Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Tukifa tunaenda wapi?
    Biblia Inatufundisha Nini?
    • SURA YA SITA

      Tukifa Tunaenda Wapi?

      1-3. Huenda ukauliza maswali gani kuhusu kifo, na baadhi ya dini hujibuje?

      BIBLIA inatuahidi kwamba “kifo hakitakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Katika Sura ya 5, tulijifunza kwamba fidia inatuwezesha kupata uzima wa milele. Lakini bado tunaendelea kufa. (Mhubiri 9:5) Kwa hiyo, swali ni, Tukifa tunaenda wapi?

      2 Jibu la swali hilo ni muhimu hasa tunapofiwa na mtu tunayempenda. Huenda tukajiuliza: ‘Ameenda wapi? Je, anatuona? Je, anaweza kutusaidia? Je, tutamwona tena?’

      3 Dini nyingi hujibu maswali hayo kwa njia tofauti. Baadhi yao hufundisha kwamba ikiwa unatenda mema utaenda mbinguni na ikiwa unatenda mabaya utaenda motoni. Nyingine hufundisha kwamba ukifa unabadilika na kuwa roho kisha unaenda kuishi na ndugu zako waliokufa. Na nyingine hufundisha kwamba baada ya kufa na kuhukumiwa, unazaliwa upya, au kuwa hai tena ukiwa na mwili tofauti, labda ukiwa mwanadamu au mnyama.

      4. Ni wazo gani kuu ambalo dini nyingi hufundisha kuhusu kifo?

      4 Mambo ambayo dini hufundisha hutofautiana. Hata hivyo, karibu dini hizo zote hufundisha wazo moja kuu. Zinafundisha kwamba mtu akifa, sehemu fulani ya mwanadamu huendelea kuishi. Je, ni kweli?

      TUKIFA TUNAENDA WAPI?

      5, 6. Tukifa tunaenda wapi?

      5 Yehova anajua hali ya wafu, na ametueleza kwamba mtu akifa, uhai wake unakoma. Kifo ni kinyume cha uhai. Kwa hiyo, mtu akifa haendelei kuishi mahali pengine, hisia na mawazo yake hupotea.a Tukifa hatuwezi kuona, kusikia, wala kufikiri.

      6 Mfalme Sulemani aliandika kwamba “waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.” Wafu hawawezi kupenda au kuchukia, na “hakuna kazi wala mipango wala ujuzi wala hekima Kaburini.” (Soma Mhubiri 9:5, 6, 10.) Na katika Zaburi 146:4, Biblia inatuambia kwamba, mtu akifa “mawazo yake” hupotea.

      YESU ALISEMA NINI KUHUSU KIFO?

      Mume na mke wakiwa bustanini wakifurahia ua

      Yehova aliwaumba wanadamu ili waishi milele duniani

      7. Yesu alisema nini kuhusu kifo?

      7 Rafiki yake mpendwa Lazaro alipokufa, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Rafiki yetu Lazaro amelala usingizi.” Lakini Yesu hakumaanisha kwamba Lazaro alikuwa amepumzika. Yesu akaendelea kusema: “Lazaro amekufa.” (Yohana 11:11-14) Kwa hiyo Yesu alilinganisha kifo na usingizi. Hakusema kwamba Lazaro alikuwa mbinguni au pamoja na watu wa familia yake waliokufa zamani. Wala hakusema Lazaro anateseka katika moto wa mateso au amezaliwa upya akiwa mwanadamu au mnyama. Alimaanisha kwamba ni kama Lazaro alikuwa amelala usingizi mzito. Maandiko mengine hufananisha kifo na usingizi mzito. Biblia inasema kwamba Stefano alipouawa, ‘alilala usingizi katika kifo.’ (Matendo 7:60) Pia, mtume Paulo aliandika kwamba baadhi ya Wakristo walikuwa “wamelala usingizi katika kifo.”—1 Wakorintho 15:6.

      8. Tunajuaje kwamba Yehova hakuwaumba wanadamu ili wafe?

      8 Je, Mungu aliwaumba Adamu na Hawa ili wafe? Hapana! Yehova aliwaumba wafurahie maisha milele wakiwa na uhai mkamilifu. Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kuishi milele. (Mhubiri 3:11) Wazazi hawapendi watoto wao wazeeke na kufa na Yehova pia anahisi hivyo kutuhusu. Hata hivyo, ikiwa Yehova alituumba ili tuishi milele, kwa nini tunakufa?

      KWA NINI TUNAKUFA?

      9. Kwa nini Adamu na Hawa walipaswa kutii amri ya Yehova?

      9 Katika bustani ya Edeni, Yehova alimwagiza Adamu hivi: “Unaweza kula matunda ya kila mti katika bustani mpaka ushibe. Lakini kuhusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya, usile matunda yake, kwa maana siku utakapokula matunda yake hakika utakufa.” (Mwanzo 2:9, 16, 17) Haikuwa vigumu kutii amri hiyo iliyo wazi na Yehova alikuwa na haki ya kuwaeleza Adamu na Hawa jambo linalofaa na lisilofaa. Kwa kumtii Yehova, wangeonyesha kwamba wanaheshimu mamlaka yake. Pia, utii ungeonyesha kwamba wanathamini mambo yote ambayo Yehova aliwapa.

      10, 11. (a) Shetani aliwadanganyaje Adamu na Hawa? (b) Kwa nini Adamu na Hawa hawakuwa na sababu ya kutotii amri ya Mungu?

      10 Inasikitisha kwamba Adamu na Hawa waliamua kutomtii Yehova. Shetani alimwuliza Hawa hivi: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Hawa akamjibu: “Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani. Lakini Mungu amesema hivi kuhusu matunda ya mti ulio katikati ya bustani: ‘Msiyale, wala msiyaguse; la sivyo mtakufa.’”—Mwanzo 3:1-3.

      11 Ndipo Shetani akamwambia: “Hakika hamtakufa. Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunguliwa nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:4-6) Shetani alitaka Hawa afikiri kwamba angeweza kujiamulia mwenyewe mambo mema na mabaya. Pia, alimdanganya kuhusu matokeo ya kutomtii Mungu. Shetani alimwambia Hawa kwamba hangekufa, hivyo akala tunda na baadaye akampa mume wake. Adamu na Hawa walijua kabisa kwamba Mungu aliwakataza kula matunda hayo. Hivyo walipokula tunda hilo, walikosa kutii amri rahisi na iliyo wazi. Jambo hilo lilionyesha wazi kwamba walimdharau Baba yao mpendwa wa mbinguni. Hawakuwa na sababu ya kutotii amri ya Mungu!

      12. Kwa nini inasikitisha kwamba Adamu na Hawa walimwasi Yehova?

      12 Inasikitisha kwamba wazazi wetu wa kwanza hawakumheshimu Muumba wao! Ungehisije ikiwa umejitahidi kuwalea vizuri watoto wako lakini baadaye wanakuasi na kufanya mambo tofauti kabisa na uliyowafundisha? Je, hungeumia sana?

      Kuumbwa kwa Adamu

      Adamu aliumbwa kwa mavumbi naye alirudi mavumbini

      13. Yehova alimaanisha nini aliposema “utarudi mavumbini”?

      13 Walipomwasi Mungu, Adamu na Hawa walipoteza fursa ya kuishi milele. Yehova alimwambia Adamu hivi: “Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Soma Mwanzo 3:19.) Jambo hilo lilimaanisha kwamba Adamu angekuwa mavumbi kana kwamba hakuwahi kuishi. (Mwanzo 2:7) Baada ya Adamu kutenda dhambi alikufa na hayupo tena.

      14. Kwa nini tunakufa?

      14 Kama Adamu na Hawa wangemtii Mungu, wangekuwa hai mpaka leo. Lakini walipokataa kumtii, walitenda dhambi na hatimaye wakafa. Dhambi ni kama ugonjwa hatari tuliorithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza. Sote huzaliwa tukiwa na dhambi na ndiyo sababu tunakufa. (Waroma 5:12) Lakini hilo halikuwa kusudi la Mungu alipowaumba wanadamu. Mungu hakutaka wanadamu wafe, ndiyo sababu Biblia hukiita kifo “adui.”—1 Wakorintho 15:26.

      UKWELI UNATUWEKA HURU

      15. Kwa nini kujua ukweli kuhusu kifo hutuweka huru?

      15 Kujua ukweli kuhusu wafu hutuweka huru na maoni yaliyopotoka. Biblia inatufundisha kwamba wafu hawahisi maumivu wala huzuni. Hatuwezi kuwasiliana nao. Hatuwezi kuwasaidia, wala hawawezi kutusaidia. Hawawezi kutudhuru, hivyo hatupaswi kuwaogopa. Hata hivyo, dini nyingi hufundisha kwamba wafu wanaendelea kuishi mahali fulani na tunaweza kuwasaidia kwa kuwapa viongozi wa kidini au watakatifu kiasi fulani cha pesa ili wawaombee. Lakini tukijua ukweli kuhusu kifo hatutadanganywa.

      16. Dini nyingi hufundisha uwongo gani kuhusu wafu?

      16 Shetani anatumia dini za uwongo kutupotosha na kufanya tuhisi kwamba wafu wako hai. Kwa mfano, baadhi ya dini hufundisha kwamba tunapokufa, roho huendelea kuishi mahali fulani. Je, dini yako imekufundisha hivyo au je, inakufundisha mambo ambayo Biblia hufundisha kuhusu wafu? Shetani anatumia uwongo kuwatenganisha watu na Yehova.

      17. Kwa nini fundisho la moto wa mateso linamshushia heshima Yehova?

      17 Mambo ambayo dini nyingi hufundisha yanatisha. Kwa mfano, baadhi ya dini hufundisha kwamba Mungu huwatesa watu waovu motoni milele. Uwongo huo humshushia heshima Yehova. Hawezi kamwe kuwatesa hivyo wanadamu! (Soma 1 Yohana 4:8.) Ungehisije ikiwa mzazi anamwadhibu mtoto wake kwa kumchoma mikono kwa moto? Bila shaka utamwona kuwa mwenye ukatili sana. Hata, hungependa awe rafiki yako. Hivyo ndivyo Shetani anavyotaka tuhisi kumhusu Yehova!

      18. Kwa nini hatupaswi kuwaogopa wafu?

      18 Baadhi ya dini hufundisha kwamba watu wakifa, wanabadilika na kuwa viumbe wa roho. Dini hizo hufundisha kwamba watu wanapaswa kuwaheshimu na kuwaogopa roho hao kwa sababu wanaweza kuwa rafiki au maadui. Watu wengi wanaamini uwongo huo. Wanawaogopa wafu, kwa hiyo wanawaabudu badala ya kumwabudu Yehova. Kumbuka kwamba wafu hawahisi chochote, hivyo basi hatupaswi kuwaogopa. Yehova ndiye aliyetuumba. Yeye ndiye Mungu wa kweli, na tunapaswa kumwabudu yeye peke yake.—Ufunuo 4:11.

      19. Kuna faida gani kujua ukweli kuhusu kifo?

      19 Kujua ukweli kuhusu kifo, hutuweka huru kutokana na mafundisho ya uwongo. Pia, ukweli huo unatusaidia kuelewa vizuri ahadi za Yehova za wakati ujao.

      20. Tutajifunza nini katika sura inayofuata?

      20 Miaka mingi iliyopita, mtumishi wa Mungu, Ayubu, aliuliza hivi: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” (Ayubu 14:14) Je, kweli mtu aliyekufa anaweza kufufuka? Mungu anatupatia jibu zuri sana katika Biblia. Tutajifunza jambo hilo katika sura inayofuata.

      a Baadhi ya watu huamini kwamba roho huendelea kuishi baada ya mtu kufa. Ili kupata habari zaidi, tafadhali soma Maelezo ya Ziada 17 na 18.

      MUHTASARI

      UKWELI WA 1: MTU AKIFA, UHAI WAKE UNAKOMA

      “Waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.”—Mhubiri 9:5

      Ni nini hutokea tukifa?

      • Zaburi 146:3, 4; Mhubiri 9:6, 10

        Tukifa hatuwezi kuona, kusikia, wala kufikiri.

      • Yohana 11:11-14

        Yesu alilinganisha kifo na usingizi.

      UKWELI WA 2: YEHOVA HAKUKUSUDIA WATU WAFE

      “Kuhusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya, usile matunda yake, kwa maana siku utakapokula matunda yake hakika utakufa.”—Mwanzo 2:17

      Kwa nini tunakufa?

      • Mwanzo 3:1-6

        Shetani alimdanganya Hawa kuhusu matokeo ya kutotii sheria ya Mungu. Adamu na Hawa walipomwasi Yehova, walitenda dhambi na hatimaye wakafa.

      • Mwanzo 3:19

        Adamu alipokufa, alikoma kuwapo.

      • Waroma 5:12

        Dhambi ni kama ugonjwa hatari ambao tumerithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza. Sote tunazaliwa tukiwa na dhambi, na ndiyo sababu tunakufa.

      • 1 Wakorintho 15:26

        Biblia inasema kwamba kifo ni adui.

      UKWELI WA 3: UKWELI KUHUSU KIFO HUTUWEKA HURU

      “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena? Nitangojea . . . mpaka kitulizo changu kitakapokuja.”​—Ayubu 14:14

      Kujua ukweli kuhusu kifo hutuwekaje huru kutokana na mafundisho ya uwongo?

      • 1 Yohana 4:8

        Fundisho la moto wa mateso linamshushia Yehova heshima. Hawezi kamwe kuwatesa watu.

      • Ufunuo 4:11

        Watu wengi huwaogopa wafu, kwa hiyo wanawaabudu badala ya kumwabudu Yehova. Yehova ndiye Mungu wa kweli, na tunapaswa kumwabudu yeye peke yake.

  • Kutakuwa na Ufufuo!
    Biblia Inatufundisha Nini?
    • SURA YA SABA

      Kutakuwa na Ufufuo!

      1-3. Sote tumehukumiwa nini, na Yehova atatuwekaje huru?

      WAZIA kwamba umehukumiwa kifungo cha maisha kwa kosa ambalo hukutenda. Hakuna uwezekano wa kuachiliwa huru. Umekata tamaa, na huna la kufanya. Hata hivyo, ukiwa umekata tamaa kabisa, unagundua kwamba mtu fulani ana uwezo wa kukuweka huru na hata ameahidi kukusaidia! Utahisije?

      2 Sote tumehukumiwa kifo. Hata tufanye nini, hatuwezi kukiepuka. Hata hivyo, Yehova ana nguvu za kutuweka huru kutokana na kifo. Ameahidi kwamba “adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”—1 Wakorintho 15:26.

      3 Wazia jinsi utakavyohisi wakati ambao watu hawatakufa! Yehova hataondoa kifo tu, bali atawafufua wale ambao wamekufa. Fikiria jinsi mambo yatakavyokuwa. Anaahidi kwamba “waliokufa ambao hawana uwezo” wataishi. (Isaya 26:19) Katika Biblia tukio hilo linaitwa ufufuo.

      MPENDWA WETU AKIFA

      4. (a) Tunaweza kupata wapi faraja mtu wa familia au rafiki akifa? (b) Baadhi ya rafiki za Yesu wa karibu walikuwa nani?

      4 Mtu wa familia au rafiki wa karibu akifa, sisi hulemewa na uchungu na huzuni. Tunahisi hatuna msaada. Hatuna uwezo wa kumrudishia uhai. Lakini tunaweza kupata faraja ya kweli katika Biblia. (Soma 2 Wakorintho 1:3, 4.) Acheni tuone mfano unaoonyesha kwamba Yehova na Yesu wanatamani kuwafufua wapendwa wetu. Yesu alipokuwa duniani, mara nyingi alimtembelea Lazaro na dada zake, Martha na Maria. Wote watatu walikuwa marafiki wazuri wa Yesu. Biblia inasema: “Yesu aliwapenda Martha na dada yake na Lazaro.” Lakini siku moja Lazaro alikufa.—Yohana 11:3-5.

      5, 6. (a) Yesu alifanya nini alipoona familia na marafiki wa Lazaro wakiomboleza? (b) Kwa nini inafariji kujua jinsi Yesu alivyohisi kuhusu kifo?

      5 Yesu alienda kuwafariji Martha na Maria. Martha aliposikia kwamba Yesu anakuja, alienda jijini kumpokea. Alifurahi kumwona Yesu, lakini akamwambia: “kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa.” Martha alifikiri Yesu amechelewa. Kisha, Yesu akamwona Maria akilia. Alipoona huzuni yao aliumia moyoni naye akalia. (Yohana 11:21, 33, 35) Aliumia sana kama vile tunavyohisi tunapofiwa na mtu tunayempenda.

      6 Tunafarijika tunapojua kwamba Yesu ana hisia kama zetu kuhusu kifo. Yesu ana sifa kama za Baba yake. (Yohana 14:9) Yehova ana uwezo wa kuondoa kifo na atafanya hivyo hivi karibuni.

      “LAZARO, NJOO HUKU NJE!”

      7, 8. Kwa nini Martha hakutaka jiwe liondolewe kwenye kaburi la Lazaro, lakini Yesu alifanya nini?

      7 Yesu alipofika kwenye kaburi ambalo Lazaro alikuwa amezikwa, mwingilio ulikuwa umefunikwa kwa jiwe kubwa. Yesu akawaambia: “Liondoeni jiwe.” Lakini Martha akapinga. Mwili wa Lazaro ulikuwa kaburini kwa siku nne. (Yohana 11:39) Hakujua kile ambacho Yesu alitaka kufanya ili kumsaidia ndugu yake.

      Yesu akimfufua Lazaro, familia na marafiki wanashangilia

      Wazia shangwe waliyohisi familia ya Lazaro alipofufuliwa!​—Yohana 11:38-44

      8 Yesu akamwambia Lazaro: “Njoo huku nje!” Martha na Maria walishangaa sana. “Mtu huyo aliyekuwa amekufa akatoka, miguu na mikono yake ikiwa imefungwa kwa vitambaa.” (Yohana 11:43, 44) Lazaro akawa hai tena! Aliungana tena na familia na rafiki zake. Wangeweza kumkumbatia, kumshika, na kuzungumza naye. Huo ulikuwa muujiza mkubwa sana! Yesu alikuwa amemfufua Lazaro.

      “MSICHANA MDOGO, NINAKUAMBIA, ‘INUKA!’”

      9, 10. (a) Ni nani aliyempa Yesu nguvu za kufufua wafu? (b) Kwa nini masimulizi ya ufufuo ni muhimu sana kwetu?

      9 Je, Yesu aliwafufua wafu kwa nguvu zake? Hapana. Yesu alimwomba Yehova ampe nguvu kabla ya kumfufua Lazaro. (Soma Yohana 11:41, 42.) Si Lazaro peke yake aliyefufuliwa. Biblia inatueleza kuhusu msichana mwenye umri wa miaka 12 aliyekuwa mgonjwa sana. Baba yake, Yairo, alikuwa amekata tamaa, akamsihi Yesu amponye. Alikuwa mtoto wake wa pekee. Alipokuwa akizungumza na Yesu, wanaume fulani walikuja na kusema: “Binti yako amekufa! Kwa nini uendelee kumsumbua Mwalimu?” Lakini Yesu akamwambia Yairo: “Usiogope, uwe tu na imani, naye ataokolewa.” Kisha wakaenda nyumbani kwa Yairo. Walipokuwa wakikaribia nyumbani kwa Yairo, Yesu akaona na kusikia watu wakilia. Yesu akawaambia: “Acheni kulia, kwa maana hajafa bali amelala usingizi.” Lazima wazazi wa binti huyo walishangazwa sana na maneno ya Yesu. Yesu akaamuru watu wote waondoke kisha akaenda pamoja na wazazi wa binti hadi mahali binti alipolazwa, akamshika mkono na kumwita, akisema: “Msichana mdogo, ninakuambia, ‘Inuka!” Wazia shangwe waliyohisi wazazi wake alipoinuka na kuanza kutembea! Yesu alikuwa amemfufua binti yao. (Marko 5:22-24, 35-42; Luka 8:49-56) Kuanzia wakati huo na kuendelea kila walipomtazama binti yao, wangekumbuka jambo ambalo Yehova aliwatendea kupitia Yesu.a

      10 Watu ambao Yesu aliwafufua walikufa tena baadaye. Lakini mambo tunayosoma kuwahusu ni muhimu sana kwetu kwa sababu yanatupa tumaini hakika. Yehova anatamani kuwafufua watu na atafanya hivyo.

      MAMBO TUNAYOJIFUNZA KUTOKANA NA MASIMULIZI YA UFUFUO

      Petro akimfufua Dorkasi, watu wengine wakitazama

      Mtume Petro alimfufua mwanamke Mkristo Dorkasi.​—Matendo 9:36-42

      Mjane akimkumbatia mwana wake baada ya kufufuliwa na Eliya

      Eliya alimfufua mwana wa mjane.​—1 Wafalme 17:17-24

      11. Kifo cha Lazaro kinathibitishaje ukweli wa andiko la Mhubiri 9:5?

      11 Biblia inasema waziwazi kwamba “waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.” Kifo cha Lazaro kilithibitisha ukweli huo. (Mhubiri 9:5) Kama Yesu alivyosema, ni kana kwamba Lazaro alikuwa amelala usingizi tu. (Yohana 11:11) Alipokuwa kaburini Lazaro hakujua “jambo lolote kamwe.”

      12. Tunajuaje kwamba ufufuo wa Lazaro ulitukia?

      12 Yesu alimfufua Lazaro mbele ya watu wengi. Hata maadui wa Yesu walijua kwamba alifanya muujiza huo. Lazaro alikuwa hai tena na hilo lilithibitisha waziwazi kwamba ufufuo huo ulitukia. (Yohana 11:47) Pia, watu wengi walimtembelea Lazaro nao wakaanza kuamini kwamba Yesu alitumwa na Mungu. Jambo hilo liliwachukiza adui za Yesu, hivyo wakapanga kumuua Yesu na Lazaro.—Yohana 11:53; 12: 9-11.

      13. Kwa nini tuwe na uhakika kwamba Yehova atawafufua wafu?

      13 Yesu alisema kwamba “wote walio katika makaburi ya ukumbusho” watafufuliwa. (Yohana 5:28) Jambo hilo linamaanisha kwamba watu wote ambao Yehova anawakumbuka watafufuliwa. Lakini ili Yehova amfufue mtu, anahitaji kukumbuka kila kitu kuhusu mtu huyo. Je, kweli anaweza kukumbuka? Kuna mabilioni ya nyota angani. Biblia inasema kwamba Yehova anajua majina ya nyota hizo zote. (Soma Isaya 40:26.) Kama anaweza kukumbuka jina la kila nyota, ni wazi kwamba atakumbuka kwa urahisi kila kitu kuhusu wale ambao atawafufua. Zaidi ya yote, Yehova aliumba kila kitu. Kwa hiyo, tuna uhakika kwamba ana uwezo wa kuwafufua wafu.

      14, 15. Tunajifunza nini kutokana na maneno ya Ayubu kuhusu ufufuo?

      14 Ayubu, aliyekuwa mwaminifu, aliamini ufufuo. Aliuliza hivi: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” Kisha akamwambia Yehova: “Utaita, nami nitakujibu. Utaitamani sana kazi ya mikono yako.” Kwa kweli, Ayubu alijua kwamba Yehova anatamani sana kuwafufua watu wakati ujao.—Ayubu 14:13-15.

      15 Unahisije kuhusu tumaini la ufufuo? Huenda ukajiuliza, ‘Je, ndugu na rafiki zangu waliokufa watafufuliwa?’ Tunafarijika kujua kwamba Yehova anatamani sana kuwafufua wafu. Acheni tuchunguze jinsi Biblia inavyosema kuhusu wale watakaofufuliwa na mahali watakapoishi.

      “WATAISIKIA SAUTI YAKE NA KUTOKA”

      16. Wale watakaofufuliwa wataishi maisha ya aina gani?

      16 Zamani, wale ambao walifufuliwa waliungana na familia na marafiki zao tena duniani. Jambo hilo litatukia pia wakati ujao, lakini kwa njia bora hata zaidi. Kwa nini? Kwa sababu wale watakaofufuliwa watapata nafasi ya kuishi milele duniani na hawatakufa tena kamwe. Pia, wataishi katika dunia iliyo tofauti sana na leo. Hakutakuwa na vita, uhalifu, na magonjwa.

      17. Ni nani watakaofufuliwa?

      17 Ni nani watakaofufuliwa? Yesu alisema kwamba “wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Pia, andiko la Ufunuo 20:13 linasema: “Na bahari ikawatoa wafu waliokuwa ndani yake, na kifo na Kaburi vikawatoa wafu waliokuwa ndani yake.” Ndiyo, mabilioni ya watu watakuwa hai tena. Mtume Paulo alisema kwamba “waadilifu na wasio waadilifu” watafufuliwa. (Soma Matendo 24:15.) Alimaanisha nini?

      Katika Paradiso wafu watafufuliwa na kuungana na wapendwa wao

      Katika Paradiso, wafu watafufuliwa na kuungana na wapendwa wao

      18. “Waadilifu” watakaofufuliwa ni nani?

      18 “Waadilifu” wanatia ndani watumishi waaminifu wa Yehova walioishi kabla ya Yesu kuja duniani. Watu kama Noa, Abrahamu, Sara, Musa, Ruthu, na Esta watafufuliwa waishi hapa duniani. Unaweza kusoma kuhusu baadhi ya wanaume na wanawake hao katika Waebrania sura ya 11. Vipi kuhusu watumishi waaminifu wa Yehova wanaokufa katika siku zetu? Wao pia ni “waadilifu,” kwa hiyo watafufuliwa.

      19. “Wasio waadilifu” ni nani? Yehova atawapa fursa gani?

      19 “Wasio waadilifu” ni mabilioni ya watu ambao hawakupata fursa ya kujifunza kumhusu Yehova. Ingawa walikufa, Yehova hajawasahau. Atawafufua, na kuwapa fursa ya kujifunza kumhusu na kumtumikia.

      20. Kwa nini si watu wote watakaofufuliwa?

      20 Je, hilo linamaanisha kwamba kila mtu aliyekufa atafufuliwa? Hapana. Yesu alisema kwamba baadhi ya watu hawatafufuliwa. (Luka 12:5) Ni nani atakayeamua ikiwa mtu anastahili kufufuliwa au la? Yehova ndiye mwamuzi mkuu, lakini amempa pia Yesu mamlaka ya “kuwa mwamuzi wa walio hai na wafu.” (Matendo 10:42) Wote watakaohukumiwa kuwa waovu hawatafufuliwa.—Soma Maelezo ya Ziada 19.

      WANAOFUFULIWA KWENDA MBINGUNI

      21, 22. (a) Wale watakaofufuliwa kwenda mbinguni watakuwa na mwili gani? (b) Ni nani aliyekuwa wa kwanza kupata ufufuo wa mbinguni?

      21 Biblia inatuambia pia kwamba baadhi ya watu wataishi mbinguni. Watu wanaofufuliwa kwenda mbinguni, hawafufuliwi na mwili wa nyama. Wanafufuliwa wakaishi mbinguni wakiwa na mwili wa roho.

      22 Yesu alikuwa mwanadamu wa kwanza kupata ufufuo huo. (Yohana 3:13) Yehova alimfufua Yesu siku tatu baada ya kifo chake. (Zaburi 16:10; Matendo 13:34, 35) Yesu hakufufuliwa akiwa na mwili wa kibinadamu. Mtume Petro anaeleza kwamba “aliuawa katika mwili, lakini akafanywa kuwa hai katika roho.” (1 Petro 3:18) Yesu alifufuliwa akiwa mtu wa roho mwenye nguvu! (1 Wakorintho 15:3-6) Hata hivyo, Biblia inasema kwamba hatakuwa peke yake.

      23, 24. “Kundi dogo” ambalo Yesu alizungumzia ni nani na ni wangapi?

      23 Kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake waaminifu: “Ninaenda zangu kuwatayarishia mahali.” (Yohana 14:2) Jambo hilo linamaanisha kwamba baadhi ya wafuasi wake wangefufuliwa ili waishi pamoja naye mbinguni. Ni wangapi? Yesu alisema kwamba wangekuwa wachache tu, “kundi dogo.” (Luka 12:32) Mtume Yohana aliona idadi kamili alipomwona Yesu akiwa “amesimama juu ya Mlima Sayuni [mbinguni], na pamoja naye 144,000.”—Ufunuo 14:1.

      24 Wakristo 144,000 walianza kufufuliwa lini? Biblia inaeleza kwamba ufufuo huo ungeanza baada ya Yesu kuanza kutawala mbinguni. (1 Wakorintho 15:23) Sasa tunaishi katika kipindi hicho, wengi kati ya hao 144,000 tayari wamefufuliwa kwenda mbinguni. Wale waliobaki duniani hufufuliwa mara tu baada ya kufa ili wakaishi mbinguni. Hata hivyo, watu wengi watafufuliwa wakati ujao ili waishi katika Paradiso duniani.

      25. Tutajifunza nini katika sura inayofuata?

      25 Hivi karibuni, Yehova atawaweka wanadamu wote huru kutokana na kifo, na hakitakuwapo tena! (Soma Isaya 25:8.) Hata hivyo, wale wanaofufuliwa kwenda mbinguni watafanya nini huko? Biblia inaeleza kwamba watatawala pamoja na Yesu katika Ufalme wa Mungu. Tutajifunza mengi kuhusu ufalme huo katika sura inayofuata.

      a Katika masimulizi mengine, Biblia inatueleza kuhusu ufufuo wa vijana na watu wazima, wanaume na wanawake, Waisraeli na wakaaji wageni. Unaweza kusoma masimulizi hayo katika 1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37; 13:20, 21; Mathayo 28:5-7; Luka 7:11-17; 8:40-56; Matendo 9:36-42; 20:7-12.

      MUHTASARI

      UKWELI WA 1: YEHOVA ATAONDOA KIFO

      “Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”—1 Wakorintho 15:26

      Biblia inawezaje kutufariji tunapofiwa?

      • 2 Wakorintho 1:3, 4

        Tunaweza kukata tamaa, mtu wa familia au rafiki mpendwa anapokufa. Lakini Biblia inatupatia faraja.

      • Isaya 25:8; 26:19

        Yehova ana uwezo wa kuondoa kifo milele. Pia, atawafufua wale waliokufa.

      UKWELI WA 2: TUNAWEZA KUAMINI UFUFUO

      “Msichana mdogo, ninakuambia, ‘Inuka!” —Marko 5:41

      Kwa nini tunaweza kuamini ufufuo?

      • Yohana 11:1-44

        Yesu alimfufua Lazaro.

      • Marko 5:22-24, 35-42

        Yesu alimfufua msichana mdogo.

      • Yohana 11:41, 42

        Yesu aliwafufua wafu kwa kutumia nguvu za Yehova.

      • Yohana 12:9-11

        Watu wengi walishuhudia Yesu alipowafufua wafu. Hata adui za Yesu walijua jambo hilo.

      UKWELI WA 3: YEHOVA ATAFUFUA MABILIONI YA WAFU

      “Utaita, nami nitakujibu. Utaitamani sana kazi ya mikono yako.”—Ayubu 14:13-15

      Ni nani watakaofufuliwa?

      • Yohana 5:28, 29

        Wale wote walio katika kumbukumbu la Yehova watafufuliwa.

      • Matendo 24:15

        Waadilifu na wasio waadilifu watafufuliwa.

      • Isaya 40:26

        Yehova anaweza kukumbuka majina ya nyota zote, basi anaweza kukumbuka kila kitu kuhusu wale ambao atawafufua.

      UKWELI WA 4: WENGINE WANAFUFULIWA WAKAISHI MBINGUNI

      “Ninaenda zangu kuwatayarishia mahali.” —Yohana 14:2

      Ni nani wanaofufuliwa wakaishi mbinguni?

      • 1 Petro 3:18

        Yesu alikuwa mtu wa kwanza kufufuliwa kwenda kuishi mbinguni.

      • Luka 12:32

        Yesu alisema kwamba ni idadi ndogo tu ya wanafunzi wake ambao wangefufuliwa wakaishi mbinguni.

      • Ufunuo 14:1

        Yehova amechagua jumla ya watu 144,000 wakaishi mbinguni.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki