Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Mfalme wa Kaskazini” Katika Wakati wa Mwisho
    Mnara wa Mlinzi (Funzo)—2020 | Mei
    • MAKALA YA 19

      “Mfalme wa Kaskazini” Katika Wakati wa Mwisho

      “Wakati wa mwisho mfalme wa kusini atasukumana naye [mfalme wa kaskazini].”—DAN. 11:40.

      WIMBO 150 Mtafute Mungu Upate Ukombozi

      MUHTASARIa

      1. Unabii wa Biblia unatusaidia kujua nini?

      NI NINI kitakachowapata watu wa Yehova hivi karibuni? Hatuhitaji kukisia. Unabii wa Biblia unatuambia kuhusu matukio makubwa ambayo yatatugusa sisi sote. Kuna unabii mmoja hususa unaotusaidia kujua mambo fulani ambayo baadhi ya serikali zenye nguvu duniani zitafanya. Unabii huo unaopatikana kwenye Danieli sura ya 11, unaonyesha historia ya wafalme wawili wanaopingana, yaani, mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Tayari sehemu kubwa ya unabii huo imetimia, hivyo tunaweza kuwa na hakika kwamba sehemu iliyobaki itatimia pia.

      2. Kama inavyotajwa kwenye Mwanzo 3:15 na Ufunuo 11:7 na 12:17, ni mambo gani muhimu ambayo ni lazima tukumbuke tunapojifunza unabii wa Danieli?

      2 Ili kuelewa unabii wa Danieli sura ya 11, tunapaswa kukumbuka kwamba unabii huo unawahusu tu watawala na serikali ambazo zimewahi kuwaathiri watu wa Mungu moja kwa moja. Na ingawa watumishi wa Mungu ni wachache ukilinganisha na idadi ya watu duniani, kwa kawaida wao hujikuta wakiwa wamehusishwa kwa njia kubwa katika matukio makubwa ya ulimwengu. Kwa nini? Kwa sababu Shetani na mfumo wake wote una lengo moja kuu, yaani, kuwaangamiza wale wanaomtumikia Yehova na Yesu. (Soma Mwanzo 3:15 na Ufunuo 11:7; 12:17.) Pia, lazima unabii wa Danieli upatane na unabii mwingine katika Neno la Mungu. Ukweli ni kwamba tunaweza kuelewa kwa usahihi unabii wa Danieli ikiwa tu tutaulinganisha na vitabu vingine vya Biblia.

      3. Tutazungumzia nini katika makala hii na ile itakayofuata?

      3 Tukiwa na hayo akilini, sasa tutazungumzia Danieli 11:25-39. Tutaona ni nani aliyekuwa mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini kuanzia mwaka wa 1870 hadi 1991, na tutaona kwa nini inafaa turekebishe uelewaji wetu kuhusu sehemu fulani ya unabii huo. Katika makala itakayofuata, tutazungumzia Danieli 11:40–12:1, na tutarekebisha uelewaji wetu kuhusu mambo yanayofunuliwa na sehemu hiyo ya unabii yanayohusu kipindi cha wakati kilichoanza mwaka wa 1991 hadi wakati wa vita vya Har–Magedoni. Unapojifunza makala hizi mbili, itafaa uchunguze chati “Wafalme Wanaopingana Katika Wakati wa Mwisho.” Hata hivyo, kwanza, tunahitaji kuwatambua wafalme hao wawili katika unabii huo.

      KUMTAMBUA MFALME WA KASKAZINI NA MFALME WA KUSINI

      4. Ni mambo gani matatu yatakayotusaidia kumtambua mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini?

      4 Mwanzoni, majina “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” yalikuwa majina yaliyotumiwa kutambulisha serikali za kisiasa zilizokuwa upande wa kaskazini na wa kusini wa nchi halisi ya Israeli. Kwa nini tunasema hivyo? Ona ujumbe huu ambao malaika alimpa Danieli: “Nimekuja kukuelewesha mambo yatakayowapata watu wako katika kipindi cha mwisho cha zile siku.” (Dan. 10:14) Kufikia Pentekoste 33 W.K., taifa halisi la Israeli ndilo lililokuwa watu wa Mungu. Hata hivyo, kuanzia wakati huo na kuendelea, Yehova alitambulisha wazi kwamba wanafunzi waaminifu wa Yesu ndio waliokuwa watu wake. Hivyo, unabii mwingi wa Danieli sura ya 11 hauhusu taifa halisi la Israeli, bali unawahusu wafuasi wa Kristo. (Mdo. 2:1-4; Rom. 9:6-8; Gal. 6:15, 16) Na kadiri muda ulivyopita, watawala au serikali tofauti-tofauti zilitambuliwa kuwa mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Hata hivyo, watawala hao wote walifanana kwa njia kadhaa. Kwanza, wafalme hao waliwatawala au kuwatesa watu wa Mungu. Pili, walionyesha kwamba wanamchukia Yehova, Mungu wa kweli kupitia jinsi walivyowatendea watu wa Mungu. Na tatu, wafalme hao wawili walikuwa wakipambana wao kwa wao ili kupata mamlaka.

      5. Je, ingewezekana kumtambua mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini kati ya mwaka wa 100 W.K. na mwaka wa 1870? Eleza.

      5 Wakati fulani katika karne ya pili W.K., Wakristo wengi wa uwongo walianza kuingia katika kutaniko la kweli la Kikristo, nao wakaanza kufundisha mafundisho ya kipagani na kuficha kweli za Neno la Mungu. Tangu wakati huo hadi kufikia mwishoni mwa karne ya 19 hakukuwa na kikundi chochote kilichopangwa cha watumishi wa Mungu duniani. Magugu ya Wakristo wa uwongo yalisitawi na ikawa vigumu kuwatambua Wakristo wa kweli. (Mt. 13:36-43) Kwa nini ni muhimu kujua jambo hilo? Kwa sababu jambo hilo linaonyesha kwamba mambo tunayosoma kuhusu mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini hayakuwahusu watawala au falme zilizokuwa zikitawala kuanzia mwaka wa 100 W.K. hadi mwaka wa 1870. Wakati huo, hakukuwa na kikundi kilichopangwa cha watu wa Mungu ambacho wangeweza kukishambulia.b Hata hivyo, muda mfupi baada ya mwaka wa 1870, ingewezekana tena kumtambua mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Kwa nini?

      6. Ni wakati gani watu wa Mungu walianza tena kumtumikia wakiwa kikundi? Eleza.

      6 Kuanzia mwaka wa 1870 na kuendelea, watu wa Mungu walianza kumtumikia wakiwa kikundi. Mwaka huo Charles T. Russell na wenzake walianzisha kikundi cha kujifunza Biblia. Ndugu Russell pamoja na wale alioshirikiana nao kwa ukaribu walitenda kama mjumbe aliyekuwa ametabiriwa ambaye ‘angefungua njia’ kabla ya Ufalme wa Kimasihi kusimamishwa. (Mal. 3:1) Kwa mara nyingine tena, kulikuwa na kikundi cha watu waliomtumikia Yehova kwa njia sahihi! Je, kulikuwa na serikali zozote za ulimwengu wakati huo ambazo ziliwatawala au kuwatesa watumishi wa Mungu? Fikiria mambo yafuatayo.

      MFALME WA KUSINI NI NANI?

      7. Ni nani aliyekuwa mfalme wa kusini, kufikia muda fulani baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu kuanza?

      7 Kufikia mwaka wa 1870, tayari nchi ya Uingereza ndiyo iliyokuwa milki kubwa zaidi duniani na yenye jeshi lenye nguvu nyingi zaidi. Katika unabii wa Danieli, milki hiyo inafananishwa na pembe ndogo ambayo ilishinda pembe nyingine tatu, yaani, Ufaransa, Hispania, na Uholanzi. (Dan. 7:7, 8) Pembe hiyo ndogo ndiyo iliyokuwa mfalme wa kusini kufikia muda fulani baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu kuanza. Wakati huo, tayari Marekani ilikuwa nchi tajiri zaidi duniani na ilikuwa imeanza kushirikiana kwa ukaribu na Uingereza.

      8. Ni nani ambaye amekuwa mfalme wa kusini katika kipindi chote cha siku za mwisho?

      8 Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, serikali ya Marekani na Uingereza ziliungana na kufanyiza jeshi lenye nguvu nyingi sana. Wakati huo, Uingereza na koloni lake la zamani, Marekani, ziliungana na kutokeza Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Kama Danieli alivyotabiri, serikali hiyo ilikuwa imejikusanyia “jeshi kubwa kupita kiasi, tena lenye nguvu.” (Dan. 11:25) Katika kipindi cha siku za mwisho, muungano wa Uingereza na Marekani umekuwa ndio mfalme wa kusini.c Hata hivyo, ni nani aliyechukua nafasi ya mfalme wa kaskazini?

      Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani Katika Unabii wa Biblia

      Mfalme wa kusini, yaani, Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani anafafanuliwa kwa njia tofauti-tofauti katika unabii mbalimbali wa Biblia. Anafafanuliwa kuwa . . .

      • Miguu ya chuma na udongo.

        miguu ya chuma na udongo (Dan. 2:41-43)

      • Kichwa cha mnyama aliye na pembe. Pembe ndogo yenye macho na mdomo inajitokeza miongoni mwa pembe za mnyama huyo.

        pembe iliyojitokeza kwenye kichwa cha mnyama mwenye kuogopesha (Dan. 7:7, 8)

      • Mnyama wa mwituni aliye na pembe kumi na vichwa saba.

        kichwa cha saba cha yule mnyama wa mwituni (Ufu. 13:1)

      • Mnyama mwenye pembe mbili.

        mnyama wa mwituni mwenye pembe mbili (Ufu. 13:11-15)

      • Majengo ya serikali yakifananisha ile Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani.

        “yule nabii wa uwongo” (Ufu. 19:20)

      MFALME WA KASKAZINI AIBUKA TENA

      9. Mfalme wa kaskazini aliibuka tena lini, na andiko la Danieli 11:25 lilitimizwaje?

      9 Katika mwaka wa 1871, mwaka mmoja baada ya Russell na wenzake kuanzisha kikundi cha kujifunza Biblia, mfalme wa kaskazini aliibuka tena. Mwaka huo, Otto von Bismarck alichangia kwa kiwango kikubwa kuanzishwa kwa Milki ya Ujerumani. Mfalme Wilhelm wa Kwanza wa Prussia akawa maliki wa kwanza wa milki hiyo, naye akamteua Bismarck kuwa waziri mkuu wa kwanza.d Katika miaka iliyofuata, Ujerumani ikawa serikali ya kikoloni ikitawala nchi za Afrika na nchi zilizo kwenye Bahari ya Pasifiki, na ikaanza kupambana na Uingereza ili kupata mamlaka zaidi. (Soma Danieli 11:25.) Milki ya Ujerumani iliunda jeshi lenye nguvu nyingi sana na jeshi lake la majini lilikuwa la pili kwa ukubwa duniani. Ujerumani ilitumia majeshi hayo kushambulia maadui wake katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.

      10. Andiko la Danieli 11:25b, 26 lilitimizwaje?

      10 Kisha Danieli anatabiri kuhusu kile kitakachoipata Milki ya Ujerumani na jeshi lake. Unabii huo unasema kwamba mfalme wa kaskazini “hatasimama.” Kwa nini? “Kwa sababu watapanga njama dhidi yake. Na wale wanaokula vyakula vyake bora watasababisha aanguke.” (Dan. 11:25b, 26a) Katika siku za Danieli, wale waliokula “vyakula bora ambavyo [mfalme] mwenyewe alikula” walitia ndani maofisa wa mfalme ‘waliomtumikia mfalme.’ (Dan. 1:5) Unabii huo unazungumza kuhusu nani? Unawahusu maofisa wa vyeo vya juu wa Milki ya Ujerumani—kutia ndani majenerali na washauri wa mambo ya kijeshi wa maliki—ambao hatimaye walipindua utawala wa maliki wa Ujerumani.e Unabii wa Danieli haukutabiri tu kuhusu kuanguka kwa milki hiyo, bali pia unataja matokeo ya vita kati ya mfalme wa kaskazini na wa kusini. Unabii huo unasema hivi kuhusu mfalme wa kaskazini: “Na jeshi lake litafagiliwa mbali, na wengi watauawa.” (Dan. 11:26b) Kama ilivyotabiriwa, jeshi la Ujerumani ‘lilifagiliwa mbali’ katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, na watu wengi ‘waliuawa.’ Watu wengi sana walikufa katika vita hivyo kuliko vita vingine vyovyote kabla ya hapo.

      11. Mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini walifanya nini?

      11 Andiko la Danieli 11:27, 28 linaeleza kuhusu mambo yaliyotukia kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Unabii huo unasema kwamba mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini “wataketi kwenye meza moja wakiambiana uwongo.” Pia, unasema kwamba mfalme wa kaskazini angejikusanyia “mali nyingi.” Na hivyo ndivyo ilivyokuwa. Serikali ya Ujerumani na ya Uingereza zilisema kwamba walitaka kuwe na amani, lakini maneno yao yalithibitika kuwa ya uwongo vita vilipozuka katika mwaka wa 1914. Vilevile, kufikia mwaka wa 1914, Ujerumani ilikuwa nchi ya pili kwa utajiri duniani. Kisha, Ujerumani ikapigana vita na mfalme wa kusini lakini ikashindwa, na hivyo kutimiza unabii wa Danieli 11:29 na sehemu ya kwanza ya mstari wa 30.

      WAFALME HAO WAPAMBANA NA WATU WA MUNGU

      12. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini walifanya nini?

      12 Tangu mwaka wa 1914 na kuendelea, wafalme hao wawili wamezidisha mashambulizi kati yao na dhidi ya watu wa Mungu. Kwa mfano, katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, serikali ya Ujerumani na serikali ya Uingereza ziliwatesa watumishi wa Mungu waliokataa kwenda vitani. Nayo serikali ya Marekani ikawatupa gerezani wale waliokuwa wakisimamia kazi ya kuhubiri. Mateso hayo yalitimiza unabii wa Ufunuo 11:7-10.

      13. Mfalme wa kaskazini alifanya nini katika miaka ya 1930 na wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu?

      13 Kisha, katika miaka ya 1930 na hasa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, mfalme wa kaskazini aliwashambulia watu wa Mungu bila huruma. Halafu chama cha Nazi kilipochukua mamlaka nchini Ujerumani, Hitler na wafuasi wake walipiga marufuku kazi ya watu wa Mungu. Wapinzani hao waliwaua mamia ya watu wa Yehova na kuwapeleka maelfu zaidi kwenye kambi za mateso. Danieli alikuwa ametabiri kuhusu matukio hayo. Mfalme wa kaskazini alifanikiwa ‘kupachafua patakatifu’ na “kuondoa ile dhabihu inayotolewa daima” kwa kuwawekea watu wa Mungu vizuizi vikali ili wasilisifu jina la Yehova hadharani. (Dan. 11:30b, 31a) Hata Hitler aliyekuwa kiongozi wao aliapa kuwafutilia mbali watu wa Mungu nchini Ujerumani.

      MFALME MPYA WA KASKAZINI AIBUKA

      14. Ni nani aliyekuwa mfalme wa kaskazini baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu? Eleza.

      14 Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, serikali ya Kikomunisti ya Muungano wa Sovieti ilianza kutawala maeneo makubwa iliyokuwa imeshinda kutoka kwa Ujerumani, nayo ikawa mfalme wa kaskazini. Kama ilivyokuwa kwa utawala wa kimabavu wa Wanazi, Muungano wa Sovieti uliwatesa sana wale wote waliotanguliza ibada yao kwa Mungu wa kweli, badala ya kujitiisha kikamili kwa serikali.

      15. Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kuisha, mfalme wa kaskazini alifanya nini?

      15 Muda mfupi baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kuisha, mfalme mpya wa kaskazini, yaani, Muungano wa Sovieti na nchi zilizounga mkono muungano huo, alianza kuwatesa vikali watu wa Mungu. Kama unabii wa Ufunuo 12:15-17 ulivyokuwa umeonyesha, mfalme huyo alipiga marufuku kazi yetu ya kuhubiri na kuwapeleka maelfu ya watu wa Yehova uhamishoni. Isitoshe, katika kipindi chote cha siku za mwisho, mfalme wa kaskazini ametapika “mto” wa mateso ili asimamishe kazi ya watu wa Mungu, lakini hajafanikiwa.f

      16. Muungano wa Sovieti ulitimizaje andiko la Danieli 11:37-39?

      16 Soma Danieli 11:37-39. Unabii huo ulitimia mfalme wa kaskazini alipokosa ‘kumjali Mungu wa baba zake.’ Jinsi gani? Muungano wa Sovieti ulikuwa na lengo la kufutilia mbali dini, hivyo ulijaribu kuyanyang’anya mashirika ya kidini mamlaka yao. Ili kutimiza lengo hilo, tayari mwaka wa 1918 serikali ya Sovieti ilikuwa imetoa agizo ambalo liliweka msingi wa kuwafundisha wanafunzi shuleni wazo la kutokuwepo kwa Mungu. Mfalme huyo wa kaskazini ‘alimpaje utukufu mungu wa ngome’? Muungano wa Sovieti ulitumia pesa nyingi sana kuimarisha jeshi lake na kutengeneza maelfu ya silaha za nyuklia ili kuimarisha mamlaka yake. Mwishowe, mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini walijikusanyia silaha za kutosha na zenye nguvu zinazoweza kuangamiza mabilioni ya watu!

      USHIRIKIANO USIO WA KAWAIDA

      17. ‘Kile kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa’ ni nini?

      17 Mfalme wa kaskazini amemuunga mkono mfalme wa kusini katika jambo moja muhimu; ‘walisimamisha kile kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa.’ (Dan. 11:31) ‘Kitu hicho chenye kuchukiza sana’ ni shirika la Umoja wa Mataifa.

      18. Kwa nini shirika la Umoja wa Mataifa linatajwa kuwa ‘kitu chenye kuchukiza sana’?

      18 Shirika la Umoja wa Mataifa linatajwa kuwa ‘kitu chenye kuchukiza sana’ kwa sababu linadai kwamba linaweza kufanya jambo ambalo Ufalme wa Mungu pekee ndio unaoweza kufanya, yaani, kuleta amani duniani. Na unabii wa Danieli unataja kwamba kitu hicho chenye kuchukiza sana ‘kinasababisha ukiwa’ kwa sababu shirika la Umoja wa Mataifa litashambulia dini zote za uwongo na kuziangamiza.—Tazama chati “Wafalme Wanaopingana Katika Wakati wa Mwisho.”

      KWA NINI TUNAHITAJI KUJUA HISTORIA HIYO?

      19-20. (a) Kwa nini tunahitaji kuijua historia hiyo? (b) Tutajibu swali gani katika makala inayofuata?

      19 Tunahitaji kujua historia hiyo kwa sababu inathibitisha kwamba kuanzia miaka ya 1870 hadi mwanzoni mwa miaka ya 1990, unabii wa Danieli kuhusu mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini umetimizwa. Hivyo, tunaweza kuwa na imani kwamba sehemu iliyobaki ya unabii huo itatimia pia.

      20 Mwaka wa 1991, Muungano wa Sovieti ulianguka. Basi mfalme wa kaskazini ni nani leo? Makala inayofuata inajibu swali hilo.

      UNGEJIBUJE?

      • Ni mambo gani matatu yanayotusaidia kumtambua “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini”?

      • Ni nani aliyekuwa mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini kuanzia miaka ya 1870 hadi mwaka wa 1991?

      • Kwa nini tunahitaji kujua historia hiyo?

      WIMBO 128 Kuvumilia Mpaka Mwisho

      a Tunajionea uthibitisho kwamba unabii wa Danieli kuhusu “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” unaendelea kutimia. Tunawezaje kuwa na uhakika kuhusu jambo hilo? Na kwa nini tunahitaji kuelewa mambo yanayohusu unabii huo?

      b Hivyo, kutokana na maelezo hayo isingefaa kusema kwamba Maliki Mroma Aurelian (270-275 W.K.) alikuwa “mfalme wa kaskazini” au kwamba Malkia Zenobia (267-272 W.K.) alikuwa “mfalme wa kusini.” Ufafanuzi huo unarekebisha uelewaji uliochapishwa kwenye sura ya 13 na ya 14 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!

      c Tazama sanduku “Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani Katika Unabii wa Biblia.”

      d Mwaka wa 1890, Maliki Wilhelm wa Pili alimwondoa Bismarck madarakani.

      e Walifanya mambo mengi yaliyosababisha milki yao ianguke haraka. Kwa mfano, waliacha kumsaidia maliki, walivujisha siri kuhusu habari nyeti za vita, na kumlazimisha maliki ajiuzulu.

      f Kama andiko la Danieli 11:34 linavyoonyesha, Wakristo walioishi chini ya mfalme wa kaskazini walipata kiasi fulani cha utulivu kutokana na mateso waliyokuwa nayo. Kwa mfano, hilo lilitukia Muungano wa Sovieti ulipoanguka mwaka wa 1991.

  • Mfalme wa Kaskazini” Ni Nani Leo?
    Mnara wa Mlinzi (Funzo)—2020 | Mei
    • MAKALA YA 20

      “Mfalme wa Kaskazini” Ni Nani Leo?

      “Atasonga kufikia mwisho wake, na hakuna atakayemsaidia.” —DAN. 11:45.

      WIMBO 95 Nuru Inazidi Kuongezeka

      MUHTASARIa

      1-2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

      LEO, kuliko wakati mwingine wowote, kuna uthibitisho mwingi zaidi unaoonyesha kwamba tunaishi mwishoni mwa siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Hivi karibuni, Yehova na Yesu Kristo wataangamiza serikali zote zinazopinga Ufalme wa Mungu. Kabla ya jambo hilo kutokea, mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wataendelea kupambana wao kwa wao na dhidi ya watu wa Mungu.

      2 Katika makala hii, tutazungumzia unabii wa Danieli 11:40–12:1. Tutajifunza mfalme wa kaskazini ni nani leo, na kuzungumzia kwa nini tunaweza kukabiliana na matatizo ya wakati ujao tukiwa na uhakika.

      MFALME MPYA WA KASKAZINI AIBUKA

      3-4. Mfalme wa kaskazini ni nani leo? Eleza.

      3 Baada ya Muungano wa Sovieti kuvunjika mwaka wa 1991, watu wa Mungu katika eneo hilo kubwa walipata “msaada kidogo,” yaani, kipindi fulani cha uhuru. (Dan. 11:34) Kwa sababu hiyo, walifanikiwa kuhubiri kwa uhuru, na baada ya muda mfupi idadi ya wahubiri katika eneo hilo lililokuwa chini ya Ukomunisti ikaongezeka kufikia mamia ya maelfu. Lakini baada ya miaka kadhaa, serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono zikawa mfalme wa kaskazini. Kama tulivyojifunza katika makala iliyopita, ili serikali iweze kuwa mfalme wa kaskazini au wa kusini, ni lazima itimize mambo haya matatu: (1) iwatawale au kuwatesa watu wa Mungu, (2) ionyeshe kwa matendo yake kwamba ni adui ya Yehova na watu wake, na (3) ipambane na mfalme mwingine.

      4 Zifuatazo ni sababu zinazofanya tuseme kwamba mfalme wa kaskazini leo, ni serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono. (1) Zimewaathiri moja kwa moja watu wa Mungu kwa kupiga marufuku kazi ya kuhubiri na kuwatesa mamia ya maelfu ya ndugu na dada wanaoishi katika maeneo yaliyo chini ya mamlaka yao. (2) Matendo hayo yanaonyesha kwamba wanamchukia Yehova na watu wake. (3) Zimekuwa zikipambana na mfalme wa kusini, yaani, Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Acheni tuone jinsi serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono zimethibitika kuwa mfalme wa kaskazini.

      MFALME WA KASKAZINI NA MFALME WA KUSINI WAENDELEA KUSUKUMANA

      5. Andiko la Danieli 11:40-43 linafafanua kipindi gani cha wakati, na nini kinachotukia katika kipindi hicho?

      5 Soma Danieli 11:40-43. Sehemu hii ya unabii inazungumzia wakati wa mwisho. Unabii huu unazungumza kuhusu pambano kati ya mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Kama Danieli alivyotabiri, katika wakati wa mwisho, mfalme wa kusini “atasukumana” na mfalme wa kaskazini au “atamenyana” naye.—Dan. 11:40; maelezo ya chini.

      6. Kuna uthibitisho gani kwamba mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wamekuwa wakisukumana?

      6 Mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wanaendelea kushindana ili serikali zao ziwe zenye nguvu zaidi duniani. Kwa mfano, fikiria kilichotukia baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu wakati ambapo Muungano wa Sovieti na nchi zilizouunga mkono zilipokuwa na mamlaka kubwa juu ya sehemu nyingi za Ulaya. Matendo ya mfalme wa kaskazini yalimlazimisha mfalme wa kusini aanzishe muungano wa kijeshi wa kimataifa, unaoitwa NATO. Mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wanaendelea kushindana wakitumia pesa nyingi ili kujipatia silaha na jeshi lenye nguvu. Mfalme wa kaskazini alipigana na mpinzani wake kwa kuunga mkono upande tofauti katika vita na maasi yaliyokuwa yakiendelea barani Afrika, Asia, na Amerika ya Latini. Katika miaka ya hivi karibuni mamlaka au nguvu ya serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono imeongezeka kotekote duniani. Pia, mfalme wa kaskazini amemshambulia mfalme wa kusini kwa kutumia kompyuta. Wafalme hao wamekuwa wakilaumiana wenyewe kwa wenyewe kwamba wametumia programu za kompyuta zilizo na madhara ambazo zimekusudiwa kuharibu mifumo yao ya kiuchumi na ya kisiasa. Na kama Danieli alivyotabiri, mfalme wa kaskazini anaendelea kuwashambulia watu wa Mungu.—Dan. 11:41.

      MFALME WA KASKAZINI AINGIA KATIKA “NCHI YA LILE PAMBO”

      7. “Nchi ya lile Pambo” ni nini?

      7 Andiko la Danieli 11:41 linasema kwamba mfalme wa kaskazini ataingia katika “nchi ya lile Pambo.” Ni nchi gani hiyo? Katika nyakati za kale, nchi halisi ya Israeli ilionwa kuwa nchi “nzuri sana kuliko nchi zote.” (Eze. 20:6) Lakini jambo hususa lililoifanya nchi hiyo iwe ya pekee sana ni kwamba ibada ya kweli iliendelezwa humo. Tangu Pentekoste 33 W.K., “nchi” hiyo si eneo fulani halisi la kijiografia; hapana, kwa sababu watu wa Yehova wameenea kotekote duniani. Badala yake, leo “nchi ya lile Pambo” ni utendaji wote wa watu wa Yehova unaotia ndani mambo kama vile ibada yao kwa Yehova kupitia mikutano na huduma ya shambani.

      8. Mfalme wa kaskazini ameingiaje katika “nchi ya lile Pambo”?

      8 Katika kipindi cha siku za mwisho, mfalme wa kaskazini ameingia tena na tena katika “nchi ya lile Pambo.” Kwa mfano, Ujerumani ya Wanazi ilipokuwa mfalme wa kaskazini, na hasa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, mfalme huyo aliingia katika “nchi ya lile Pambo” kwa kuwatesa na kuwaua watu wa Mungu. Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, wakati Muungano wa Sovieti ulipokuwa mfalme wa kaskazini, mfalme huyo aliingia katika “nchi ya lile Pambo” kwa kuwatesa watu wa Mungu na kuwapeleka uhamishoni.

      9. Katika miaka ya karibuni, serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono zimeingiaje katika “nchi ya lile Pambo”?

      9 Pia, katika miaka ya hivi karibuni, Serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono zimeingia katika “nchi ya lile Pambo.” Jinsi gani? Katika mwaka wa 2017, mfalme huyo wa sasa wa kaskazini alipiga marufuku kazi ya watu wa Yehova na kuwatupa gerezani baadhi ya ndugu na dada zetu. Pia, aliyapiga marufuku machapisho yetu, kutia ndani Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Isitoshe, alichukua kwa lazima ofisi yetu ya tawi huko Urusi na pia Majumba ya Ufalme na Majumba ya Makusanyiko. Baada ya vitendo hivyo, katika mwaka wa 2018 Baraza Linaloongoza lilitambulisha serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono kuwa mfalme wa kaskazini. Hata wanapoteswa vikali, watu wa Yehova hawatajihusisha kwa vyovyote na vitendo vya kujaribu kupindua au kubadili serikali za wanadamu. Badala yake, wanafuata shauri la Biblia la kusali kwa ajili ya “wote wenye vyeo vya juu,” hasa wanapofanya maamuzi yanayoweza kuathiri uhuru wa ibada.—1 Tim. 2:1, 2.

      JE, MFALME WA KASKAZINI ATAMSHINDA MFALME WA KUSINI?

      10. Je, mfalme wa kaskazini atamshinda mfalme wa kusini? Eleza.

      10 Unabii wa Danieli 11:40-45 unakazia hasa utendaji wa mfalme wa kaskazini. Je, hilo linamaanisha kwamba mfalme huyo atamshinda mfalme wa kusini? Hapana. Mfalme wa kusini atakuwa angali “hai” Yehova na Yesu watakapoangamiza serikali zote za wanadamu katika vita vya Har–Magedoni. (Ufu. 19:20) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika huo? Fikiria mambo yanayotajwa katika unabii wa Danieli na Ufunuo.

      Jiwe linalotoka mlimani linapiga sanamu kubwa.

      Katika vita vya Har–​Magedoni, Ufalme wa Mungu, ambao unalinganishwa na jiwe, utakomesha utawala wa wanadamu, ambao unafananishwa na sanamu kubwa (Tazama, fungu la 11)

      11. Andiko la Danieli 2:43-45 linaonyesha nini? (Tazama picha kwenye jalada.)

      11 Soma Danieli 2:43-45. Nabii Danieli anafafanua mfululizo wa serikali za wanadamu ambazo zimewaathiri watu wa Mungu. Serikali hizo zinafananishwa na sehemu mbalimbali za sanamu kubwa sana. Serikali ya mwisho ya wanadamu katika sanamu hiyo imefananishwa na miguu iliyofanyizwa kwa chuma kilichochanganyika na udongo. Miguu hiyo inafananisha Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Unabii huo unaonyesha kwamba serikali hiyo itakuwa bado ikitawala Ufalme wa Mungu utakapokuja na kuziangamiza serikali za wanadamu.

      12. Kichwa cha saba cha mnyama wa mwituni kinafananisha nini, na kwa nini ni muhimu kujua hilo?

      12 Mtume Yohana pia anaeleza kuhusu mfululizo wa serikali za ulimwengu ambazo zimewatawala watu wa Yehova. Katika unabii wa Yohana, serikali hizo zinafananishwa na mnyama wa mwituni mwenye vichwa saba. Kichwa cha saba cha mnyama huyo kinafananisha Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Hilo ni jambo muhimu kwa sababu mnyama huyo hatajwi kwamba atatokeza vichwa vingine. Kichwa cha saba cha mnyama huyo kitakuwa bado kinatawala wakati Kristo na majeshi yake ya mbinguni watakapokiangamiza pamoja na sehemu nyingine zote za mnyama huyo.b​—Ufu. 13:1, 2; 17:13, 14.

      MFALME WA KASKAZINI ATAFANYA NINI HIVI KARIBUNI?

      13-14. “Gogu wa nchi ya Magogu” ni nani, na huenda ni nini kitakachomchochea awashambulie watu wa Mungu?

      13 Ezekieli aliandika unabii unaotueleza mambo ambayo huenda yatatukia kabla ya mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini kuharibiwa. Inaonekana kwamba unabii wa Ezekieli 38:10-23; Danieli 2:43-45; 11:44–12:1; na Ufunuo 16:13-16, 21 unazungumza kuhusu matukio yanayotukia katika kipindi kilekile cha wakati. Ikiwa hilo ni kweli, inaonekana tunaweza kutarajia kwamba mambo yafuatayo yatatokea.

      14 Wakati fulani baada ya dhiki kuu kuanza, “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” wataanzisha muungano wa mataifa. (Ufu. 16:13, 14; 19:19) Biblia inauita muungano huo wa mataifa “Gogu wa nchi ya Magogu.” (Eze. 38:2) Muungano huo wa mataifa utawashambulia watu wote wa Mungu na kujaribu kuwaangamiza kabisa. Ni nini kitakachoyachochea mataifa yawashambulie watu wa Mungu? Akizungumza kuhusu wakati huo, mtume Yohana aliona dhoruba ya mvua kubwa ya mawe isiyo ya kawaida ikiwanyeshea maadui wa Mungu. Huenda mvua hiyo ya mfano ya mawe ikafananisha ujumbe mkali wa hukumu utakaotolewa na watu wa Yehova. Huenda ujumbe huo utamfanya Gogu wa Magogu awashambulie watu wa Mungu akikusudia kuwafutilia mbali kutoka duniani.—Ufu. 16:21.

      15-16. (a) Huenda andiko la Danieli 11:44, 45 linarejelea tukio gani? (b) Ni nini kitakachompata mfalme wa kaskazini na mataifa mengine yanayofanyiza Gogu wa Magogu?

      15 Huenda ujumbe huo mkali wa hukumu na shambulizi la mwisho la maadui wa Mungu ni matukio yaleyale yanayorejelewa kwenye Danieli 11:44, 45. (Soma.) Katika andiko hilo, Danieli anasema kwamba “habari kutoka mashariki na kutoka kaskazini” zitamhangaisha mfalme wa kaskazini, ambaye atatoka kwa “hasira kali.” Mfalme wa kaskazini atakusudia “kuwaua wengi.” Inaonekana neno “wengi” linarejelea watu wa Yehova.c Hivyo huenda Danieli anazungumzia shambulizi la mwisho dhidi ya watu wa Mungu.

      16 Shambulizi hilo la mfalme wa kaskazini akishirikiana pamoja na serikali nyingine za ulimwengu, litamkasirisha Mweza-Yote na vita vya Har–Magedoni vitaanza. (Ufu. 16:14, 16) Wakati huo, mfalme wa kaskazini pamoja na mataifa mengine yanayofanyiza Gogu wa Magogu, atafikia mwisho wake, na “hakuna atakayemsaidia.”—Dan. 11:45.

      Yesu akiwa amepanda farasi mweupe na akiwa tayari kupiga mshale. Malaika wengine wakiwa wamepanda farasi weupe wakiwa wameshika panga zao.

      Katika vita vya Har–Magedoni, Yesu Kristo na majeshi yake ya mbinguni watauharibu ulimwengu mwovu wa Shetani na kuwaokoa watu wa Mungu (Tazama fungu la 17)

      17. Mikaeli “yule mkuu” anayetajwa katika Danieli 12:1 ni nani, naye anafanya nini sasa, na atafanya nini hivi karibuni?

      17 Mstari unaofuata katika unabii huo wa Danieli unatupatia habari zaidi kuhusu jinsi mfalme wa kaskazini na wale wanaomuunga mkono watakavyofikia mwisho wao na jinsi tutakavyookolewa. (Soma Danieli 12:1.) Mstari huo unamaanisha nini? Mikaeli ni jina lingine la Mfalme wetu anayetawala, Kristo Yesu. Amekuwa ‘akisimama kwa ajili’ ya watu wa Mungu tangu mwaka wa 1914 wakati ambapo Ufalme wake ulisimamishwa mbinguni. Hivi karibuni, “atasimama,” au atawaangamiza maadui wake katika vita vya Har–Magedoni. Vita hivyo ndivyo vitakavyohitimisha kipindi cha wakati ambacho Danieli alikiita “wakati wa taabu” ambao haujawahi kamwe kutokea katika historia. Unabii wa Yohana katika kitabu cha Ufunuo unakiita kipindi hicho, “ile dhiki kuu.”—Ufu. 6:2; 7:14.

      JE, JINA LAKO ‘LITAANDIKWA KATIKA KILE KITABU’?

      18. Kwa nini tunaweza kuutarajia wakati ujao tukiwa na uhakika?

      18 Tunaweza kuutarajia wakati ujao tukiwa na uhakika kwa sababu Danieli na Yohana wanatuhakikishia kwamba wale wanaomtumikia Yehova na Yesu, wataokoka wakati huo wa taabu usioweza kulinganishwa na chochote. Danieli anasema kwamba watu watakaookoka ni wale ambao majina yao yatakuwa ‘yameandikwa katika kile kitabu.’ (Dan. 12:1) Tunaweza kufanya nini ili majina yetu yaandikwe katika kitabu hicho? Ni lazima tuthibitishe waziwazi kwamba tuna imani katika Yesu, Mwanakondoo wa Mungu. (Yoh. 1:29) Tunahitaji kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa. (1 Pet. 3:21) Na ni lazima tuunge mkono Ufalme wa Mungu kwa kufanya yote tuwezayo ili kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova.

      19. Tunapaswa kufanya nini sasa, na kwa nini?

      19 Sasa ndio wakati wa kumtumaini Yehova hata zaidi na pia tengenezo lake la watu wanaomtumikia kwa ushikamanifu. Sasa ndio wakati wa kuunga mkono Ufalme wa Mungu. Ikiwa tutafanya hivyo, tutaokolewa wakati mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini watakapoharibiwa na Ufalme wa Mungu.

      UNGEJIBUJE?

      • “Mfalme wa kaskazini” ni nani leo?

      • Mfalme wa kaskazini ameingiaje katika “nchi ya lile Pambo”?

      • Ni nini kitakachompata mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini?

      WIMBO 149 Wimbo wa Ushindi

      a “Mfalme wa kaskazini” ni nani leo, naye atafikiaje mwisho wake? Kujua majibu ya maswali hayo kunaweza kuimarisha imani yetu na kututayarisha kwa ajili ya majaribu tutakayokabili hivi karibuni.

      b Kwa habari zaidi kuhusu ufafanuzi wa Danieli 2:36-45 na Ufunuo 13:1, 2, tazama toleo la Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 2012, uku. 7-19.

      c Kwa habari zaidi, tazama toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2015, uku. 29-30.

  • Wafalme Wanaopingana Katika Wakati wa Mwisho
    Mnara wa Mlinzi (Funzo)—2020 | Mei
    • Wafalme Wanaopingana Katika Wakati wa Mwisho

      Baadhi ya unabii unaotajwa kwenye chati hii unafafanua matukio yanayotendeka katika kipindi kilekile cha wakati. Unabii huo unatoa uthibitisho mbalimbali kwamba tunaishi katika “wakati wa mwisho.”—Dan. 12:4.

      Chati inayoonyesha unabii mbalimbali na utambulisho wa mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini kuanzia mwaka wa 1870 mpaka leo.
      • Chati ya 1, inaonyesha unabii unaotimia katika kipindi kilekile cha wakati katika siku za mwisho kuanzia mwaka wa 1870 hivi hadi mwaka wa 1918. Kipindi kinachoanzia mwaka wa 1914 na kuendelea kinatambulishwa kuwa wakati wa mwisho. Unabii wa 1: Mnyama wa mwituni mwenye vichwa saba ambaye kuonekana kwake kunaanza hata kabla ya tarehe ya mwanzoni kabisa ya chati. Katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, kichwa cha saba cha mnyama huyo kinajeruhiwa. Kuanzia mwaka wa 1917 na kuendelea, kichwa cha saba cha mnyama huyo kinapona na mnyama huyo wa mwituni anapata nguvu tena. Unabii wa 2: Mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wanaweza kutambuliwa mwaka wa 1870. Mfalme wa kaskazini anaibuka tena mwaka wa 1871 akiwa serikali ya Ujerumani. Mwanzoni mfalme wa kusini anatambuliwa kuwa Uingereza, lakini katika mwaka wa 1917 mahali pake panachukuliwa na Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Unabii wa 3: Kuanzia miaka ya 1870, Charles T. Russell na wenzake wanatambuliwa kuwa yule ‘mjumbe.’ Mwanzoni mwa miaka ya 1880, gazeti la ‘Zion’s Watch Tower’ linawatia moyo wasomaji wake wahubiri habari njema. Unabii wa 4: Kuanzia mwaka wa 1914 na kuendelea ni kipindi cha mavuno. Magugu yanatenganishwa na ngano. Unabii wa 5: Kuanzia mwaka wa 1917 na kuendelea, miguu ya chuma na udongo inatokea. Pia tunaona yafuatayo: Matukio ya ulimwengu kuanzia mwaka wa 1914 hadi mwaka wa 1918, Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Matukio yanayowaathiri watu wa Yehova: Kuanzia mwaka wa 1914 hadi mwaka wa 1918, Wanafunzi wa Biblia nchini Uingereza na Ujerumani wanafungwa gerezani. Mwaka wa 1918, akina ndugu kutoka makao makuu nchini Marekani wanafungwa gerezani.
        Unabii wa 1.

        Maandiko Ufu. 11:7; 12:13, 17; 13:1-8, 12

        Unabii “Mnyama wa mwituni” amewatawala watu duniani kwa zaidi ya miaka 3,000. Katika wakati wa mwisho, kichwa chake cha saba kinajeruhiwa. Baadaye, kichwa hicho kinapona na “dunia yote” inamfuata mnyama huyo. Shetani anamtumia mnyama huyo wa mwituni “kupigana na wale waliobaki.”

        Utimizo Baada ya Gharika, serikali za wanadamu zinazompinga Yehova zajitokeza. Karne nyingi baadaye, wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Milki ya Uingereza inadhoofika sana. Inapata nguvu tena inapoungana na Marekani. Katika wakati wa mwisho, Shetani amekuwa akitumia mfumo wake wote wa kisiasa kuwatesa watu wa Mungu.

      • Unabii wa 2.

        Andiko Dan. 11:25-45

        Unabii Mapambano kati ya mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini katika wakati wa mwisho.

        Utimizo Serikali ya Ujerumani na ile Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani zapambana. Katika mwaka wa 1945 Muungano wa Sovieti na nchi zinazouunga mkono zinakuwa mfalme wa kaskazini. Mwaka wa 1991, Muungano wa Sovieti unavunjika, na baadaye, serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono zinakuwa mfalme wa kaskazini.

      • Unabii wa 3.

        Maandiko Isa. 61:1; Mal. 3:1; Luka 4:18

        Unabii Yehova anamtuma “mjumbe” wake ili ‘afungue njia’ kabla ya Ufalme wa Kimasihi kusimamishwa. “Mjumbe” huyo anaanza ‘kuwatangazia wapole habari njema.’

        Utimizo Kuanzia mwaka wa 1870 na kuendelea, C. T. Russell na wenzake wanajifunza Biblia kwa bidii ili wafafanue mafundisho ya kweli. Katika miaka ya 1880, wanaanza kukazia kwamba watumishi wa Mungu wanapaswa kuhubiri. Wanachapisha makala kama vile “Wahubiri 1,000 Wanahitajika” na “Walitiwa Mafuta Ili Kuhubiri.”

      • Unabii wa 4.

        Andiko Mt. 13:24-30, 36-43

        Unabii Adui anapanda magugu katika shamba la ngano, na magugu hayo yanaachwa yaendelee kukua, nayo yanaficha ngano hadi kipindi cha mavuno kitakapofika; kisha magugu yanatenganishwa na ngano.

        Utimizo Kuanzia mwaka wa 1870 na kuendelea, tofauti kati ya Wakristo wa kweli na wa uwongo inazidi kuwa wazi. Katika wakati wa mwisho, Wakristo wa kweli wanakusanywa na kutenganishwa na Wakristo wa uwongo.

      • Unabii wa 5.

        Andiko Dan. 2:31-33, 41-43

        Unabii Miguu ya chuma na udongo ni sehemu ya sanamu iliyotengenezwa kwa madini mbalimbali.

        Utimizo Udongo unafananisha watu wanaotawaliwa na Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ambao wanapinga utawala wa serikali hiyo. Watu hao wanadhoofisha uwezo wa serikali hiyo ya ulimwengu wa kutumia nguvu zake kikamili kama chuma.

      • Chati ya pili, inaonyesha unabii unaotimia katika kipindi kilekile cha wakati katika siku za mwisho kuanzia mwaka wa 1919 hivi hadi mwaka wa 1945. Mfalme wa kaskazini anatambuliwa kuwa serikali ya Ujerumani hadi kufikia mwaka wa 1945. Mfalme wa kusini anatambuliwa kuwa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Unabii wa 6: Katika mwaka wa 1919, Wakristo watiwa-mafuta wanakusanywa katika kutaniko lililopangwa upya. Kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, kazi ya kuhubiri yapamba moto na kusonga mbele. Unabii wa 7: Katika mwaka wa 1920, Ushirika wa Mataifa waanzishwa na unaendelea kuwapo hadi Vita vya Pili vya ulimwengu vinapoanza. Pia tunaona yafuatayo: Unabii wa 1, mnyama wa mwituni mwenye vichwa saba anaendelea. Unabii wa 5, miguu ya chuma na udongo inaendelea. Matukio ya ulimwengu kuanzia mwaka wa 1939 hadi mwaka wa 1945, Vita vya Pili vya Ulimwengu. Matukio yanayowaathiri watu wa Yehova: Nchini Ujerumani kuanzia mwaka wa 1933 mpaka mwaka wa 1945, zaidi ya Mashahidi 11,000 wanafungwa gerezani. Nchini Uingereza kuanzia mwaka wa 1939 hadi mwaka wa 1945, karibu Mashahidi 1,600 wanafungwa gerezani. Nchini Marekani kuanzia mwaka wa 1940 mpaka mwaka wa 1944, kuna mashambulizi zaidi ya 2,500 dhidi ya Mashahidi.
        Unabii wa 6.

        Maandiko Mt. 13:30; 24:14, 45; 28:19, 20

        Unabii “Ngano” inakusanywa “ghalani,” na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anawekwa rasmi ili asimamie “watumishi wa nyumbani.” Kazi ya kuhubiri “habari njema ya Ufalme” inaanza kuenea katika “dunia yote inayokaliwa.”

        Utimizo Mwaka wa 1919 mtumwa mwaminifu anawekwa rasmi ili awasimamie watu wa Mungu. Kuanzia wakati huo na kuendelea, Wanafunzi wa Biblia wamekuwa wakihubiri zaidi na zaidi. Leo, Mashahidi wa Yehova wanahubiri katika nchi zaidi ya 200 na wanachapisha machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha zaidi ya 1,000.

      • Unabii wa 7.

        Maandiko Dan. 12:11; Ufu. 13:11, 14, 15

        Unabii Mnyama wa mwituni mwenye pembe mbili anawaambia watu duniani watengeneze “sanamu ya yule mnyama wa mwituni” na anaipa ‘pumzi sanamu hiyo.’

        Utimizo Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani yawa mstari wa mbele katika kuanzisha Ushirika wa Mataifa. Ushirika huo unaungwa mkono na mataifa mengine. Hatimaye, mfalme wa kaskazini anajiunga na Ushirika huo pia—lakini anafanya hivyo kuanzia mwaka wa 1926 hadi 1933 tu. Kama ilivyo kwa Umoja wa Mataifa (UM) leo, Ushirika huo unasifiwa kwamba unaweza kutimiza mambo yanayoweza tu kutimizwa na Ufalme wa Mungu.

      • Chati ya 3, unabii unaotimia katika kipindi kilekile cha wakati katika siku za mwisho kuanzia mwaka wa 1945 mpaka mwaka wa 1991. Mfalme wa kusini anatambuliwa kuwa Muungano wa Sovieti na nchi zinazouunga mkono hadi kufikia mwaka wa 1991, na baada ya hapo ni serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono. Mfalme wa kusini anatambuliwa kuwa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Unabii wa 8: Moshi mzito wa bomu la atomu, ukiashiria uharibifu mkubwa uliosababishwa na Serikali Kuu ya Uingereza na Marekani. Unabii wa 9: Shirika la Umoja wa Mataifa laanzishwa mwaka wa 1945, likichukua mahali pa Ushirika wa Mataifa. Pia tunaona yafuatayo: Unabii wa 1, mnyama wa mwituni mwenye vichwa saba anaendelea. Unabii wa 5, miguu ya chuma na udongo inaendelea. Unabii wa 6, mwaka wa 1945 kuna zaidi ya wahubiri 156,000. Mwaka wa 1991, kuna zaidi ya wahubiri 4,278,000. Matukio yanayowaathiri watu wa Yehova: Katika Muungano wa Sovieti kuanzia mwaka wa 1945 mpaka mwaka wa 1951, maelfu ya Mashahidi walipelekwa uhamishoni Siberia.
        Unabii wa 8.

        Andiko Dan. 8:23, 24

        Unabii Mfalme mwenye uso mkali analeta “uharibifu kwa njia isiyo ya kawaida.”

        Utimizo Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani imesababisha uharibifu mkubwa sana. Kwa mfano, wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Marekani ilisababisha uharibifu ambao haujawahi kuonekana kamwe ilipomwangushia adui yake mabomu mawili ya atomu.

      • Unabii wa 9.

        Maandiko Dan. 11:31; Ufu. 17:3, 7-11

        Unabii Mnyama wa mwituni mwenye “rangi nyekundu” na pembe kumi anapanda kutoka katika shimo refu lisilo na mwisho, naye ni mfalme wa nane. Kitabu cha Danieli kinamtaja mfalme huyo wa nane kuwa, “kile kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa.”

        Utimizo Ushirika wa Mataifa unaingia katika kipindi cha kutotenda wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Baada ya vita, UM ‘unasimamishwa.’ Kama ilivyokuwa kwa Ushirika wa Mataifa, UM unapewa utukufu ambao Ufalme wa Mungu unapaswa kupewa. UM utashambulia dini.

      • Chati ya 4, unabii unaotimia katika kipindi kilekile cha wakati katika siku za mwisho na unahusu siku zetu hadi kufikia vita vya Har–​Magedoni. Mfalme wa kaskazini anatambuliwa kuwa serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono. Mfalme wa kusini anatambuliwa kuwa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Unabii wa 10: Viongozi wa ulimwengu watangaza ‘amani na usalama.’ Baada ya hapo, dhiki kuu yaanza. Unabii wa 11: Mataifa yashambulia mashirika ya dini ya uwongo. Unabii wa 12: Serikali za ulimwengu zawashambulia watu wa Mungu. Watiwa-mafuta waliobaki wanakusanywa kwenda mbinguni. Unabii wa 13: Har–​Magedoni. Yule anayeketi juu ya farasi mweupe anakamilisha ushindi wake. Yule mnyama wa mwituni mwenye vichwa saba anaharibiwa; ile sanamu kubwa inapondwapondwa kwenye miguu yake ya chuma na udongo. Pia tunaona yafuatayo: Unabii wa 1, mnyama wa mwituni mwenye vichwa saba aendelea mpaka wakati wa Har–​Magedoni. Unabii wa 5, miguu ya chuma na udongo inaendelea mpaka wakati wa Har–​Magedoni. Unabii wa 6, leo kuna zaidi ya wahubiri 8,580,000. Matukio yanayowaathiri watu wa Yehova: Mwaka wa 2017, wenye mamlaka nchini Urusi wawafunga Mashahidi na kuchukua kwa lazima majengo ya ofisi ya tawi.
        Unabii wa 10 na 11.

        Maandiko 1 The. 5:3; Ufu. 17:16

        Unabii Mataifa yanatangaza “amani na usalama,” kisha “zile pembe kumi” na “yule mnyama wa mwituni” wanamshambulia “yule kahaba” na kumwangamiza. Baada ya hapo, mataifa yanaharibiwa.

        Utimizo Mataifa yatadai kwamba yamefanikiwa kupata amani na usalama. Kisha, mataifa yanayounga mkono UM yataharibu mashirika ya dini ya uwongo. Huo utakuwa mwanzo wa dhiki kuu. Dhiki hiyo itakwisha wakati mfumo wote wa ulimwengu utakapoharibiwa katika vita vya Har–Magedoni.

      • Unabii wa 12.

        Maandiko Eze. 38:11, 14-17; Mt. 24:31

        Unabii Gogu ashambulia nchi ya watu wa Mungu. Kisha, malaika wanawakusanya wale “waliochaguliwa.”

        Utimizo Mfalme wa kaskazini, pamoja na serikali nyingine za ulimwengu, zitawashambulia watu wa Mungu. Wakati fulani baada ya shambulizi hilo kuanza, watiwa-mafuta waliobaki watakusanywa kwenda mbinguni.

      • Unabii wa 13.

        Maandiko Eze. 38:18-23; Dan. 2:34, 35, 44, 45; Ufu. 6:2; 16:14, 16; 17:14; 19:20

        Unabii “Yule aliyeketi” juu ya “farasi mweupe” anakamilisha “ushindi wake” kwa kumharibu Gogu na jeshi lake. “Yule mnyama wa mwituni” ‘anatupwa ndani ya ziwa la moto,’ na sanamu ile kubwa inapondwapondwa.

        Utimizo Yesu, Mfalme anayetawala wa Ufalme wa Mungu anawaokoa watu wa Mungu. Akiwa pamoja na watawala wenzake 144,000 na majeshi ya malaika, Yesu anauharibu muungano wa mataifa, yaani, mfumo wote wa kisiasa wa Shetani.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki