Barua ya Pekee kwa Wazazi Wao
Hivi karibuni wasichana wawili matineja katika Hispania waliwaandikia wazazi wao barua ya kuonyesha uthamini. Yafuatayo ni madondoo fulani:
Kwa wazazi wetu wapendwa, Pepe na Vicenta:
Tuanzie wapi? Kuna mambo mengi sana tunayotaka kusema, na ni vigumu kuyaandika yote kwa maneno machache. Tunataka kuwashukuru kwa miaka ambayo tumeishi 17 na 15, miaka ambayo imejawa na utunzaji na shauku.
Sikuzote tumefahamu maoni yenu na sheria zenu. Nyakati nyingine tulishangaa ni kwa nini tulihitaji kufika nyumbani kwa wakati uliowekwa, lakini sasa, baada ya kuona jinsi ambavyo mambo yamekuwa kwa vijana ambao wazazi wao hawakuwawekea vizuizi vya saa za kurudi nyumbani, tunatambua kwamba tumelindwa na sheria hizo.
Kielelezo chenu cha kutokosa mkutano hata mmoja wa Kikristo kwenye Jumba la Ufalme, isipokuwa kuwe na sababu nzuri, kimetusaidia sana, kama ambavyo tumesaidiwa na kuhubiri pamoja nanyi Jumapili. Jumapili asubuhi hatuhitaji kuuliza ikiwa tutaenda kwenye utumishi wa shambani. Tunajua vizuri sana kwamba tutaenda!
Malezi yetu pia yametia ndani kujifunza ukaribishaji-wageni. Watu wengi sana wamezuru nyumbani kwetu, na sikuzote mnawapa vitu bora mlivyo navyo. Tumejionea mambo haya wenyewe, na tumethamini kwamba tuna wazazi ambao ni wa pekee.
Hakuna mtu atujuaye au kutuelewa vizuri zaidi kuliko nyinyi. Nyinyi ni marafiki zetu walio bora, tunaowatumaini kabisa.
Kwa kumalizia, tunataka kuwaambia kwamba twawapenda. Nyinyi ni wazazi wetu, na hatungeweza kuwabadilisha na mtu mwingine yeyote. Ikiwa kwa njia fulani tungehitaji kuchagua tena wazazi wetu na njia yetu ya maisha, bila shaka, tungewachagua nyinyi, na tungechagua tena kuishi maisha ambayo tumekuwa nayo.
Busu nyingi zenye shauku, binti zenu,
ESMERALDA NA YOLANDA