Uzima wa Milele Duniani—Tumaini Lililofunuliwa Tena
“Ee Danieli, yafanye siri maneno hayo . . . mpaka wakati wa mwisho. Wengi watakwenda huku na huku, na ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.”—DAN. 12:4.
1, 2. Tutachunguza maswali gani katika habari hii?
MAMILIONI ya watu leo wanaelewa wazi msingi wa Kimaandiko wa tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani. (Ufu. 7:9, 17) Mwanzoni mwa historia ya wanadamu, Mungu alifunua kwamba mwanadamu hakuumbwa ili aishi miaka michache tu kisha afe, bali aliumbwa aishi milele.—Mwa. 1:26-28.
2 Waisraeli walitumaini kwamba wanadamu watarudishiwa hali ya ukamilifu ambayo Adamu alipoteza. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanaeleza jinsi ambavyo Mungu atawawezesha wanadamu kuishi milele katika Paradiso duniani. Hivyo basi, kwa nini tumaini la wanadamu lilihitaji kufunuliwa tena? Lilifunuliwa jinsi gani na kutangazwa kwa mamilioni ya watu?
Tumaini Ambalo Lilikuwa Limefichwa
3. Kwa nini haishangazi kwamba tumaini la wanadamu la kuishi milele duniani lilifichwa?
3 Yesu alitabiri kwamba manabii wa uwongo wangepotosha mafundisho yake na kwamba watu wengi wangepotoshwa. (Mt. 24:11) Mtume Petro aliwaonya Wakristo hivi: ‘Pia kutakuwa na walimu wa uwongo katikati yenu.’ (2 Pet. 2:1) Mtume Paulo alisema kuhusu ‘kipindi cha wakati ambapo watu hawangevumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, wangejikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe.’ (2 Tim. 4:3, 4) Shetani anahusika katika kuwapotosha watu na ametumia Wakristo waasi-imani kuficha kweli zenye kuchangamsha moyo kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu na dunia.—Soma 2 Wakorintho 4:3, 4.
4. Viongozi wa kidini waasi-imani wamekataa tumaini gani la wanadamu?
4 Maandiko yanaeleza kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali iliyo mbinguni ambayo itaziponda na kuzikomesha serikali zote za wanadamu. (Dan. 2:44) Wakati wa utawala wa miaka elfu wa Kristo, Shetani atafungiwa ndani ya abiso, wafu watafufuliwa, na wanadamu watainuliwa na kuwa wakamilifu hapa duniani. (Ufu. 20:1-3, 6, 12; 21:1-4) Hata hivyo, viongozi waasi-imani wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wamekubali mawazo mengine. Kwa mfano, Origen wa Aleksandria, Baba wa Kanisa katika karne ya tatu aliwashutumu watu walioamini kwamba Utawala wa Miaka Elfu utaleta baraka duniani. Mwanatheolojia Mkatoliki Augustine wa Hippo (354-430 W.K.) “aliamini kwamba hakutakuwa na utawala wa miaka elfu,” kinasema kitabu kimoja (The Catholic Encyclopedia).a
5, 6. Kwa nini Origen na Augustine walipinga fundisho la utawala wa miaka elfu?
5 Kwa nini Origen na Augustine walipinga fundisho la utawala wa miaka elfu? Origen alikuwa mwanafunzi wa Clement wa Aleksandria, ambaye alikubali wazo la kutokufa kwa nafsi ambalo lilitegemea mapokeo ya Wagiriki. Origen alifuata sana mawazo ya Plato kuhusu nafsi hivi kwamba “akaingiza katika mafundisho ya Kikristo mawazo ya Plato kuhusu nafsi na mahali inapoenda,” anasema mwanatheolojia Werner Jaeger. Kwa hiyo, Origen alifundisha kwamba baraka zozote za Utawala wa Miaka Elfu hazingekuwa duniani bali zingekuwa katika makao ya roho.
6 Kabla ya kuwa “Mkristo” akiwa na umri wa miaka 33, Augustine alikuwa mfuasi wa falsafa mpya za Plato ambazo zilianzishwa na Plotinus katika karne ya tatu. Baada ya Augustine kuwa Mkristo, aliendelea kufuata falsafa hizo mpya za Plato. Kitabu kimoja (The New Encyclopædia Britannica) kinasema hivi kumhusu Augustine: “Alitimiza fungu kubwa sana katika kuchanganya kabisa mafundisho ya Agano Jipya na mafundisho ya Plato ya falsafa za Kigiriki.” Kitabu kingine (The Catholic Encyclopedia) kinasema kuwa Augustine alieleza kwamba Utawala wa Miaka Elfu unaotajwa katika kitabu cha Ufunuo sura ya 20 ulikuwa wa “mfano” tu. Kinaongezea hivi: “Maelezo hayo . . . yalikubaliwa na wanatheolojia wa nchi za Magharibi walioishi baadaye, na fundisho la mwanzoni la utawala wa miaka elfu halikuungwa mkono tena.”
7. Ni imani gani ya uwongo iliyoficha tumaini la wanadamu la kuishi milele duniani, na ililificha jinsi gani?
7 Tumaini la wanadamu la kuishi milele duniani lilifichwa na wazo ambalo lilifundishwa katika Babiloni la kale na kuenea ulimwenguni pote, wazo la kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa au roho inayokaa tu katika mwili wa mwanadamu. Dini zinazodai kuwa za Kikristo zilipokubali wazo hilo, wanatheolojia walipotosha Maandiko ili kufanya mistari inayozungumzia tumaini la mbinguni ionekane kwamba inafundisha kuwa watu wote wazuri wanaenda mbinguni. Kulingana na maoni hayo, maisha ya mtu duniani yamekusudiwa kuwa mafupi tu, yaani, anajaribiwa ili kuona ikiwa anastahili kuishi mbinguni. Jambo fulani kama hilo lilitukia kuhusiana na tumaini la mwanzoni la Wayahudi la kuishi milele duniani. Wayahudi walipokubali hatua kwa hatua wazo la Wagiriki la kwamba nafsi haiwezi kufa, tumaini lao la hapo mwanzoni la kuishi duniani lilitoweka. Wazo hilo ni tofauti kabisa na fundisho la Biblia kuhusu mwanadamu! Mwanadamu ni kiumbe aliye na mwili wa nyama, wala si kiumbe wa roho. Yehova alimwambia mwanadamu wa kwanza hivi: “Wewe ni mavumbi.” (Mwa. 3:19) Dunia ndiyo makao ya milele ya mwanadamu, bali si mbingu.—Soma Zaburi 104:5; 115:16.
Kweli Inaangaza Gizani
8. Wasomi fulani katika miaka ya 1600 walisema nini kuhusu tumaini la wanadamu?
8 Ingawa dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo zinakataa tumaini la kuishi milele duniani, sikuzote Shetani hakufaulu kuficha ukweli. Tangu zamani, wasomaji wachache waangalifu wa Biblia waliona nuru ya kweli ikiangaza walipoendelea kuelewa mambo fulani yanayoonyesha jinsi Mungu atakavyowarudisha wanadamu kwenye ukamilifu. (Zab. 97:11; Mt. 7:13, 14; 13:37-39) Kufikia miaka ya 1600, kazi ya kutafsiri na kuchapisha Biblia iliwawezesha watu wengi kupata Maandiko Matakatifu. Mwaka wa 1651, msomi mmoja aliandika kwamba kwa kuwa kupitia Adamu watu “wamepoteza Paradiso, na Uzima wa Milele Duniani,” hivyo katika Kristo, “watu wote watawezeshwa kuishi Duniani; ikiwa sivyo, ulinganifu huo haufai.” (Soma 1 Wakorintho 15:21, 22.) Mmoja wa watungaji maarufu wa mashairi katika nchi zinazozungumza Kiingereza ulimwenguni, John Milton (1608-1674), aliandika shairi lenye kichwa Paradiso Iliyopotea na la pili Paradiso Iliyopatikana. Katika mashairi hayo, Milton alitaja thawabu ambayo waaminifu watapata katika paradiso duniani. Ingawa Milton alitumia wakati mwingi wa maisha yake kujifunza Biblia, alitambua kwamba kweli ya Kimaandiko haingeeleweka kikamili mpaka wakati wa kuwapo kwa Kristo.
9, 10. Isaac Newton aliandika nini kuhusu tumaini la wanadamu? (b) Kwa nini Newton aliona kwamba wakati wa kuwapo kwa Kristo ulikuwa mbali sana?
9 Pia, mtaalamu mashuhuri wa hesabu Sir Isaac Newton (1642-1727) alipendezwa sana na Biblia. Alielewa kwamba watakatifu watafufuliwa na kuishi mbinguni nao watatawala bila kuonekana pamoja na Kristo. (Ufu. 5:9, 10) Aliandika hivi kuhusu raia wa Ufalme huo: “Dunia itaendelea kukaliwa na wanadamu wanaoweza kufa baada ya siku ya hukumu na si kwa miaka 1000 tu bali hata kwa umilele wote.”
10 Newton alikuwa na maoni ya kwamba kuwapo kwa Kristo kungetukia karne nyingi baadaye. Mwanahistoria Stephen Snobelen alisema hivi: “Sababu moja iliyomfanya Newton aseme kwamba Ufalme wa Mungu ungekuja baada ya muda mrefu ni kwamba alitilia shaka sana fundisho la uasi-imani la Utatu ambalo lilikuwa limeenea sana.” Habari njema ilikuwa bado imefichwa. Na Newton hakuona kikundi chochote cha Kikristo ambacho kingeweza kuhubiri habari hiyo njema. Aliandika hivi: “Unabii huu wa Danieli na wa Yohana [ambao unapatikana katika kitabu cha Ufunuo] hautaeleweka mpaka wakati wa mwisho.” Newton alieleza hivi: “‘Kisha,’ Danieli akasema, ‘wengi watakimbia huku na huku, na ujuzi utaongezeka.’ Ni lazima Injili ihubiriwe katika mataifa yote kabla ya ile dhiki kuu na mwisho wa ulimwengu. Umati mkubwa unaobeba matawi ya mitende mikononi, ambao unatoka katika hiyo dhiki kuu, hauwezi kuwa na watu wengi wasiohesabika kutoka katika mataifa yote, isipokuwa Injili ihubiriwe kabla ya dhiki hiyo kufika.”—Dan. 12:4; Mt. 24:14; Ufu. 7:9, 10.
11. Kwa nini tumaini la wanadamu liliendelea kufichwa kwa watu wengi katika siku za Milton na Newton?
11 Katika siku za Milton na Newton, ilikuwa hatari kupinga mafundisho rasmi ya kanisa. Kwa hiyo, maandishi mengi kuhusu utafiti wao wa Biblia hayakuchapishwa mpaka baada ya kifo chao. Marekebisho ya Kidini ya karne ya 16 yalishindwa kurekebisha fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa, na makanisa makubwa ya Kiprotestanti yaliendelea kufundisha wazo la Augustine la kwamba Utawala wa Miaka Elfu ulikuwa umepita, na haungekuja wakati ujao. Je, ujuzi umeongezeka wakati huu wa mwisho?
“Ujuzi wa Kweli Utakuwa Mwingi”
12. Ujuzi wa kweli ungekuwa mwingi wakati gani?
12 Danieli alitabiri kwamba jambo zuri sana lingetukia katika “wakati wa mwisho.” (Soma Danieli 12:3, 4, 9, 10.) Yesu alisema: “Wakati huo waadilifu watang’aa kwa uangavu kama jua.” (Mt. 13:43) Ujuzi wa kweli ulikuwa mwingi jinsi gani katika wakati wa mwisho? Chunguza matukio fulani ya kihistoria katika makumi ya miaka kabla ya mwaka wa 1914, mwaka ambao wakati wa mwisho ulianza.
13. Charles Taze Russell aliandika nini baada ya kuchunguza kuhusu kurudishwa kwa wanadamu kwenye ukamilifu?
13 Katika miaka ya mwisho ya 1800, watu wachache wanyoofu walikuwa wakijitahidi kuelewa “kielelezo cha maneno yenye afya.” (2 Tim. 1:13) Mmoja wa watu hao alikuwa Charles Taze Russell. Katika mwaka wa 1870, yeye na watu wengine wachache waliokuwa wakitafuta kweli walianzisha kikundi cha kujifunza Biblia. Katika mwaka wa 1872, walichunguza kuhusu kurudishwa kwa wanadamu kwenye ukamilifu. Baadaye, Russell aliandika: “Kufikia wakati huo, hatukuwa tumeona wazi tofauti kubwa kati ya thawabu ya kanisa ambalo linajaribiwa sasa na thawabu ya wanadamu wote waaminifu.” Wanadamu waaminifu “watarudishwa katika hali ya ukamilifu ambayo pindi moja babu yao na kichwa, Adamu, alifurahia katika Edeni.” Russell alikiri kwamba watu wengine walimsaidia kujifunza Biblia. Ni nani hao?
14. (a) Henry Dunn alielewa jinsi gani andiko la Matendo 3:21? (b) Dunn alisema ni nani watakaoishi milele duniani?
14 Mmoja wao alikuwa Henry Dunn. Alikuwa ameandika kuhusu “kurudishwa kwa mambo yote ambayo Mungu alisema kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu wa nyakati za kale.” (Mdo. 3:21) Dunn alijua kwamba kurudishwa huko kulitia ndani kuinuliwa kwa wanadamu kwenye ukamilifu duniani wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Pia, Dunn alichunguza swali ambalo liliwatatanisha wengi, Ni nani watakaoishi milele duniani? Alieleza kwamba mamilioni ya watu watafufuliwa, wafundishwe kweli, kisha wapewe nafasi ya kuonyesha imani katika Kristo.
15. George Storrs alielewa nini kuhusu ufufuo?
15 Mwaka wa 1870, George Storrs alikata kauli pia kwamba watu wasio waadilifu watafufuliwa na kupewa nafasi ya kuishi milele. Pia, alielewa kutokana na Maandiko kwamba mtu atakayefufuliwa ambaye hatatumia vizuri nafasi hiyo “atakufa, hata ingawa ‘mtenda-dhambi huyo atakuwa na umri wa miaka mia moja.’” (Isa. 65:20) Storrs aliishi Brooklyn, New York, na alikuwa mhariri wa gazeti lililoitwa Bible Examiner.
16. Ni nini kilichowatofautisha Wanafunzi wa Biblia na dini zinazodai kuwa za Kikristo?
16 Russell alitambua kutokana na Biblia kwamba wakati ulikuwa umefika wa kutangaza habari njema ulimwenguni pote. Hivyo, katika mwaka wa 1879, alianza kuchapisha gazeti Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence, sasa linaitwa Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Kabla ya hapo, ni watu wachache sana walioelewa ukweli kuhusu tumaini la wanadamu, lakini sasa vikundi vya Wanafunzi wa Biblia katika nchi nyingi vilikuwa vikipokea na kujifunza gazeti la Mnara wa Mlinzi. Imani ya kwamba ni watu wachache tu ndio wanaoenda mbinguni, huku mamilioni ya watu wakipewa uhai mkamilifu wa kibinadamu duniani, iliwafanya Wanafunzi wa Biblia wawe tofauti kabisa na dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo.
17. Ujuzi wa kweli uliongezeka sana jinsi gani?
17 “Wakati wa mwisho” uliotabiriwa ulianza mwaka wa 1914. Je, ujuzi wa kweli kuhusu tumaini la wanadamu uliongezeka sana? (Dan. 12:4) Kufikia mwaka wa 1913, hotuba za Russell zilichapishwa katika magazeti 2,000 yaliyosomwa na jumla ya wasomaji milioni 15. Kufikia mwisho wa mwaka wa 1914, watu zaidi ya milioni 9 katika mabara matatu walikuwa wameona sinema ya picha na slaidi ya “Photo-Drama of Creation” (Photo-Drame de la Création) ambayo ilieleza kuhusu Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Kuanzia mwaka wa 1918 mpaka 1925, hotuba yenye kichwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe,” ambayo ilieleza kuhusu tumaini la uzima wa milele duniani, ilitolewa na watumishi wa Yehova katika lugha zaidi ya 30 ulimwenguni pote. Kufikia mwaka wa 1934, Mashahidi wa Yehova walitambua kwamba wale wanaotumaini kuishi milele duniani walipaswa kubatizwa. Uelewaji huo uliwachochea kuwa na bidii zaidi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Leo, mamilioni ya watu wanamshukuru sana Yehova kutoka moyoni kwa sababu ya tumaini la kuishi milele duniani.
“Uhuru Wenye Utukufu” Uko Mbele!
18, 19. Ni maisha ya aina gani yanayotabiriwa kwenye Isaya 65:21-25?
18 Nabii Isaya aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kuhusu maisha ambayo watu wa Mungu watafurahia duniani. (Soma Isaya 65:21-25.) Kwa kweli, miti fulani ambayo ilikuwepo miaka 2,700 hivi iliyopita Isaya alipoandika maneno hayo bado ipo leo. Je, unaweza kujiwazia ukiishi kwa muda mrefu hivyo ukiwa na nguvu na afya nzuri?
19 Badala ya wanadamu kuishi kwa muda mfupi na kisha kufa, watakuwa na nafasi nyingi za kujenga, kupanda, na kujifunza. Fikiria nafasi utakazokuwa nazo za kupata marafiki wengi. Mahusiano hayo yenye upendo yatadumu milele. “Watoto wa Mungu” watafurahia “uhuru wenye utukufu” kama nini duniani!—Rom. 8:21.
[Maelezo ya chini]
a Augustine alidai kwamba Utawala wa Miaka Elfu wa Ufalme wa Mungu haukuwa wa wakati ujao bali ulianza wakati kanisa lilipoanzishwa.
Je, Unaweza Kueleza?
• Tumaini la wanadamu la kuishi milele duniani lilifichwa jinsi gani?
• Wasomaji fulani wa Biblia walielewa nini katika miaka ya 1600?
• Mwaka wa 1914 ulipokuwa ukikaribia tumaini la kweli la wanadamu lilieleweka wazi zaidi jinsi gani?
• Ujuzi kuhusu tumaini la kuishi duniani umekuwa mwingi jinsi gani?
[Picha katika ukurasa wa 13]
Mtungaji wa mashairi John Milton (kushoto) na mtaalamu wa hesabu Isaac Newton (kulia) walijua kuhusu tumaini la kuishi milele duniani
[Picha katika ukurasa wa 15]
Wanafunzi wa Biblia wa mapema walielewa kutokana na Maandiko kwamba wakati ulikuwa umefika wa kutangaza ulimwenguni pote tumaini la kweli la wanadamu