwao. Wawakilishi wa Waisraeli walichunguza na kukubali uthibitisho waliokuwa nao hivyo wakafanya agano nao ili kuwaacha waishi.—Yos 9:3-15.
Hazina za Kiroho
it-1 1030
Kutundika
Chini ya sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli, huenda wahalifu fulani walitundikwa mtini baada ya kuuawa kwa sababu walikuwa “kitu kilicholaaniwa na Mungu,” na kutundikwa mahali ambapo wangeonwa na watu ili wawe kama onyo kwao. Maiti iliyotundikwa mtini ilipaswa kuzikwa kabla ya giza kuingia kwa sababu kuiacha mtini usiku kucha kungeichafua nchi ambayo Waisraeli walipewa na Mungu. (Kum 21:22, 23) Waisraeli walifuata mwongozo huo hata ikiwa aliyetundikwa hakuwa Mwisraeli.—Yos 8:29; 10:26, 27.
OKTOBA 11-17
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOSHUA 10-11
“Yehova Aliwapigania Waisraeli”
it-1 50
Adoni-sedeki
Alikuwa mfalme wa Yerusalemu wakati ambapo Waisraeli walikuwa wakipigana ili kuimiliki Nchi ya Ahadi. Adoni-sedeki aliungana na falme nyingine ndogondogo zilizo Magharibi mwa Mto Yordani ili kupigana na jeshi la Yoshua. (Yos 9:1-3) Hata hivyo, wakaaji Wahivi wa Gibeoni walifanya amani na Yoshua. Ili kuwazuia wengine wasijiunge na adui yao, Adoni-sedeki aliunganisha jeshi lake na majeshi ya wale wafalme wengine wanne wa Waamori, wakazingira Gibeoni na kuwashambulia. Njia ambayo Yoshua alitumia kuwakomboa Wagibeoni na ushindi wake dhidi ya majeshi hayo yaliyoungana, uliwafanya wafalme hao watano wakimbilie Makeda ambako walifungiwa katika pango. Yoshua mwenyewe alimuua Adoni-sedeki pamoja na wale wafalme wengine wanne mbele ya jeshi lake na kuwatundika juu ya miti. Hatimaye, maiti zao zilitupwa kwenye lile pango nalo likawa kaburi lao.—Yos 10:1-27.
it-1 1020
Mvua ya Mawe
Ilitumiwa na Yehova. Yehova amewahi kutumia mvua ya mawe ili kutimiza Neno lake na kuonyesha nguvu zake kuu. (Zb 148:1, 8; Isa 30:30) Mara ya kwanza iliyorekodiwa ambapo Yehova alitumia mvua ya mawe ni wakati alipoleta pigo la saba dhidi ya taifa la kale la Misri, ambapo mvua kubwa ya mawe iliharibu mimea na kuvunjavunja miti na kuwaua wanadamu na wanyama ambao walikuwa nje lakini haikuwaathiri Waisraeli waliokuwa Gosheni. (Kut 9:18-26; Zb 78:47, 48; 105:32, 33) Baadaye, katika nchi ya Ahadi, Waisraeli wakiwa chini ya uongozi wa Yoshua, walipowasaidia Wagibeoni waliokuwa wakishambuliwa na majeshi ya muungano ya wafalme watano wa Waamori, Yehova alitumia mvua ya mawe kuwaangamiza Waamori hao. Katika pindi hii idadi kubwa zaidi iliuawa na mvua ya mawe kuliko waliouawa na majeshi ya Waisraeli.—Yos 10:3-7, 11.
OKTOBA 18-24
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOSHUA 12-14
Hazina za Kiroho
it-1 902-903
Gebali
Yehova alitia ndani “nchi ya Wagebali” katika orodha ya maeneo ambayo hayakuwa yametwaliwa na Waisraeli katika siku ya Yoshua. (Yos 13:1-5) Wachambuzi wanatumia huo kuwa mfano wa ukosefu wa upatano kwa sababu jiji la Gebali lilikuwa mbali sana Kaskazini ya Israeli (kilomita 100 hivi Kaskazini ya Dani) na huenda hakuna wakati ambapo liliwahi kumilikiwa na Waisraeli. Wasomi fulani wamependekeza kwamba huenda maandishi ya Kiebrania katika mstari huo yalifutika na wanasema simulizi hilo zamani lilisema “nchi iliyo kando ya Lebanoni,” au ‘hadi kwenye mpaka wa Gebali.’ Hata hivyo, ni vizuri kukumbuka kwamba ahadi ambayo Yehova alitoa kwenye Yoshua 13:2-7 ilikuwa yenye masharti. Hivyo, huenda Waisraeli hawakumiliki Gebali kwa sababu ya kutotii kwao.—Linganisha Yos 23:12, 13.
OKTOBA 25-31
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOSHUA 15-17
“Linda Urithi Wako Wenye Thamani”
it-1 1083 ¶3
Hebroni
Kampeni ya Waisraeli kusini mwa Kanaani ilipokuwa ikiendelea wakaaji wa Hebroni kutia ndani mfalme wao (huenda yule aliyemrithi Hohamu), waliangamizwa. (Yos 10:36, 37) Hata hivyo, ingawa Waisraeli wakiwa chini ya Yoshua walivunja nguvu za Kanaani, inaonekana kwamba hawakuweka kambi za kijeshi moja kwa moja ili kulinda majiji waliyoshinda. Inaonekana kwamba Waisraeli walipokuwa wakipigana katika maeneo mengine, Waanaki walirudi kwenye makao yao ya Hebroni na hivyo kumfanya Kalebu (au wana wa Yuda walioongozwa na Kalebu) wapigane ili kupata jiji hilo muda fulani baadaye. (Yos 11:21-23; 14:12-15; 15:13, 14; Amu 1:10) Ingawa mwanzoni Kalebu wa kabila la Yuda alipewa jiji la Hebroni, baadaye jiji hilo lilitakaswa na kuwa jiji la makimbilio. Lilikuwa pia jiji la kikuhani. Hata hivyo, “mashamba ya jiji hilo [Hebroni]” na vijiji vyake vilikuwa urithi wa Kalebu.—Yos 14:13, 14; 20:7; 21:9-13.
it-1 848
Kazi za Kulazimishwa
Inaonekana “kazi za kulazimishwa” (Kiebrania, mas) zilikuwepo sana nyakati za Biblia, kwa kuwa watu walioshindwa katika vita walitumiwa kama watumwa. (Kum 20:11; Yos 16:10; 17:13; Est 10:1; Isa 31:8; Omb 1:1) Waisraeli walipokuwa watumwa wa kazi za kulazimishwa, wasimamizi Wamisri waliwaonea na kuwalazimisha wajenge majiji yenye maghala, yaani, Pithomu na Raamsesi. (Kut 1:11-14) Kisha, walipoingia kwenye nchi ya Ahadi, badala ya kufuata maagizo waliyopewa na Yehova ya kuwafukuza wakaaji wote wa Kanaani na kuwaangamiza, Waisraeli waliamua kuwafanyisha kazi kama watumwa. Walipata matokeo mabaya na kuanza kuabudu miungu wa uwongo. (Yos 16:10; Amu 1:28; 2:3, 11, 12) Mfalme Sulemani aliendelea kuwatoza ushuru wazao wa Wakanaani, yaani, Waamori, Wahiti, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi ili wafanye kazi ya kulazimishwa kama watumwa.—1Fa 9:20, 21.
it-1 402 ¶3
Kanaani
Ingawa Wakanaani wengi hawakuuawa wakati wa vita na walikataa kutiishwa, bado ingeweza kusemwa kwamba ‘Yehova aliwapa Waisraeli nchi yote ambayo aliapa angewapa mababu zao,’ kwamba aliwapa “amani katika nchi yote,” na kwamba “hakuna ahadi hata moja iliyokosa kutimia kati ya ahadi zote nzuri ambazo Yehova aliwaahidi Waisraeli; zote zilitimia.” (Yos 21:43-45) Maadui wote waliowazunguka Waisraeli waliogopa sana na hivyo hawangeweza kuwa tisho kwa usalama wao. Hapo awali Mungu alisema kwamba angewafukuza Wakanaani “hatua kwa hatua” ili wanyama-mwitu wasiongezeke na kuijaza nchi iliyokuwa ukiwa. (Kut 23:29, 30; Kum 7:22) Licha ya kwamba Wakanaani walikuwa na vifaa vya vita vya hali ya juu kama vile magari ya vita yenye miundu ya chuma, kushindwa kwa Waisraeli kumiliki maeneo mengine hakukuwa kwa sababu ya Yehova kushindwa kutimiza ahadi yake. (Yos 17:16-18; Amu 4:13) Badala yake, masimulizi yanaonyesha kwamba pindi chache ambazo Waisraeli walishindwa vita, zilisababishwa na ukosefu wa uaminifu wa Waisraeli wenyewe.—Hes 14:44, 45; Yos 7:1-12.