Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu
Kuhusu Sala Ambazo Mungu Anasikiliza
Mara nyingi Yesu alitafuta mahali pa faragha ili asali, na alipendekeza kwamba wafuasi wake wafanye vivyo hivyo. Biblia inasema: “Alipokuwa mahali fulani akisali, alipoacha, mmoja wa wanafunzi wake akamwambia: ‘Bwana, tufundishe jinsi ya kusali’ . . . Ndipo akawaambia: ‘Wakati wowote mnaposali, semeni, “Baba, jina lako na litakaswe.”’” (Luka 5:16; 11:1, 2) Hivyo, Yesu alionyesha kwamba sala zinapaswa kuelekezwa kwa Baba yake, Yehova. Yeye peke yake ndiye Muumba wetu na “Msikiaji wa sala.”—Zaburi 65:2.
Je, sala zote zinampendeza Mungu?
Sala zinazokaririwa hazimpendezi Mungu. Yesu alisema: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena.” (Mathayo 6:7) Tunapaswa kuzungumza kutoka moyoni na Baba yetu wa mbinguni. Wakati mmoja, Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba sala za mtenda-dhambi mmoja ambaye kwa unyoofu alitaka kubadilika, zilikubaliwa na Mungu lakini sala za mtu mwenye kiburi ambaye alishikilia sana mapokeo ya kidini hazikusikilizwa. (Luka 18:10-14) Hivyo, ili sala zetu zisikilizwe, tunapaswa kwa unyenyekevu kujitahidi kufanya mambo ambayo Mungu anatuambia. Hata Yesu alisema hivi: “Kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya . . . sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.” (Yohana 8:28, 29) Yesu alisali hivi: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.”—Luka 22:42.
Tunapaswa kusali kuhusu mambo gani?
Kwa kuwa jina la Mungu limechafuliwa, Yesu alisema: “Basi, ninyi msali hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.’” (Mathayo 6:9, 10) Tunapaswa kusali Ufalme wa Mungu uje kwa sababu hiyo ndiyo serikali ambayo Mungu atatumia kutimiza mapenzi yake mbinguni na duniani. Yesu alisema tunaweza kusali tupate “mkate wetu kwa ajili ya siku.” Pia, tunaweza kusali kwa Yehova kuhusu kupata kazi, nyumba, mavazi, mambo ya afya, na mahangaiko mengine. Kwa kuongezea, Yesu alisema tunapaswa kusali ili tusamehewe.—Luka 11:3, 4.
Je, tunapaswa kusali kwa ajili ya wengine?
Yesu alisali kwa ajili ya wengine. Biblia inatuambia hivi: “Ndipo akaletewa watoto wachanga, ili aweke mikono yake juu yao na kutoa sala.” (Mathayo 19:13) Yesu alimwambia hivi mtume Petro: “Nimeomba dua kwa ajili yako ili imani yako isififie.” (Luka 22:32) Yesu aliwatia moyo wafuasi wake wasali kwa ajili ya wengine, hata wale wanaowatesa na kuwatukana.—Mathayo 5:44; Luka 6:28.
Kwa nini tudumu katika sala?
Yesu alitenga wakati ili asali na aliwatia moyo wafuasi wake ‘wasali sikuzote bila kukata tamaa.’ (Luka 18:1) Yehova anatutia moyo tuonyeshe kwamba tunamtumaini kwa kumwambia mahangaiko yetu tena na tena. “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa,” akasema Yesu. Lakini hilo halimaanishi kwamba Yehova hataki kujibu sala za wale wanaompenda na kumheshimu kama Baba. Badala yake Yesu alisema: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!”—Luka 11:5-13.
Kwa habari zaidi, ona sura ya 17 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?a
[Maelezo ya chini]
a Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.