Vijana—Msidanganywe
“Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru.”—2 WAKORINTHO 11:14.
1. (a) Ni kwa njia gani wengi wetu tumedanganywa? (b) Kwa ujumla ni nani walio rahisi zaidi kudanganywa?
BILA shaka sisi sote tumedanganywa wakati fulani. Labda ulikuwa ukicheza mchezo fulani na mchezaji wa upande ule mwingine akakupiga chenga iliyokudanganya ukaacha mahali pako na hivyo yeye akaingiza bao na kushinda mchezo. Au huenda ikawa ulinunua vazi fulani lenye kuonekana kuwa zuri, kumbe baada ya kulivaa kwa muda mfupi na kulifua unakuta kwamba halina ubora ule lililoonekana kuwa nao. Kwa ujumla, ni akina nani wanaodanganywa kwa urahisi zaidi, yaani, kupumbazwa au kutiwa kiini-macho? Je! si wale walio na ujuzi mchache zaidi? Na mara nyingi matokeo yanakuwa mazito zaidi ya kushindwa tu katika mchezo fulani au kupunjwa juu ya kitu fulani kilichonunuliwa.
2. Vijana wengine wameingizwaje katika makosa mazito?
2 Kwa mfano, Julie, alikuwa angali mpya-mpya katika shule ya sekondari wakati, kama yeye anavyosema: ‘Alipopendana’ na “jamaa aliye na sura nzuri zaidi na sifa nyingi katika shule yote.” Anaeleza: “Mimi nikamwambia sikuwa na nia ya kufanya alilotaka, lakini yeye akaendelea kuniambia alivyonipenda sana, na kwamba hakungetokea ubaya wo wote. Bado nilipokataa, hapo ndipo aliponguruma. Akasema, ‘Hakika mimi nilikuwa nikikujali sana, na nilifikiri hata wewe ulinijali. Kama hutanihakikishia kwamba unanijali, inaonekana ni afadhali tuache kuonana.’ ” Kwa hiyo Julie akajiachilia na kufanya uasherati. Siku ya pili yake, alipogundua kwamba mvulana yule alikuwa amejigamba juu ya “ushindi” wake, Julie akatambua jinsi alivyokuwa amedanganywa kabisa. Ingalimpasa kujua kwamba kama kweli mvulana yule alimpenda asingalimtenda hivyo.
3. (a) Kwa sababu gani uasherati ni kosa zito sana? (b) Shabaha ya Shetani Ibilisi ni nini?
3 Kitendo ambacho Julie alipumbazwa au akatiwa kiini-macho ili akitende kilikuwa uvunjaji mzito wa sheria ya Mungu. Kwa sababu hiyo Biblia inahimiza hivi: “Ukimbieni uasherati.” Tena inasema hivi waziwazi: “Hakuna mwasherati . . . aliye na urithi wo wote katika ufalme wa Kristo na wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:18; Waefeso 5:5, NW ) Kwa hiyo ingawa Shetani Ibilisi anaweza kuwa hajali kama wewe unashinda au unashindwa katika mchezo wa mpira unatumia au hutumii hekima katika kununua kitu, hakika yeye anajaribu kukudanganya uvunje sheria ya Mungu. “Mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze,” Biblia inaonya. (1 Petro 5:8) Kwa kweli, yeye anatumia fikira zake zote za werevu, pamoja na kukaa kama kwamba ni malaika wa nuru, ili atuondoe katika kumtumikia Yehova Mungu! Je, hilo si wazo la kufanya mtu afikiri sana?—2 Wakorintho 11:14.
Jifunze Kutokana na Yaliopata Hawa
4. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba vijana ni lengo la pekee la Shetani?
4 Lakini kwenu ninyi vijana hili ni wazo lililo la kufikiria kwa uzito hata zaidi: Ninyi ni lengo la pekee la Shetani. Kwa sababu gani? Kwa sababu ya ujana wenu, ninyi mumekuwa na wakati mchache zaidi wa kujipatia maarifa na hekima, na Shetani anachagua wale wasio na ujuzi mwingi. Hivyo ndivyo yeye alivyofanya tangu pale pale mwanzoni pa uasi wake. Kumbuka kwamba yeye alimkaribia Hawa katika bustani ya Edeni, wala si Adamu mume wake aliyekuwa ameumbwa muda fulani kabla ya Hawa. Na Shetani alifanikiwa. Alidanganya, ndiyo, akapoteza Hawa mwenye ujuzi mchache zaidi na mchanga zaidi kwa, kutumia visingizio. “Kwa maana Adamu ndiye aliyeumbwa kwanza,” Biblia inaeleza, “na Hawa baadaye. Wala Adamu hakudanganywa, ila mwanamke alidanganywa kabisa akaingia katika hali ya kukosa.”—1 Timotheo 2:13, 14.
5. (a) Haitupasi kamwe tutiwe katika usingizi wa kufikiri nini? (b) Hangaiko la mtume Paulo lilikuwa nini, na kwa sababu gani lilifaa?
5 Usitiwe kamwe katika usingizi au kufikiria kwamba njia za Shetani haziwezi kuwa na matokeo juu yako, kwamba yeye hawezi kamwe kukufanya wewe uvunje sheria za Mungu. Kumbuka onyo la kimungu kwamba “Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:14) Mtume Paulo kwa kufaa alihangaika juu ya uwezekano wa kwamba yule Fundi wa Udanganyifu angeweza kufanikiwa katika njia zake za kuwafikia Wakristo wenzi wa Paulo wasio na ujuzi mwingi. Paulo aliandika: “Mimi naogopa kwamba kwa njia fulani, kama vile yule nyoka alivyotongoza Hawa kwa ujanja wake, huenda akili zenu zikapotoshwa kutoka kwenye weupe wa moyo na usafi unaomstahili Kristo.”—2 Wakorintho 11:3 NW.
6. Maana yake nini kutongozwa?
6 Angalia kwamba Hawa hakudanganywa tu au kutiwa kiini-macho tu; yeye alitongozwa pia. Hiyo inamaanisha alivutwa akaingizwa katika mwendo wenye msiba kwa kishawishi au jaribu lenye kumvuta kando. Kulingana na kamusi Webster’s Third New International Dictionary, kutongoza kunamaanisha “kubembeleza na kuingiza katika hali ya kutokutii,” “kuvutia kitu au kukipata kwa kutumia au kufanya kama kwamba unatumia nguvu za kupendeza kwa ujanja.” Kwa kutaja waziwazi, kamusi hiyo inasema, kutongoza maana yake ni “kubembeleza (mwanamke) ili kufanya ngono kwa mara ya kwanza.” Tunaweza kufaidika kwa kurudia kujikumbusha njia ambayo Shetani alitumia kutongoza Hawa (ingawa ngono haikuhusika katika kisa hiki), na pia kwa kuona njia zinazofanana na hiyo ambazo anatumia leo.
7, 8. (a) Ni nini lililokuwa kusudi la ulizo ambalo Shetani alimwuliza Hawa? (b) Shetani alifanyaje kula kutokana na mti ule kukaonekana kuwa jambo la kuvutia sana?
7 Pale pale mwanzoni mwa kutumia njia yake, Shetani, alitumia nyoka kwa ujanja kumfanya Hawa aanze kutia shaka juu ya sheria ya Mungu. Kwa maneno yaliyotungwa kwa uangalifu ili kuamsha shuku na kutosadiki, yeye aliuliza: “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani? ” Kwa ulizo hilo lenye kudokeza mashaka, Shetani alikuwa akimaanisha kwamba lilikuwa jambo la kusikitisha kwamba mwanamke huyo hangeweza kula kutokana na miti yote ya bustani. Kwa kweli, yeye alibisha kwamba, mwanamke huyo angefaidika kweli kweli kwa kula kutokana na mti uliokatazwa badala ya kufa kama vile Mungu alivyokuwa amesema. “Kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo,” Shetani akamhakikishia mwanamke, “mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”—Mwanzo 3:1-5
8 Hapo Shetani alitumia ujanja mbovu sana kudokeza kwamba Mungu alikuwa akijaribu kumficha Hawa maarifa yenye faida! Kulingana na Shetani, Mungu hata alikuwa akitumia tisho la bure tu kuhusu kifo ili amzuie kutumia uwezo wa kujiamulia mambo. ‘Hei, unakosa faida fulani! ’ akawa ni kama anamwambia Hawa hivyo. ‘Hutakufa. Unaweza kufurahia kile ambacho Mungu mwenyewe anafurahia. Unaweza kujiamulia mwenyewe yaliyo mema au mabaya.’ Hawa alivutwa na jambo la kwamba angeweza kufanya maamuzi yake mwenyewe bila kuwa chini ya wajibu wa mtu ye yote.
9. Kama inavyoonyesha katika Yakobo 1:14, 15, ni mfululizo gani wa matukio ulioongoza kwenye dhambi ya Hawa na kifo cha hatimaye?
9 Matokeo yakawa kwamba, Hawa alianza kuutazama mti ule kwa tamaa. “Mwanamke alipoona ya kuwa ule mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika kwa maarifa, basi alitwaa katika matunda yake akala.” (Mwanzo 3:6) Lakini baadaye, Hawa alipogundua kwamba hakupokea kile alichokuwa ameahidiwa, alieleza hivi: “Nyoka alinidanganya.” (Mwanzo 3:13) Kwa kweli, nyoka huyo alikuwa amemtongoza pia, akamwongoza kwa ushawishi au jaribu lenye kuvuta macho kando mpaka tamaa ya kichoyo ikamfanya atende dhambi na, kwa hiyo, hatimaye akafa.—Yakobo 1:14, 15.
Jihadhari na Mbinu za Shetani
10. Kwa sababu gani si lazima sisi tukose kuzijua mbinu za Shetani, nasi ni wenye hekima tukifuata maagizo gani?
10 Shetani anatumia mbinu zinazofanana na hiyo, yaani, hila, vipengee, na maarifa ya ujanja, ili kudanganya na kutongoza vijana leo. Lakini kwa kuwa Biblia inatoa historia kamili juu ya njia, za udanganyifu anazotumia Shetani, wewe huhitaji kukaa bila kujua mbinu zake. (2 Wakorintho 2:11, NW ) Unalohitaji ni hisia nzuri ya kutii maonyo na maagizo anayotoa Yehova Mungu kupitia Neno na tengenezo lake.—Mithali 2:1-6; 3:1-7, 11, 12;4:1, 2, 20-27; 7:1-4.
11. Mara nyingi Shetani anatongoza au anadanganyaje vijana waingie katika makosa?
11 Mara nyingi Shetani anavuta au anashawishije walio wadogo kwa umri ili wafanye makosa? Ni kwa kufanya mambo ambayo Mungu anakataza, au utendaji unaoweza kufanya mtu apoteze kibali ya Mungu, yaonekane kuwa ya kuvutia sana, na wakati ule ule kuwa yasiyodhuru, kama vile lile tunda lilivyoonekana kwa Hawa. Na kama vile alivyofanya kwa Hawa, yeye atajaribu kuendeleza wazo la kwamba unakosa bure tu kujipatia jambo fulani lenye raha. Hivyo, kwa njia ya ujanja na udanganyifu Shetani anajaribu kuharibu heshima yako kwa Neno la Yehova, pia kwa maagizo unayopata kutokana na wazazi wako wanaomwogopa Mungu na yenye kutokana na tengenezo la Mungu. Kwa hiyo Biblia ina sababu nzuri kuhimiza kwamba, “mpate kuweza kusimama imara kushindana na hila [au kama vile inavyosema The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures, ‘vitendo vya kiufundi’] za Ibilisi.”—Waefeso 6:11, NW.
12. (a) Ni uhakika gani unaohusu Shetani ambao inatupasa sisi sote tuuchukue kwa uzito, na kwa sababu gani? (b) Wewe unayaonaje maneno yanayosemwa kwenye 1 Yohana 2:15 na Yakobo 4:4? (c) Shetani angependa kukudanganya wewe uamini nini?
12 Kwa wazi Hawa alikuwa mpumbavu kuamini uwongo wa Shetani. Lakini je! leo vijana wengi kwa njia inayofanana na hiyo hawayapuuzi maonyo yaliyo katika Neno la Yehova au yale wanayopewa na wazazi wao au wazee Wakristo? Namna gani wewe? Kwa mfano, je, wewe unachukua kwa uzito jambo la kwamba Shetani Ibilisi ndiye mtawala wa ulimwengu huu na kwamba akiwa ndiye mungu wa mfumo huu wa mambo anapofusha akili za watu? (1 Yohana 5:19; Yohana 12:31; 14:30; 16:11; 2 Wakorintho 4:4) Je! wewe unajaribu kweli kweli kutii amri ya Mungu inayosema, “Msiwe mkipenda wala ulimwengu wala vitu vilivyomo katika ulimwengu”? (1 Yohana 2:15, NW) Tena jiulize, ‘Kweli mimi nayaamini maneno haya ya Kimaandiko, “Kwa hiyo ye yote anayetaka kuwa rafiki wa ulimwengu anajifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu’ ”? (Yakobo 4:4, NW ) Shetani angependa akudanganye uamini kwamba ulimwengu hautokezi tisho lo lote, kwamba utendaji mbalimbali unaoendelezwa nao hauna madhara. Lakini jihadhari! Usidanganywe!
Vivuta-Macho Vyenye Udanganyifu Leo
13. Ni desturi gani ambayo imekuwa ikifuatwa na watu wengi mahali pengi, na Shetani angependa sisi tuamini nini kuihusu?
13 Mara Nyingi Shetani anashawishi watu watende makosa kwa kutumia vitu ambavyo huenda visiwe vibaya vyenyewe au vile visivyokatazwa waziwazi katika Biblia. Kwa mfano, ingawa watu wengi waliooana wanafurahia kukumbuka nyakati za kupendeza walizofurahia siku zao za kuchumbiana, kunaweza kuwa na hatari mbalimbali wakati watu wanapokuwa pamoja pekee yao katika matembezi ya kirafiki. Kwa kweli, matembezi kati ya mvulana na msichana ni desturi ambayo haikuanza zamani sana ambayo imeanza kufuatwa sana mahali pengi baada tu ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Shetani angependa uamini kwamba desturi hiyo ni namna ya tafrija isiyo mbaya inayowezesha vijana wafahamiane na watu wa jinsia ile nyingine wakiwa mmoja mmoja. Lakini, kusema kweli, desturi hiyo ina hatari nyingi za kiadili.
14. (a) Desturi ya matembezi kati ya wavulana na wasichana inaweza kukadiriwaje? (b) Ni hali za kujisikiaje zinazoweza kusitawi katika matembezi kati ya wavulana na wasichana?
14 Kwa sababu ya ujuzi wao, Wakristo wenye umri mkubwa na waliokomaa wanazijua zaidi hatari hizo na hivyo wanaweza kutoa mwelekezo wenye msaada. (Mithali 27:12) Lakini labda wewe unaona kwamba hakuna hatari ya kufanya matembezi ya wavulana na wasichana, na kwamba wazazi wako wanaweka vizuizi vingi mno, wakikunyima raha. Lakini kama vile watu wanavyoweza kuhukumiwa jinsi walivyo kutokana na matunda wanayozaa, ndivyo na desturi kama ile ya matembezi ya wavulana na wasichana. (Mithali 20:11; Mathayo 7:16) Kwa mfano, msichana wa miaka 18 aliyekuwa akitembea na mvulana kwa ukawaida kisha akapata mimba alisema hivi: “Mimi nilikuwa mmoja wa maelfu ya watoto waliofikiri jambo hilo halingeweza kunipata mimi.” Yeye alikiri kwamba baada ya kufanya matembezi hayo ya kirafiki kwa muda fulani “kushikana mikono na kubusiana kunapoteza utamu.” Vivyo hivyo msichana wa miaka 17 aliyefanya matembezi ya kirafiki mara nyingi, anaripoti hivi: “Kubusiana na kushikana karibu-karibu kunaongezeka mpaka ninataka sana yule mvulana afanye ngono nami.” Je! hiyo ni hisia isiyo ya kawaida? Hata kidogo.
15. Ni lazima matembezi kati ya wavulana na wasichana yalaumike sana kwa sababu ya misiba gani?
15 Wakati vijana wanaovutiana kimwili mtu na mwenzake wanapokuwa mahali peke yao, kama ilivyo kawaida wakati wa matembezi ya kirafiki, nyege zinaweza kuongezeka mpaka ziwakumbe hata vijana wenye makusudi mazuri wavunje sheria ya Mungu. Fikiria kwamba wasichana matineja ambao ni zaidi ya milioni moja katika United States wanapata mimba kila mwaka na kwamba mamia ya maelfu yao wanatoa mimba au wanazaa watoto wao bila kufunga ndoa. Jambo la kusikitisha ni kwamba, pindi kwa pindi wengine wa wasichana hao matineja ni watoto wa Mashahidi wa Yehova na ndivyo ilivyo pia kuhusu wavulana wanaowatia mimba. Ile desturi ya kisasa ya matembezi ya wavulana na wasichana ni lazima ilaumike sana kwa misiba hiyo, na pia labda kwa sababu ya mamilioni ya visa vipya vya magonjwa yanayoambukia watu kila mwaka kupitia ngono.
16. (a) Ni wapi tu tamaa za ngono zinapotoshelezwa kwa kufaa? (b) Ni jambo gani linalotukia kwa watu wengi wa Mungu?
16 Mungu alikusudia kwamba nyege zitoshelezwe ndani ya kifungo cha ndoa, ambamo zinaweza kuleta raha inayofaa na uradhi. (Waebrania 13:4; Mithali 5:15-19) Hata hivyo Shetani ametumia kwa ufundi zawadi hiyo iliyotolewa na Mungu ili kutongoza watu watumie ngono vibaya na kufanya uasherati. Katika nyakati za kale, Waisraeli 24,000 waliuawa siku moja kwa kufanya kosa hilo dhidi ya Mungu, na wakati wa sasa maelfu kila mwaka wanatengwa na ushirika wa kundi la Kikristo kwa sababu ya uasherati. Kwa hiyo uwe mwenye hekima. Sikiliza mashauri na mwelekezo. Usijiache udanganywe.—Hesabu 25:1-9, 16-18; 31:16.
17. (a) Ni maoni gani ya udanganyifu ambayo Shetani ameendeleza juu ya mambo kama vile michezo, muziki, na kucheza dansi? (b) Kwa sababu gani vitumbuizo vya ulimwengu vinatokeza tisho kubwa kwa watu wa Mungu?
17 Uwe chonjo, pia, kuziona mbinu nyingine za Shetani. Kwa mfano, michezo, muziki, na kucheza dansi ni mambo ambayo yamekuwa sehemu kubwa ya vitumbuizo vya ulimwengu wake. Ni kweli kwamba vitu hivyo vyenyewe si vibaya kwa lazima na vinaweza kufurahisha na hata kufaidi. (1 Timotheo 4:8; Zekaria 8:5; Luka 15:25) Lakini, Shetani ameendeleza kwa udanganyifu maoni ya kwamba mambo hayo hayaelekei kuleta madhara, hata mtu anapoyashiriki kwa ukawaida akiwa pamoja na watu wa ulimwengu. Lakini Neno la Mungu linaonya hivi: “Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri,” (1 Wakorintho 15:33, NW ) Fikiria jambo hili: Ikiwa dini na siasa ni sehemu ya mfumo wa Shetani, je! si upumbavu kuamini kwamba vitumbuizo vinavyoendelezwa na ulimwengu havina mavutano yake? Unahitaji daima kujihadhari ‘usiache ulimwengu unaokuzunguka ukufinyange katika umbo lao wenyewe.’—Warumi 12:2, The New Testament in Modern English, ya J. B. Phillips.
Maandalizi ya Kulinda Vijana
18. Kwa sababu gani inakupasa uthamini wazazi wanaokufundisha na kukuongoza?
18 Yehova Mungu amefanya kwa upendo maandalizi ya kuwalinda ninyi mlio na umri mdogo msidanganywe. Kwanza yeye amewaandalia ninyi wazazi wenu ili wawafundishe na kuwaongoza. Na mnaweza kufurahi wanapofanya hivyo. Msichana mmoja mwenye huzuni wa miaka 18, aliyepata mtoto bila kufunga ndoa, alilalamika kwamba jambo hilo lisingalitokea “kama wazazi wangu wangalifanya kazi inayowapasa wazazi, wakaniambia mitego ya kuendelea kufanya urafiki na mvulana, wakanikataza nisiendeleze urafiki huo.” Kwa hiyo shukuru ikiwa wewe una wazazi wanaomwogopa Mungu. Wao hawajaribu kukufinya na kufanya maisha yawe yasiyopendeza kwa kukuwekea vizuizi. Kinyume cha hivyo, wao wanakupenda na wanataka kukulinda. Tumia kwa faida ujuzi na hekima yao kwa kutafuta mashauri yao.
19. Ni misaada gani ya ziada ambayo imeandaliwa ili kulinda vijana?
19 Tena, Yehova ameandaa tengenezo lake la kidunia ili kukusaidia. Kwa mfano, kila toleo la Amkeni! linakuwa na ile sehemu inayosema “Vijana Wanauliza . . .” inayoonyesha mafaa yasiyopita kiasi ya viwango vya Yehova. Vivyo hivyo, ile broshua inayoitwa Shule na Mashahidi wa Yehova iliandaliwa ili kukusaidia wewe ukae kulingana na sheria na kanuni za Mungu katika mazingira ya shule. Kitia-moyo na mashauri zaidi yanatolewa kupitia kurasa za Mnara wa Mlinzi na kwenye mikutano ya kundi, makusanyiko ya mzunguko, na mikusanyiko ya wilaya. Kwa kweli, habari ii hii yenyewe, “Vijana—Msidanganywe,” ilikuwa hotuba kwenye mkusanyiko wa wilaya wa juzijuzi na pia ikawa ni habari ya sehemu moja ya Mkutano wa Utumishi.
20. (a) Kwa sababu gani vijana wanaandaliwa misaada mingi? (b) Ni kuwa na mwelekeo gani kutakusaidia upinge vishawishi vya Shetani vinavyokusudiwa kukudanganya?
20 Usifikiri kwamba kwa kukuonyesha yote haya tunajaribu kukukaza mno na mambo mengi ili tukunyanganye furaha yako. Bali, tengenezo la Mungu linakupenda, na kila jambo linalochapwa na kusemwa linakusudiwa kukulinda wewe—kuokoa uhai wako! Jifunze kuthamini maandalizi hayo. Ifanye iwe tabia yako kujifunza Biblia kwa kutumia vichapo vya Sosaiti; acha kweli za Biblia zikusisimue kwa njia yenye uthamini. Na uwe na mwelekeo ule wa kijana wa miaka 18 ambaye, baada ya kufikiria mashauri ambayo vijana walitobolewa waziwazi, aliandika: “Yalinifanya nitambua jinsi tulivyopendelewa sana sisi vijana tulio katika ukweli! Hakuna tengenezo jingine lo lote duniani linalojali na kupenda vijana wao kadiri hiyo! ” Na tuungane sana pamoja tuvipinge vishawishi vya Ibilisi vinavyokusudiwa kwa kutudanganya, kwa maana sisi twazijua zake!
SANDUKU LA KURUDIA
◻ Kwa sababu gani vijana ni lengo la pekee la Shetani?
◻ Shetani alimtongozaje Hawa akamwingiza katika kosa?
◻ Mara nyingi leo Shetani anatongozaje vijana waingie katika makosa?
◻ Kuna maandalizi gani ya kulinda vijana?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Sawa na vile Shetani alivyotafuta kupoteza Hawa, mwenye ujuzi mchache zaidi ya Adamu, ndivyo vijana walivyo lengo la pekee la Shetani
[Picha katika ukurasa wa 13]
Wakati vijana wanapokaa wakiwa pekee yao tu, tamaa ya ngono inaweza kuongezeka na kuwaongoza wavunje sheria ya Mungu