-
Ni Wakati Gani Ambapo Mtu Anakuwa Amepita Mipaka?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 4
Ni Wakati Gani Ambapo Mtu Anakuwa Amepita Mipaka?
Kweli au si kweli . . .
Ni kosa kwa watu wawili walio na urafiki wa kimapenzi kushikana katika hali yoyote ile.
□ Kweli
□ Si kweli
Watu wawili wanaweza kuwa na hatia ya uasherati hata ikiwa hawajafanya ngono.
□ Kweli
□ Si kweli
Wapenzi wasipofanya mambo kama vile kubusiana na kukumbatiana, basi hawapendani kikweli.
□ Kweli
□ Si kweli
HAPANA shaka umefikiria jambo hilo sana. Kwa kweli, ikiwa uko katika urafiki wa kimapenzi, inaweza kuwa vigumu kujua mipaka ambayo unapaswa kuweka kuhusu kuonyeshana mahaba. Acheni tuzungumzie taarifa tatu zilizo juu na tuone jinsi Neno la Mungu linavyotusaidia kujibu swali hili, “Ni wakati gani ambapo mtu anakuwa amepita mipaka?”
● Ni kosa kwa watu wawili walio na urafiki wa kimapenzi kushikana katika hali yoyote ile.
Si kweli. Biblia haikatazi kuonyeshana mahaba kwa njia iliyo safi. Kwa mfano, Biblia inazungumzia kisa cha msichana Mshulami na mvulana mchungaji waliopendana. Uchumba wao ulikuwa safi. Hata hivyo, inaonekana kwamba walionyeshana mahaba kwa njia fulani kabla ya kufunga ndoa. (Wimbo wa Sulemani 1:2; 2:6; 8:5) Leo watu wawili wanaofikiria kwa uzito kufunga ndoa wanaweza kuhisi kwamba hakuna ubaya kuonyeshana mahaba katika njia fulani safi.a
Hata hivyo, watu wawili wenye urafiki wa kimapenzi wanapaswa kuwa waangalifu sana. Kubusiana, kukumbatiana, au kufanya jambo lolote linaloamsha tamaa ya ngono kunaweza kuongoza katika mwenendo mpotovu kingono. Ni rahisi sana hata kwa watu wawili ambao hawana nia mbaya kupoteza usawaziko na kutumbukia katika upotovu wa kingono.—Wakolosai 3:5.
● Watu wawili wanaweza kuwa na hatia ya uasherati hata ikiwa hawajafanya ngono.
Kweli. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “uasherati” (por·neiʹa) lina maana pana. Linatia ndani mahusiano yote ya ngono nje ya ndoa na linakazia matumizi yasiyofaa ya viungo vya uzazi. Hivyo, zaidi ya kufanya ngono, uasherati unatia ndani matendo kama vile kumpiga mtu mwingine punyeto, iwe ni mwanamume au mwanamke, na pia ngono ya kinywa na ulawiti au ufiraji.
Isitoshe, zaidi ya kushutumu uasherati, Biblia inashutumu mambo mengine pia. Mtume Paulo aliandika: “Matendo ya mwili ni wazi, nayo ni uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu.” Kisha akaongeza: “Wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”—Wagalatia 5:19-21.
“Uchafu,” au “ukosefu wa usafi,” ni nini? Neno la Kigiriki linatia ndani uchafu wa kila namna, iwe ni katika maneno au matendo. Kwa kweli, ni tendo chafu kuingiza mikono ndani ya nguo za mtu, kumvua mtu nguo, au kumpapasa-papasa mtu sehemu za siri, kama vile matiti. Katika Biblia kuyapapasa matiti kunahusianishwa na shangwe inayopaswa kufurahiwa tu na watu wawili waliofunga ndoa.—Methali 5:18, 19.
Vijana fulani wanakaidi viwango vya Mungu. Wanapita mipaka kimakusudi, au wanatafuta kwa pupa watu mbalimbali wanaoweza kushiriki pamoja nao uchafu wa kingono. Vijana hao wanaweza kuwa na hatia ya kile ambacho mtume Paulo alikiita “mwenendo mpotovu.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mwenendo mpotovu” linamaanisha ‘matendo ya kupita kiasi, ya kupindukia, ufidhuli, uchu usiozuilika.’ Bila shaka hungependa kufikia hatua ya “kuishiwa na ufahamu wote” kwa kujitoa mwenyewe ili kuwa na “mwenendo mpotovu na kufanya ukosefu wa usafi wa kila namna kwa pupa.”—Waefeso 4:17-19.
● Wapenzi wasipofanya mambo kama vile kubusiana na kukumbatiana, basi hawapendani kikweli.
Si kweli. Tofauti na maoni ya watu fulani, kufanya mambo kama vile kubusiana na kukumbatiana hakuzidishi urafiki. Badala yake, kunafanya watu wasiheshimiane wala kuaminiana. Fikiria kisa cha Laura. “Siku moja wakati mama yangu hakuwapo, mpenzi wangu alikuja nyumbani eti ili kutazama televisheni,” anasema. “Mwanzoni alinishika mkono tu. Kisha, akaanza kunipapasa-papasa. Niliogopa kumwambia aache; nilidhani kwamba atakasirika na kuondoka.”
Una maoni gani? Je, mpenzi wa Laura alimjali kikweli, au alitaka tu kutosheleza tamaa yake? Je, mtu anayejaribu kukuingiza katika mwenendo mchafu anakupenda kweli?
Mvulana anapomchochea msichana kukaidi mazoezi yake ya Kikristo na dhamiri yake, anavunja sheria ya Mungu na hapaswi kudai kwamba anampenda msichana huyo kikweli. Vilevile, msichana anayekubali, anajiachilia atumiwe vibaya. Zaidi ya yote, msichana huyo ameshiriki tendo chafu—pengine hata uasherati.b—1 Wakorintho 6:9, 10.
Weka Mipaka Iliyo Wazi
Ikiwa mna urafiki wa kimapenzi, mnaweza kufanya nini ili mwepuke kuonyeshana mahaba kwa njia zisizofaa? Njia ya hekima ni kuweka mipaka iliyo wazi mapema. Andiko la Methali 13:10 linasema: “Wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.” Hivyo, zungumza na mpenzi wako kuhusu njia zinazofaa za kuonyeshana mahaba. Kujaribu kuweka mipaka baada ya tamaa kuwaka ni kama kuweka king’ora cha moto katika nyumba baada ya nyumba hiyo kushika moto.
Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kuzungumzia mambo hayo—hata linaweza kuwa jambo lenye kuaibisha—hasa mwanzoni mwa uchumba. Lakini kuweka mipaka kunaweza kusaidia sana kuzuia matatizo makubwa yasitokee baadaye. Mipaka inayowekwa kwa hekima ni kama vifaa vya kutambua moshi ambavyo vinawasha king’ora mara tu vinapotambua dalili ya moto. Isitoshe, kufaulu kwenu kuzungumzia mambo hayo kunaweza kuonyesha pia ikiwa urafiki wenu utafanikiwa. Kwa hakika, kujizuia, subira, na kutokuwa na ubinafsi ndio msingi wa mahusiano mazuri ya ngono katika ndoa.—1 Wakorintho 7:3, 4.
Kusema kweli, kushikamana na viwango vya Mungu si rahisi. Lakini unaweza kutegemea mashauri ya Yehova. Katika Isaya 48:17, Yehova anasema kwamba yeye ndiye “Anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake.” Yehova anakutakia kila la heri!
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 24
Kuwa bikira si kasoro. Badala yake, kutunza ubikira ndilo jambo la hekima. Pata kujua ni kwa nini.
[Maelezo ya Chini]
a Katika sehemu fulani za ulimwengu, watu ambao hawajafunga ndoa wanapoonyeshana mahaba mbele ya watu, hilo huonwa kuwa jambo lisilofaa na lenye kuchukiza. Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu wasijiendeshe kwa njia inayoweza kuwakwaza wengine.—2 Wakorintho 6:3.
b Bila shaka, mambo yanayozungumziwa katika fungu hili yanawahusu watu wa jinsia zote.
MAANDIKO MUHIMU
“Upendo . . . haujiendeshi bila adabu.”—1 Wakorintho 13:4, 5.
PENDEKEZO
Fanyeni mambo mkiwa pamoja na wengine, au usisitize kuwe na mtu wa tatu. Epukeni hali hatari, kama vile kuwa peke yenu katika gari lililoegeshwa au katika nyumba au chumba.
JE, WAJUA . . .?
Ikiwa mnachumbiana, mnahitaji kuzungumzia mambo fulani ya siri. Lakini kuzungumzia mambo waziwazi mkiwa na kusudi la kuamsha tamaa ya ngono ni mojawapo ya mambo machafu —hata mambo hayo yakizungumziwa kupitia simu au ujumbe mfupi.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ninaweza kuepuka kushawishiwa kutumbukia katika mwenendo usiofaa kwa ․․․․․
Mpenzi wangu akijaribu kunishawishi nishiriki katika mwenendo mchafu, nita ․․․․․
Maswali ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu jambo hili ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Ni mipaka gani ambayo unaweza kuweka kuhusu kuonyeshana mahaba na mtu wa jinsia tofauti?
● Eleza tofauti kati ya uasherati, uchafu, na mwenendo mpotovu.
[Blabu katika ukurasa wa 46]
Mimi na mchumba wangu tumesoma pamoja makala za Biblia zinazozungumzia jinsi ya kuendelea kuwa safi kiadili. Tunathamini jinsi ambavyo zimetusaidia kuendelea kuwa na dhamiri safi.’’—Leticia
[Sanduku katika ukurasa wa 44]
Namna Gani Ikiwa Tumepita Mipaka?
Namna gani ikiwa umetumbukia katika mwenendo usiofaa? Usijidanganye kwa kufikiri kwamba unaweza kutatua tatizo hilo mwenyewe. Kijana mmoja alisema: “Nyakati nyingine ningesali hivi, ‘Tusaidie tusifanye hivyo tena.’ Nyakati nyingine kufanya hivyo kulisaidia, lakini nyakati fulani hakukusaidia.” Hivyo, zungumza na wazazi wako. Pia, Biblia inatoa shauri hili zuri: ‘Waite wanaume wazee wa kutaniko.’ (Yakobo 5:14) Wachungaji hao Wakristo wanaweza kukupa mashauri na karipio ili urekebishe uhusiano wako pamoja na Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 47]
Je, ungeweka king’ora cha moto katika nyumba baada ya nyumba hiyo kushika moto? Basi msingoje mpaka wakati ambapo tamaa zenu zimewaka ndipo mjaribu kuweka mipaka kuhusu kuonyeshana mahaba
-
-
Kwa Nini Uendelee Kuwa Bikira?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 5
Kwa Nini Uendelee Kuwa Bikira?
“Kuna mkazo mwingi wa kufanya ngono.”—Kelly.
“Ninahisi kana kwamba nina kasoro kwa kuwa bado mimi ni bikira.”—Jordon.
“BADO wewe ni bikira?” Swali hilo linaweza kukushtua! Katika sehemu nyingi, kijana ambaye bado ni bikira anaweza kuonwa kuwa mtu wa ajabu au mwenye kasoro. Ndiyo sababu vijana wengi wanafanya ngono mapema maishani!
Kuvutwa na Tamaa, Kusukumwa na Marika
Ikiwa wewe ni Mkristo, unajua kwamba Biblia inakuambia ‘ujiepushe na uasherati.’ (1 Wathesalonike 4:3) Hata hivyo, huenda ikawa vigumu kwako kudhibiti tamaa zako za ngono. Kijana mmoja anayeitwa Paul anakiri hivi: “Nyakati nyingine, mimi huanza tu kufikiri kuhusu ngono bila sababu yoyote hususa.”
Uwe na hakika kwamba hizo ni hisia za kawaida. Hata hivyo, kudhihakiwa na kusumbuliwa sikuzote kwa sababu ya kuwa bikira si jambo la kupendeza! Kwa mfano, namna gani marafiki wako wakikwambia kwamba wewe si mwanamume au mwanamke halisi ikiwa hujafanya ngono? “Marafiki huzungumzia ngono kana kwamba ni raha tupu na jambo la kawaida,” Ellen anasema. “Ikiwa hujihusishi na ngono unaonwa kuwa mshamba.”
Lakini huenda marafiki wako wasikuambie matokeo ya kufanya ngono kabla ya ndoa. Kwa mfano, Maria ambaye alifanya ngono na mvulana aliyekuwa rafiki yake anakumbuka: “Baadaye nilifedheheka na kuona aibu. Nilijichukia na kumchukia mvulana huyo.” Hali kama hizo hutokea mara nyingi kuliko vijana wengi wanavyofikiri. Ukweli ni kwamba, kufanya ngono kabla ya ndoa mara nyingi hutokeza maumivu ya kihisia na madhara makubwa!
Hata hivyo, msichana anayeitwa Shanda anauliza, “Kwa nini Mungu aliwapa vijana tamaa za ngono akijua kwamba hawapaswi kuzitosheleza kabla ya ndoa?” Hilo ni swali zuri. Lakini fikiria mambo yafuatayo:
Je, tamaa za ngono tu ndizo hisia zenye nguvu unazopata? Hapana. Yehova Mungu alikuumba na uwezo wa kuwa na tamaa na hisia nyingi mbalimbali.
Je, ni lazima utosheleze kila tamaa mara tu inapotokea? Hapana, kwa sababu Mungu alikupa pia uwezo wa kudhibiti matendo yako.
Basi, tuseme nini? Huenda huwezi kuzuia tamaa fulani zisitokee, lakini unaweza kudhibiti matendo yako. Kwa hakika, kutosheleza tamaa yako ya ngono kila mara inapotokea ni kosa na ni kutotumia akili sawa tu na kumpiga mtu kila mara unapokuwa na hasira.
Ukweli ni kwamba Mungu hakukusudia tutumie vibaya nguvu zetu za uzazi. Biblia inasema: “Kila mmoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe [au, mwili wake mwenyewe] katika utakaso na heshima.” (1 Wathesalonike 4:4) Kama vile kuna “wakati wa kupenda na wakati wa kuchukia,” vivyo hivyo kuna wakati wa kutosheleza tamaa za ngono na wakati wa kuepuka kufanya hivyo. (Mhubiri 3:1-8) Vyovyote vile, wewe tu ndiwe unayeweza kudhibiti tamaa zako!
Lakini namna gani mtu akikudhihaki kwa kusema hivi kwa mshangao, “Eti bado wewe ni bikira?” Usiogope. Ikiwa mtu huyo anataka tu kukuaibisha, unaweza kusema: “Ndiyo, bado mimi ni bikira, na ninafurahia jambo hilo.” Au unaweza kusema, “Hilo ni jambo la kibinafsi ambalo silizungumzii na wengine.”a (Methali 26:4; Wakolosai 4:6) Kwa upande mwingine, huenda ukahisi kwamba mtu anayekuuliza swali hilo anahitaji kujua zaidi. Hivyo, unaweza kuamua kumweleza msimamo wako unaotegemea Biblia.
Je, unaweza kufikiria njia nyingine za kujibu unapoulizwa hivi kwa dhihaka “Eti bado wewe ni bikira?” Ikiwa ndivyo, andika majibu hayo hapa chini.
․․․․․
Zawadi Yenye Thamani
Mungu anahisi jinsi gani watu wanapofanya ngono kabla ya ndoa? Wazia kwamba umemnunulia rafiki yako zawadi. Lakini kabla hata hujampa zawadi hiyo, anaifungua kwa sababu ya udadisi! Ungeudhika, sivyo? Wazia basi jinsi ambavyo Mungu angehisi ikiwa ungefanya ngono kabla ya ndoa. Anataka ungoje mpaka utakapofunga ndoa ili ufurahie zawadi ya ngono.—Mwanzo 1:28.
Unapaswa kufanya nini kuhusu hisia zako za ngono? Jizoeze kuzidhibiti. Inawezekana! Mwombe Yehova akusaidie. Roho yake inaweza kuzidisha uwezo wako wa kujizuia. (Wagalatia 5:22, 23) Kumbuka kwamba Yehova “hatawanyima jambo lolote jema wale wanaotembea bila kosa.” (Zaburi 84:11) Kijana mmoja anayeitwa Gordon anasema: “Ninapoanza kufikiria kwamba hakuna ubaya wowote wa kufanya ngono kabla ya ndoa, ninakumbuka hatari za kiroho na kutambua kwamba uhusiano wangu na Yehova ni wenye thamani sana hivi kwamba siwezi kuruhusu uharibiwe na dhambi yoyote ile.”
Ukweli ni kwamba kuwa bikira si jambo la kushangaza wala haimaanishi kwamba una kasoro. Kwa upande mwingine, upotovu katika ngono unasababisha aibu, kuvunjika moyo, na madhara mengine. Kwa hiyo, usiruhusu propaganda ya ulimwengu ikudanganye kufikiri kwamba una kasoro ukishikamana na viwango vya Biblia. Kwa kutunza ubikira wako, unatunza afya yako, hisia zako, na zaidi ya yote, uhusiano wako pamoja na Mungu.
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 24
[Maelezo ya Chini]
a Wakati mmoja, Yesu aliamua kunyamaza Herode alipomuuliza maswali. (Luka 23:8, 9) Mara nyingi hakuna haja ya kujibu maswali ya upuuzi.
MAANDIKO MUHIMU
“Ikiwa yeyote . . . amefanya uamuzi huu katika moyo wake mwenyewe, kutunza ubikira wake mwenyewe, yeye atafanya vema.”—1 Wakorintho 7:37.
PENDEKEZO
Epuka kushirikiana na watu ambao hawafuati viwango vya juu vya maadili, hata wakidai kwamba wana imani kama yako.
JE, WAJUA . . .?
Ni vigumu sana kwa watu wenye mwenendo mpotovu kingono kuacha tabia hiyo eti kwa sababu wamefunga ndoa. Lakini kuna uwezekano mkubwa kwamba wale ambao ni washikamanifu kwa viwango vya Mungu vya maadili kabla ya kufunga ndoa watakuwa washikamanifu kwa wenzi wao baadaye.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ikiwa ninataka kutunza ubikira mpaka nitakapofunga ndoa, ninahitaji ․․․․․
Ikiwa rafiki zangu wanafanya iwe vigumu kushikilia azimio langu, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa maoni yako, unafikiri ni kwa nini watu huwadhihaki wale ambao ni mabikira?
● Kwa nini inaweza kuwa vigumu kutunza ubikira?
● Kuna faida gani za kutunza ubikira mpaka wakati utakapofunga ndoa?
● Ni jinsi gani unaweza kumweleza mdogo wako faida za ubikira?
[Blabu katika ukurasa wa 51]
“Mimi huepuka kishawishi cha kufanya ngono kwa kukumbuka sikuzote kwamba ‘hakuna mwasherati au mtu asiye safi aliye na urithi wowote katika ufalme wa Mungu.’’’ (Waefeso 5:5)—Lydia
[Sanduku katika ukurasa wa 49]
Ukurasa wa Mazoezi
Ni Nini Hasa Kinachotokea Baadaye?
Mara nyingi marafiki wako na burudani zinazopendwa wanatumia ujanja kuficha matokeo mabaya ya kufanya ngono kabla ya ndoa. Ona mambo matatu yanayofuata. Unafikiri ni nini hasa kitakachowapata vijana hawa?
● Mwanafunzi mmoja anajigamba kwamba amefanya ngono na wasichana wengi. Anasema kwamba ni raha na hakuna madhara yoyote. Ni nini hasa kitakachotokea baadaye—kwake na kwa wasichana hao? ․․․․․
● Sinema inaisha ikionyesha vijana wawili ambao hawajafunga ndoa wakifanya ngono ili kuonyeshana upendo. Ni nini kinachoweza kutokea baadaye kihalisi? ․․․․․
● Unakutana na mvulana mwenye sura ya kuvutia anayetaka ufanye ngono naye. Anakuambia kwamba hakuna mtu atakayejua. Ukikubali na kisha ujaribu kuficha jambo hilo, ni nini hasa kinachoweza kutokea baadaye? ․․․․․
[Picha katika ukurasa wa 54]
Kufanya ngono kabla ya ndoa ni kama kufungua zawadi kabla ya kukabidhiwa
-
-
Kwa Nini Mwili Wangu Unabadilika?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 6
Kwa Nini Mwili Wangu Unabadilika?
“Nilirefuka haraka sana. Nilikuwa na maumivu mengi. Ingawa nilipenda kuwa mrefu, nilikuwa na maumivu ya miguu. Hilo halikunifurahisha hata kidogo!”—Paul.
“Unajua kwamba mwili wako unabadilika, hata hivyo hungependa yeyote atambue. Kisha, mtu fulani anakuambia kwamba una kiuno cha mwanamke aliyekomaa—unatamani dunia ipasuke na kukumeza!”—Chanelle.
UMEWAHI kuhamia eneo lingine pamoja na familia yenu? Yalikuwa mabadiliko makubwa, sivyo? Uliacha kila kitu ulichokuwa umezoea—nyumba yenu, shule yenu, na marafiki wako. Yaelekea ilikuchukua muda mrefu kuzoea mazingira yako mapya.
Mwanzoni mwa kipindi cha kubalehe—wakati ambapo mwili wako unaanza kukomaa—unaingia katika kipindi cha baadhi ya mabadiliko makubwa zaidi maishani. Ni kana kwamba unahamia “eneo” jipya. Bila shaka ni jambo lenye kusisimua! Lakini kuingia katika kipindi cha utu uzima kwaweza kukutatanisha na huenda isiwe rahisi kwako kuzoea hali hiyo. Ni nini kinachotukia katika kipindi hicho kigumu maishani?
Mabadiliko ya Wasichana
Kipindi cha kubalehe ni wakati wa mabadiliko makubwa. Mabadiliko mengine yataonekana wazi. Kwa mfano, homoni zitasababisha nywele ziote kwenye maeneo ya viungo vyako vya uzazi. Pia, matiti, kiuno, mapaja, na makalio yatakuwa makubwa. Mwili wako utaanza kubadilika na kuchukua umbo la mwanamke mkomavu. Usiwe na wasiwasi. Hupaswi kushangazwa—mabadiliko hayo ni mambo ya kawaida kabisa. Na yanaonyesha kwamba mwili wako unajitayarisha kwa ajili ya wakati ambapo utaweza kupata mtoto!
Muda fulani baada ya kuanza kubalehe, utaanza kupata hedhi. Usipojitayarisha vya kutosha, badiliko hilo kubwa maishani mwako linaweza kuogopesha. “Nilipoanza kupata hedhi, sikuwa tayari hata kidogo,” asema Samantha. “Nilijiona kuwa mchafu. Nilikuwa nikijisugua sana nilipokuwa nikioga. Nilijiona kuwa ‘mwenye kuchukiza sana.’ Niliogopa sana nilipofikiria kwamba kwa miaka mingi nitakuwa nikipata hedhi kila mwezi!”
Hata hivyo, kumbuka kwamba kupata hedhi kunaonyesha kwamba nguvu zako za uzazi zinakua. Ijapokuwa miaka mingi itapita kabla hujawa mzazi, unaendelea kukomaa na kuwa mwanamke. Vyovyote vile, kuanza kupata hedhi kunaweza kuwa jambo la kuhangaisha. “Jambo kubwa zaidi nililolazimika kukabili ni kubadilika-badilika kwa hisia,” asema Kelli. “Nilifadhaika sana kwa kuwa sikujua kwa nini ningeweza kuwa na furaha mchana kutwa, na kulia kwelikweli usiku wa siku hiyohiyo.”
Ikiwa hivyo ndivyo unavyohisi sasa, uwe na subira. Baada ya muda utazoea. Annette, mwenye umri wa miaka 20, anasema: “Nakumbuka wakati nilipofikia hatua ya kukubali kwamba ili niwe mwanamke mkomavu mabadiliko hayo lazima yatokee na kwamba Yehova amenipa zawadi ya uzazi. Inachukua muda kukubali jambo hilo, na inakuwa vigumu sana kwa wasichana fulani; lakini baada ya muda unajifunza kukubali mabadiliko hayo.”
Je, umeanza kujionea yoyote kati ya mabadiliko hayo ambayo yamezungumziwa? Katika nafasi zilizo hapa chini, andika maswali yoyote uliyo nayo kuhusu mabadiliko yanayokupata.
․․․․․
Mabadiliko ya Wavulana
Ikiwa wewe ni mvulana, kipindi cha kubalehe kitabadili sana sura yako. Kwa mfano, huenda mara nyingi ngozi yako ikawa na mafuta mengi na kutokeza chunusi.a “Inafadhaisha na kuvunja moyo sana kuwa na chunusi,” asema Matt mwenye umri wa miaka 18. “Unahitaji kupigana vita vikali na chunusi hizo. Huwezi kujua ikiwa zitakwisha au zitaacha makovu au ikiwa watu watakudharau kwa sababu una chunusi.”
Kwa upande mwingine, huenda ukaona kwamba unazidi kuwa mkubwa na mwenye nguvu na kwamba mabega yako yanaanza kupanuka. Pia, wakati wa kubalehe, nywele zinaweza kuota kwenye miguu, kifua, na uso wako, na pia kwenye makwapa yako. Hata hivyo, kumbuka kwamba kuwa na nywele nyingi hakumaanishi kwamba wewe ni dume sasa; hilo ni jambo linalotegemea urithi tu.
Kwa kuwa sehemu mbalimbali za mwili wako hukua kwa viwango tofauti, unaweza kuhisi kwamba sura yako haipendezi. Dwayne anasema hivi kuhusu wakati alipobalehe: “Nilionekana kama ngamia mwenye miguu ya twiga. Ilionekana kana kwamba ujumbe kutoka kwenye ubongo wangu ungechukua juma moja kabla ya kufika kwenye miguu!”
Katika miaka ya katikati ya utineja sauti yako inakuwa nzito zaidi hatua kwa hatua. Kwa muda fulani, sauti nzito inaweza kukatizwa-katizwa na sauti nyembamba na kali, jambo ambalo linaweza kukufanya uaibike. Hata hivyo, usijali. Baada ya muda, sauti yako itasawazika. Kwa sasa, kujifunza kutohangaishwa na hali hiyo kutakupunguzia aibu.
Mfumo wako wa uzazi unapozidi kukomaa, viungo vyako vya uzazi vitakuwa vikubwa na nywele zitaota kandokando. Pia vitaanza kutokeza umajimaji unaoitwa shahawa. Umajimaji huo huwa na mamilioni ya mbegu za uzazi zisizoweza kuonekana kwa macho, ambazo hupitishwa wakati wa ngono. Mbegu moja inaweza kutungisha mimba yai la mwanamke na kutokeza mtoto.
Umajimaji huo unapoongezeka mwilini, kiasi fulani hufyonzwa mwilini, lakini mara kwa mara, mwingine unatoka usiku unapolala. Hilo ni jambo la kawaida. Hata Biblia hulizungumzia. (Mambo ya Walawi 15:16, 17) Jambo hilo linaonyesha kwamba mfumo wako wa uzazi unafanya kazi na kwamba unaelekea kuwa mwanamume mkomavu.
Je, umeanza kujionea yoyote kati ya mabadiliko hayo ambayo yamezungumziwa? Katika nafasi zilizo hapa chini, andika maswali yoyote uliyo nayo kuhusu mabadiliko yanayokupata.
․․․․․
Kushughulika na Mabadiliko ya Kihisia
Mfumo wa uzazi unapoendelea kukomaa, wavulana na wasichana huanza kuvutiwa na watu wa jinsia tofauti. “Nilipoingia kipindi cha kubalehe, ghafula nilianza kuona wasichana wengi kuwa warembo,” anasema Matt. “Lilikuwa jambo lenye kuvunja moyo sana, kwa kuwa singeweza kufanya lolote mpaka wakati ambapo ningekuwa na umri mkubwa zaidi.” Sura ya 29 ya kitabu hiki itazungumzia zaidi hali hiyo. Hata hivyo, kwa sasa unapaswa kutambua kwamba unahitaji kujifunza kuzuia tamaa zako za ngono. (Wakolosai 3:5) Amini usiamini, unaweza kuamua kutozitosheleza!
Kuna hisia nyingine pia ambazo hutokea katika kipindi cha kubalehe. Kwa mfano, huenda ukajiona kuwa mtu asiyefaa kitu. Vijana wengi huwa wapweke na kushuka moyo mara kwa mara. Pindi hizo, ni vizuri kuzungumza na mzazi au mtu mwingine mzima unayemwamini. Andika jina la mtu mzima ambaye wewe unaweza kuzungumza naye kuhusu hisia zako.
․․․․․
Ukuzi wa Maana Zaidi
Ukuzi wa maana zaidi si wa kimo, umbo, wala sura yako, bali utu wako, yaani, ukuzi wa kiakili, kihisia na, zaidi ya yote, wa kiroho. Mtume Paulo alisema hivi: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa nikisema kama mtoto, nikifikiri kama mtoto, nikiwaza kama mtoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za mtoto.” (1 Wakorintho 13:11) Ndiyo, haitoshi tu kuonekana kama mtu mzima. Lazima ujifunze kutenda, kuzungumza, na kufikiri kama mtu mzima. Usijihangaishe sana na mabadiliko ya mwili hivi kwamba umpuuze yule mtu wa ndani!
Pia, kumbuka kwamba Mungu “huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Samweli 16:7) Biblia inasema kwamba Mfalme Sauli alikuwa mrefu na mwenye sura nzuri, lakini hakupata mafanikio akiwa mfalme wala maishani. (1 Samweli 9:2) Tofauti naye, Zakayo alikuwa “mfupi,” hata hivyo alikuwa na ujasiri wa kubadili maisha yake na kuwa mwanafunzi wa Yesu. (Luka 19:2-10) Ni wazi kwamba jinsi mtu alivyo kwa ndani ndilo jambo la maana.
Ukweli ni kwamba: Hakuna njia yoyote salama ya kuharakisha au kukawiza jinsi mwili unavyokua. Kwa hiyo, badala ya kuchukia na kuogopa mabadiliko hayo, jipe moyo na usihangaishwe na mambo kupita kiasi. Kubalehe si ugonjwa, wala wewe si mtu wa kwanza kubalehe. Uwe na hakika kabisa kwamba maisha yako hayako hatarini hata kidogo. Dhoruba ya kubalehe itakapokuwa imepita, utaibuka ukiwa mtu mzima aliyekomaa!
Namna gani ikiwa hufurahishwi na kile unachoona unajipotazama kwenye kioo? Unaweza kufanya nini ili uwe na maoni yanayofaa kuhusu sura yako?
[Maelezo ya Chini]
a Wasichana pia hupata chunusi. Tatizo hilo linaweza kupunguzwa kwa kutunza ngozi ifaavyo.
MAANDIKO MUHIMU
“Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha.”—Zaburi 139:14.
PENDEKEZO
Mwili wako unapoanza kukua, epuka kuvalia mavazi yanayochochea hamu ya ngono. Sikuzote, valia kwa “kiasi na utimamu wa akili.”—1 Timotheo 2:9.
JE, WAJUA . . . ?
Kipindi cha kubalehe chaweza kuanza mapema sana, kuanzia umri wa miaka minane hivi, au kinaweza kuchelewa na kuanza mtu anapokuwa katika miaka ya katikati ya utineja. Hata mtu aanze kubalehe wakati gani, haimaanishi kwamba ana kasoro.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ninapozidi kukomaa na kuwa mtu mzima, sifa ninayohitaji kufanyia kazi sana ni ․․․․․
Ili kukua kiroho, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini ni vigumu sana kushughulika na mabadiliko ya kimwili na ya kihisia wakati wa kipindi cha kubalehe?
● Ni nini unachoona kuwa kigumu sana katika mabadiliko hayo?
● Kwa nini huenda upendo wako kwa Mungu ukaelekea kupungua katika kipindi cha kubalehe, lakini unaweza kuzuia jinsi gani jambo hilo lisitokee?
[Blabu katika ukurasa wa 61]
Kuna hali nyingi zenye kutia wasiwasi katika kipindi cha kubalehe, na huenda usijue jinsi mwili wako utakavyokuwa siku inayofuata. Lakini kadiri unavyokua, unajifunza kukubali mabadiliko hayo na hata kuyafurahia.’’—Annette
[Sanduku katika ukurasa wa 63, 64]
Ninaweza Kuzungumza Namna Gani na Baba Yangu au Mama Yangu Kuhusu Ngono?
“Nikiwa na swali lolote kuhusu ngono, siwezi kamwe kuwauliza wazazi wangu.”—Beth.
“Siwezi hata kupata ujasiri wa kutaja mambo hayo.”—Dennis.
Ikiwa uko kama Beth au Dennis, uko katika hali ngumu sana. Ungependa kujua kuhusu ngono, lakini watu walio na majibu ndio watu ambao hungependa kuwauliza—wazazi wako! Una maswali mengi yanayokuhangaisha:
Wataniona namna gani?
“Sitaki waanze kunishuku kwa sababu ya kuuliza.”—Jessica.
“Wanataka uendelee kuwa mtoto asiyejua chochote milele, na siku utakapoanza kuzungumza nao kuhusu ngono, mambo kwisha.”—Beth.
Watafikiri nini?
“Naogopa kwamba wazazi wangu watanihukumu na kuanza kunigombeza hata kabla sijamaliza kuzungumza.”—Gloria.
“Wazazi wangu hawajui kuficha hisia zao, kwa hiyo, naogopa kwamba sura zao zitaonyesha kwamba wamevunjika moyo. Kwanza, huenda hata baba yangu akaanza kufikiria jinsi ya kunigombeza huku nikiendelea kuzungumza.”—Pam.
Je, watakosa kunielewa?
“Huenda wakakasirika na kuanza kuuliza maswali kama vile, ‘Kuna mtu anayekushawishi mfanye ngono?’ au ‘Rafiki zako wanakushinikiza?’ Lakini huenda tu unataka kujua.”—Lisa.
“Kila mara nikitaja tu mvulana yeyote, baba yangu huingiwa na wasiwasi. Kisha anaanza kunionya kuhusu ngono. Kisha nawaza, ‘Ni nani aliyesema kuhusu ndoa au ngono? Nimesema tu kwamba ana sura ya kuvutia.’”—Stacey.
Huenda ikakuliwaza kujua kwamba wazazi wako pia wanaona ugumu kuzungumza na wewe kuhusu ngono, kama vile tu unavyoona ugumu kuzungumza nao! Huenda ndiyo sababu uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 65 ya wazazi walidai kwamba wamezungumza na watoto wao kuhusu ngono, hali ni asilimia 41 tu ya watoto wanaokumbuka mazungumzo hayo kati yao na wazazi wao.
Ukweli ni kwamba, huenda wazazi wako wakasita kuzungumzia ngono. Kama ilivyo katika visa vingi, huenda wazazi wao hawakuzungumza nao kamwe kuhusu ngono! Hata sababu iwe gani, waelewe wazazi wako. Labda hata wewe mwenyewe unaweza kuanzisha mazungumzo hayo. Ingawa kufanya hivyo kunahitaji ujasiri mwingi, ninyi nyote, wewe na wao pia, mtafaidika. Jinsi gani?
Kuanzisha Mazungumzo
Wazazi wako wana hekima na mashauri mengi kuhusu ngono. Unachohitaji tu ni njia ya kuanzisha mazungumzo hayo. Jaribu njia inayofuata:
1 Eleza wasiwasi wako tangu mwanzo. “Nasita kuongea nawe kuhusu habari hii kwa kuwa huenda ukafikiri . . . ”
2 Kisha mwambie mzazi wako kwa nini umemwendea yeye. “Hata hivyo nina swali, na nimeona afadhali nikuulize wewe kuliko kumwuliza mtu mwingine yeyote.”
3 Halafu taja jambo linalokusumbua. “Swali langu ni . . . ”
4 Mwishoni mwa mazungumzo, hakikisha kwamba kuna nafasi ya kuendeleza mazungumzo hayo wakati ujao. “Nikiwa na swali lingine lolote, je, naweza kukuuliza tena?”
Hata ikiwa unajua atajibu ndiyo, kumsikia mzazi wako akisema hivyo kwaweza kufanya iwe rahisi kuzungumzia habari hiyo wakati ujao uhitaji utakapotokea. Basi jaribu njia hiyo! Huenda ukakubaliana na Trina. Sasa, akiwa na umri wa miaka 24, anasema: “Mimi na mama yangu tulipokuwa tukizungumza, nakumbuka nikitamani dunia ipasuke. Lakini sasa, nafurahi kwamba mama yangu aliniambia mambo waziwazi. Huo umekuwa ulinzi kwelikweli!”
[Picha katika ukurasa wa 59]
Kuyaaga maisha ya utotoni ni kama kuhamia eneo lingine—lakini unaweza kuzoea mabadiliko hayo
-
-
Nifanye Nini Ili Niache Kufikiria Ngono Saa Zote?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 29
Nifanye Nini Ili Niache Kufikiria Ngono Saa Zote?
“MIMI hujikuta nikifikiria wasichana saa zote—hata wakati ambapo hawapo,” asema kijana mmoja anayeitwa Michael. “Sielewi. Nyakati nyingine siwezi kukazia fikira jambo lolote!”
Je, wewe hutumia saa nyingi ukiwaza juu ya watu wa jinsia tofauti, kama anavyofanya Michael? Ikiwa ndivyo, huenda ukahisi kana kwamba unapigana vita na akili yako. Fikira za ngono huingia akilini mwako kama jeshi la adui. “Fikira hizo zinaweza kukutawala,” asema Michael. “Zinaweza kukufanya uzunguke njia ndefu ili tu umtupie jicho msichana fulani mrembo, au kutembea-tembea dukani wakati ambapo hukusudii kununua chochote ili tu umtazame mtu fulani kwa ukaribu.”
Hata hivyo, kumbuka kwamba kuwa na hisia za ngono si dhambi. Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke wakiwa na uvutano wenye nguvu kati yao, na hakuna ubaya wa kutosheleza tamaa za ngono katika mpango wa ndoa. Kabla ya kufunga ndoa, huenda ukawa na tamaa kali za ngono. Hilo likitokea, usidhani kwamba wewe ni mtu mwovu au kwamba huwezi kuishi maisha safi. Unaweza kudumisha usafi wa kiadili ukiamua kufanya hivyo! Lakini ili ufanikiwe, utahitaji kudhibiti mawazo yako kuhusu watu wa jinsi tofauti. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani?
Angalia watu unaoshirikiana nao. Wanafunzi wenzako wakianza kuzungumzia mambo ya ngono, huenda ukataka kuchangia mazungumzo hayo—ili tu usionekane mshamba. Hata hivyo, kwa kweli kushiriki mazungumzo hayo kutafanya iwe vigumu zaidi kwako kudhibiti mawazo yako. Ufanye nini? Usimame tu na kuondoka? Ndiyo, na usione aibu kufanya hivyo! Mara nyingi inawezekana kuondoka pasipo kuonekana “mtakatifu” au kuwafanya wenzako wakucheke.
Epuka kujifurahisha kwa mambo machafu. Bila shaka, haimaanishi kwamba sinema zote, au miziki yote ni mibaya. Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo burudani nyingi zimekusudiwa kuamsha tamaa zisizofaa za ngono. Biblia inatoa shauri gani? “Acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Epuka kabisa burudani zote zinazoweza kuchochea tamaa zisizofaa za ngono.a
Tatizo la Kupiga Punyeto
Vijana fulani hujaribu kupunguza tamaa ya ngono kwa kupiga punyeto. Lakini kufanya hivyo kunaweza kutokeza matatizo makubwa. Biblia inawahimiza Wakristo hivi: “Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani.” (Wakolosai 3:5) Kupiga punyeto ni kinyume kabisa cha ‘kuua hamu ya ngono.’ Kwa kweli, kupiga punyeto huchochea na kukuza hamu hiyo!
Kupiga punyeto kwaweza kukufanya kuwa mtumwa wa tamaa zako. (Tito 3:3) Hatua moja unayoweza kuchukua ili kushinda zoea hilo ni kuzungumza na mtu unayemtumaini. Mkristo aliyekuwa na tatizo la kupiga punyeto kwa miaka mingi anasema hivi: “Laiti ningeweza kupata ujasiri wa kuzungumza na mtu fulani kuhusu tatizo hilo nilipokuwa kijana! Kwa miaka mingi nilisumbuliwa na hisia za hatia, nazo ziliathiri sana uhusiano wangu na wengine, na zaidi ya yote, uhusiano wangu na Yehova.”
Ni nani unayeweza kuongea naye? Mara nyingi ingefaa kuzungumza na mzazi. Au huenda Mkristo mkomavu kutanikoni anaweza kukusaidia. Unaweza kuanza kwa kusema, “Ningependa kuzungumza nawe kuhusu tatizo linalonisumbua sana.”
André aliongea na mzee Mkristo, naye anafurahi kwamba alifanya hivyo. “Mzee huyo alipokuwa akinisikiliza, alilengwa-lengwa na machozi,” André anasema. “Nilipomaliza kuzungumza, alinihakikishia kwamba Yehova ananipenda. Aliniambia kwamba watu wengi wana tatizo kama langu. Aliahidi kwamba atakuwa akizungumza nami mara kwa mara kuona nimefanya maendeleo kiasi gani na kuniletea habari zaidi kutoka katika vitabu vinavyotegemea Biblia. Baada ya kuongea naye, niliazimia kupiga vita zoea hilo—hata ikiwa ningeanguka mara moja moja.”
Mário aliamua kuongea na baba yake, aliyemjali sana na kuelewa hali yake. Hata alikiri mbele za Mário kwamba alipokuwa kijana haikuwa rahisi kwake kushinda zoea hilo. “Nilitiwa moyo sana na mazungumzo hayo ya waziwazi na unyoofu wa baba yangu,” asema Mário. “Nilijiambia, ikiwa alifaulu, hata mimi nitafaulu. Niliguswa moyo sana na mtazamo wa baba yangu hivi kwamba sikujizuia kulia.”
Kama André na Mário, wewe pia unaweza kupata msaada wa kushinda zoea la kupiga punyeto. Hata ukijikuta umetumbukia tena, usikate tamaa! Uwe na hakika kwamba unaweza kushinda vita hivyo.b
Dhibiti Fikira Zako
Mtume Paulo alisema: “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa.” (1 Wakorintho 9:27) Vivyo hivyo, huenda wewe pia ukahitaji kujitia nidhamu wakati mawazo yasiyofaa kuhusu watu wa jinsia tofauti yanapoingia katika akili yako. Mawazo hayo yakiendelea, jaribu kufanya mazoezi ya kimwili. Biblia inasema: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo.” (1 Timotheo 4:8) Kutembea kasi kwa muda au kufanya mazoezi ya kimwili kwa dakika chache kwaweza kukusaidia kuondolea mbali mawazo hayo yasiyofaa.
Zaidi ya yote, usipuuze msaada kutoka kwa Baba yako wa mbinguni. Mkristo mmoja anasema hivi: “Tamaa za ngono zinapoanza kuamka najilazimisha kusali.” Si kwamba Mungu atakufanya uache kupendezwa na watu wa jinsia tofauti. Lakini anaweza kukusaidia kuona kwamba kuna mambo mengine mengi unayoweza kukazia fikira zako.
[Maelezo ya Chini]
a Tafrija na burudani zinazungumziwa kwa mapana na marefu katika Sehemu ya 8 ya kitabu hiki.
b Habari zaidi kuhusu zoea la kupiga punyeto zinazungumziwa katika Buku la 1, sura ya 25.
MAANDIKO MUHIMU
“Wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.”—Wafilipi 4:8.
PENDEKEZO
Ikiwa umetumbukia tena katika zoea la kupiga punyeto, endelea kupambana! Chunguza kwa makini kilichokufanya urudie zoea hilo, na ujaribu kukiepuka.
JE, WAJUA . . .?
Mambo unayoruhusu yakae akilini mwako yanaweza kuwa na uvutano juu ya utu wako na kuathiri matendo yako.—Yakobo 1:14, 15.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ili niache kufikiria sana watu wa jinsia tofauti, nita ․․․․․
Wanafunzi wenzangu wakianza kuzungumzia mambo yasiyofaa au machafu kiadili, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini hisia za ngono hazipaswi kuonwa kuwa “adui” nyakati zote?
● Kwa nini unahitaji kudhibiti hisia zako za ngono?
● Ni burudani za aina gani zinazoweza kukufanya ukazie fikira watu wa jinsia tofauti?
● Kwa nini ni muhimu kuondoka wakati mazungumzo yanapoanza kuwa yasiyofaa au machafu?
[Blabu katika ukurasa wa 240]
‘‘Kinachonisaidia ni kuanza kufikiria mambo mengine—kutoa fikira zangu katika mambo yanayoamsha tamaa za ngono. Mimi hujikumbusha kwamba hisia na tamaa hizo zitakwisha mwishowe.’’—Scott
[Picha katika ukurasa wa 239]
Ungekubali kompyuta yako iingiwe na virusi? Basi kwa nini uingize mawazo yasiyofaa akilini mwako?
-