Jihadhari Usidanganywe
DON QUIXOTE ni mtu wa kuwaziwa tu anayejulikana sana katika hadithi iliyotungwa na mwandishi wa karne ya 16, Miguel de Cervantes katika kitabu chake kinachoitwa Don Quixote. Katika kitabu hicho, mtu huyo wa kubuniwa Don Quixote anasoma vitabu vya hadithi na hekaya kuhusu mashujaa waliovaa mavazi ya kivita yanayong’aa, wakiwaokoa wanawake fulani waliopatwa na shida na waliohitaji msaada. Baada ya muda anaanza kuamini kwamba yeye pia ni shujaa. Katika simulizi fulani maarufu, anavishambulia vinu vya upepo ambavyo anadhani ni majitu hatari. Akiwa amesadiki akilini mwake kwamba kwa kuua majitu hayo anafanya mapenzi ya Mungu, anaishia kuaibika sana.
Bila shaka, Don Quixote, ni mtu wa kubuniwa tu, hata hivyo, kudanganywa si jambo la mzaha. Kwa mfano, fikiria mtu anayekunywa kupita kiasi ambaye anaamini kwamba anaweza kunywa kadiri apendavyo, lakini mwishowe anahatarisha afya yake na kuharibu maisha ya familia yake. Au fikiria hali yenye kusikitisha ya mwanamke aliye na tatizo la kujinyima chakula ambaye anafikiri anapata lishe bora na ana afya nzuri, lakini kwa kweli hapati chakula cha kutosha na anajiua polepole.
Je, yeyote kati yetu anaweza kudanganywa? Kwa kusikitisha, jibu ni ndiyo. Kusema kweli, sote tunaweza kudanganywa. Hilo linatia ndani uwezekano wa kudanganywa kuhusu mafundisho ya kidini tunayoyapenda sana—jambo linaloweza kusababisha msiba mbaya sana. Kwa nini? Unaweza kujihadhari au kujilinda jinsi gani ili usidanganywe?
Hatari za Kudanganywa
Kamusi fulani inasema neno danganya linamaanisha, “kumfanya mtu aamini jambo lisilo la kweli kuwa ni la kweli.” Neno hilo pia linatoa wazo la “kumfanya mtu awe na mawazo au aamini mambo yasiyo ya kweli ambayo yanasababisha hali ya kuvurugika, kuchanganyikiwa, au kutojua jambo.” Maana ya msingi ya neno hilo, na maneno mengine kama vile “potosha” na “laghai,” ni kumwongoza mtu vibaya kwa kutumia ujanja. Bila shaka, mtu ambaye hana habari kwamba amewekwa katika hali ya “kutojua, kutatanika, au kuchanganyikiwa” kwa sababu ya kutoambiwa habari za kweli kimakusudi, yuko katika hatari kubwa.
Jambo lenye kusikitisha hasa kuhusu hali hiyo ni kwamba mara nyingi mtu ambaye amedanganywa au kulaghaiwa huamua kushikilia mafundisho ya kidini ijapokuwa anaonyesha waziwazi kwamba mafundisho hayo si ya kweli. Huenda akashikamana sana na mafundisho hayo hivi kwamba akaamua kufumba macho na masikio yake kuelekea uthibitisho wowote unaofichua kwamba mafundisho hayo ni ya uwongo.
Je, Tuko Katika Hatari ya Kudanganywa?
Huenda ukauliza, ‘Je, haitakuwa ni kutia chumvi kusema kwamba sote tuko katika hatari ya kudanganywa kuhusu mafundisho ya kidini tunayoamini?’ Bila shaka, hapana. Hilo ni kwa sababu Shetani Ibilisi, ambaye Yesu alimwita “baba ya uwongo,” amekusudia kutudanganya na kutulaghai sote. (Yohana 8:44) Pia, Biblia inaeleza kuwa Shetani ni “mungu wa mfumo huu wa mambo.” Yeye “amezipofusha akili” za mamilioni ya watu kwa miaka mingi. (2 Wakorintho 4:4) Hata sasa, ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’—Ufunuo 12:9.
Shetani alianza kuwadanganya wanadamu tangu mwanzo wa historia ya mwanadamu. Kwa mfano, alimdanganya Hawa aamini kwamba haikuwa lazima atii sheria za Muumba wake na kwamba ‘atakuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya,’ yaani, akijiamulia mwenyewe lililo jema na lililo baya. (Mwanzo 3:1-5) Huo ulikuwa uwongo wa kwanza, kwa kuwa hata ingawa wanadamu walipewa uhuru wa kuchagua kile watakachofanya, hawakuumbwa wakiwa na mamlaka ya kujiamulia lililo jema na lililo baya. Mungu peke yake akiwa Muumba na Mwenye Enzi Kuu, ndiye mwenye haki na mamlaka hiyo. (Yeremia 10:23; Ufunuo 4:11) Huo ulikuwa udanganyifu mkubwa kama nini kuamini kwamba haki ya kuchagua jema na baya ni sawa na mamlaka ya kuamua kati ya lililo jema na lililo baya! Inasikitisha kwamba sisi wanadamu tusiokamilika tunanaswa kwa urahisi na mtego huo.
Je, Unaweza Kudanganywa?
Huenda mafundisho fulani ya kidini unayoamini yamekuwapo kwa miaka mingi, na labda yamekuwa yakipitishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba mafundisho hayo ni ya kweli. Kwa nini? Masimulizi ya Biblia yanaonyesha kwamba baada ya kufa kwa mitume wa Kristo, watu wadanganyifu wangetokea katika kutaniko la Kikristo na kufundisha “mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Matendo 20:29, 30) Kwa ujanja wa hali ya juu waliwapotosha watu “kwa hoja zenye kushawishi” na vilevile “kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu.”—Wakolosai 2:4, 8.
Je, mambo yako tofauti leo? Bila shaka, hapana, kwa kuwa mtume Paulo alionya kwamba mambo yatakuwa mabaya hata zaidi katika “siku za mwisho,” wakati tunaoishi sasa. Aliandika: “Watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, wakipotosha na kupotoshwa [au, “wakidanganya na kudanganyika,” Union Version].”—2 Timotheo 3:1, 13.
Hivyo, ni jambo la busara kuzingatia kwa makini onyo lililotolewa na mtume Paulo: “Kwa hiyo yeye anayefikiri kuwa amesimama na ajihadhari kwamba asianguke.” (1 Wakorintho 10:12) Bila shaka, Paulo alikuwa akizungumza kuhusu msimamo wa mtu mbele za Mungu. Kwa kweli, kufikiri kwamba Shetani hawezi kukudanganya ni kujidanganya sana. Hakuna mtu yeyote ambaye hawezi kupotoshwa na “hila” za Shetani. (Waefeso 6:11) Ndio maana mtume Paulo alielezea hofu yake kuelekea Wakristo wenzake kwamba “kwa njia fulani, kama nyoka alivyomshawishi Hawa kwa ujanja wake, huenda akili [zao] zikaharibiwa kutoka kwenye unyoofu wa moyo na usafi wa kiadili ambao unamfaa Kristo.”—2 Wakorintho 11:3.
Unaweza Kujilinda Jinsi Gani Usidanganywe?
Hivyo basi, unaweza kujilinda jinsi gani usidanganywe na Shetani? Unaweza kuhakikisha jinsi gani kwamba ‘unamwabudu Mungu kwa roho na kweli’? (Yohana 4:24) Tumia kile ambacho Yehova Mungu amekupa. Kwanza kabisa amekupa “uwezo wa akili” ili uweze kutofautisha uwongo na ukweli. (1 Yohana 5:20) Pia, amekuwezesha kutambua mbinu za Shetani. (2 Wakorintho 2:11) Kwa kweli, amekupa kila kitu unachohitaji ili kupinga jitihada za Shetani za kukupotosha.—Methali 3:1-6; Waefeso 6:10-18.
Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba Mungu ametuandalia njia hakika ambayo tunaweza kuitumia ili kujilinda. Ni njia gani hiyo? Ni ileile ambayo mtume Paulo alimtia moyo mwandamani wake Timotheo aitegemee kuhusiana na imani ya kidini. Baada ya kutoa onyo kuhusu “watu waovu na wajanja,” mtume Paulo alimwambia Timotheo awapinge kwa kutegemeza kila kitu alichoamini kwa “maandishi matakatifu” yaani, katika Neno takatifu la Mungu, Biblia.—2 Timotheo 3:15.
Bila shaka, huenda wengine wakasema kwamba mtu yeyote anayeamini kwamba kuna Mungu na kuikubali Biblia kuwa Neno Lake lililoongozwa na roho yake amepotoshwa. Hata hivyo, ukweli ni kwamba watu ambao wamepotoshwa ni wale wanaokataa uthibitisho ulio wazi kwamba kuna Muumba na uthibitisho unaounga mkono madai ya Biblia kwamba ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake.a—Waroma 1:18-25; 2 Timotheo 3:16, 17; 2 Petro 1:19-21.
Badala ya kudanganywa na ule “unaoitwa kwa uwongo ‘ujuzi,’” tumia Neno la Mungu kuthibitisha ukweli. (1 Timotheo 6:20, 21) Uwe kama wanaume na wanawake wasikivu ambao mtume Paulo aliwahubiria huko Beroya. “Walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili.” Hawakuamini tu yale aliyofundisha mtume Paulo, lakini ‘waliyachunguza pia Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.’—Matendo 17:11.
Usihofu chochote unapochunguza kwa njia hiyo mambo unayoamini. Kwa kweli, Biblia inakutia moyo ‘kuhakikisha mambo yote’ kabla ya kuyakubali kuwa kweli. (1 Wathesalonike 5:21) Kuelekea mwisho wa karne ya kwanza, mtume Yohana aliwahimiza Wakristo wenzake hivi: “Wapendwa, msiamini kila neno lililoongozwa na roho, lakini yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu.” (1 Yohana 4:1) Ndiyo, hata ingawa mafundisho fulani ya dini yanaonekana kuwa ‘yameongozwa na roho’—au yametoka kwa Mungu—ni jambo la hekima kuyachunguza Maandiko kabla ya kukubali mafundisho hayo kuwa ya kweli.—Yohana 8:31, 32.
Tenda Kupatana na Mambo Unayojifunza
Kuna jambo lingine ambalo unahitaji kufanya. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Iweni watendaji wa neno, na si wasikiaji tu, mkijidanganya wenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli.” (Yakobo 1:22) Haitoshi tu kujua yale ambayo Biblia inafundisha. Unapaswa kutenda kupatana na mambo unayojifunza. Jinsi gani? Kwa kufanya yale ambayo Mungu anakuamuru ufanye na kutofanya mambo anayokataza.
Kwa mfano, ona ukosefu wa maadili uliopo leo. Je, hilo halionyeshi jinsi ambavyo Shetani amekuwa akiwalaghai watu wafikiri kwamba wanaweza kupuuza viwango vya Mungu vya maadili bila kupatwa na matokeo yoyote mabaya? Kwa sababu hiyo, mtume Paulo aliwapa Wakristo onyo hili la wazi: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.”—Wagalatia 6:7.
Usiwe kama “mtu mpumbavu” ambaye Yesu alimtaja kuwa ‘anayeyasikia’ maneno yake lakini “hayatendi.” Kama vile Don Quixote ambaye alidanganywa na mawazo yake mwenyewe, mtu huyo alidanganyika kwa sababu alifikiri kwamba anaweza kujenga nyumba imara na salama juu ya msingi wa mchanga. Badala yake, uwe kama yule mtu “aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba.” Yesu alisema mtu huyo ni “mwenye busara” kwa sababu anasikiliza maneno ya Yesu “na kuyatenda.”—Mathayo 7:24-27.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa maelezo zaidi ona vitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? na Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12, 13]
Je, Unaona Mambo Jinsi Yalivyo Kikweli?
Katika miaka ya 1930, mchoraji kutoka Sweden Oscar Reutersvärd, alichora na kuionyesha hadharani michoro ambayo inafanya macho yasione kitu jinsi kilivyo. Mfano wa kisasa wa michoro kama hiyo unaonyeshwa upande wa kushoto. Unapoutazama kijuujuu tu, mchoro huo unadanganya macho na hivyo kuonekana tofauti na jinsi ulivyo kikweli. Lakini, unapouchunguza kwa uangalifu, utaona kwamba mchoro huo ni kazi ya ujanja ya kisanii inayokusudiwa kuchanganya macho na akili ya mtazamaji.
Pamoja na michoro hiyo, kuna mambo mengine ambayo yanaonekana tofauti na jinsi yalivyo kihalisi. Miaka elfu mbili hivi iliyopita, Biblia ilionya hivi: “Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.”—Wakolosai 2:8.
Kinachofanya onyo hilo liwe na uzito zaidi ni kwamba mwandishi wa onyo hilo mwenyewe aliwahi kudanganywa. Kwa kuwa alielimishwa miguuni pa mmoja wa walimu wa kidini aliyejulikana sana wakati huo na alijuana na watu wenye mamlaka ya juu, huenda ukafikiri kwamba haingekuwa rahisi kwa mtu kama huyo kudanganywa.—Matendo 22:3.
Mtu huyo—Sauli wa Tarso—alikuwa amefundishwa aamini kwamba mtu yeyote ambaye hakufuata mapokeo na desturi za dini ya Kiyahudi alikuwa amelaaniwa. Viongozi wa dini ya Kiyahudi walimpa mamlaka iliyomfanya aone kuwa ana daraka kutoka kwa Mungu la kumkamata yeyote ambaye alikataa kukana imani yake ya Kikristo. Hata aliunga mkono mauaji ya Myahudi mwenzake ambaye alishtakiwa kimakosa kwamba amekufuru.—Matendo 22:4, 5, 20.
Baadaye, Sauli alisaidiwa kuona tofauti kati ya jema na baya, na yale ambayo Mungu anakubali na anayokataa. Mara tu Sauli alipogundua kwamba mambo aliyokuwa akifanya yalikuwa si sawa, mwanamume huyo mwenye bidii alibadili njia zake na akaja kujulikana kama Paulo, mtume wa Yesu Kristo. Paulo aliipata njia sahihi ya kuabudu na hakudanganywa tena.—Matendo 22:6-16; Waroma 1:1.
Kama Paulo, watu wengi wanyofu walidanganywa wakati fulani kwa mafundisho ya uwongo ambayo yanaweza kulinganishwa na ile michoro inayodanganya macho, yaani, mafundisho yanayoweza kuonekana kuwa ya kweli lakini hayategemei Neno la Mungu. (Methali 14:12; Waroma 10:2, 3) Kisha, walisaidiwa kuona jinsi mafundisho na matunda ya dini zao yalivyo hasa. (Mathayo 7:15-20) Hivyo, kadiri walivyoendelea kupata ujuzi sahihi wa Biblia, ndivyo walivyofanya mabadiliko katika mambo waliyoamini na mienendo yao ili wakubaliwe na Mungu.
Je, uko tayari kufuata mfano wa mtume Paulo na kuchunguza yale unayoamini ukitumia Neno la Mungu, Biblia? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Engravings by Doré