-
Wazee, Mna Maoni Gani Kuhusu Kuwazoeza Wengine?Mnara wa Mlinzi—2015 | Aprili 15
-
-
Wazee, Mna Maoni Gani Kuhusu Kuwazoeza Wengine?
“Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu.” —MHU. 3:1.
1, 2. Waangalizi wa mzunguko wameona nini katika makutaniko mengi?
MWANGALIZI wa mzunguko alikuwa akimalizia mkutano na baraza la wazee. Aliwatazama usoni na kuonyesha jinsi anavyowapenda wachungaji hao wenye bidii, ambao baadhi yao walikuwa kama baba zake. Lakini pia kuna jambo lililomhangaisha, hivyo akawauliza, “Akina ndugu, mmefanya nini ili kuwazoeza wengine kushughulikia majukumu kutanikoni?” Walikumbuka vizuri kuwa mwangalizi wa mzunguko aliwasihi katika ziara yake iliyopita watumie muda mwingi zaidi kuwazoeza wengine. Mwishowe, mzee mmoja akasema, “Kusema kweli, hatujafanya mengi.” Wazee wengine wakatikisa vichwa kuonyesha wanakubaliana naye.
2 Ikiwa wewe ni mzee Mkristo, je, umewahi kujikuta katika hali kama hiyo? Huenda umewahi. Waangalizi wa mzunguko wameona kwamba kwenye makutaniko mengi duniani kote kuna uhitaji wa kuwazoeza akina ndugu, vijana kwa wazee, ili wasaidie kulichunga kundi. Lakini si rahisi kufanya hivyo. Kwa nini?
3. (a) Maandiko yanaonyeshaje umuhimu wa kuwazoeza wengine, na kwa nini sote tunapaswa kupendezwa na jambo hilo? (Tazama maelezo ya chini.) (b) Kwa nini wazee fulani huona ni vigumu kuwazoeza wengine?
3 Ukiwa mchungaji, bila shaka unajua kuwa ni muhimu kuwazoeza akina ndugu.a Unajua kwamba ndugu wengi zaidi wanahitajika ili kuyaimarisha kiroho makutaniko na kusaidia kuanzisha makutaniko mapya. (Soma Isaya 60:22.) Pia, unajua kuwa Neno la Mungu linakuhimiza ‘uwafundishe wengine.’ (Soma 2 Timotheo 2:2.) Ingawa hivyo, kama ilivyokuwa kwa wazee waliotajwa mwanzoni, huenda ukaona ni vigumu kuwazoeza wengine. Baada ya kutimiza mahitaji ya familia, majukumu ya kazi, wajibu wa kutaniko, na mambo mengine yanayohitaji kushughulikiwa haraka, huenda ikaonekana kwamba hakuna wakati wa kuwazoeza wengine kutanikoni. Hivyo basi, acheni tuchunguze kwa nini ni muhimu kuwazoeza wengine.
NI MUHIMU SANA KUWAZOEZA WENGINE
4. Ni sababu gani inayoweza kuwafanya wazee waahirishe kuwazoeza wengine?
4 Ni sababu gani inayoweza kuwafanya wazee waone ni vigumu kutenga wakati ili kuwazoeza wengine? Labda wengine hufikiri hivi: ‘Ni muhimu kuwazoeza wengine, lakini kuna mambo mengine ya kutaniko ambayo yanahitaji kushughulikiwa haraka. Hata nikiahirisha kuwazoeza wengine kwa muda fulani, kutaniko litasonga mbele tu.’ Ijapokuwa ni kweli kwamba una mambo mengi yanayohitaji kushughulikiwa haraka, kuahirisha kuwazoeza wengine kunaweza kudhuru hali ya kiroho ya kutaniko.
5, 6. Tunajifunza nini katika mfano wa dereva na maoni yake kuhusu kubadilisha oili kwenye injini ya gari? Na mfano huo unahusianaje na kuwazoeza wengine kutanikoni?
5 Fikiria mfano huu: Dereva anajua kwamba ni lazima abadilishe oili kwa ukawaida ili injini ya gari ifanye kazi vizuri, na gari lake libaki katika hali nzuri. Lakini huenda akafikiri kwamba kubadilisha oili si jambo la haraka sana kama kujaza mafuta kwenye gari. Isitoshe, asipojaza mafuta, gari lake halitatembea kabisa. Kwa hiyo anaweza kujiambia hivi, ‘Nisipopata muda wa kubadilisha oili, bado injini itaendelea kufanya kazi, angalau kwa muda fulani.’ Lakini kuna hatari gani? Ikiwa dereva ataendelea kuahirisha kubadilisha oili, mwishowe gari lake litaharibika kabisa. Hilo linapotokea, atahitaji kutumia muda na pesa nyingi sana kutengeneza gari ili lifanye kazi tena. Tunajifunza nini?
6 Wazee hushughulikia mambo mengi yanayohitaji kufanywa haraka; wasipofanya hivyo kutaniko litaathirika sana. Kwa hiyo, kama vile dereva anavyohakikisha kuwa anajaza gari mafuta kwa ukawaida, vivyo hivyo ni lazima wazee ‘wahakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Flp. 1:10) Hata hivyo, baadhi ya wazee wanatumia muda mwingi kushughulikia mambo ya haraka hivi kwamba wanakosa wakati wa kuwazoeza wengine, yaani, ni kana kwamba wanapuuza kubadilisha oili kwenye injini ya gari. Lakini ikiwa wazee wataendelea kuahirisha kuwazoeza wengine, hatimaye kutaniko litakosa ndugu wa kutosha wanaostahili kushughulikia majukumu kutanikoni.
7. Tunapaswa kuwaonaje wazee wanaotenga muda ili kuwazoeza wengine kutanikoni?
7 Hivyo basi, hatupaswi kufikiri kwamba mambo mengine ni muhimu zaidi kuliko kuwazoeza wengine. Wazee wanaofikiria wakati ujao na kutumia muda wao kuwazoeza ndugu wasio na uzoefu, ni wasimamizi-nyumba wenye hekima na ni baraka kutanikoni. (Soma 1 Petro 4:10.) Kutaniko linafaidikaje?
KUTUMIA WAKATI VIZURI
8. (a) Ni sababu gani zinazowachochea wazee wawazoeze wengine? (b) Wazee wanaotumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wanahitaji kutimiza wajibu gani wa haraka? (Tazama sanduku lenye kichwa “Kazi ya Haraka.”)
8 Hata wazee wenye uzoefu mwingi wanapaswa kuwa wenye kiasi na kutambua kwamba umri unaposonga, pole kwa pole watashindwa kutimiza mambo mengi kutanikoni. (Mika 6:8) Pia, wanapaswa kuzingatia kwamba ‘wakati na matukio yasiyotazamiwa’ yanaweza kubadili mambo ghafla, na kuwafanya washindwe kutimiza majukumu yao kutanikoni. (Mhu. 9:11, 12; Yak. 4:13, 14) Kwa sababu wanawapenda sana kondoo wa Yehova, wazee wanaofikiria wakati ujao wanawazoeza ndugu vijana na kuwafundisha mambo ambayo wamejifunza kwa miaka mingi.—Soma Zaburi 71:17, 18.
9. Ni tukio gani la wakati ujao linalofanya kazi ya kuwazoeza wengine iwe muhimu sana?
9 Isitoshe, wazee wanaowazoeza wengine ni baraka kutanikoni kwa sababu wanaimarisha ulinzi wa kutaniko. Jinsi gani? Mazoezi hayo yanawasaidia ndugu wengi wawe tayari kulisaidia kutaniko libaki imara na lenye umoja katika siku hizi za mwisho, na yatawasaidia zaidi wakati wa dhiki kuu inayokuja. (Eze. 38:10-12; Mika 5:5, 6) Kwa hiyo, wazee wapendwa, tunawasihi muanze leo kuwazoeza wengine kutanikoni kwa ukawaida.
10. Huenda mzee akahitaji kufanya nini ili apate wakati wa kuwazoeza wengine?
10 Bila shaka, tunaelewa kwamba mnatumia muda mwingi sana kutimiza utendaji muhimu kutanikoni. Hata hivyo, huenda mkahitaji kupunguza wakati mnaotumia katika utendaji huo na muutumie kuwazoeza wengine. (Mhu. 3:1) Hiyo ni njia nzuri sana ya kutumia wakati wenu.
TAYARISHA MOYO WA NDUGU UNAYEMZOEZA
11. (a) Ni jambo gani linalovutia kuhusiana na mapendekezo yaliyotolewa na wazee kutoka nchi mbalimbali? (b) Kulingana na Methali 15:22, kuna faida gani kuzungumzia mapendekezo ya wazee wengine?
11 Hivi karibuni, kikundi cha wazee ambao wamefanikiwa kuwasaidia ndugu wengine wakue kiroho waliulizwa wanatumia njia gani kufanya hivyo.b Ijapokuwa hali za wazee hao zinatofautiana sana, ushauri waliotoa unafanana sana. Hilo linaonyesha nini? Mazoezi yanayotegemea Biblia yanaweza kutumiwa kuwazoeza wale wasio na uzoefu “kila mahali katika kila kutaniko”—kama ilivyokuwa katika siku za Paulo. (1 Kor. 4:17) Hivyo, katika makala hii na ile inayofuata, tutazungumzia baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa na wazee hao.—Met. 15:22.
12. Mzee anahitaji kutayarisha nini, na kwa nini?
12 Mzee anahitaji kuutayarisha kwanza moyo wa ndugu anayemzoeza. Kama vile mtunza bustani anavyohitaji kulima au kutifua udongo kabla ya kupanda mbegu, ndivyo ambavyo mzee anahitaji kuutayarisha moyo wa ndugu anayemzoeza kabla ya kuanza kumfundisha mbinu mpya. Hivyo, wazee wanaweza kuitayarishaje mioyo ya wale wanaowazoeza? Kwa kutumia njia kama ile aliyotumia nabii fulani wa kale. Ni njia gani hiyo?
13-15. (a) Samweli alipewa mgawo gani? (b) Samweli alitimizaje mgawo wake? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 3.) (c) Kwa nini wazee wanapaswa kupendezwa na simulizi la Samweli?
13 Siku moja, zaidi ya miaka 3,000 iliyopita, Yehova alimwambia hivi Samweli aliyekuwa amezeeka: “Karibu wakati kama huu kesho nitatuma mtu kwako kutoka katika nchi ya Benyamini, nawe umtie mafuta awe kiongozi juu ya watu wangu Israeli.” (1 Sam. 9:15, 16) Samweli alitambua kwamba hangeendelea kuliongoza taifa la Israeli, na Yehova alimwagiza amtie mafuta mtu ambaye angechukua nafasi yake. Labda Samweli alijiuliza, ‘Nitamtayarishaje mtu huyo kwa ajili ya mgawo wake?’ Alipata wazo na akapanga jinsi atakavyofanya.
14 Siku iliyofuata, Samweli alipomwona Sauli, Yehova alimwambia hivi: “Huyu ndiye.” Kisha Samweli akafanya kama alivyopanga. Alimwalika Sauli wale mlo pamoja katika jumba la kulia chakula. Halafu akampa Sauli na mtumishi wake sehemu nzuri ya kuketi na vipande bora vya nyama, naye akasema: “Ule, kwa maana wamekuwekea hicho akiba.” Baada ya hapo, Samweli alimkaribisha Sauli nyumbani kwake. Walipokuwa njiani walizungumza mambo mbalimbali. Samweli alimstarehesha Sauli kwa kumwandalia mlo mzuri na kuzungumza naye kirafiki walipokuwa wakitembea, naye alitaka kutumia vizuri hali hiyo. Hivyo walipofika, Samweli akamkaribisha Sauli darini. Upepo mwanana wa jioni ulipokuwa ukivuma, Samweli “akaendelea kusema na Sauli darini” hadi walipoenda kulala. Siku iliyofuata, Samweli alimtia mafuta Sauli, akambusu, na kumpa maagizo zaidi. Kisha, akamruhusu Sauli aende—akiwa tayari kwa ajili ya matukio yatakayofuata.—1 Sam. 9:17-27; 10:1.
15 Bila shaka kumtia mtu mafuta ili awe kiongozi wa taifa, si sawa na kumzoeza ndugu ili awe mzee au mtumishi wa huduma kutanikoni. Hata hivyo, wazee wanaweza kujifunza mambo kadhaa kutokana na njia aliyotumia Samweli. Acheni tuchunguze mambo mawili.
MARAFIKI WA KWELI NA WALIO TAYARI KUWAZOEZA WENGINE
16. (a) Samweli alihisije Waisraeli walipoomba wapewe mfalme? (b) Samweli alitendaje alipoambiwa amtie mafuta Sauli?
16 Uwe tayari, usisite. Mwanzoni, Samweli aliposikia kwamba Waisraeli wanataka mfalme, alivunjika moyo na alihisi watu wake wamemkataa. (1 Sam. 8:4-8) Alisita kufanya kile ambacho watu walitaka hivi kwamba Yehova akamwambia mara tatu awasikilize. (1 Sam. 8:7, 9, 22) Hata hivyo, Samweli hakumwekea kinyongo yule atakayechukua nafasi yake. Yehova alipomwambia amtie mafuta Sauli, nabii huyo alitii, si kwa shingo upande au ili tu kutimiza wajibu, bali kwa kupenda.
17. Wazee leo huigaje mtazamo wa Samweli, nao huridhika wanapoona nini?
17 Kama Samweli, wazee wenye uzoefu leo wanawaonyesha fadhili wale wanaowazoeza. (1 Pet. 5:2) Wazee hao wako tayari kuwazoeza wengine na hawaogopi kwamba wale wanaozoezwa watachukua baadhi ya mapendeleo yao kutanikoni. Wazee wenye mtazamo mzuri huwaona wale wanaozoezwa kuwa “wafanyakazi wenzi” wenye thamani kutanikoni na si washindani wao. (2 Kor. 1:24; Ebr. 13:16) Wazee hao wasio na ubinafsi huridhika sana wanapowaona wale wanaowazoeza wakitumia uwezo wao kunufaisha kutaniko.—Mdo. 20:35.
18, 19. Mzee anaweza kuutayarishaje moyo wa yule anayemzoeza, na kwa nini ni muhimu kufanya hivyo?
18 Jenga urafiki. Siku ambayo nabii Samweli alikutana na Sauli, angeweza kumtia mafuta mara moja ili awe mfalme kwa kuchukua mafuta, kummiminia kichwani, na kisha kumwacha aende. Mfalme huyo angekuwa ametiwa mafuta, lakini hangekuwa ametayarishwa kuwaongoza watu wa Mungu. Badala yake, Samweli alitumia wakati kuutayarisha moyo wa Sauli hatua kwa hatua. Baada ya kula mlo mzuri, kutembea pamoja, kuzungumza kwa muda mrefu, na kupumzika vizuri ndipo nabii huyo aliona kuwa wakati umefika wa kumtia mafuta Sauli.
Kusitawisha urafiki wa karibu ni hatua ya kwanza katika kuwazoeza wengine (Tazama fungu la 18, 19)
19 Vivyo hivyo, mzee anapaswa kuanza kumzoeza ndugu kwa kutumia wakati kutayarisha mazingira mazuri yenye kustarehesha, na kujenga urafiki kati yake na anayemzoeza. Hatua hususa ambazo mzee anachukua kujenga urafiki zinaweza kutofautiana kati ya nchi moja na nyingine, ikitegemea hali na desturi za eneo hilo. Lakini, hata iwe unaishi wapi au una shughuli nyingi kadiri gani, ukitumia wakati pamoja na yule unayemzoeza, atajua kwamba unamwona kuwa mtu muhimu. (Soma Waroma 12:10.) Kwa hakika, wale unaowazoeza watathamini sana upendo na uangalifu unaowapa.
20, 21. (a) Mzee anapaswa kufanya nini ili afanikiwe? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?
20 Wazee, kumbukeni hili: Ili mzee afanikiwe, ni lazima apende kuwazoeza wengine na awapende wale anaowazoeza. (Linganisha na Yohana 5:20.) Ndugu anayezoezwa atatambua haraka mtazamo huo mzuri wa mzee na utamfanya akubali mazoezi anayopata. Kwa hiyo, wazee wapendwa, mnapowazoeza wengine, jitahidini kujenga urafiki pamoja nao.—Met. 17:17; Yoh. 15:15.
21 Baada ya kuutayarisha moyo wa ndugu anayetaka kumzoeza, mzee ataanza kumzoeza ndugu huyo. Mzee anaweza kutumia njia gani? Jambo hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.
a Makala hii na ile inayofuata zimeandaliwa hasa kwa ajili ya wazee, hata hivyo wengine kutanikoni wanapaswa kupendezwa na mambo yanayozungumziwa. Kwa nini? Kwa sababu itawachochea wanaume waliobatizwa watambue kwamba wanahitaji kuzoezwa ili wasaidie majukumu mbalimbali kutanikoni. Ndugu wengi wanapozoezwa, sisi sote tutafaidika.
b Wazee hao wanaishi nchini Afrika Kusini, Australia, Bangladesh, Brazili, Guiana ya Ufaransa, Japani, Korea, Marekani, Mexico, Namibia, Nigeria, Réunion, Ubelgiji, Ufaransa, na Urusi.
-
-
Jinsi Wazee Wanavyowazoeza WengineMnara wa Mlinzi—2015 | Aprili 15
-
-
Jinsi Wazee Wanavyowazoeza Wengine
“Mambo uliyoyasikia kutoka kwangu . . . , uwakabidhi watu waaminifu.”—2 TIM. 2:2.
1. (a) Tangu zamani, watumishi wa Mungu wamekuwa na maoni gani kuhusu mazoezi? Leo tuna maoni gani kuhusu jambo hilo? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?
TANGU zamani, watumishi wa Mungu wanaelewa kwamba mazoezi huchangia mafanikio. Mzee wa ukoo, Abramu, ‘aliwakusanya watu wake waliozoezwa’ ili kumwokoa Loti—nao walifanikiwa. (Mwa. 14:14-16) Katika siku za Mfalme Daudi, waimbaji katika nyumba ya Mungu ‘walizoezwa’ kuimba nyimbo za kumsifu Yehova. (1 Nya. 25:7) Leo, tunapigana vita dhidi ya Shetani na wafuasi wake. (Efe. 6:11-13) Pia, tunajitahidi sana kumsifu Yehova. (Ebr. 13:15, 16) Hivyo, kama ilivyokuwa kwa watumishi wa Mungu wa kale, tunahitaji kuzoezwa ili tufanikiwe. Katika kutaniko, Yehova amewakabidhi wazee wajibu wa kuwazoeza wengine. (2 Tim. 2:2) Wazee wenye uzoefu wanatumia njia gani kuwazoeza wengine ili wastahili kulichunga kundi?
MWIMARISHE KIROHO NDUGU UNAYEMZOEZA
2. Huenda mzee akahitaji kufanya nini kabla ya kumzoeza ndugu, na kwa nini?
2 Mzee anaweza kufananishwa na mtunza bustani. Kabla ya kupanda mbegu huenda mtunza bustani akahitaji kuweka mbolea ili udongo uwe na rutuba zaidi. Vivyo hivyo, kabla ya kumzoeza ndugu, huenda ikafaa kuzungumzia naye kanuni fulani za Biblia ambazo zitamsaidia awe tayari zaidi kupokea mazoezi utakayompa.—1 Tim. 4:6.
3. (a) Unaweza kutumiaje andiko la Marko 12:29, 30 unapomzoeza ndugu? (b) Sala ya mzee inaweza kuwa na matokeo gani kwa ndugu anayezoezwa?
3 Ili kujua ni kwa kadiri gani ndugu anafikiri na kutenda kupatana na kweli ya Ufalme, unaweza kumuuliza hivi, ‘Wakfu wako kwa Yehova umebadilije njia yako ya maisha?’ Swali hilo linaweza kuanzisha mazungumzo mazuri kuhusu jinsi tunavyoweza kumtumikia Yehova kwa nafsi yote. (Soma Marko 12:29, 30.) Huenda baada ya mazungumzo ukaamua kusali ili Yehova ampe ndugu huyo roho takatifu itakayomsaidia katika mazoezi yake. Bila shaka atatiwa moyo sana akikusikia ukisali kwa niaba yake!
4. (a) Ni masimulizi gani ya Biblia yanaweza kumchochea ndugu anayezoezwa afanye maendeleo ya kiroho? (b) Wazee wanapaswa kuwa na lengo gani wanapomzoeza ndugu?
4 Unapoanza kumzoeza ndugu, zungumzieni masimulizi ya Biblia yanayoweza kumsaidia awe tayari, mwenye kutegemeka, na mnyenyekevu. (1 Fal. 19:19-21; Neh. 7:2; 13:13; Mdo. 18:24-26) Sifa hizo ni muhimu sana kama vile rutuba kwenye udongo. Zitamsaidia akue haraka kiroho. Jean-Claude, mzee kutoka Ufaransa, anasema hivi: “Ninapomzoeza ndugu, lengo langu kuu ni kumsaidia awe mtu wa kiroho. Ninatafuta nafasi za kusoma naye andiko fulani ili kumsaidia aone ‘mambo ya ajabu’ yaliyo katika Neno la Mungu.” (Zab. 119:18) Je, kuna njia nyingine za kumwimarisha ndugu anayezoezwa?
TOA MAPENDEKEZO—ELEZA SABABU
5. (a) Kwa nini ni muhimu kuzungumza na ndugu unayemzoeza kuhusu malengo ya kiroho? (b) Kwa nini wazee wanapaswa kuwazoeza vijana? (Tazama maelezo ya chini.)
5 Muulize ndugu unayemzoeza, ‘Una malengo gani ya kiroho?’ Ikiwa hana miradi au malengo yoyote hususa, msaidie ajiwekee lengo linalomfaa ambalo anaweza kutimiza. Mwambie lengo hususa ambalo wewe ulijiwekea, na ueleze kwa shauku jinsi ulivyofurahi ulipolitimiza. Ingawa huenda njia hiyo ikaonekana kuwa rahisi, inafaa sana. Victor, mzee na painia kutoka Afrika, anakumbuka hivi: “Nilipokuwa kijana, mzee fulani aliniuliza maswali machache kuhusu malengo yangu. Maswali hayo yalinifanya nianze kufikiria kwa kina kuhusu huduma yangu.” Wazee wenye uzoefu wanasema kwamba ni muhimu kuanza kuwazoeza ndugu wakiwa vijana—mwanzoni mwa miaka yao ya ujana—kwa kuwapa migawo inayolingana na umri wao. Mazoezi hayo yatawasaidia vijana kukazia fikira malengo ya kiroho wanapozidi kukua na kupambana na vishawishi mbalimbali.—Soma Zaburi 71:5, 17.a
Eleza kwa nini kazi inapaswa kufanywa, na umpongeze ndugu anapojitahidi kuitimiza (Tazama fungu la 5-8)
6. Yesu alitumia njia gani muhimu kuwazoeza wengine?
6 Ili kumchochea ndugu unayemzoeza awe na tamaa ya kutumikia ni vizuri umweleze jambo la kufanya na sababu ya kulifanya. Unapofanya hivyo, unamwiga Yesu, yule Mwalimu Mkuu. Kwa mfano, kabla ya kuwaagiza mitume wake wakafanye wanafunzi, Yesu aliwaeleza sababu ya kutii agizo hilo. Alisema hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” Kisha akaongezea: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mt. 28:18, 19) Unawezaje kuiga njia ambayo Yesu alitumia kuwazoeza wengine?
7, 8. (a) Wazee wanawezaje kuiga njia ya Yesu ya kuzoeza? (b) Kwa nini ni muhimu kumpongeza ndugu unayemzoeza? (c) Ni mapendekezo gani yatakayowasaidia wazee kuwazoeza wengine? (Ona sanduku “Jinsi ya Kuwazoeza Wengine.”)
7 Mweleze yule unayemzoeza sababu za Kimaandiko za kufanya jambo analoombwa afanye. Unapofanya hivyo, unamfundisha kufanya mambo kwa kutegemea kanuni za Biblia. Kwa mfano, wazia unamwomba ndugu ahakikishe kwamba eneo la kuingia Jumba la Ufalme ni safi na halihatarishi usalama. Unaweza kutumia andiko la Tito 2:10 na kueleza jinsi ambavyo kazi hiyo ‘italipamba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu.’ Pia, mchochee ndugu afikirie jinsi kazi hiyo itakavyowanufaisha wale waliozeeka kutanikoni. Mazungumzo kama hayo yatamchochea kufikiria zaidi jinsi ambavyo ndugu na dada wanafaidika kutokana na kazi yake, badala ya kufanya tu kulingana na anavyoagizwa. Atapata shangwe anapoona jinsi utumishi wake unavyowanufaisha ndugu na dada kutanikoni.
8 Zaidi ya hayo, usisahau kumpongeza ndugu unayemzoeza anapojitahidi kutumia mapendekezo yako. Kwa nini ni muhimu kafanya hivyo? Pongezi za kutoka moyoni ni kama maji katika mmea—zitamchochea kufanya maendeleo.—Linganisha na Mathayo 3:17.
CHANGAMOTO
9. (a) Baadhi ya wazee wanakabili changamoto gani katika nchi tajiri? (b) Kwa nini vijana fulani hawajawahi kutanguliza utumishi wao kwa Mungu?
9 Katika nchi tajiri, huenda wazee wakakabili changamoto fulani: wanawezaje kuwachochea vijana waliobatizwa wenye umri wa miaka 20 au 30 na kitu hivi kushiriki katika utendaji wa kutaniko? Tuliwauliza wazee kutoka nchi 20 za Magharibi kwa nini vijana wengi wanasita kukubali mapendeleo kutanikoni. Wengi wao walisema kwamba baadhi ya vijana hawakutiwa moyo kujiwekea malengo ya kiroho walipokuwa wadogo. Katika visa fulani, vijana ambao walikuwa na mwelekeo wa kujiwekea malengo ya kiroho walichochewa na wazazi wao kujiwekea malengo ya kimwili! Hivyo, vijana hao hawajawahi kutanguliza utumishi wao kwa Mungu.—Mt. 10:24.
10, 11. (a) Mzee anaweza kumsaidiaje ndugu ambaye hajihusishi sana na utendaji wa kutaniko abadili mtazamo wake? (b) Mzee anaweza kutumia kanuni gani za Kimaandiko, na kwa nini? (Tazama maelezo ya chini.)
10 Ikionekana kwamba ndugu hapendi kujihusisha sana na utendaji wa kutaniko, jitihada nyingi na subira zinahitajika ili kubadili mtazamo wake, hata hivyo inawezekana kuubadili. Kama vile mtunza bustani anavyojitahidi kunyoosha shina la mmea kadiri unavyokua,ndivyo unavyoweza kumsaidia hatua kwa hatua ndugu anayesita kukubali mapendeleo abadili mtazamo wake. Jinsi gani?
11 Sitawisha urafiki wa karibu pamoja naye. Mfanye ahisi kwamba anahitajika kutanikoni. Kisha, baada ya muda, zungumzia naye Maandiko yatakayomsaidia kufikiria wakfu wake kwa Yehova. (Mhu. 5:4; Isa. 6:8; Mt. 6:24, 33; Luka 9:57-62; 1 Kor. 15:58; 2 Kor. 5:15; 13:5) Unaweza kumuuliza hivi, ‘Ulimwahidi nini Yehova ulipojiweka wakfu kwake?’ Jaribu kuchochea moyo wake kwa kumuuliza hivi, ‘Unafikiri Yehova alihisije ulipobatizwa?’ (Met. 27:11) ‘Unafikiri Shetani alihisije?’ (1 Pet. 5:8) Maandiko yaliyochaguliwa vizuri yanaweza kumchochea sana ndugu huyo.—Soma Waebrania 4:12.b
MNAOZOEZWA, IWENI WAAMINIFU
12, 13. (a) Elisha alikuwa na mtazamo gani alipokuwa akizoezwa? (b) Yehova alimthawabishaje Elisha kwa uaminifu wake?
12 Vijana, kutaniko linahitaji msaada wenu! Mnapaswa kuwa na mtazamo gani ili mfanikiwe katika utumishi wenu? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze matukio fulani ya wakati uliopita kumhusu Elisha.
13 Karibu miaka 3,000 hivi iliyopita, nabii Eliya alimwomba kijana Elisha awe msaidizi wake. Elisha alikubali mara moja mwaliko huo na kumhudumia Eliya kwa uaminifu akifanya kazi za hali ya chini. (2 Fal. 3:11) Baada ya kuzoezwa kwa miaka sita, Elisha alitambua kwamba kazi ya Eliya katika Israeli ilikaribia kwisha. Wakati huo, Eliya alimwambia Elisha asiendelee kufuatana naye, lakini mara tatu Elisha alimwambia Eliya hivi: “Sitakuacha.” Aliazimia kuandamana na Eliya kwa muda mrefu iwezekanavyo. Yehova alimthawabisha Elisha kwa sababu ya uaminifu na ushikamanifu wake; alishuhudia Eliya akichukuliwa katika dhoruba ya upepo.—2 Fal. 2:1-12.
14. (a) Wale wanaozoezwa wanawezaje kumwiga Elisha? (b) Kwa nini wanaozoezwa wanapaswa kuwa waaminifu?
14 Unawezaje kumwiga Elisha? Kubali migawo bila kusita, hata ikiwa ni ya hali ya chini. Mwone anayekuzoeza kuwa rafiki, na umweleze jinsi unavyothamini jitihada zake za kukuzoeza. Ukifanya hivyo, ni kana kwamba utakuwa ukimwambia: “Sitakuacha.” Zaidi ya yote, timiza kwa uaminifu mgawo wowote unaopewa. Kwa nini ni muhimu kufanya hivyo? Ukiwa mwaminifu na mwenye kutegemeka, wazee watakuwa na uhakika kwamba Yehova anataka ukabidhiwe majukumu zaidi kutanikoni.—Zab. 101:6; soma 2 Timotheo 2:2.
WAHESHIMU WANAOKUZOEZA
15, 16. (a) Elisha alionyeshaje kwamba alimheshimu yule aliyemzoeza? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 9.) (b) Kwa nini manabii wengine walimtumaini Elisha?
15 Simulizi la Elisha linaonyesha pia jinsi ndugu wanavyoweza kuwaheshimu wazee wenye uzoefu. Baada ya Eliya na Elisha kukutana na kundi la manabii huko Yeriko, walielekea kwenye Mto Yordani. Wakiwa hapo, “Eliya akachukua vazi lake rasmi, akalifunga, akapiga maji, nayo mwishowe yakagawanyika.” Baada ya kuvuka, waliendelea ‘kuzungumza huku wakitembea.’ Bila shaka, Elisha hakufikiri kwamba sasa anajua kila kitu. Alisikiliza kwa makini kila jambo ambalo Eliya alisema na kujifunza kutoka kwake. Kisha Eliya akachukuliwa na dhoruba ya upepo. Baadaye, Elisha alipofika kwenye Mto Yordani, aliyapiga maji kwa kutumia vazi la Eliya na kusema: “Yuko wapi Yehova Mungu wa Eliya?” Kwa mara nyingine, maji yakagawanyika.—2 Fal. 2:8-14.
16 Je, umetambua kwamba muujiza wa kwanza wa Elisha ulikuwa sawa kabisa na muujiza wa mwisho wa Eliya? Jambo hilo linatufundisha nini? Elisha hakuhisi kwamba alihitaji kufanya mambo kwa njia tofauti na ile iliyotumiwa na Eliya kwa sababu tu sasa yeye ndiye aliyekuwa na mamlaka. Badala yake, alimheshimu yule aliyemzoeza, yaani Eliya, kwa kuendeleza njia aliyotumia katika kutimiza huduma yake. Jambo hilo lilifanya manabii wenzake wamtumaini. (2 Fal. 2:15) Hata hivyo, katika miaka 60 ya huduma ya Elisha akiwa nabii, Yehova alimwezesha kufanya miujiza mingi zaidi kuliko Eliya. Wale wanaozoezwa wanajifunza nini?
17. (a) Wale wanaozoezwa wanawezaje kuiga mtazamo wa Elisha? (b) Yehova anaweza kuwatumiaje ndugu wanaozoezwa ambao ni waaminifu?
17 Usifikiri kwamba baada tu ya kukabidhiwa majukumu kutanikoni, basi unapaswa kubadili kila kitu, yaani, kufanya mambo kwa njia tofauti kabisa na yalivyokuwa yakifanywa mwanzoni. Mabadiliko hayafanywi kwa sababu tu unatamani kubadili mambo, badala yake hufanywa ikitegemea uhitaji wa kutaniko na mwongozo tunaopata kutoka katika tengenezo la Yehova. Elisha alifanya manabii wenzake wamtumaini na alimheshimu Eliya kwa kuendelea kutumia njia ambazo alitumia. Vivyo hivyo, ndugu na dada watakutumaini na utaonyesha unawaheshimu wazee wenye uzoefu kwa kuendelea kutumia njia zao zinazotegemea Biblia. (Soma 1 Wakorintho 4:17.) Hata hivyo, unapozidi kupata uzoefu, bila shaka utashiriki kufanya mabadiliko yatakayolisaidia kutaniko kwenda sambamba na tengenezo la Yehova. Kwa kweli, kama ilivyokuwa katika kisa cha Elisha, baada ya muda Yehova anaweza kukutumia kufanya kazi kubwa zaidi kuliko wale waliokuzoeza.—Yoh. 14:12.
18. Kwa nini ni muhimu sana kuwazoeza ndugu sasa?
18 Tunatumaini kwamba makala hii na ile iliyotangulia zitawachochea wazee wengi zaidi watenge wakati wa kuwazoeza wengine. Pia, tunatumaini kwamba ndugu wanaozoezwa watakubali kwa moyo mkunjufu mazoezi hayo na kuyatumia kwa hekima kuwatunza kondoo wa Yehova. Kufanya hivyo kutayaimarisha makutaniko ulimwenguni pote na kumsaidia kila mmoja wetu aendelee kuwa mwaminifu wakati wa matukio makubwa yaliyo mbele yetu.
a Ikiwa kijana Mkristo amekomaa kiroho, ni mnyenyekevu, na anatimiza matakwa ya Kimaandiko, wazee wanaweza kumpendekeza kuwa mtumishi wa huduma hata kama hajafikia umri wa miaka 20.—1 Tim. 3:8-10, 12; tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1989, ukurasa wa 29.
b Katika mazungumzo yako unaweza kutumia habari iliyo katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 2012, ukurasa wa 14-16, fungu la 8-13; na kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” sura ya 16, fungu la 1-3.
-