-
Ndoa—Zawadi Kutoka kwa Mungu Mwenye Upendo“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
-
-
SURA YA 10
Ndoa—Zawadi Kutoka kwa Mungu Mwenye Upendo
“Kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.”—MHUBIRI 4:12.
1, 2. (a) Nyakati nyingine tunajiuliza nini kuhusu wenzi wapya wa ndoa, na kwa nini? (b) Tutazungumzia maswali gani katika sura hii?
JE, UNAPENDA kwenda kwenye arusi? Wengi wanapenda, kwa sababu mara nyingi hizo huwa pindi zenye kufurahisha sana. Bwana na bibi-arusi wanavalia mavazi yenye kupendeza kwelikweli. Zaidi ya hilo, nyuso zao zinaonyesha kwamba wana shangwe nyingi! Siku hiyo, wana furaha nyingi na inaonekana wana matazamio mengi mazuri ya wakati ujao.
2 Hata hivyo, ukweli ni kwamba ndoa nyingi leo ziko mashakani. Ingawa tunawatakia mema wenzi wapya wa ndoa, nyakati nyingine tunajiuliza: ‘Je, ndoa hii itakuwa na furaha? Itadumu?’ Majibu ya maswali hayo yanategemea ikiwa mume na mke wanaamini na kutumia shauri la Mungu kuhusu ndoa. (Methali 3:5, 6) Wanahitaji kufanya hivyo ili waendelee kukaa katika upendo wa Mungu. Acheni tuchunguze majibu ya Biblia kwa maswali haya manne: Kwa nini ufunge ndoa? Ikiwa utafunga ndoa, utachagua mwenzi wa aina gani? Unaweza kujitayarisha jinsi gani kwa ajili ya ndoa? Na ni nini kinachoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa waendelee kuwa na furaha?
KWA NINI UFUNGE NDOA?
3. Kwa nini si jambo la hekima kufunga ndoa kwa sababu ndogo-ndogo?
3 Watu fulani wanaamini kwamba siri ya kuwa na furaha ni kufunga ndoa na kwamba huwezi kamwe kutosheka au kuwa na furaha maishani ikiwa huna mwenzi wa ndoa. Hilo si kweli hata kidogo! Yesu, ambaye alikuwa mseja, alisema useja ni zawadi, naye aliwahimiza wale wanaoweza waupe nafasi. (Mathayo 19:11, 12) Mtume Paulo pia alizungumzia faida za useja. (1 Wakorintho 7:32-38) Hata hivyo, Yesu na Paulo hawakuweka sheria kuhusu jambo hilo; na ‘kukataza kufunga ndoa’ ni ‘fundisho la roho waovu.’ (1 Timotheo 4:1-3) Lakini wale wanaotaka kumtumikia Yehova bila kukengeushwa wanaweza kufaidika kwa kuendelea kuwa waseja. Basi, si jambo la hekima kufunga ndoa kwa sababu ndogo-ndogo, kama vile kufunga ndoa kwa sababu tu wenzako wamefunga ndoa au kwamba wanakutia moyo ufanye hivyo.
4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba ndoa nzuri huandaa mazingira yanayofaa ya kuwalea watoto?
4 Kwa upande mwingine, je, kuna sababu nzuri za kufunga ndoa? Ndiyo. Ndoa pia ni zawadi kutoka kwa Mungu mwenye upendo. (Mwanzo 2:18) Kwa hiyo, inatimiza mambo fulani mazuri na inaweza kuleta furaha. Kwa mfano, ndoa nzuri ndio msingi bora wa maisha ya familia. Watoto wanahitaji kulelewa katika mazingira yanayofaa wakiwa na wazazi wanaowapenda, wanaowatia nidhamu, na kuwapa mwongozo. (Zaburi 127:3; Waefeso 6:1-4) Hata hivyo, kusudi la ndoa si kupata na kulea watoto tu.
5, 6. (a) Kulingana na Mhubiri 4:9-12, urafiki wa karibu una faida gani? (b) Ndoa inaweza kuwa kama kamba yenye nyuzi tatu jinsi gani?
5 Fikiria andiko la msingi la sura hii pamoja na mistari inayotangulia: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake. Lakini itakuwaje kwa yule aliye peke yake akianguka wakati ambapo hakuna mwingine wa kumwinua? Tena, wawili wakilala pamoja, watapata joto; lakini aliye peke yake anawezaje kupata joto? Na mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake. Nayo kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.”—Mhubiri 4:9-12.
6 Andiko hilo linazungumzia hasa faida ya urafiki. Bila shaka, ndoa ni muungano wa marafiki wa karibu zaidi. Kama andiko hilo linavyoonyesha, katika muungano huo wenzi wa ndoa wanaweza kupata msaada, faraja, na ulinzi. Ili kifungo cha ndoa kiwe imara zaidi, mengi zaidi yanahitajika. Kamba yenye nyuzi mbili, kama mstari huo unavyodokeza, inaweza kukatika. Lakini kamba yenye nyuzi tatu zilizosokotwa au kufumwa pamoja haikatiki kwa urahisi. Lengo kuu la mume na mke linapokuwa kumpendeza Yehova, ndoa yao ni kama kamba yenye nyuzi tatu. Kwa kuwa Yehova anahusishwa kabisa, ndoa hiyo inakuwa muungano imara sana.
7, 8. (a) Paulo aliwapa shauri gani Wakristo ambao hawajafunga ndoa wanaopambana na tamaa za ngono? (b) Biblia inatusaidia jinsi gani kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu ndoa?
7 Pia, katika ndoa ndipo tu tamaa za ngono zinaweza kutoshelezwa inavyofaa. Ni katika kifungo hicho tu ambapo mahusiano ya kingono huonwa kwa kufaa kuwa chanzo cha shangwe. (Methali 5:18) Hata baada ya mtu kupita kipindi ambacho Biblia inakiita “upeo wa ujana”—wakati ambapo tamaa za ngono huanza kuwaka—huenda bado akahitaji kuzuia tamaa hizo. Zisipozuiliwa, tamaa hizo zinaweza kumwingiza katika mwenendo mchafu au usiofaa. Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuwapa watu ambao hawajafunga ndoa shauri hili: “Ikiwa hawawezi kujizuia, acheni wafunge ndoa, kwa maana ni bora kufunga ndoa kuliko kuwaka tamaa.”—1 Wakorintho 7:9, 36; Yakobo 1:15.
8 Hata kuwe na sababu gani za kufunga ndoa, mtu anapaswa kuona mambo kihalisi. Kama Paulo alivyosema, wale wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Watu waliofunga ndoa hupata matatizo fulani ambayo waseja hawapati. Hata hivyo, ukiamua kufunga ndoa, unaweza kufanya nini ili upunguze matatizo na kuwa na furaha zaidi? Njia moja ni kuchagua mwenzi wa ndoa kwa hekima.
KUCHAGUA MWENZI WA NDOA ANAYEFAA
9, 10. (a) Paulo alionyesha jinsi gani hatari ya kuwa na urafiki wa karibu pamoja na wasioamini? (b) Mara nyingi kupuuza shauri la Mungu la kutofunga ndoa na mtu asiyeamini huwa na matokeo gani?
9 Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kanuni ya maana ambayo mtu anapaswa kutumia anapochagua mwenzi wa ndoa: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” (2 Wakorintho 6:14) Mfano aliotumia unatokana na maisha ya ukulima. Wanyama wawili wanaotofautiana sana kwa ukubwa au nguvu wakifungwa nira pamoja, wote wawili wataumia. Vivyo hivyo, mwamini na mtu asiyeamini wanapofungwa nira pamoja katika ndoa, bila shaka watakwaruzana na kugongana-gongana. Ikiwa mmoja wao anataka kuendelea kukaa katika upendo wa Yehova naye yule mwingine hajali hata kidogo, mambo wanayotanguliza maishani yatatofautiana na huenda hilo likatokeza mkazo mwingi. Hivyo, Paulo aliwasihi Wakristo wafunge ndoa “katika Bwana tu.”—1 Wakorintho 7:39.
10 Nyakati nyingine, Wakristo fulani ambao hawajafunga ndoa wanaona kwamba ni afadhali kufungwa nira isivyo sawa kuliko kuishi maisha ya upweke. Wengine wanaamua kupuuza shauri la Biblia na kufunga ndoa na mtu ambaye hamtumikii Yehova. Mara nyingi matokeo yamekuwa yenye kusikitisha. Watu hao hujikuta wamefunga ndoa na mtu ambaye hawawezi kuzungumza pamoja naye mambo ya maana zaidi maishani. Wanakuwa wapweke hata zaidi kuliko walivyokuwa kabla ya kufunga ndoa. Inafurahisha kwamba kuna maelfu ya Wakristo waseja wanaotegemea na kushikamana na mashauri ya Mungu kuhusu jambo hilo. (Zaburi 32:8) Ingawa wanatarajia kwamba siku moja watafunga ndoa, wanaendelea kuwa waseja mpaka watakapopata mwenzi kati ya wale wanaomwabudu Yehova Mungu.
11. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuchagua mwenzi wa ndoa kwa hekima? (Ona pia sanduku “Ninatafuta Mwenzi wa Aina Gani?”)
11 Hata hivyo, haimaanishi kwamba kila mtumishi wa Yehova anaweza kuwa mwenzi wa ndoa anayefaa. Ikiwa unafikiria kufunga ndoa, tafuta mtu ambaye utu na miradi yake ya kiroho inapatana na yako, na anampenda Mungu kama wewe. Jamii ya mtumwa mwaminifu imechapisha habari nyingi kuhusu jambo hilo, na ingefaa ufikirie kwa uzito na kusali kuhusu mashauri hayo ya Kimaandiko, na kuwa tayari kuongozwa nayo unapofanya uamuzi huo muhimu.a—Zaburi 119:105.
12. Ni desturi gani kuhusu ndoa inayofuatwa katika nchi nyingi, na ni mfano gani wa Biblia unaotoa mwongozo?
12 Katika nchi nyingi, wazazi humchagulia mtoto wao mwenzi. Kulingana na utamaduni wa watu katika maeneo hayo, wazazi huonwa kuwa wana hekima na uzoefu mwingi zaidi ambao unahitajiwa ili kufanya uamuzi huo wa maana. Mara nyingi ndoa hizo zinafaulu, kama ilivyokuwa nyakati za Biblia. Mfano wa Abrahamu wa kumtuma mtumishi wake akamtafutie Isaka mke unaweza kuwasaidia wazazi walio katika hali kama hiyo leo. Abrahamu hakuhangaikia pesa wala umaarufu. Badala yake, alifanya juu chini kumtafutia Isaka mke kati ya watu wanaomwabudu Yehova.b—Mwanzo 24:3, 67.
KUJITAYARISHIA NDOA YENYE MAFANIKIO
13-15. (a) Kanuni iliyo katika Methali 24:27 inaweza kumsaidia jinsi gani mwanamume anayefikiria kufunga ndoa? (b) Mwanamke anaweza kufanya nini ili kujitayarisha kwa ajili ya ndoa?
13 Ikiwa unafikiria kwa uzito kufunga ndoa, unapaswa kujiuliza, ‘Niko tayari kweli?’ Jibu la swali hilo halitegemei tu maoni yako kuhusu upendo, ngono, kuwa na mwenzi, au kulea watoto. Badala yake, kuna miradi hususa ambayo kila mwanamume au mwanamke anayetaka kufunga ndoa anapaswa kufikiria.
14 Mwanamume anayetafuta mke anapaswa kufikiria kwa uzito kanuni hii: “Tayarisha kazi yako huko nje, uifanye tayari kwa ajili yako shambani. Kisha ujenge nyumba yako.” (Methali 24:27) Andiko hilo linamaanisha nini? Katika siku hizo, mwanamume alipotaka ‘kujenga nyumba yake’ au kuwa na familia kwa kufunga ndoa, alipaswa kujiuliza, ‘Ninaweza kumtunza na kumtegemeza mke na watoto wowote tunaoweza kuwapata baadaye?’ Kwanza alipaswa kufanya kazi, atunze mashamba au mazao yake. Kanuni hiyohiyo inatumika leo. Mwanamume anayetaka kuoa anapaswa kujitayarisha kwa ajili ya majukumu ya ndoa. Maadamu afya yake inamruhusu, ana wajibu wa kufanya kazi. Neno la Mungu linaonyesha kwamba mtu ambaye haandalii familia yake mahitaji ya kimwili, kihisia, na kiroho ni mbaya kuliko asiye na imani!—1 Timotheo 5:8.
15 Vivyo hivyo, mwanamke anayeamua kuolewa anakubali kuchukua majukumu mazito. Biblia inataja stadi na sifa ambazo mke anahitaji anapomsaidia mume wake na anapoitunza familia yake. (Methali 31:10-31) Wanaume na wanawake wanaokimbilia maisha ya ndoa bila kuwa tayari kwa ajili ya majukumu yanayohusika ni wenye ubinafsi, nao hawafikirii wanachoweza kuchangia katika ndoa. Zaidi ya yote, wale wanaofikiria kufunga ndoa wanahitaji kujitayarisha kiroho.
16, 17. Wale wanaopanga kufunga ndoa wanapaswa kufikiria kwa uzito kanuni gani za Maandiko?
16 Kujitayarisha kwa ajili ya ndoa kunatia ndani kufikiria kwa uzito majukumu ambayo Mungu amempa mume na mke. Mwanamume anapaswa kujua maana ya kuwa kichwa katika familia ya Kikristo. Jukumu hilo si leseni ya kupiga ubwana. Badala yake, lazima amwige Yesu katika kuutumia ukichwa. (Waefeso 5:23) Vivyo hivyo, mwanamke Mkristo anapaswa kuelewa jukumu lake lenye heshima akiwa mke. Je, yuko tayari kujitiisha chini ya “sheria ya mume wake”? (Waroma 7:2) Tayari yuko chini ya sheria ya Yehova na ya Kristo. (Wagalatia 6:2) Mamlaka ya mume wake katika familia ni sheria nyingine. Je, anaweza kuunga mkono na kutii mamlaka ya mwanamume asiye mkamilifu? Ikiwa hayuko tayari kufanya hivyo, afadhali asiolewe.
17 Zaidi ya hilo, kila mmoja anapaswa kuwa tayari kutosheleza mahitaji ya pekee ya mwenzi wake wa ndoa. (Wafilipi 2:4) Paulo aliandika: “Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” Akiongozwa na roho ya Mungu, Paulo alitambua kwamba mwanamume ana uhitaji wa pekee wa kuhisi kwamba mke wake anamheshimu sana. Naye mke ana uhitaji wa pekee wa kuhisi kwamba mume wake anampenda.—Waefeso 5:21-33.
Wakati wa uchumba, wachumba wengi hutenda kwa hekima kwa kuambatana na mtu mwingine katika matembezi yao
18. Kwa nini wachumba wanapaswa kuonyesha sifa ya kujizuia wakati wa uchumba?
18 Kwa hiyo basi, uchumba si kipindi cha kujifurahisha tu. Ni wakati wa mwanamume na mwanamke kujifunza kutendeana inavyofaa na kuona ikiwa wanafaana kwa ajili ya ndoa. Pia ni wakati wa kuonyesha sifa ya kujizuia! Kupita mipaka katika kuonyeshana mahaba kunaweza kuwa kishawishi chenye nguvu sana, kwa kuwa kila mmoja anavutiwa na mwenzake. Hata hivyo, wale wanaopendana kikweli wataepuka matendo yoyote yanayoweza kuharibu uhusiano wa mpendwa wao pamoja na Mungu. (1 Wathesalonike 4:6) Kwa hiyo, ikiwa una uchumba, onyesha sifa ya kujizuia; sifa hiyo inaweza kukusaidia katika maisha yako yote, iwe utafunga ndoa au hapana.
UNAWEZA KUFANYA NINI ILI NDOA IDUMU?
19, 20. Toa mfano unaoonyesha jinsi maoni ya Mkristo kuhusu ndoa yanavyopaswa kutofautiana na maoni ya watu wengi ulimwenguni leo.
19 Ikiwa wenzi wanataka ndoa yao idumu, wanapaswa kuwa na maoni yanayofaa kuhusu uwajibikaji. Mara nyingi sinema na vitabu vya hadithi huisha watu wawili wanaopendana wakifunga ndoa na kuishi raha mustarehe, maisha ambayo wengi hutamani sana. Lakini, katika maisha halisi, ndoa si mwisho bali ni mwanzo—mwanzo wa kitu ambacho Yehova alitaka kidumu. (Mwanzo 2:24) Kwa kusikitisha, watu wengi ulimwenguni leo hawana maoni hayo. Watu fulani hulinganisha kufunga ndoa na “kufunga pingu za.” Huenda wasitambue jinsi hilo linavyofafanua vizuri maoni ya wengi leo kuhusu ndoa. Namna gani? Ingawa pingu zinaweza kufunga kitu kwa nguvu kwa muda unaohitajika, zinaweza pia kufunguliwa kwa urahisi.
20 Wengi leo huona ndoa kuwa ya muda tu. Wanaingia katika ndoa haraka-haraka kwa kuwa wanafikiri itatosheleza mahitaji yao, lakini wanatazamia kwamba watatoka kwa urahisi mambo yakichacha. Hata hivyo, kumbuka kwamba Biblia inapozungumzia kifungo, kama vile kifungo cha ndoa, inatumia mfano wa kamba. Kamba za meli hukusudiwa kudumu, zisikatike-katike wala kufumuka hata kunapokuwa na dhoruba kali sana. Vivyo hivyo, ndoa imekusudiwa kudumu. Kumbuka kwamba Yesu alisema: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mathayo 19:6) Ukifunga ndoa, unapaswa kuwa na maoni hayohayo kuhusu ndoa. Je, uwajibikaji wa aina hiyo huifanya ndoa iwe mzigo? Hapana.
21. Mume au mke anapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mwenzi wake, na ni nini kinachoweza kuwasaidia kufanya hivyo?
21 Kila mmoja anapaswa kuendelea kuwa na maoni yanayofaa kuhusu mwenzi wake wa ndoa. Kila mmoja wao akifanya yote awezayo kukazia fikira sifa nzuri na bidii ya mwenzake, ndoa hiyo itakuwa yenye furaha na yenye kuburudisha. Je, kuwa na maoni yanayofaa kuhusu mwenzi asiye mkamilifu ni kujifanya kipofu? Yehova hawezi kamwe kuwa kipofu, hata hivyo, sisi hutazamia awe na maoni yanayofaa kutuelekea. Mtunga-zaburi alisema: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Waume na wake pia wanapaswa kuwa na maoni yanayofaa na kuwa tayari kuwasamehe wenzi wao wa ndoa.—Wakolosai 3:13.
22, 23. Abrahamu na Sara waliweka mfano gani mzuri kwa wenzi wa ndoa leo?
22 Kadiri miaka inavyopita, ndoa inaweza kuwa baraka hata zaidi. Biblia inazungumzia ndoa ya Abrahamu na Sara walipokuwa wazee. Bila shaka maisha yao yalikuwa na mabonde na milima. Wazia hali ya Sara. Huenda alikuwa na umri wa miaka 60 na kitu alipoondoka makao yake yenye starehe katika jiji lenye ufanisi la Uru na kwenda kuishi katika mahema maisha yake yote. Hata hivyo, alijitiisha chini ya ukichwa wa mume wake. Alikuwa kikamilisho na msaidizi kwelikweli kwa Abrahamu, na kwa heshima alimsaidia kufanikisha maamuzi yake. Ujitiisho wake haukuwa wa kijuujuu. Hata “ndani yake mwenyewe,” alimwita mume wake bwana. (Mwanzo 18:12; 1 Petro 3:6) Alimheshimu Abrahamu kutoka moyoni.
23 Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba Abrahamu na Sara walikubaliana katika kila jambo. Siku moja alitoa pendekezo ambalo “halikumpendeza Abrahamu hata kidogo.” Lakini Abrahamu alitii maagizo ya Yehova, na kwa unyenyekevu akaisikiliza sauti ya mke wake, nayo familia yao ikabarikiwa. (Mwanzo 21:9-13) Waume na wake leo, hata wale ambao wamekuwa katika kifungo cha ndoa kwa miaka mingi, wanaweza kujifunza mengi kutokana na wenzi hao wenye kumwogopa Mungu.
24. Ni ndoa za aina gani zinazomletea heshima Yehova Mungu, na kwa nini?
24 Katika kutaniko la Kikristo, kuna maelfu ya ndoa zenye furaha—ambamo mke anamheshimu sana mume wake, mume anampenda na kumstahi mke wake, na wote wawili wanatanguliza mapenzi ya Yehova maishani mwao. Ukiamua kufunga ndoa, chagua mwenzi wa ndoa kwa hekima, jitayarishe vizuri kwa ajili ya ndoa, na ufanye yote uwezayo kuwa na ndoa yenye amani na upendo ambayo inamletea heshima Yehova Mungu. Ukifanya hivyo, ndoa yako itakusaidia kukaa katika upendo wa Mungu.
a Ona sura ya 2 ya kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
b Katika taifa la Israeli, watu fulani waaminifu walikuwa na wake wengi. Ingawa Yehova hakuanzisha zoea hilo, aliliruhusu, naye alitoa mwongozo ambao ungefuatwa katika ndoa za aina hiyo. Hata hivyo, Wakristo wanajua kwamba Yehova haruhusu tena waabudu wake wawe na wake wengi.—Mathayo 19:9; 1 Timotheo 3:2.
-
-
“Ndoa na Iheshimiwe”“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
-
-
SURA YA 11
“Ndoa na Iheshimiwe”
“Ushangilie pamoja na mke wa ujana wako.”—METHALI 5:18.
1, 2. Tutazungumzia swali gani, na kwa nini?
JE, UMEFUNGA ndoa? Ikiwa ndivyo, je, unapata furaha katika ndoa yako au kuna matatizo mazito? Je, pengo kati yako na mwenzi wako linazidi kuongezeka? Je, unavumilia maisha ya ndoa badala ya kuyafurahia? Ikiwa ndivyo, inaelekea unasikitika kwamba upendo uliokuwapo mwanzoni katika ndoa yako umepoa. Ukiwa Mkristo, ni wazi kwamba ungependa ndoa yako imletee utukufu Yehova, Mungu unayempenda. Hivyo, huenda hali ya ndoa yako sasa inakuhangaisha na kukuvunja moyo sana. Hata hivyo, tafadhali usikate kauli kwamba ndoa yako imegonga mwamba.
2 Leo, kuna wenzi wa ndoa Wakristo ambao ndoa zao zilikuwa katika hali mahututi wakati fulani. Hata hivyo, walipata njia ya kuimarisha uhusiano wao. Wewe pia unaweza kupata furaha katika ndoa. Jinsi gani?
KUMKARIBIA MUNGU NA MWENZI WAKO
3, 4. Toa mfano unaoonyesha kwa nini wenzi wa ndoa wanaweza kukaribiana wakijitahidi kumkaribia Mungu.
3 Wewe na mwenzi wako mtazidi kuwa na uhusiano wa karibu ikiwa mtajitahidi kumkaribia Mungu. Kwa nini? Hebu fikiria mfano huu: Wazia mlima ulio mpana chini na ambao umechongoka juu. Tuseme kwamba mwanamume amesimama chini ya mlima huo upande wa kaskazini huku mwanamke akiwa amesimama chini ya mlima huo upande wa kusini. Wote wawili wanaanza kuupanda. Mwanzoni wanatenganishwa na sehemu pana ya mlima. Lakini kadiri wanavyoendelea kupanda juu zaidi na zaidi kuelekea kilele cha mlima huo, ndivyo wanavyozidi kukaribiana. Je, unaona jambo lenye kutia moyo katika mfano huo?
4 Jitihada zako za kumtumikia Yehova kikamili zinaweza kulinganishwa na jitihada za kupanda mlima. Kwa kuwa unampenda Yehova, tayari unajitahidi sana kuupanda mlima huo wa mfano. Lakini, ikiwa kuna pengo kati yako na mwenzi wako, huenda mko pande tofauti za mlima. Hata hivyo, ni nini kinachotukia mnapozidi kuupanda? Ni kweli kwamba mwanzoni kila mmoja yuko mbali sana na mwingine. Hata hivyo, kadiri mnavyotia bidii kumkaribia Mungu, yaani, kuzidi kuupanda mlima huo wa mfano, ndivyo wewe na mwenzi wako mnavyozidi kukaribiana. Kwa kweli, kumkaribia Mungu ndiyo siri ya kumkaribia mwenzi wako. Lakini unaweza kufanya hivyo jinsi gani?
Ujuzi wa Biblia unapotumiwa, unaweza kuimarisha ndoa yenu
5. (a) Taja njia moja ya kumkaribia Yehova na mwenzi wa ndoa. (b) Yehova ana maoni gani kuhusu ndoa?
5 Njia moja muhimu ambayo wewe na mwenzi wako mnaweza kuupanda mlima huo wa mfano ni kwa kutii shauri la Neno la Mungu kuhusu ndoa. (Zaburi 25:4; Isaya 48:17, 18) Hivyo basi, fikiria shauri hususa ambalo mtume Paulo alitoa. Alisema: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote.” (Waebrania 13:4) Hilo linamaanisha nini? Neno “iheshimiwe” linadokeza wazo la kuona kitu kuwa cha maana sana na chenye thamani. Na hivyo ndivyo Yehova anavyoiona ndoa—anaiona kuwa yenye thamani kubwa.
KUMPENDA YEHOVA NA KUKUCHOCHEE
6. Muktadha wa shauri la Paulo kuhusu ndoa unaonyesha nini, na kwa nini hilo ni jambo la maana kukumbuka?
6 Bila shaka, kwa kuwa wewe na mwenzi wako ni watumishi wa Mungu, tayari mnajua kwamba ndoa ni yenye thamani na takatifu. Yehova mwenyewe ndiye aliyeanzisha mpango wa ndoa. (Mathayo 19:4-6) Hata hivyo, ikiwa kwa sasa una matatizo katika ndoa, kujua tu kwamba ndoa inaheshimika hakutoshi kukuchochea wewe na mwenzi wako kupendana na kuheshimiana. Ni nini basi kitakachowachochea? Ona jinsi Paulo alivyozungumzia suala la kuonyesha heshima katika ndoa. Hakusema, “ndoa inaheshimiwa”; badala yake alisema, “ndoa na iheshimiwe.” Paulo hakuwa akisema jinsi mambo yalivyo; bali alikuwa akitoa himizo.a Kukumbuka jambo hilo kunaweza kukuchochea hata zaidi kuanza tena kumthamini mwenzi wako. Kwa nini?
7. (a) Ni amri gani za Kimaandiko tunazotii, na kwa nini? (b) Ni matokeo gani mazuri yanayotokana na utii?
7 Hebu fikiria jinsi unavyoona amri nyingine za Kimaandiko, kama vile utume wa kufanya wanafunzi au shauri la kukutana pamoja ili kuabudu. (Mathayo 28:19; Waebrania 10:24, 25) Ni kweli kwamba nyakati nyingine si rahisi kutimiza amri hizo. Watu unaowahubiria wanaweza kukupinga, au unaweza kuchoka sana kwa sababu ya kazi ya kimwili unayofanya hivi kwamba inakuwa vigumu sana kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hata hivyo, unaendelea kuhubiri ujumbe wa Ufalme, na unaendelea kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hakuna mtu anayeweza kukuzuia—hata Shetani! Kwa nini? Kwa sababu kumpenda Yehova kutoka moyoni kunakuchochea kutii amri zake. (1 Yohana 5:3) Kufanya hivyo kuna matokeo gani mazuri? Kuhubiri na kuhudhuria mikutano kunakuwezesha kuwa na amani ya akili na shangwe moyoni kwa sababu unajua kwamba unafanya mapenzi ya Mungu. Na unapohisi hivyo, unapata nguvu mpya. (Nehemia 8:10) Tunajifunza nini?
8, 9. (a) Ni nini kinachoweza kutuchochea kutii himizo la kuiheshimu ndoa, na kwa nini? (b) Tutazungumzia hoja gani mbili?
8 Kama vile kumpenda Mungu sana kunavyokuchochea kutii amri ya kuhubiri na kukutanika pamoja hata kunapokuwa na vizuizi, ndivyo kumpenda Yehova kunavyoweza pia kukuchochea kutii himizo la Biblia la kuifanya ‘ndoa yako iheshimiwe,’ hata inapoonekana kuwa vigumu. (Waebrania 13:4; Zaburi 18:29; Mhubiri 5:4) Pia, kama vile Mungu anavyobariki sana jitihada zako za kuhubiri na kuhudhuria mikutano, ndivyo anavyoona na kubariki jitihada zako za kuiheshimu ndoa yako.—1 Wathesalonike 1:3; Waebrania 6:10.
9 Basi, unaweza kufanya nini ili ndoa yako iheshimiwe? Unahitaji kuepuka mwenendo ambao utaharibu mpango wa ndoa. Vilevile, unahitaji kuchukua hatua ambazo zitaimarisha kifungo cha ndoa.
EPUKA USEMI NA MWENENDO UNAOFANYA NDOA ISIHESHIMIKE
10, 11. (a) Ni mwenendo gani unaofanya ndoa isiheshimike? (b) Tunaweza kumuuliza nini mwenzi wa ndoa?
10 Wakati fulani, mke mmoja Mkristo alisema: “Mimi husali kwa Yehova anipe nguvu za kuvumilia.” Kuvumilia nini? Alieleza hivi: “Mume wangu hunishambulia kwa maneno. Sina majeraha mwilini, lakini maneno yake yenye kuchoma anayosema kila wakati, kama vile ‘Umenichosha!’ na ‘Wewe ni bure kabisa!’ yananiumiza sana moyoni.” Mke huyo anataja jambo zito sana—maneno yenye kuumiza katika ndoa.
11 Ni jambo lenye kusikitisha kama nini wakati wenzi wa ndoa Wakristo wanaporushiana maneno yenye kuchoma na kusababisha maumivu ya kihisia ambayo si rahisi kupona! Bila shaka, wenzi wa ndoa wanapotumia usemi wenye kuumiza, ndoa yao haiheshimiki. Je, hivyo ndivyo ndoa yako ilivyo? Unaweza kujua kwa kumuuliza mwenzi wako kwa unyenyekevu, “Je, maneno yangu yanakuumiza?” Ikiwa mwenzi wako anahisi kwamba mara kwa mara maneno yako yanamuumiza kihisia, unapaswa kuwa tayari kufanya marekebisho.—Wagalatia 5:15; Waefeso 4:31.
12. Ni nini kinachoweza kufanya ibada ya mtu iwe ubatili machoni pa Mungu?
12 Usisahau kamwe kwamba uhusiano wako pamoja na Yehova unaweza kuwa mzuri au mbaya ikitegemea jinsi unavyoutumia ulimi wako katika ndoa. Biblia inasema: “Ikiwa mtu yeyote anajiona kuwa mwabudu anayeshikilia vizuri namna ya ibada na bado hauongozi ulimi wake, bali anaendelea kuudanganya moyo wake mwenyewe, namna ya ibada ya mtu huyo ni ya ubatili.” (Yakobo 1:26) Maneno yako yanahusiana sana na ibada yako. Biblia haiungi mkono maoni ya kwamba chochote kinachotendeka nyumbani si neno mradi mtu anadai kumtumikia Mungu. Tafadhali usijidanganye. Hilo ni jambo zito. (1 Petro 3:7) Unaweza kuwa mtu mwenye vipawa na bidii nyingi, lakini ikiwa unamuumiza mwenzi wako kwa maneno yanayomkatakata, unakosa kuuheshimu mpango wa ndoa na huenda Mungu akaiona ibada yako kuwa ubatili mtupu.
13. Mwenzi wa ndoa anaweza kusababisha maumivu ya moyoni jinsi gani?
13 Wenzi wa ndoa wanapaswa pia kuwa waangalifu wasisababishe maumivu ya moyoni kwa njia nyingine zisizo za moja kwa moja. Fikiria mifano miwili: Mama asiye na mwenzi anampigia simu kwa ukawaida mwanamume Mkristo katika kutaniko lao ambaye amefunga ndoa ili kumwomba mashauri, nao wanazungumza kwa muda mrefu; ndugu Mkristo aliye mseja anahubiri kwa muda mrefu kila juma pamoja na dada Mkristo aliyeolewa. Katika mifano hiyo, huenda watu hao waliofunga ndoa hawana nia mbaya; hata hivyo, mwenendo wao unawafanya wenzi wao wa ndoa wajisikie namna gani? Mke aliyekuwa katika hali kama hiyo alisema: “Ninaumia ninapoona mume wangu akitumia muda mwingi sana ili kumhangaikia dada mwingine kutanikoni. Hilo hunifanya nihisi kwamba sifai.”
14. (a) Ni wajibu gani wa ndoa unaokaziwa katika Mwanzo 2:24? (b) Tunapaswa kujiuliza nini?
14 Mwenzi huyo na wenzi wengine wa ndoa walio katika hali kama hiyo wanaumia kihisia kwa sababu wenzi wao wanapuuza agizo hili la msingi ambalo Mungu alitoa kuhusiana na ndoa: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.” (Mwanzo 2:24) Bila shaka, wale wanaofunga ndoa bado wanawaheshimu wazazi wao; hata hivyo, kulingana na mpango wa Mungu wajibu wao mkuu ni kuelekea mwenzi wao wa ndoa. Vivyo hivyo, Wakristo wanawapenda sana waamini wenzao; lakini daraka lao kuu ni kuelekea mwenzi wao wa ndoa. Hivyo, Wakristo waliofunga ndoa wanapotumia wakati mwingi mno au kuzoeana kupita kiasi na waamini wenzao, hasa wa jinsia tofauti, wanafanya ndoa iwe na mikazo. Je, inawezekana kwamba jambo hilo linasababisha mkazo katika ndoa yako? Jiulize, ‘Je, kweli ninatumia wakati pamoja na mwenzi wangu wa ndoa, ninamhangaikia, na kumwonyesha upendo anavyostahili?’
15. Kulingana na Mathayo 5:28, kwa nini Wakristo waliofunga ndoa wanapaswa kuepuka kumhangaikia isivyofaa mtu wa jinsia tofauti?
15 Zaidi ya hilo, Wakristo waliofunga ndoa wanacheza na moto wanapowahangaikia isivyofaa watu wa jinsia tofauti ambao si wenzi wao wa ndoa. Inasikitisha kwamba Wakristo fulani waliofunga ndoa wameanza kuwa na hisia za kimapenzi kuelekea watu ambao wamezoeana nao kupita kiasi. (Mathayo 5:28) Hisia hizo zimewatumbukiza katika mwenendo unaofanya ndoa isiheshimike hata zaidi. Fikiria yale ambayo mtume Paulo alisema kuhusu jambo hilo.
“KITANDA CHA NDOA KIWE BILA UNAJISI”
16. Ni amri gani ambayo Paulo anatoa kuhusu ndoa?
16 Baada tu ya Paulo kutoa himizo la kwamba “ndoa na iheshimiwe,” alitoa onyo hili: “Kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Paulo alitumia maneno “kitanda cha ndoa” kurejelea mahusiano ya ngono. Mahusiano hayo hayana “unajisi,” nayo ni safi kiadili, yakiwa tu kati ya watu waliofunga ndoa. Kwa hiyo, Wakristo wanatii maneno haya yaliyoongozwa na roho: “Ushangilie pamoja na mke wa ujana wako.”—Methali 5:18.
17. (a) Kwa nini Wakristo hawaongozwi na maoni ya ulimwengu kuhusu uzinzi? (b) Ni kwa njia gani tunaweza kufuata mfano wa Ayubu?
17 Wale wanaofanya ngono na mtu ambaye si mwenzi wao wa ndoa wanaonyesha kwamba hawaheshimu hata kidogo sheria za Mungu za maadili. Ni kweli kwamba watu wengi leo wanaona uzinzi kuwa jambo la kawaida. Lakini, hata wanadamu wengine wawe na maoni gani kuhusu uzinzi, maoni yao hayapaswi kubadili maoni ya Wakristo kuhusu jambo hilo. Wanatambua kwamba mwishowe, si mwanadamu, bali ‘Mungu ndiye atakayewahukumu waasherati na wazinzi.’ (Waebrania 10:31; 12:29) Hivyo, Wakristo wa kweli hushikamana sana na maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo. (Waroma 12:9) Kumbuka kwamba Ayubu alisema: “Nimefanya agano pamoja na macho yangu.” (Ayubu 31:1) Ndiyo, ili kuepuka hata hatua ya kwanza ambayo inaweza kuelekeza kwenye uzinzi, Wakristo wa kweli huzuia macho yao, nao hawamtazami hata kidogo kwa tamaa mtu wa jinsia tofauti ambaye si mwenzi wao wa ndoa.—Ona nyongeza “Maoni ya Biblia Kuhusu Talaka na Kutengana.”
18. (a) Uzinzi ni jambo zito kadiri gani machoni pa Yehova? (b) Kuna ulinganifu gani kati ya uzinzi na ibada ya sanamu?
18 Uzinzi ni jambo zito kadiri gani machoni pa Yehova? Sheria ya Musa inatusaidia kuelewa maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo. Katika Israeli, uzinzi na ibada ya sanamu ni kati ya dhambi zilizostahili adhabu ya kifo. (Mambo ya Walawi 20:2, 10) Je, unaona ulinganifu kati ya mambo hayo mawili? Mwisraeli aliyeabudu sanamu alivunja agano kati yake na Yehova. Vivyo hivyo, Mwisraeli aliyefanya uzinzi alivunja agano kati yake na mwenzi wake wa ndoa. Wote wawili walitenda kwa hila. (Kutoka 19:5, 6; Kumbukumbu la Torati 5:9; Malaki 2:14) Kwa hiyo, wote wawili walikuwa na hatia mbele za Yehova, Mungu mwaminifu na mwenye kuaminika.—Zaburi 33:4.
19. Ni nini kinachoweza kumchochea mtu aazimie hata zaidi kuepuka uzinzi, na kwa nini?
19 Ni kweli kwamba Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa. Hata hivyo, kukumbuka kwamba katika Israeli la kale uzinzi ulionwa kuwa dhambi nzito kunaweza kuwachochea Wakristo waazimie hata zaidi kutotenda dhambi hiyo. Kwa nini? Fikiria ulinganifu huu: Je, unaweza kuingia kanisani, upige magoti, na kusali mbele ya sanamu? ‘Siwezi hata kidogo!’ ndivyo utakavyosema. Lakini je, unaweza kushawishiwa kufanya hivyo ukipewa pesa nyingi? ‘Haiwezekani!’ utasema. Bila shaka, wazo lenyewe la kumsaliti Yehova kwa kuabudu sanamu linamchukiza Mkristo wa kweli. Vivyo hivyo, Wakristo wanapaswa kuchukizwa na wazo la kumsaliti Mungu wao Yehova na mwenzi wao wa ndoa kwa kufanya uzinzi—hata washawishiwe na jambo gani kutenda dhambi hiyo. (Zaburi 51:1, 4; Wakolosai 3:5) Hatungependa kamwe kutenda jambo ambalo litamfanya Shetani ashangilie na kumvunjia heshima Yehova na mpango mtakatifu wa ndoa.
JINSI YA KUIMARISHA KIFUNGO CHA NDOA
20. Ndoa fulani zimepatwa na nini? Toa mfano.
20 Mbali na kuepuka mwenendo unaofanya ndoa isiheshimike, ni hatua gani unazoweza kuchukua ili uanze tena kumheshimu mwenzi wako wa ndoa? Tunaweza kupata jibu la swali hilo kwa kulinganisha mpango wa ndoa na nyumba. Kisha, maneno ya fadhili, matendo mazuri, na mambo mengine ambayo wenzi wa ndoa hutendeana ili kuonyeshana heshima yanaweza kulinganishwa na vitu vinavyoipamba nyumba. Ikiwa mnahisi kwamba mna uhusiano wa karibu, basi ndoa yenu ni kama nyumba iliyo na mapambo yanayoifanya iwe maridadi na yenye kupendeza. Upendo wenu ukipungua, mapambo hayo yanatoweka pole kwa pole, na kufanya ndoa isivutie tena kama nyumba isiyo na mapambo yoyote. Kwa kuwa unataka kutii amri ya Mungu ya kuifanya ‘ndoa iheshimike,’ utachochewa kurekebisha hali hiyo. Kwa kweli, kitu chenye thamani na chenye kuheshimika kinastahili kurekebishwa. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Neno la Mungu linasema: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa utambuzi itasimamishwa imara. Na kwa ujuzi vyumba vya ndani vitajazwa vitu vyote vyenye thamani na vyenye kupendeza.” (Methali 24:3, 4) Fikiria jinsi maneno hayo yanavyoweza kutumiwa kuhusu ndoa.
21. Ni kwa njia gani tunaweza kuimarisha ndoa yetu hatua kwa hatua? (Ona pia sanduku“Ninaweza Kufanya Nini Ili Kuimarisha Ndoa Yangu?”)
21 ‘Vitu vyenye thamani’ vinavyoijaza nyumba yenye furaha vinatia ndani sifa kama vile upendo wa kweli, kumwogopa Mungu, na imani yenye nguvu. (Methali 15:16, 17; 1 Petro 1:7) Sifa hizo zinaifanya ndoa iwe imara. Lakini je, ulitambua jinsi vyumba vinavyotajwa katika methali hiyo vimejazwa vitu vyenye thamani? “Kwa ujuzi.” Ndiyo, ujuzi wa Biblia unapotumiwa, unaweza kubadili maoni ya watu na kuamsha tena upendo wao. (Waroma 12:2; Wafilipi 1:9) Hivyo, wakati wowote ambapo wewe na mwenzi wako mnaketi pamoja na kuchunguza kwa utulivu andiko fulani la Biblia, kama vile andiko la siku, au makala inayozungumzia ndoa kwa kutegemea Biblia katika gazeti la Mnara wa Mlinzi au Amkeni!, ni kana kwamba mnatazama pambo linaloweza kurembesha nyumba yenu. Kumpenda Yehova kunapowachochea kutumia shauri hilo katika ndoa yenu, ni kana kwamba mnaingiza pambo hilo katika “vyumba vya ndani.” Kwa njia hiyo, huenda upendo na uchangamfu ambao ulikuwepo katika ndoa yenu ukarudi.
22. Ni uradhi gani ambao tunaweza kupata tukijikakamua kufanya sehemu yetu katika kuimarisha ndoa yetu?
22 Ni kweli kwamba inaweza kuchukua muda na kazi nyingi kurudisha pambo moja baada ya lingine. Hata hivyo, ukijikakamua kufanya sehemu yako, utapata uradhi mwingi kwa kujua kwamba unatii amri hii ya Biblia: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Waroma 12:10; Zaburi 147:11) Zaidi ya hilo, jitihada zako za kuiheshimu ndoa yako zitakusaidia kukaa katika upendo wa Mungu.
a Muktadha unaonyesha kwamba Paulo alitoa shauri hilo kuhusu ndoa pamoja na mahimizo mengine mengi.—Waebrania 13:1-5.
-