Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
© 2023 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
JULAI 3-9
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | EZRA 4-6
“Msiingilie Kazi”
w86 2/1 29, sanduku ¶2-3
Macho ya Yehova “Yalithibitika Kuwa Juu ya Wanaume Wazee”
Baada ya Wayahudi kurudi kutoka Babiloni, kipindi cha miaka 16 kisicho na utendaji kilianza. Manabii Hagai na Zekaria waliwachochea Wayahudi wawe na bidii tena na kazi ya kujenga upya hekalu la Yehova ikaanza tena. Hata hivyo, baada ya muda mfupi kazi hiyo ilipingwa na maofisa wa Uajemi. Wapinzani hao waliuliza hivi: “Ni nani aliyewaagiza mjenge nyumba hii?”—Ezra 5:1-3.
Jibu la swali hilo lilikuwa muhimu. Ikiwa wazee hao wangekubali kutishwa, kazi hiyo ya kujenga upya hekalu ingekoma. Kwa upande mwingine, ikiwa wazee wangewakasirisha maofisa hao, kazi hiyo ingepigwa marufuku mara moja. Kwa hiyo, wazee (bila shaka, wakiongozwa na Gavana Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua) walijibu kwa busara na uthabiti. Waliwakumbusha maofisa hao kuhusu agizo la Koreshi lililokuwa limesahaulika lililotolewa miaka mingi iliyopita, ambalo liliwapa Wayahudi ruhusa ya kifalme ya kufanya kazi hiyo. Kwa kuwa maofisa hao walifahamu sera ya Uajemi ya kutobadili sheria iliyowekwa, kwa werevu waliamua kutopinga agizo la kifalme. Hivyo, kazi iliruhusiwa kuendelea mpaka wakati ambapo baadaye Mfalme Dario alitoa agizo lake rasmi lililounga mkono kazi hiyo!—Ezra 5:11-17; 6:6-12.
JULAI 10-16
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | EZRA 7-8
“Matendo ya Ezra Yalimletea Yehova Heshima”
it-1 1158 ¶4
Unyenyekevu
Hutoa Mwongozo Unaofaa. Mtu anayejinyenyekeza mbele za Mungu anaweza kutarajia kupata mwongozo kutoka kwa Mungu. Ezra alikuwa na wajibu mzito wa kuwaongoza wanaume zaidi ya 1,500 kutoka Babiloni hadi Yerusalemu, bila kuhesabu makuhani, Wanethini, na wanawake na watoto. Kwa kuongezea, walibeba kiasi kikubwa cha dhahabu na fedha kwa ajili ya kurembesha hekalu lililokuwa Yerusalemu. Walihitaji ulinzi wakati wa safari, lakini Ezra hakutaka kumwomba mfalme wa Uajemi wanajeshi wa kuandaa ulinzi kwa sababu hilo lingeonyesha anategemea uwezo wa wanadamu. Isitoshe, alikuwa amemwambia Mfalme: “Mkono mwema wa Mungu wetu uko juu ya wale wote wanaomtafuta.” Kwa hiyo, aliagiza watu wafunge na kujinyenyekeza mbele za Yehova. Walimwomba Mungu msaada, naye aliwasikiliza na kuwapa ulinzi kutokana na maadui na wavamizi njiani hivi kwamba walifika Yerusalemu wakiwa salama. (Ezr 8:1-14, 21-32) Mungu alimwonyesha nabii Danieli kibali akiwa uhamishoni Babiloni kwa kumtuma malaika aliyemwonyesha maono, kwa sababu Danieli alijinyenyekeza mbele za Mungu na akatafuta mwongozo na uelewaji kutoka kwake.—Da 10:12.
AGOSTI 14-20
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | NEHEMIA 8-9
Hazina za Kiroho
it-1 145 ¶2
Kiaramu
Miaka kadhaa baada ya Wayahudi kurudi kutoka uhamishoni Babiloni, kuhani Ezra alisoma kitabu cha Sheria mbele ya Wayahudi waliokusanyika Yerusalemu na Walawi mbalimbali waliwafafanulia watu sheria hiyo. Nehemia 8:8 inasema: “Wakaendelea kukisoma kitabu hicho kwa sauti kubwa, wakaisoma Sheria ya Mungu wa kweli, huku wakiifafanua waziwazi na kueleza maana yake; hivyo wakawasaidia watu kuelewa mambo yaliyokuwa yakisomwa.” Ufafanuzi huo huenda ulihusisha kukalimani maneno ya Kiebrania katika Kiaramu, kwa sababu inaonekana Waisraeli walikuwa wamezoea kutumia Kiaramu walipokuwa Babiloni. Bila shaka, ufafanuzi huo, ulihusisha pia kuelewesha maana ili Wayahudi, hata ingawa walijua Kiebrania, waelewe vizuri zaidi uzito wa kile kilichokuwa kinasomwa.
AGOSTI 28–SEPTEMBA 3
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | NEHEMIA 12-13
“Uwe Mshikamanifu kwa Yehova Unapochagua Marafiki”
it-1 95 ¶5
Waamoni
Baada ya Tobia kufukuzwa kutoka hekaluni, Sheria ya Mungu katika Kumbukumbu la Torati 23:3-6 iliyokataza Waamoni na Wamoabu kuingia ndani ya kutaniko la Waisraeli ilisomwa na kutekelezwa. (Ne 13:1-3) Inaeleweka kwamba Sheria hiyo, iliyowekwa miaka 1,000 hivi mapema kwa sababu Waamoni na Wamoabu walikataa kuwasaidia Waisraeli walipokuwa wakielekea kwenye Nchi ya Ahadi, ilimaanisha kwamba kisheria watu hao hawangeweza kuwa raia kamili wa taifa la Israeli na kupata faida au mapendeleo yanayotokana na kuwa raia. Hilo halimaanishi kwamba Waamoni na Wamoabu mmoja mmoja hawangeweza kushirikiana na Waisraeli au kuishi miongoni mwao na hivyo kufaidika kutokana na baraka ambazo Mungu aliwapa watu wake. Tunaweza kuona hilo kutokana na kuongezwa kwa Seleki, aliyetajwa mapema, katika orodha ya mashujaa wa Daudi, na kutokana na simulizi la Ruthu Mmoabu.—Ru 1:4, 16-18.
Hazina za Kiroho
it-2 452 ¶9
Muziki
Kuimba hekaluni kulionwa kuwa jambo muhimu sana. Hilo linaweza kuonekana kutokana na marejeo mengi ya Maandiko yanayowataja waimbaji, na pia kutokana na kwamba “hawakupewa kazi nyingine” zilizofanywa na Walawi wengine, ili wajitoe kikamili katika huduma yao. (1Nya 9:33) Waliendelea kuwa kikundi cha pekee cha Walawi, na hilo linaonekana kwa sababu wanaorodheshwa tofauti na wengine waliorudi kutoka Babiloni. (Ezr 2:40, 41) Hata Mfalme Artashasta (Longimano) wa Uajemi, alitumia mamlaka yake kwa niaba yao kwa kuagiza kwamba wao pamoja na vikundi vingine vya pekee visitozwe ‘kodi, wala ushuru, wala ada.’ (Ezr 7:24) Baadaye, Mfalme alitoa amri kwamba kulipaswa kuwa na “mpango hususa kuhusu mahitaji yao ya kila siku.” Ingawa inasemekana kwamba Artashasta ndiye aliyeota agizo hilo, uwezekano mkubwa ni kwamba lilitolewa na Ezra akitumia mamlaka aliyopewa na Mfalme Artashasta. (Ne 11:23; Ezr 7:18-26) Hivyo, inaeleweka kwamba ingawa waimbaji wote walikuwa Walawi, Biblia inawarejelea kuwa kikundi maalumu, inaposema “waimbaji, na Walawi.”—Ne 7:1; 13:10.