Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g16 Na. 2 kur. 3-7
  • Je, Biblia Ni Kitabu Chenye Manufaa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Biblia Ni Kitabu Chenye Manufaa?
  • Amkeni!—2016
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Biblia Inatupa Ufahamu wa Kiroho na wa Maadili
  • Biblia Inaeleza kwa Nini Wanadamu Wanateseka
  • Biblia Inatupa Tumaini
  • Mema na Mabaya: Biblia​—⁠Mwongozo Unaotegemeka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2024
  • Biblia Inazungumzia Nini?
    Amkeni!—2007
  • Mafundisho ya Kweli Yanayompendeza Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Je, Sayansi Inapatana na Biblia?
    Amkeni!—2011
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2016
g16 Na. 2 kur. 3-7
Mwanamume akisoma Biblia

HABARI KUU

Je, Biblia Ni Kitabu Chenye Manufaa?

Biblia ilikamilishwa miaka elfu mbili hivi iliyopita. Tangu wakati huo vitabu vingine vingi vimeandikwa na vikapitwa na wakati. Lakini Biblia haijapitwa na wakati. Fikiria mambo yafuatayo.

  • Biblia imeokoka mashambulizi mengi yaliyofanywa na watu wenye mamlaka. Kwa mfano, katika Enzi za Kati, katika nchi fulani zilizodai kuwa za Kikristo, “kumiliki na kusoma Biblia katika lugha ya kienyeji [lugha ya watu wa kawaida] kulihusianishwa na uasi na upinzani,” kinasema kitabu An Introduction to the Medieval Bible. Wasomi waliotafsiri Biblia katika lugha za kienyeji au waliowachochea watu kujifunza Biblia walihatarisha maisha yao. Hata baadhi yao waliuawa.

  • Licha ya kwamba Biblia ina maadui wengi, bado ndicho kitabu kilichosambazwa zaidi kuliko vingine vyote. Inakadiriwa kwamba nakala bilioni tano za Biblia, iwe ni Biblia nzima au sehemu, zimechapishwa katika lugha zaidi ya 2,800. Ni tofauti kabisa na vitabu vya falsafa, sayansi, na nyanja nyingine kama hizo, ambavyo huenda visisambazwe sana na vinapitwa upesi na wakati.

  • Kutafsiriwa kwa Biblia katika lugha mbalimbali kumesaidia kudumisha na kukuza baadhi ya lugha hizo. Tafsiri ya Kijerumani ya Martin Luther imeathiri sana lugha hiyo. Toleo la kwanza la King James Version limefafanuliwa kuwa “kitabu pekee chenye uvutano mkubwa zaidi kuwahi kuchapishwa” katika Kiingereza.

  • Biblia “imeathiri sana utamaduni wa nchi za Ulaya, ikaathiri si tu imani na desturi za kidini, bali pia sanaa, fasihi, sheria, siasa, na nyanja nyingine nyingi sana.”—The Oxford Encyclopedia of the Books of the Bible.

Hayo ni baadhi tu ya mambo hakika yanayoitofautisha Biblia na vitabu vingine. Lakini kwa nini Biblia ni maarufu sana? Kwa nini watu wamehatarisha maisha yao kwa ajili ya Biblia? Huenda sababu zikatia ndani mambo yafuatayo: Biblia ina mafundisho ya kimaadili na ya kiroho yenye hekima isiyo na kifani. Biblia inatusaidia kuelewa chanzo cha kuteseka na matatizo ya wanadamu. Pia, Biblia inaahidi kwamba matatizo hayo yatakwisha na inafunua jinsi hilo litakavyotimizwa.

TAARIFA FUPI

Biblia iliyofunguliwa

Biblia ni mkusanyo wa vitabu 66; kitabu hicho kitakatifu kilikamilishwa katika kipindi cha miaka 1,600 hivi.

Biblia iliandikwa na watu 40 hivi, ambao baadhi yao walikuwa wakulima, wavuvi, waamuzi, wafalme, na wanamuziki.

Kichwa kikuu cha Biblia ni Ufalme wa Mungu, serikali ya kimbingu itakayotawala dunia. (Danieli 2:44; 7:13, 14) Ufalme huo utaondoa uovu, kuteseka, na kifo kwa kuwaunganisha wanadamu chini ya Muumba wetu, Yehova Mungu, ambaye ana haki ya kutawala.—1 Wakorintho 15:24-26.

Biblia Inatupa Ufahamu wa Kiroho na wa Maadili

Elimu ni muhimu. Lakini “elimu . . . inayokufanya ujipatie vyeo . . . si lazima ikusaidie uwe na uwezo wa kufanya maamuzi yanayopatana na maadili,” inasema makala moja katika gazeti Ottawa Citizen la Kanada. Kwa kweli, uchunguzi uliofanywa ulimwenguni pote na shirika la Edelman la kuchunguza mahusiano ya umma, ulionyesha kwamba watu wengi wenye elimu ya juu, kutia ndani viongozi wa kibiashara na wa serikali, hudanganya, hufanya ulaghai, na kuiba, na hilo “huwafanya watu waache kuwaamini.”

Biblia inakazia hasa elimu ya maadili na ya kiroho. Inatusaidia kujua ni nini kinachomaanishwa na “uadilifu na hukumu na unyoofu, njia yote ya yaliyo mema.” (Methali 2:9) Kwa mfano, mwanamume mwenye umri wa miaka 23, ambaye tutamwita Stephen, alifungwa gerezani nchini Poland. Akiwa gerezani, alianza kujifunza Biblia na kuthamini ushauri wake. Aliandika hivi: “Sasa ninaelewa maana ya maneno ‘mheshimu baba yako na mama yako.’ Pia nimejifunza kuzuia hisia zangu, hasa hasira.”—Waefeso 4:31; 6:2.

Stephen alizingatia sana kanuni inayopatikana kwenye Methali 19:11: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita kosa.” Sasa, Stephen anapokabili hali inayomtatanisha, yeye hujaribu kuichanganua kwa utulivu na kufuata kanuni za Biblia zinazofaa. Anasema hivi: “Niligundua kwamba Biblia ndicho kitabu kilicho na mwongozo bora zaidi.”

Maria, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alitukanwa hadharani na mwanamke mwenye ubaguzi, ambaye alitokeza vurugu kubwa sana. Badala ya kulipiza kisasi, Maria aliondoka kwa utulivu. Mwanamke huyo akajihisi vibaya kwa sababu ya jambo alilofanya na akaanza kuwatafuta Mashahidi. Mwezi mmoja hivi baadaye, mwanamke huyo alipokutana na Maria, alimkumbatia na kumwomba msamaha. Isitoshe, alitambua kwamba imani ya Maria ndiyo iliyomfanya awe mpole na ajizuie. Ikawaje? Mwanamke huyo ambaye zamani alikuwa na ubaguzi, pamoja na watu watano wa familia yake, waliamua kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.

Yesu alisema kwamba hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matokeo yake. (Mathayo 11:19) Kwa hiyo, kuna uthibitisho mwingi kwamba kanuni za Biblia zina faida! Zinaboresha maisha yetu. ‘Zinamfanya asiye na uzoefu awe na hekima,’ na ‘zinaufanya moyo ushangilie,’ na ‘kuyafanya macho yang’ae’ kwa uelewaji wa kiroho na wa maadili.—Zaburi 19:7, 8.

Biblia Inaeleza kwa Nini Wanadamu Wanateseka

Wachunguzi wanapofanya utafiti kuhusu magonjwa ya mlipuko, wao hujaribu kupata kisababishi cha mlipuko huo. Kanuni hiyohiyo inatumika tunapotaka kuelewa chanzo cha migogoro na kuteseka kwa wanadamu. Biblia inatusaidia sana kuelewa wakati ambapo matatizo yetu yalianza, kwa kuwa inaeleza mambo yaliyotukia tangu mwanzo.

Kitabu cha Mwanzo kinafunua kwamba matatizo yetu yalianza wanadamu wa kwanza walipomwasi Mungu. Waliamua kujiamulia mema na mabaya—jambo ambalo ni Muumba peke yake aliye na haki ya kufanya. (Mwanzo 3:1-7) Inasikitisha kwamba tangu wakati huo watu kwa ujumla wamekuwa na mtazamo huo wa kujitegemea. Hali imekuwaje? Historia inaonyesha kwamba wanadamu hawana uhuru wala furaha, badala yake maisha yamejaa mizozo, ukandamizaji, na mvurugo wa maadili na wa kiroho. (Mhubiri 8:9) Biblia inasema hivi: “Mwanadamu . . . hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Lakini inapendeza kwamba hivi karibuni jitihada za wanadamu za kujitegemea zitakwisha.

Biblia Inatupa Tumaini

Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu hatavumilia ubaya na kuteseka milele, kwa kuwa anawapenda wale wanaoheshimu mamlaka yake na viwango vyake. Waovu “watakula matunda ya njia yao.” (Methali 1:30, 31) Lakini “wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.

Biblia iliyofunguliwa na kikombe kiko kando yake

“Mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:3, 4

Mungu atatimiza kusudi lake la kuleta amani duniani kupitia “ufalme wa Mungu.” (Luka 4:43) Ufalme huo ni serikali ya ulimwenguni pote, na kupitia ufalme huo Mungu ataonyesha kwamba ana haki ya kuwatawala wanadamu. Yesu alionyesha kwamba Ufalme huo utaitawala dunia, aliposema hivi katika sala ya mfano: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani.”—Mathayo 6:10.

Naam, raia wa Ufalme wa Mungu watafanya mapenzi ya Mungu, huku wakimtambua Muumba kuwa ndiye anayestahili kutawala, si mwanadamu yeyote. Ufisadi, pupa, matatizo ya kiuchumi, ubaguzi wa rangi, na vita vitakoma. Kihalisi kutakuwa na ulimwengu mmoja, serikali moja, na viwango vinavyofanana vya maadili na vya kiroho.—Ufunuo 11:15.

Kujipatia elimu ndiyo njia pekee ya kuingia katika ulimwengu huo mpya. Andiko la 1 Timotheo 2:3, 4 linasema hivi: “Mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” Kweli hiyo inatia ndani mafundisho ya Biblia kuhusu kile tunachoweza kulinganisha na katiba ya Ufalme huo, yaani, sheria na kanuni ambazo Ufalme huo utatumia kutawala. Yesu Kristo alizungumza kuhusu sheria na kanuni hizo katika Mahubiri yake ya Mlimani. (Mathayo, sura ya 5-7) Unaposoma sura hizo tatu, jaribu kuwazia jinsi maisha yatakavyokuwa wakati kila mtu atakapofuata hekima ya Yesu.

Je, tunapaswa kushangazwa kwamba Biblia ndicho kitabu kilichosambazwa zaidi ulimwenguni? La hasha! Mafundisho yake yanathibitisha wazi kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu. Kusambazwa kwake kunaonyesha kwamba Mungu anatamani watu wa lugha na mataifa yote wajifunze kumhusu na kufaidika kutokana na baraka ambazo Ufalme wake utaleta.—Matendo 10:34, 35.

Anga lenye nyota

Biblia inasema kwamba kuna sheria zinazoongoza mbingu

KITABU KINACHOFICHUA USHIRIKINA

Watu wa kale “waliamini kwamba ulimwengu unadhibitiwa na mapendezi ya miungu,” kinasema kitabu Encyclopedia of Science and Religion. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba ulimwengu unaongozwa na sheria za asili. Kwa mfano, miaka 3,500 hivi iliyopita, Biblia ilitaja kuhusu “sheria za mbingu [na za] duniani.” (Ayubu 38:33) Yeremia 31:35 inataja kuhusu “sheria za mwezi na nyota.” Watu waliokubali maoni hayo walilindwa na ibada ya uwongo na ushirikina.—Ayubu 31:26-28; Isaya 47:1, 13.

KITABU KILICHOANDIKWA KWA UNYOOFU

Sifa yenye kupendeza ya waandikaji wa Biblia ni unyoofu. Waliandika kwa unyoofu hata kuhusu makosa yao wenyewe. Kwa mfano, baada ya Mfalme Daudi kufanya uzinzi na mwanamke anayeitwa Bath-sheba, alisema hivi kwa unyoofu: “Nimefanya lililo baya machoni [pa Mungu].” (Zaburi 51:4) Mtume Yohana alikiri kwamba alianguka na kumwabudu malaika mara mbili. Malaika huyo alimwambia: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! . . . Mwabudu Mungu.” (Ufunuo 19:10; 22:8, 9) Tofauti na waandikaji wa kale, waandikaji wa Biblia walikuwa wanyoofu nyakati zote.

KITABU KINACHOWASAIDIA WATU KUWA NA AFYA NZURI YA AKILI

Biblia inatutia moyo tusitawishe sifa zinazoweza kutusaidia kuwa na afya nzuri ya akili, sifa kama vile huruma na kusamehe. Waefeso 4:32 inasema: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari.”

Makala moja iliyochapishwa na Kliniki ya Mayo, nchini Marekani inasema, “huenda wewe ndiye utakayepatwa na madhara makubwa ikiwa hutawasamehe watu.” Makala hiyo ilieleza kwamba kuwasamehe wengine kunaweza kumletea mtu faida, kama vile kuwa na “mahusiano mazuri zaidi; hali nzuri zaidi ya kiroho na kisaikolojia; kupunguza wasiwasi, mkazo, na uhasama; shinikizo la chini la damu; kupunguza uwezekano wa kushuka moyo; na kupunguza hatari ya kutumia vibaya kileo na dawa za kulevya.”

KITABU KINACHOJIBU MASWALI MUHIMU ZAIDI MAISHANI

Kiini-tete cha mwanadamu

Kiini-tete cha mwanadamu

Sayansi inajibu maswali ya aina nyingi. Hata hivyo, ina mipaka. Kitabu Biotechnology—Changing Life Through Science kinasema: “Wanasayansi, madaktari, na wanafalsafa wengi wanakubali kwamba sayansi haiwezi kujibu maswali kuhusu maadili au dini.”

  • SAYANSI INAWEZA kutueleza kuhusu sheria zinazoongoza ulimwengu wetu kwa kutumia hisabati, lakini haiwezi kutueleza kwa nini ulimwengu wetu upo au kwa nini unaongozwa na sheria hususa.

  • SAYANSI INAWEZA kueleza jinsi viungo vya uzazi vinavyofanya kazi, lakini haiwezi kutusaidia kufanya maamuzi mazuri na ya kimaadili kuhusu ngono.

  • SAYANSI INAWEZA kueleza jinsi kiini-tete cha mwanadamu kinavyokua, lakini haiwezi kutusaidia kuamua ikiwa kutoa mimba ni jambo jema au baya.

Biblia inajibu maswali hayo muhimu na mengine mengi, na hivyo kutusaidia kuelewa “uadilifu na hukumu na unyoofu, njia yote ya yaliyo mema.”—Methali 2:9.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki