-
Ninaweza Kuelezaje Maoni ya Biblia Kuhusu Ugoni-Jinsia-Moja?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
-
-
SURA YA 23
Ninaweza Kuelezaje Maoni ya Biblia Kuhusu Ugoni-Jinsia-Moja?
Umati unashangilia huku wasanii wawili wa kike wanapobusiana kimapenzi katika sherehe ya kuwatuza wasanii! Watazamaji wavuta pumzi kwa mshangao, kisha waanza kushangilia. Wagoni-jinsia-moja wauona huo kuwa ushindi. Wengine waliona jambo hilo kuwa kituko cha kujitafutia umaarufu tu. Picha za video za wasanii hao wakibusiana zitaonyeshwa tena na tena kwenye televisheni—na kuvutia upendezi wa wengi katika Intaneti—kwa siku nyingi.
KAMA inavyoonyeshwa katika kisa kinachotajwa hapo juu, mtu mashuhuri anapodokeza au kutangaza waziwazi kwamba yeye ni mgoni-jinsia-moja au mgoni-jinsia-mbili, hizo huwa habari moto-moto kwenye vyombo vya habari. Watu fulani huwasifu watu kama hao kwa kuonyesha ujasiri; wengine huwashutumu wakiwaona kuwa wapotovu. Hata hivyo, walio wengi huuona ugoni-jinsia-moja kuwa tu mtindo tofauti wa maisha. “Nilipokuwa shuleni,” asema Daniel mwenye umri wa miaka 21, “hata vijana ambao hawakuwa wagoni-jinsia-moja, walimwona yeyote aliyechukizwa na wazo la ugoni-jinsia-moja kuwa mwenye ubaguzi na mwenye kuhukumu wengine.”
Maoni kuhusu ugoni-jinsia-moja yanaweza kutofautiana kutoka kwa kizazi kimoja hadi kingine au nchi moja hadi nyingine. Hata hivyo, Wakristo ‘hawachukuliwi huku na huku na kila upepo wa fundisho.’ (Waefeso 4:14) Badala yake, wanashikamana na maoni ya Biblia.
Biblia ina maoni gani? Na ikiwa unaishi kulingana na viwango vya Biblia vya maadili, unaweza kuwajibu namna gani wale wanaokuona kuwa mwenye ubaguzi, mwenye kuwahukumu wengine, au hata mwenye chuki kuelekea vikundi fulani vya watu? Fikiria maswali au taarifa zifuatazo na jinsi zinavyoweza kujibiwa.
“Biblia inasema nini kuhusu ugoni-jinsia-moja?”
“Biblia inaonyesha wazi kwamba Mungu alikusudia ngono iwe kati ya mwanamume na mwanamke katika mpango wa ndoa tu. (Mwanzo 1:27, 28; Mambo ya Walawi 18:22; Methali 5:18, 19) Biblia inaposhutumu uasherati, inatia ndani mazoea kati ya watu wa jinsia moja na pia ngono haramu kati ya watu wa jinsia tofauti.”a—Wagalatia 5:19-21.
“Una maoni gani kuhusu ugoni-jinsia-moja?”
“Siwachukii watu wenyewe, hata hivyo sikubaliani na mwenendo wao.”
Kumbuka: Ikiwa unaongozwa na viwango vya Biblia vya maadili, basi huo ni mtindo wako wa maisha, na una haki ya kuwa na msimamo huo. (Yoshua 24:15) Usionee haya maoni yako.—Zaburi 119:46.
“Wakristo wanapaswa kuwaheshimu watu wote, haidhuru maelekeo yao ya kingono, sivyo?”
“Ni kweli. Biblia inasema: ‘Waheshimuni watu wa namna zote.’ (1 Petro 2:17) Kwa hiyo, Wakristo hawawachukii. Wakristo huwatendea watu wote kwa fadhili, kutia ndani wagoni-jinsia-moja.”—Mathayo 7:12.
“Huoni kwamba maoni yako kuhusu ugoni-jinsia-moja yanaweza kuchochea ubaguzi dhidi yao?”
“Hapana. Ninachokataa ni mwenendo wenyewe, bali si watu wenyewe.”
Unaweza kuongeza hivi: “Kwa mfano, nimeamua pia kutovuta sigara. Hata wazo lenyewe naliona kuwa lenye kuchukiza. Lakini tuseme wewe ni mvutaji wa sigara nawe huoni ubaya wowote. Siwezi kukubagua kwa sababu ya maoni yako, nami nina hakika pia huwezi kunibagua kwa sababu ya maoni yangu—sivyo? Ndivyo pia na maoni yetu yanayotofautiana kuhusu ugoni-jinsia-moja.”
“Kwa kuwa Yesu alitufundisha kuwavumilia wengine, Wakristo wanapaswa kuyakubali maoni ya wengine kuhusu ugoni-jinsia-moja, sivyo?”
“Yesu hakuwahimiza wafuasi wake wakubali mitindo yoyote ile ya maisha. Badala yake, alifundisha kwamba njia ya wokovu iko wazi kwa ‘kila mtu anayemwamini.’ (Yohana 3:16) Kumwamini Yesu kunatia ndani kuishi kulingana na kanuni za Biblia za maadili, vinavyokataza aina fulani za mwenendo, kutia ndani ugoni-jinsia-moja.”—Waroma 1:26, 27.
“Wagoni-jinsia-moja hawawezi kujibadili wawe kitu wasicho; walizaliwa hivyo.”
“Biblia haizungumzii maumbile ya wagoni-jinsia-moja, ijapokuwa inakubali kwamba mazoea fulani yametia mizizi. (2 Wakorintho 10:4, 5) Hata ikiwa watu fulani wana maelekeo hayo, Biblia inawaambia Wakristo wajiepushe na mazoea ya ugoni-jinsia-moja.”
Pendekezo: Badala ya kunaswa katika mtego wa kujadiliana kuhusu chanzo hasa cha tamaa za kigoni-jinsia-moja, kazia kwamba Biblia inaukataza mwenendo huo. Kwa mfano, unaweza kusema: “Unajua watu wengi hudai kwamba watu fulani wamerithi maelekeo ya kutenda kijeuri, kwamba walizaliwa hivyo. (Methali 29:22) Huenda ni kweli, hata hivyo, kama ujuavyo, Biblia inashutumu milipuko ya hasira. (Zaburi 37:8; Waefeso 4:31) Je, tunaweza kusema kanuni hiyo haifai eti kwa sababu watu fulani huenda wakawa na maelekeo ya kutenda kijeuri?”
“Mungu anaweza kumwagizaje mtu anayevutiwa na watu wa jinsia yake ajiepushe na ugoni-jinsia-moja? Huo ni ukatili.”
“Maoni hayo yanatokana na wazo lenye kosa kwamba wanadamu hawana budi kutosheleza tamaa zao za ngono. Biblia inawakweza wanadamu kwa kuwahakikishia kwamba wanaweza kuchagua kutotenda kulingana na tamaa zao zisizofaa za ngono ikiwa kwa kweli wanataka kufanya hivyo.”—Wakolosai 3:5.
“Hata kama wewe si mgoni-jinsia-moja, unahitaji kubadili maoni yako.”
“Tuseme sipendi kamari, lakini wewe unapenda. Utasisitiza nibadili maoni yangu, eti kwa sababu mamilioni ya watu wanapenda kucheza kamari?”
Kumbuka: Wagoni-jinsia-moja, na watu wengine wengi, wana misimamo fulani ambayo inawafanya wachukizwe na mambo fulani, huenda mambo kama vile udanganyifu, ukosefu wa haki, au vita. Biblia inakataza mambo hayo; pia inakataza mwenendo fulani wa ngono, kutia ndani ugoni-jinsia-moja.—1 Wakorintho 6:9, 10.
Biblia haidai mno wala haiwatii watu moyo waonyeshe ubaguzi. Badala yake, inawaagiza wote ‘waukimbie uasherati,’ iwe wana tamaa za ugoni-jinsia-moja au ugoni-jinsia-tofauti.—1 Wakorintho 6:18.
Ukweli ni kwamba, hata mamilioni ya wagoni-jinsia-tofauti wanaotaka kuishi kulingana na viwango vya Biblia, wanahitaji sifa ya kujizuia ili kutoshindwa na vishawishi vyovyote wanavyoweza kupata. Miongoni mwao kuna wengi ambao ni waseja, wasio na matumaini ya kufunga ndoa, na wengi ambao wamefunga ndoa na mwenzi ambaye kwa sababu moja au nyingine hawezi kushiriki tendo la ngono. Wameweza kuishi kwa furaha bila kutosheleza tamaa zao za ngono. Walio na maelekeo ya ugoni-jinsia-moja wanaweza kufanya hivyo pia ikiwa kwa kweli wanataka kumpendeza Mungu.—Kumbukumbu la Torati 30:19.
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 2, SURA YA 28
Wasichana fulani wanaamini kwamba kufanya ngono na wapenzi wao kutaimarisha uhusiano wao. Sivyo hata kidogo! Sura inayofuata inaeleza ni kwa nini.
[Maelezo ya Chini]
a Neno “uasherati” katika Biblia halimaanishi ngono tu bali pia linatia ndani vitendo kama vile kuchua au kupiga punyeto viungo vya uzazi vya mtu mwingine, ngono ya kinywa, au ngono ya mkundu.
ANDIKO MUHIMU
“Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.”—Wakolosai 3:5.
PENDEKEZO
Ijapokuwa mwenendo wa wengine unaweza kukuudhi, unapozungumza nao epuka kuonekana kana kwamba unajiona kuwa mwadilifu. Ukweli ni kwamba wana haki ya kuchagua mambo wanayotaka kuamini, kama vile wewe ulivyo na haki ya kufanya hivyo.
JE, WAJUA . . . ?
Wakristo fulani wa karne ya kwanza ambao hapo awali walifanya ngono na watu wa jinsia moja waliacha njia zao chafu, ‘wakaoshwa wakawa safi’ mbele za Mungu.—1 Wakorintho 6:9-11.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Mtu akisema kwamba maoni ya Biblia kuhusu ugoni-jinsia-moja ni ya zamani, nitasema ․․․․․
Ili iwe wazi kwamba ninachukia mwenendo wa ugoni-jinsia-moja bali si watu wenyewe, nitasema ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini Mungu ana haki ya kuwawekea wanadamu sheria za maadili?
● Unapata faida gani kwa kushikamana na sheria za Biblia za maadili?
[Blabu katika ukurasa wa 170]
“Mvulana mmoja shuleni alichukizwa nami kwa sababu niliukataa mtindo wake wa maisha. Lakini nilipomweleza kwamba simkatai yeye binafsi—na alipogundua kwamba sichukizwi tu na ugoni-jinsia-moja bali pia upotovu wowote wa maadili—alianza kuniheshimu na hata kunitetea wengine walipoleta upinzani.”—Aubrey
[Sanduku katika ukurasa wa 168]
Namna Gani Ugoni-Jinsia-Mbili?
Ingawa watu wa jinsia zote mbili wanaweza kuwa na maelekeo hayo, inaonekana walio wengi hasa ni wasichana. Kwa baadhi yao ni “kutaka tu kujua.” Lisa, mwenye umri wa miaka 26, anasema: “Vijana wanapotazama sinema, televisheni, na kusikiliza muziki wenye mazoea ya wasichana kuwabusu wasichana wenzao, wanaanza kushawishika kujaribu, hasa ikiwa hawaoni ubaya wowote wa kufanya hivyo.”
Kwa wengine, inaonekana kwa kweli wanavutiwa na watu wa jinsia yao. “Nilipokuwa kwenye karamu fulani, nilikutana na wasichana wawili ambao ni wagoni-jinsia-mbili,” asema Vicky, mwenye umri wa miaka 13, “baadaye rafiki yangu akaniambia kwamba wanavutiwa nami. Punde si punde tukaanza kuwasiliana kupitia ujumbe mfupi na mmoja wao, nami nikaanza kuvutiwa naye.”
Umewahi kuhisi jinsi Vicky alivyohisi? Huenda watu wengi wakakuhimiza ukubali ukweli wa mambo na kujitokeza waziwazi utambuliwe kuwa mgoni-jinsia mbili. Hata hivyo, unapaswa kujua kwamba kuvutiwa na mtu wa jinsia yako mara nyingi huwa jambo la kupita tu. Hivyo ndivyo, Vicky, alivyotambua. Na ndivyo ilivyokuwa pia kwa Lisette, mwenye umri wa miaka 16. Anasema: “Nilitulia baada ya kuzungumza na wazazi wangu kuhusu hisia zangu. Pia, nilijifunza shuleni katika somo la biolojia kwamba katika miaka ya kubalehe, kiasi cha homoni mwilini hubadilika-badilika sana. Ikiwa tu vijana wangejua mengi zaidi kuhusu miili yao, wangeelewa kwamba kuvutiwa kingono na mtu wa jinsia yako ni jambo la muda tu, na kwa hiyo hakuna haja ya kushinikizwa kuwa wagoni-jinsia-moja.”
Hata ikiwa hisia zako zinaonekana kuwa zimetia mizizi na si za muda mfupi tu ujanani, kumbuka kwamba Biblia inakupa mradi unaoweza kufikia: Unaweza kuamua kutotosheleza tamaa zisizofaa, hata ziwe za aina gani.
[Picha katika ukurasa wa 169]
Kuhusu maoni yanayopendwa na wengi, Wakristo huwa na ujasiri wa kuwa tofauti
-
-
Ninaweza Kushinda Jinsi Gani Mazoea ya Kupiga Punyeto?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
-
-
SURA YA 25
Ninaweza Kushinda Jinsi Gani Mazoea ya Kupiga Punyeto?
“Nilianza kupiga punyeto nikiwa na umri wa miaka minane. Baadaye nikajifunza maoni ya Mungu kuhusu zoea hilo. Kila nilipoangukia mtego huo, nilihisi vibaya sana. ‘Kweli Mungu anaweza kumpenda mtu kama mimi?’ nilijiuliza.”—Luiz.
UNAPOANZA kubalehe, tamaa za ngono zinaweza kuwa zenye nguvu sana. Kwa sababu hiyo, huenda ukaangukia mazoea ya kupiga punyeto.a Wengi husema kwamba si neno kufanya hivyo. “Hakuna mtu anayeumia,” wanasema. Hata hivyo, kuna sababu nzuri ya kuepuka mazoea hayo. Mtume Paulo aliandika: “Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu . . . kwa habari ya . . . hamu ya ngono.” (Wakolosai 3:5) Kupiga punyeto hakuui hamu ya ngono bali kunaichochea. Isitoshe, fikiria yafuatayo:
● Kupiga punyeto humfanya mtu kuwa mwenye ubinafsi. Kwa mfano, mtu anapopiga punyeto, anakazia fikira hisia zake mwenyewe za kimwili.
● Kupiga punyeto humfanya mtu kuwaona watu wa jinsia tofauti kuwa vitu au vifaa vya kujitosheleza tu.
● Maoni ya kibinafsi yanayotokana na zoea la kupiga punyeto yanaweza kufanya iwe vigumu kutosheleza uhusiano wa ngono katika ndoa.
Badala ya kuamua kupiga punyeto ili kuzima tamaa za ngono, jitahidi kukuza sifa ya kujizuia. (1 Wathesalonike 4:4, 5) Ili ufaulu, kwanza kabisa Biblia inapendekeza ujiepushe na hali zinazoweza kuamsha tamaa ya ngono. (Methali 5:8, 9) Namna gani ikiwa umekuwa mtumwa wa zoea la kupiga punyeto? Labda umejaribu kuacha lakini hujafanikiwa. Ni rahisi kukata kauli kwamba huwezi kubadilika, na kwamba huwezi kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Hivyo ndivyo mvulana anayeitwa Pedro alivyojiona. “Niliporudia zoea hilo, nilihisi vibaya sana,” anasema. “Nilifikiri kwamba siwezi kamwe kusamehewa. Nilishindwa kusali.”
Ikiwa hivyo ndivyo unavyohisi, jipe moyo. Kuna tumaini. Vijana wengi, na watu wazima pia, wamefaulu kushinda mazoea hayo ya kupiga punyeto. Wewe pia unaweza kufaulu!
Unapojiona Kuwa Mwenye Hatia
Kama ilivyotajwa mapema, wale walio na mazoea ya kupiga punyeto mara nyingi hujiona kuwa wenye hatia. Bila shaka, ‘kuhuzunishwa kwa njia ya kimungu’ kunaweza kukuchochea ushinde mazoea hayo. (2 Wakorintho 7:11) Lakini kujiona kuwa mwenye hatia kupita kiasi kunaweza kuwa na matokeo mabaya. Kunaweza kukuvunja moyo sana mpaka utake kukata tamaa.—Methali 24:10.
Kwa hiyo, jaribu kuwa na usawaziko. Kupiga punyeto ni uchafu. Mazoea hayo yanaweza kukufanya uwe ‘mtumwa wa tamaa na raha za namna mbalimbali’ na kukufanya uwe na maoni yasiyofaa. (Tito 3:3) Hata hivyo, kupiga punyeto si upotovu wa kingono, kama vile uasherati. (Yuda 7) Ikiwa una tatizo la kupiga punyeto, usikate kauli kwamba umefanya dhambi isiyoweza kusamehewa. Siri ni kupinga tamaa ya kufanya hivyo na kutokubali kamwe kushindwa!
Ni rahisi kuvunjika moyo baada ya kurudia zoea hilo. Ukirudia, kumbuka maneno ya Methali 24:16: “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama; lakini waovu watakwazwa na msiba.” Kujikwaa hakumaanishi kwamba wewe ni mwovu. Kwa hiyo, usikate tamaa. Badala yake, chunguza jambo lililofanya urudie zoea hilo, kisha ujaribu kuliepuka.
Tafakari kuhusu upendo na rehema za Mungu. Mtunga-zaburi Daudi, ambaye pia nyakati fulani alifanya dhambi kwa sababu ya udhaifu wake, alisema: “Kama vile baba anavyowaonyesha wanawe rehema, ndivyo ambavyo Yehova amewaonyesha rehema wale wanaomwogopa. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:13, 14) Ndiyo, Yehova hukumbuka hali yetu ya kutokamilika na ‘yuko tayari kusamehe.’ (Zaburi 86:5) Kwa upande mwingine, anataka tujitahidi na kufanya marekebisho. Hivyo basi, unaweza kuchukua hatua gani ili kushinda zoea hilo?
Chunguza burudani yako. Je, wewe hutazama sinema au programu za televisheni au hutembelea vituo vya Intaneti vyenye kusisimua kingono? Kwa hekima, mtunga-zaburi alisali kwa Mungu: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa.”b—Zaburi 119:37.
Kazia akili yako mambo mengine. Mkristo anayeitwa William anashauri: “Kabla ya kwenda kulala, soma jambo fulani linalohusiana na mambo ya kiroho. Ni muhimu sana kwamba wazo la mwisho la siku liwe la kiroho.”—Wafilipi 4:8.
Zungumza na mtu mwingine kuhusu tatizo hilo. Aibu inaweza kufanya iwe vigumu kwako kumweleza mtu mwingine tatizo lako. Hata hivyo, kuzungumzia tatizo hilo kunaweza kukusaidia kulishinda! Mkristo anayeitwa David alitambua ukweli huo. Anasema: “Nilizungumza na baba yangu faraghani. Sitasahau kamwe aliyosema. Akiwa na tabasamu, aliniambia, ‘Ninakuonea fahari.’ Alijua kwamba nilihitaji ujasiri ili kuzungumza naye kuhusu jambo hilo. Alinitia moyo sana na kufanya niazimie kujitahidi hata zaidi.
“Kisha baba yangu alinionyesha maandiko machache ili kunisaidia kuona kwamba bado ninaweza kubadilika, halafu akanionyesha maandiko mengine ili kunisaidia kuona uzito wa mwenendo wangu. Aliniambia nijaribu kuepuka zoea hilo mpaka wakati fulani, kisha tulizungumzie tena wakati huo. Pia, aliniambia nikijikuta nimerudia zoea hilo, nisikate tamaa, bali nijitahidi wakati mwingine kwa muda mrefu zaidi.” David alifikia mkataa gani? Anasema: “Faida kubwa niliyopata ni kuwa na mtu anayeelewa tatizo langu na kunisaidia.”c
Kufanya ngono bila kuwajibika ni jambo zito. Pata kujua ni kwa nini.
[Maelezo ya Chini]
a Kupiga punyeto ni tofauti na kusisimka kingono bila kukusudia. Kwa mfano, huenda mvulana akaamka akiwa amesisimka kingono au ametokwa na shahawa usiku. Vilevile, wasichana wengine husisimka kingono bila kukusudia, hasa kabla tu au baada ya kipindi cha hedhi. Tofauti na hali hizo, kupiga punyeto kunatia ndani kujisisimua kimakusudi.
b Unaweza kupata habari zaidi katika Buku la 2, Sura ya 33.
c Unaweza kupata habari zaidi katika Buku la 2, ukurasa wa 239-241.
ANDIKO MUHIMU
“Zikimbie tamaa zinazotukia ujanani, lakini fuatilia uadilifu, imani, upendo, amani, pamoja na wale wanaomwitia Bwana kutokana na moyo safi.”—2 Timotheo 2:22.
PENDEKEZO
Sali kabla tamaa haijatia mizizi. Mwombe Yehova Mungu akupe “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili ukabiliane na kishawishi.—2 Wakorintho 4:7.
JE, WAJUA . . . ?
Mtu yeyote aliye dhaifu anaweza kushindwa kuzuia tamaa yake ya ngono. Lakini mwanamume halisi au mwanamke halisi ataonyesha sifa ya kujizuia hata anapokuwa peke yake.
HARUA ZA KUCHUKUA!
Ninaweza kukaza akili yangu juu ya mambo yaliyo safi ikiwa nita ․․․․․
Badala ya kushindwa na tamaa, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini ni vizuri kukumbuka kwamba Yehova yuko “tayari kusamehe”?—Zaburi 86:5.
● Kwa kuwa Mungu aliyeumba tamaa za ngono ndiye pia anayesema kwamba unapaswa kujizuia, lazima awe ana hakika kwamba unaweza kufanya nini?
[Blabu katika ukurasa wa 182]
“Tangu niliposhinda tatizo hilo, nina dhamiri safi mbele za Yehova, na hilo ni jambo ambalo siwezi kubadilishana na kitu chochote!”—Sarah
[Picha katika ukurasa wa 180]
Ukianguka unapokimbia haimaanishi kwamba ni lazima uanze tena kutoka mwanzo, hivyo pia, ukijikuta umerudia kupiga punyeto, haimaanishi kwamba jitihada zako kufikia sasa ni za bure
-
-
Ninawezaje Kujilinda na Washambuliaji wa Kingono?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
-
-
SURA YA 32
Ninawezaje Kujilinda na Washambuliaji wa Kingono?
Kila mwaka, mamilioni ya watu hubakwa au kutendewa vibaya kingono, na kulingana na uchunguzi, vijana ndio wanaolengwa hasa. Kwa mfano, inakadiriwa kwamba nchini Marekani, karibu nusu ya watu wote wanaotendewa vibaya kingono wako chini ya umri wa miaka 18. Kwa sababu ya kuenea kwa uovu huo, ni muhimu kuchunguza habari hii.
“Alinishika na kabla ya kujua kilichokuwa kinaendelea, akaniangusha chini. Nilijaribu kila niwezalo kumzuia. Nilivuta mkebe uliokuwa na pilipili lakini akaugonga kutoka mkononi mwangu. Nilijaribu kupiga mayowe, lakini wapi. Nilimsukuma, nikatupa mateke, nikampiga ngumi, na kumkwaruza. Ndipo nikasikia kisu kikinidunga. Mwili wangu wote ukadhoofika kabisa.”—Annette.
WASHAMBULIAJI wa kingono ni wengi leo, na mara nyingi wanawalenga vijana. Vijana fulani, kama Annette, wanatendewa vibaya na watu wasiowajua. Wengine wanashambuliwa na jirani. Ndivyo ilivyokuwa katika kisa cha Natalie, ambaye alipokuwa na umri wa miaka 10 tu, alitendewa vibaya kingono na kijana aliyekuwa akiishi karibu na kwao. Anasema: “Niliogopa na kuona haya sana hivi kwamba mwanzoni sikumwambia yeyote.”
Vijana wengi wametendewa vibaya na mtu wa familia. “Nilipokuwa na umri wa kati ya miaka 5 na 12, nilitendewa vibaya kingono na baba yangu,” asema mwanamke anayeitwa Carmen. “Mwishowe nilizungumza naye kuhusu jambo hilo nilipokuwa na umri wa miaka 20. Aliomba msamaha, lakini miezi kadhaa baadaye, alinifukuza kutoka nyumbani.”
Inasikitisha sana kwamba leo, ni jambo la kawaida kutendewa vibaya kingono na jirani, rafiki, au mtu wa familia.a Hata hivyo, vijana wametendewa vibaya tangu zamani. Hata nyakati Biblia ilipokuwa ikiandikwa, mwenendo huo wenye kusikitisha ulikuwako. (Yoeli 3:3; Mathayo 2:16) Leo, tunaishi katika nyakati za hatari. Watu wengi hawana “upendo wa asili,” na ni kawaida wasichana (na hata wavulana) kutendewa vibaya kingono. (2 Timotheo 3:1-3) Ingawa hakuna tahadhari inayoweza kukuhakikishia usalama, kuna mengi unayoweza kufanya ili kujilinda. Fikiria mapendekezo yafuatayo:
Kuwa macho. Unapotembea, kuwa macho kujua kinachoendelea mbele yako, nyuma yako, upande huu na upande ule. Maeneo fulani ni hatari, hasa usiku. Ikiwezekana, epuka kabisa maeneo hayo au usitembee ukiwa peke yako.—Methali 27:12.
Epuka kueleweka vibaya. Epuka kuchezea hisia za wengine au kuvalia kwa njia inayowavutia kingono. Matendo kama hayo yanaweza kufanya watu wakuelewe kimakosa kwamba ungependa kufanya ngono, au huwezi kukataa nafasi ya kufanya hivyo ikitokea.—1 Timotheo 2:9, 10.
Zungumzia mipaka. Ikiwa mna uhusiano wa kimapenzi, zungumza na mwenzako kuhusu mwenendo unaofaa na usiofaa.b Baada ya kuweka mipaka, epuka hali zinazoweza kukuhatarisha.—Methali 13:10.
Usinyamaze. Hakuna ubaya kusema hivi kwa uthabiti, “Usifanye hivyo!” au “Usiniguse!” Usinyamaze eti kwa sababu unaogopa mpenzi wako atakuacha. Akivunja uhusiano wenu kwa sababu hiyo, basi hakufai! Isitoshe, unahitaji mwanamume anayeheshimu mwili wako na kanuni zako.c
Kuwa mwangalifu unapotumia Intaneti. Hupaswi kutoa habari za kibinafsi au kuweka picha zinazoonyesha mahali ulipo.d Ukipokea ujumbe unaozungumzia ngono waziwazi, kwa kawaida jibu bora ni kutojibu. Watu wengi wanaoshambulia kupitia Intaneti hukosa la kufanya wasipojibiwa.
Hatua hizo zinaweza kukusaidia usishambuliwe kwa urahisi. (Methali 22:3) Hata hivyo, jambo la hakika ni kwamba, huenda nyakati zote mambo yasiwe kama unavyotaka. Kwa mfano, huenda kila wakati isiwezekane kuwa na mwandamani au isiwezekane kuepuka maeneo hatari. Labda hata unaishi katika eneo hatari.
Huenda kutokana na hali yenye kusikitisha iliyokupata, unajua kwamba mambo mabaya yanaweza kutokea hata baada ya kujaribu sana kuepuka matatizo. Kama Annette, aliyetajwa mwanzoni, labda ulishambuliwa bila kutarajia na ukashindwa nguvu. Au kama Carmen, labda ulishambuliwa ukiwa mtoto, na kwa hiyo hukuwa na uwezo wa kuzuia hali hiyo, au hata hukuelewa kabisa yaliyokuwa yakitokea. Unaweza kushughulikia jinsi gani hisia za hatia ambazo mara nyingi huwasumbua watu ambao wamewahi kutendewa vibaya kingono?
Kupambana na Hisia za Hatia
Mpaka sasa Annette anapambana na hisia za hatia kuhusu mambo yaliyompata. “Najiona kuwa adui yangu mwenyewe,” anasema. “Naufikiria usiku huo tena na tena. Nahisi nilipaswa kujaribu zaidi kumzuia mtu huyo. Ukweli ni kwamba, baada ya kudungwa kisu, niliogopa sana. Sikuweza kufanya lolote, lakini nahisi kwamba nilipaswa kufanya jambo fulani.”
Natalie pia anapambana na hisia za hatia. Anasema: “Sikupaswa kumwamini mtu yeyote. Wazazi wetu walituamuru mimi na dada yangu tuwe tukicheza pamoja, lakini sikutii. Kwa hiyo, nahisi kwamba nilimpa jirani yangu nafasi ya kuniumiza. Mambo yaliyonipata yaliumiza familia yetu, nami najilaumu kwa kuwasababishia uchungu mwingi. Hilo linaniumiza hata zaidi.”
Unaweza kupambana jinsi gani na hatia ikiwa hisia zako ni kama za Annette au Natalie? Kwanza, kumbuka kwamba ikiwa ulilalwa kinguvu, hukutaka kufanya hivyo. Watu fulani hupunguza uzito wa kosa hilo kwa kusema kwamba ni kawaida kwa wanaume kufanya hivyo na kwamba wanaolalwa kinguvu ndio wenye kulaumiwa. Hata hivyo, hakuna mtu anayepaswa kulalwa kinguvu. Ikiwa ulitendewa uovu huo, huwezi kulaumiwa!
Ni kweli kwamba ni rahisi kusoma taarifa inayosema “huwezi kulaumiwa,” lakini si rahisi kuiamini. Wengine hawasemi kuhusu mambo yaliyotokea nao wanaumia kutokana na hisia za hatia, na hisia nyingine mbaya. Hata hivyo, kukaa kimya kunamsaidia nani—wewe au mshambuliaji wako? Unahitaji kuchukua hatua nyingine.
Sema Yaliyokupata
Biblia inasema kwamba Ayubu, yule mwanamume mwadilifu, akiwa amechanganyikiwa sana alisema: “Nitaonyesha hangaiko langu kujihusu mwenyewe. Nitasema kwa uchungu wa nafsi yangu!” (Ayubu 10:1) Utafaidika kwa kufanya hivyo pia. Kuzungumza na mtu ambaye unamtumaini kuhusu mambo yaliyokupata kunaweza kukusaidia kupambana na hali hiyo na kupata kitulizo kutokana na hisia zako zenye kuumiza.
Ikiwa wewe ni Mkristo, ni muhimu kuzungumza na mzee wa kutaniko kuhusu mambo yaliyokupata. Maneno yenye kufariji ya mchungaji mwenye upendo yatakuhakikishia kwamba kwa kulalwa kinguvu hutaonwa kuwa mchafu kutokana na dhambi ya mtu mwingine. Hivyo ndivyo Annette alivyotambua. Anasema: “Nilizungumza na rafiki yangu wa karibu, naye akanihimiza nizungumze na wazee wawili Wakristo katika kutaniko letu. Nafurahi nilifanya hivyo. Walizungumza nami mara kadhaa na kuniambia kwamba yaliyotokea hayakuwa makosa yangu. Sikufanya kosa lolote.”
Kuzungumza kuhusu mambo yaliyotokea na kueleza hisia zako kunaweza kukusaidia usilemewe na hasira na kinyongo. (Zaburi 37:8) Huenda pia kukakusaidia kupata kitulizo, labda kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi. Natalie aliona ukweli wa maneno hayo baada ya kuwaambia wazazi wake kuhusu jinsi alivyotendewa vibaya. Anasema: “Walinisaidia. Walinitia moyo kuzungumza, na hilo likanisaidia kutohuzunika sana na kuwa na hasira nyingi.” Pia, Natalie alipata faraja kwa kusali. Anasema: “Kuzungumza na Mungu kulinisaidia hasa nyakati ambazo niliona kwamba siwezi kuzungumza na mwanadamu. Ninaweza kuzungumza kwa uhuru ninaposali. Kufanya hivyo kunanipa amani ya kweli na utulivu.”e
Huenda wewe pia ukatambua kwamba kuna ‘wakati wa kupona.’ (Mhubiri 3:3) Tegemea marafiki wanaoweza kukusaidia ambao ni kama wazee Wakristo wanaofafanuliwa kuwa sawa na “mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua.” (Isaya 32:2) Jitunze kimwili na kihisia. Pumzika vya kutosha. Na zaidi ya yote, mtegemee Mungu wa faraja yote, Yehova, ambaye karibuni ataleta ulimwengu mpya ambamo “watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia.”—Zaburi 37:9.
[Maelezo ya Chini]
a Visa fulani vinatokea wakati wa matembezi ya kimapenzi, ambapo msichana hulazimishwa kufanya ngono au anakubali baada ya kulishwa dawa za kulevya.
b Pata habari zaidi katika Buku la 2, Sura ya 4.
c Bila shaka, shauri hilo linatumika pia ikiwa msichana anamlazimisha mvulana wafanye ngono.
d Pata habari zaidi katika Buku la 2, Sura ya 11.
e Nyakati nyingine watu ambao wametendewa vibaya wanashuka moyo sana. Katika hali kama hizo, huenda ikafaa kumwona daktari. Pata habari zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na hisia zenye kuumiza katika Sura ya 13 na 14 ya kitabu hiki.
ANDIKO MUHIMU
“Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio na upendo wa asili, . . . wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema.”—2 Timotheo 3:1-3.
PENDEKEZO
Ikiwa umewahi kutendewa vibaya kingono, hifadhi orodha ya maandiko yanayoweza kukufariji. Maandiko hayo yanaweza kutia ndani Zaburi 37:28; 46:1; 118:5-9; Methali 17:17; na Wafilipi 4:6, 7.
JE, WAJUA . . . ?
Nchini Marekani, zaidi ya asilimia 90 ya vijana wanaotendewa vibaya kingono wanawajua washambuliaji wao.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Nikihisi hatia kuhusu mambo yaliyotendeka nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kuna faida gani kuzungumza na mtu fulani unapotendewa vibaya?
● Ni nini kinachoweza kukupata wewe na wengine usipozungumza kuhusu jambo hilo?
[Blabu katika ukurasa wa 232]
“Si rahisi kumwambia mtu kwamba umetendewa vibaya kingono, hata hivyo, ni vizuri kufanya hivyo. Kumwambia mtu kunakusaidia kuondolea mbali huzuni na hasira na kurudia hali yako ya kawaida.”—Natalie
[Sanduku katika ukurasa wa 230]
“Ikiwa Unanipenda . . . ”
Washambuliaji fulani hawawalazimishi wasichana wafanye ngono nao lakini kwa ujanja wanachezea hisia zao. Jinsi gani? Kwa kuwaambia maneno kama, “Kila mtu anafanya ngono,” “Hakuna atakayejua,” au, kama ilivyotajwa katika Sura ya 24 ya kitabu hiki, “Ikiwa unanipenda, utafanya ninavyokuambia.” Usidanganywe na mvulana anayejaribu kukufanya uamini kwamba ikiwa unampenda mtu lazima ufanye ngono naye. Ukweli ni kwamba, yeyote anayefikiria hivyo anataka tu kutosheleza tamaa yake. Hakujali wala hajali hali yako. Tofauti na mtu huyo, mwanamume mzuri atatanguliza faida zako na ataonyesha kwamba anashikamana na kanuni za maadili za Mungu. (1 Wakorintho 10:24) Mwanamume halisi hawatendei wasichana kama vyombo vya ngono. Badala yake, anawaona “wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili.”—1 Timotheo 5:1, 2.
[Picha katika ukurasa wa 233]
Hisia zinazotokana na kutendewa vibaya ni nzito sana, huwezi kuzibeba peke yako. Kwa nini usitafute msaada kwa kuzungumza na mtu fulani?
-