Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 6/15 kur. 3-14
  • Kuzifunua Hila za Ibilisi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuzifunua Hila za Ibilisi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Namna Shetani Anavyotenda Kazi
  • Namna za Mitego Isiyotambulika Wazi ya Utafutaji wa Vitu vya Kimwili
  • Namna Isiyotambulika Wazi ya Kupashana Habari na Roho Waovu
  • Epuka Kuwaza kwa Njia ya Kujitegemea Mwenyewe
  • Jihadhari na Adui Yako, Ibilisi!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Uwe Macho​—Shetani Anataka Kukumeza!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Adui wa Uzima wa Milele
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Simama Imara Dhidi ya Hila za Shetani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 6/15 kur. 3-14

Kuzifunua Hila za Ibilisi

“Mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.”​—1 PETRO 5.8.

1, 2. (a) Ni hali gani ambayo ingeweza kuogopesha sana ambayo Yesu mwenyewe alielekeana nayo? (b) Kwa sababu gani watu walikuwa wakijaribu kumwua Yesu?

TUSEME umepata habari kwamba mtu fulani amepewa pesa ili akuue. Namna gani ukijua kwamba sasa hivi anakunyemelea-nyemelea, akiungoja wakati unaofaa kabisa ili akushambulie. Jambo hilo lingekushtua sana! Je! wewe ulijua kwamba Yesu Kristo alielekeana na hali kama hiyo?

2 Biblia inasema: “Yesu alikuwa akitembea katika Galilaya; maana hakutaka kutembea katika Uyahudi, kwa sababu Wayahudi walikuwa wakitafuta kumwua.” Walakini, maisha yake yajapoelekewa na hatari hiyo, katika mwaka wa 32 W.K. Yesu alipanda Yerusalemu akahudhurie Sikukuu ya Mahema. Katika wakati huo, “baadhi ya watu wa Yerusalemu wakasema, Je! huyu siye wanayemtafuta ili wamwue?” (Yohana 7:1, 25) Kwa sababu gani watu walikuwa wakijaribu kumwua Yesu? Ni kwa sababu walikuwa wamechochewa na Ibilisi! Kama ilivyoandikwa katika Yohana 8:44, Yesu mwenyewe alisema: “Ibilisi . . . alikuwa mwuaji tangu mwanzo.”

3. Kwa sababu gani onyo la mtume Petro juu ya Ibilisi linafaa hasa leo?

3 Basi, tusishangae kwamba Ibilisi (Diabolo) amejiondokea akawanase watu wenye kumcha Mungu leo, hasa tangu wakati ambao ametupwa nje ya mbingu. Biblia inaeleza hivi: “Ole wao wanaokaa kwa dunia na bahari! Kwani yule Diabolo ameshuka kwenu mwenye gazabu nyingi kwa sababu anajua ana wakati mufupi tu.” (Ufunuo 12:7-12, ZSB) Maana yake ni kwamba Shetani na mashetani wake wanapiga juu yetu vita ya kufa au kupona! Basi onyo hili linafaa sana sasa: “Mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.” Mtu huyo ni kutia ndani wewe, ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ndiyo sababu Petro alisema hivi pia: “Mwe na kiasi na kukesha.”​—1 Petro 5:8.

4. (a) Kusudi la Ibilisi ni nini anapotukaribia sisi kwa ujanja? (b) Ni kwa njia gani moja tu Ibilisi anavyoweza kufanikiwa katika makaribio yake?

4 Lakini kusudi la Ibilisi ni nini anapotukaribia sisi kwa ujanja? Si kutuua papo hapo. Kwa kutumia njia ya ulaghai amkaribie Yesu, kusudi la Shetani lilikuwa ni kumfanya akubali kuchanganya ibada yake kwa Yehova na ibada nyingine. (Mathayo 4:3-10) Wakati jitihada zake za kushawishi Yesu asimtii Mungu zilipokosa matokeo, lengo la Shetani lilikuwa kumfanya atafute faraja ya kumtulizia matisho aliyofanyiwa ya kumwua, kwa kusababisha aache ukamilifu wake kwa Mungu. Vivyo hivyo leo, kusudi halisi la karibio la Shetani ni kuharibu kabisa uhusiano mwema tulio nao pamoja na Mungu. Je! atafanikiwa? Kuna njia moja tu anavyoweza kufanikiwa. Biblia inaionyesha njia hiyo inaposema hivi: “[Yehova] yu pamoja nanyi, mkiwa pamoja naye; . . . lakini mkimwacha atawaacha ninyi.”​—2 Mambo ya Nyakati 15:2.

5. (a) Inaweza kusemwa nini juu ya kufanikiwa kwa njia za Shetani? (b) Ili tuweze kusimama imara, ni lazima tuendelee kuwa macho tuone nini?

5 Jambo la kusikitisha ni kwamba kila mwaka wengine wanashindwa nguvu na njia za Shetani. Wanamwacha Yehova. Kwa kweli, inakuwa lazima wengi wao watengwe na ushirika wa kundi la Kikristo kwa sababu ya mwenendo wao wa kutokumcha Mungu. (1 Wakorintho 5:13) Tunaweza kusema wengine wanakuwa ‘mahabusu (wafungwa) wa vita’ kwa kunaswa katika mfumo wa Ibilisi. Je! wewe utasimama imara dhidi ya jitihada zote za Shetani za kukufanya umwache Yehova? Ili uweze kufanya hivyo, unahitaji kuendelea kuwa macho uzione hila za Ibilisi.

Namna Shetani Anavyotenda Kazi

6. Kwa sababu gani hatuhitaji kuwa gizani kuhusiana na hila za Shetani?

6 Sisi hatuachwi gizani tusijue namna Shetani anavyotenda kazi. “Hatukosi kuzijua fikira [hila, NW] zake,” akaeleza mtume Paulo. (2 Wakorintho 2:11) Maana yake ni kwamba Shetani amekaza fikira zake juu yetu​—anafikiri juu yetu, akitumia mawazo yake yote ya busara atuondoe katika njia ya kumtumikia Mungu. Je! hilo si wazo la kutufanya tufikiri kwa uzito? Lakini katika Biblia tuna historia kamili kabisa ya hila za Shetani, yaani, mipango yake, njia zake za werevu na mipango ya kiufundi, hivi kwamba hakuna mtu anayehitaji kukosa ufahamu katika jambo hilo. Askari mwema anachunguza habari za mapigano yaliyofanywa zamani na kuyatumia anayojifunza kwa njia yenye faida. Vivyo hivyo, sisi ‘askari wema wa Kristo Yesu’ tunaweza kuchunguza njia mbalimbali za kiufundi zinazotumiwa na Shetani na hivyo tuepuke kunaswa na yo yote ya njia zake za kufanyia kazi tukiwa hatuna habari.​—2 Timotheo 2:3.

7. (a) Nyakati nyingine Shetani anafanya makaribio gani ya uso kwa uso? (b) Ni njia gani nyingine anazotumia, na kwa sababu gani?

7 Hatimaye mawakili wa Shetani walimtenda Yesu makatili ya ajabu kisha wakamwua. (Yohana 19:1; Mathayo 27:49, 50) Na Yesu alitabiri hivi juu ya wafuasi wake: “Wakati huo watawasaliti ninyi mpate dhiki, nao watawaua.” (Mathayo 24:9) Walakini, makaribio hayo ya uso kwa uso mara nyingi yanawageuka wakabiliaji wenyewe, na matokeo yanakuwa kwamba watumishi wa Mungu wenye kuteswa wanakuwa na juhudi kubwa zaidi kwa ajili ya utumishi wake. (Matendo 5:41, 42) Basi, Shetani anajaribu mara nyingi zaidi kutumia njia tofauti​—hila zisizotambulika kwa wepesi—​ili avunje ukamilifu wa watumishi wa Mungu.

8. Biblia Inafunuaje kwamba Shetani angetumia hila?

8 Biblia inaelekeza fikira kwenye hila hizo inapotia moyo hivi: “Simameni imara dhidi ya mitungo ya mashauri mabovu, ya yule Ibilisi.” (Waefeso 6:11, NW) Neno la Kigiriki hapa linalosimamia “mitungo ya mashauri mabovu” linamaanisha “matendo ya kiufundi.” (Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures) inaonyeshwa kwamba Shetani ni stadi wa udanganyifu, mwenye ujanja na werevu wa kupindukia, wakati Biblia inaposema hivi pia: “Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru.”​—2 Wakorintho 11:14.

9, 10. (a) Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza mtungo wa kwanza wa shauri bovu la Shetani ambalo lilifanikiwa? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba yeye anaendelea kutumia werevu ule ule na ufundi wenye ujanja?

9 Ufikirie mtungo wa shauri bovu la kwanza la Shetani ambao ulifanikiwa. Alipokuwa akimkaribia Hawa hakujaribu kutokeza ubishi kusema kwamba Mungu angekubaliana na Hawa akila tunda lile lililokatazwa. Hawa alikuwa na akili za kutosha kugundua hoja hiyo. Kwa hiyo Shetani alilifanya tunda lile lionekane kuwa la kutamanika kweli kweli machoni pa Hawa. Akamwambia kwamba akilila hali yake ingepata maendeleo kweli kweli, hivyo akampa mwanamke huyo apate taraja la kuvutia. “Mtakuwa kama Mungu,” akasema. (Mwanzo 3:5) Hawa alijiacha akashindwa nguvu na ushawishi wa Shetani. Mwanamke huyo alisitawisha tamaa mbaya, nayo ikamwongoza kutenda dhambi.​—Yakobo 1:14, 15.

10 Shetani anaendelea kutumia werevu na ufundi wenye ujanja, kama vile mtume Paulo alivyoandika: “Lakini nachelea; kama yule nyoka alivyomdanganya [alivyomshawishi, NW] Hawa kwa hila yake, asije akawaharibu fikira zenu, mkauacha unyofu na usafi kwa Kristo.” (2 Wakorintho 11:3) Kama njia za Shetani za kufikia watu zisingekuwa za hila nyingi hivyo, haielekei kwamba watu wengi hivyo wangetekwa wakiwa majeruhi wa vita. Yeye anatokeza daima mapotovu yenye ushawishi, akijaribu kwa ujanja kutufanya tupendezwe na mambo ambayo hatimaye yatagandamiza hali yetu ya kiroho. Lengo lake ni kutudhoofisha mpaka tumwache Yehova hatua kwa hatua, au kusudi shambulio fulani la uso kwa uso lifaulu kuvunja ukamilifu wetu kwa Mungu.

11. (a) Ni kwa njia gani njia za Shetani zinaweza kulinganishwa na zile zinazotumiwa na mvuvi wa samaki? (b) Ni jambo gani tusilopaswa kulisahau kamwe?

11 Njia za Shetani zinaweza kulinganishwa na zile za mvuvi wa samaki anayetumia vyambo (vidonge vidogo vya chakula n.k.) ili kutega samaki. Mvuvi huyo anafanya majaribio ya vyambo mbalimbali aone ni chambo kipi kitakachowaleta samaki karibu. Bila shaka, wakati samaki wanapokiuma chambo hawajui kwamba nyuma ya chambo hicho pana ndoana. Namna gani sisi? Je! tunavijua vyambo anavyotumia Shetani? Je! tunafahamu kwa ukamili matokeo ya ‘kunaswa katika ndoana’? Usidanganywe! Shetani na mashetani wake ni maadui halisi ambao wamejiondokea wakiwa wamepiga moyo konde kwamba watatupata! Kwa hiyo usisahau kamwe kwamba “ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu.” Yeye amepofusha akili za walio wengi wasiuone uhakika huo. Wewe usimwache apofushe akili zako.​—1 Yohana 5:19, NW; 2 Wakorintho 4:4.

Namna za Mitego Isiyotambulika Wazi ya Utafutaji wa Vitu vya Kimwili

12. (a) Ni chombo gani hasa ambacho Shetani anatumia? (b) Jicho linaweza kutamani vitu gani?

12 Chambo kimoja kikuu ambacho Shetani anatumia ni kupenda vitu vya kimwili na anasa. (1 Timotheo 6:10) Biblia inaitaja “tamaa ya macho,” kisha inaonya kwamba tamaa ya namna hiyo ‘haitokani na Baba, bali yatokana na ulimwengu.’ (1 Yohana 2:16, NW) Katika ulimwengu wetu wa kisasa vitu vya kutamaniwa na macho vimeongezeka kweli kweli. Kuna mamboleo ya nyumba mpya-mpya, magari, vilori, mashua, mavazi, televisheni, vinanda vyenye kutokeza midundo mizuri sana, saa za mikononi, makompyuta, sinema zilizorekodiwa katika ukanda za kuonea nyumbani na vifaa vingine vya namna zote vinavyotumia umeme. Pia, kuna anasa nyingi za kufurahiwa, kama muziki, kuchezwa dansi, kwenda sinema, maonyesho ya kuigizwa, utazamaji wa televisheni, michezo ya namna nyingi sana, na kadhalika.

13. (a) Shetani anaweza kutumiaje vitu vinavyoweza kuwa na faida vitege Wakristo kwa kuwavuta wasimtumikie Mungu?

13 Bila shaka vitu vya kimwili vyenyewe wala anasa zenyewe tu si mbaya. Yehova alifanya ulimwengu mzima wa vyote vilivyoumbwa ukiwa na vitu vya kimwili vyenye kupendeza, kutia ndani dunia yetu pamoja na uzuri wayo wote, ili kufurahisha maono yetu na hisi zile nyingine. Ni wazi kwamba namna mbalimbali za tafrija na kujiburudisha zinaweza kufaidi zisiporuka mpaka unaozipasa. (1 Timotheo 4:8) Hata hivyo, wakati ule ule tunahitaji kujua kwamba mara nyingi Shetani anatumia vitu vivi hivi kuwavuta Wakristo kwa vyambo vyake waache kumtumikia Mungu. Bila shaka Shetani mwenyewe amehusika sana katika maendeleo na matumizi ambayo yamefanyiwa vitu hivyo vya kimwili na anasa za kimamboleo ambazo zimepotosha fikira za watu wengi sana wasimtumikie Yehova Mungu. Usidharau nguvu za adui yetu yule Ibilisi. Yeye amekwisha kuwa stadi wa mashambulio ya kuotea-otea.

14. (a) Ni mifano gani inayoweza kudokezea mtu kwamba anaendelea kuvutwa na namna zisizotambulika wazi za utafutaji wa vitu vya kimwili? (b) Kwa sababu gani kupeperuka kwa kumwacha Mungu kunaweza kuwa ni kama jambo lisiloonekana?

14 Unaweza kujuaje kwamba umeanza kuvutwa-vutwa na chambo cha Shetani kisichotambulika wazi cha utafutaji wa vitu vya kimwili? Unaweza kujua ikiwa namna yo yote ya burudisho au ufuatiaji wa mali imeanza kuvuruga mpango wako wa kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida au kufanya huduma ya shambani ya kila juma. Kwa kweli, kuna uhitaji wa kuwa macho. Chambo cha utafutaji wa vitu vya kimwili kinaweza kukupeperusha kwa kuzidi tu kukumalizia wakati wako, mapendezi yako na nishati zako hatua kwa hatua tu. (Waebrania 2:1) Wakati mashua inaposonga-songa kwa kupepewa na upepo huenda usigundue kwamba inasonga. Huenda ukasema haisongi kamwe. Lakini uthibitisho wa kwamba inasonga unaonekana kwa vile pole kwa pole inafikia mahali tofauti na pale pa kwanza. Ndivyo ilivyo na mtu anayepeperuka kwa kumwacha Mungu na tengenezo Lake.

15, 16. (a) Lingekuwa Jambo la hekima tujichunguze wenyewe juu ya nini? (b) Ni hali gani inayoonyesha kwamba ni jambo la hekima kujichunguza hivyo?

15 Basi, imetupasa tutumie hekima kuchunguza mara nyingi utendaji wetu wenyewe wa Kikristo, kwa kujiuliza: “Je! mimi najifunza Biblia kwa ukawaida kama zamani? Je! nahudhuria mikutano kwa ukawaida kama wakati uliopita? Je! nafanya saa nyingi katika huduma ya shambani kama hapo kwanza?” Labda wewe utasema: “Lakini mambo yamenizidia siku hizi.” Lakini yamekuzidia ukiwa unafanya nini? Je! inaweza kuwa kwamba unatumia wakati mwingi zaidi kufuatia anasa, labda ukiwa unatazama televisheni? Je! inaweza kuwa kwamba umekuwa ukijilundikia vitu vya kimwili na ukawa ukivitunza hivyo hata vikawa vinakuzuia badala ya kukusaidia kumtumikia Mungu? Je! wewe unatii kweli kweli shauri la Yesu la kutokuhangaikia vitu vya kimwili bali kutafuta Ufalme wa Mungu kwanza?​—Mathayo 6:31-33.

16 Kote kote ulimwenguni kuna majeruhi wa vita​—Wakristo ambao wamevutwa-vutwa na kunaswa na namna zisizotambulika wazi za Ibilisi za utafutaji wa vitu vya kimwili, nao wameanguka wakauacha utumishi wa Mungu. Labda katika kundi lenu wenyewe unaweza kuwa na wazo juu ya watu fulani ambao zamani walikuwa wafanya kazi wenzako waaminifu, lakini sasa si watendaji tena katika utumishi wa Mungu kwa sababu ya kujiacha wanaswe na vyambo visivyotambulika wazi vya utafutaji wa vitu vya kimwili ambavyo pole kwa pole vimewapeperusha (Wafilipi 3:18) Kwa hiyo ‘uwe na kiasi na kukesha.’ Usimwache Ibilisi akumeza wewe!​—1 Petro 5:8.

Namna Isiyotambulika Wazi ya Kupashana Habari na Roho Waovu

17. (a) Kwa sababu gani malaika waliacha vyeo vyao mbinguni. na ni jambo gani lililowapata wakati maji ya Gharika yalipomiminika? (b) Malaika hao ndio wamesababisha nini?

17 Je! wewe unaukumbuka wakati ule malaika wengine walipojiunga na Shetani kumwasi Yehova? Ulikuwa ni muda mfupi kabla ya Gharika. Biblia inafunua kwamba binti za wanadamu wenye sura za kuvutia walikuwa kama chambo cha kuwatega malaika. Wengine wao waliacha vyeo vyao vya kimbingu vya utumishi waje duniani kufanya ngono pamoja na wanawake hao warembo. Tendo lao lilikuwa kosa sawa-sawa na yale matendo ya kulalana wanaume kwa wanaume ya watu Sodoma na Gomora. (Mwanzo 6:1, 2; Yuda 6, 7) Wakati maji ya Gharika yalipomiminika, malaika hao walivua miili yao ya nyama wakarudi mbinguni. Ingawa walinyimwa kabisa uwezo wa kuvaa tena miili ya kibinadamu ili kutosheleza nyege zao zisizo za asili, malaika hao wamekuwa watendaji sana katika kuichafua jamaa ya kibinadamu katika tabia. Ongezeko kubwa lililopo leo katika uasherati wa namna zote limetokana moja kwa moja na kutupwa kwao watoke mbinguni na kuzuiliwa kwenye ujirani wa dunia.​—1 Timotheo 4:1; Ufunuo 12:9, 12.

18. Ni ushuhuda gani, wa zamani na wa sasa, unaofunua kwamba uasherati umekuwa moja ya njia zilizo kubwa zaidi zinazotumiwa na Shetani kuchafua watumishi wa Mungu?

18 Chambo cha uasherati kimekuwa sikuzote moja ya njia kubwa zaidi ambazo Ibilisi anatumia kuchafua watumishi wa Yehova. Muda mfupi kabla watu wa Mungu Israeli hawajaiingia Nchi ya Ahadi, Shetani alitumia wanawake Wamoabi wenye sura za kuvutia kama chambo cha kuwaondoa Waisraeli katika utumishi wa Yehova. Maelfu ya Waisraeli ‘walinaswa katika ndoana’ wakaingizwa katika uasherati, na, kwa sababu hiyo, waliuawa kwa makosa yao. (Hesabu 25:1-3) Kuhusiana na pindi hiyo, Wakristo wanaonywa hivi: “Wala tusifanye uasherati, kama wengine wao walivyofanya, wakaanguka siku moja watu ishirini na tatu elfu.” (1 Wakorintho 10:7, 8, 11) Hila hiyo ya Shetani ilifaulu wakati huo, na inaendelea kufaulu leo. Watu wengi zaidi wanatengwa na ushirika kwa sababu ya uasherati kuliko hesabu inayotengwa kwa sababu nyinginezo zote hata zikijumlishwa pamoja.

19. (a) Kwa sababu gani wengi sana wa watumishi wa Yehova wanahusika katika uasherati na hali wanajua unamchukiza Mungu? (b) Ni nini kitakachokusaidia uepuke kuhusika katika uasherati?

19 Lakini kwa kuwa watumishi wa Yehova wanajua kwamba uasherati na uzinzi ni mambo yaliyo kinyume cha sheria za Mungu, kwa sababu gani wengi sana kati yao wanahusika katika utendaji huo? Haya basi, ni kwa sababu gani Hawa hakutii sheria ya Mungu? Ni kwa sababu Shetani alifanya kutokutii kuonekane kuwa jambo la kuvutia kabisa; ilikuwa ni nafasi ambayo yeye aliwaza hangeweza kukubali impite. Vivyo hivyo leo, kwa kutumia njia zake za kueneza porojo​—televisheni, sinema, magazeti, na kadhalika​—Shetani anafanya uasherati na uzinzi yaonekane kuwa mambo yenye kukubalika, licha ya kuwa yenye kufurahika. Kwa hiyo wewe ukijinyosha uume kile chambo kinachotolewa kupitia njia za Ibilisi za kueneza porojo, itakuwaje? Hata wewe ‘utanaswa katika ndoana’!

Epuka Kuwaza kwa Njia ya Kujitegemea Mwenyewe

20. (a) Ni hila gani nyingine inayotumiwa na Ibilisi? (b) Shetani amekuwa akitumiaje hila hiyo kwa karibu miaka 6,000?

20 Tangu mwanzo wenyewe wa kuasi kwake, Shetani alitilia mashaka njia ya Mungu ya kufanya mambo. Alianzisha katika watu hali ya kuwaza kwa njia ya kujitegemea wenyewe. ‘Unaweza kujiamulia mwenyewe yaliyo mema na mabaya,’ Shetani akamwambia Hawa. ‘Si lazima mmsikilize Mungu. Kusema kweli yeye hawaambii ile kweli.’ (Mwanzo 3:1-5) Mpaka leo hii, hila ya Shetani imekuwa ni kuambukiza watu wa Mungu namna hiyo ya kuwaza.​—2 Timotheo 3:1, 13.

21. Ni mifano gani inayoonyesha hali ya kuwaza kwa kujitegemea nyakati za kisasa, na matokeo yamekuwa nini?

21 Hali hiyo ya kuwaza kwa njia ya kujitegemea mwenyewe inaonyeshwa wazi namna gani? Njia moja inayotumiwa sana ni kutokeza mashaka juu ya mashauri yanayotolewa na tengenezo linaloonekana la Mungu. Kwa mfano, mara kwa mara tengenezo la Mungu limetoa maonyo juu ya kusikiliza namna fulani za muziki wa uasherati na wenye kudokeza maoni ya ngono, na juu ya kwenda-kwenda kwenye madisko (dansi) na namna nyingine za majumba ya dansi za kilimwengu ambako muziki wa namna hiyo unapigwa na watu wanafanyia uasherati huko. (1 Wakorintho 15:33, NW) Hata hivyo watu fulani wamejidai kuwa wao ndio wanajua mambo zaidi. Wameasi mashauri hayo wakafanya yaliyo haki machoni pao wenyewe. Matokeo yamekuwa nini? Mara nyingi sana wameingilia uasherati kisha wakapata madhara makali ya kiroho. Lakini hata kama hawakupatwa na madhara makubwa hivyo, je! wao si watu wa kulaumika ikiwa wengine watafuata mfano wao kisha wapatwe na mabaya?​—Mathayo 18:6.

22. (a) Ni lazima tuendelee kukumbuka nini nyakati zote? (b) Ni nini kitakachofaa kuangaliwa katika funzo letu la safari ijayo?

22 Uhakika huu unapasa kukaziwa sana: Sisi tuko vitani pamoja na maadui wenye nguvu zinazozidi zile za kibinadamu, na tunahitaji daima kukumbuka jambo hilo. Shetani na mashetani wake ni watu waliopo kweli; wao si fikira tu za kuwaziwa akilini. Wao ndio “watawala wa ulimwengu wa giza hili,” nasi tuna pigano la kiroho pamoja nao. (Waefeso 6:12, NW) Ni jambo la maana kabisa tutambue hila zao wala tusijiachilie watupate. Basi, inafaa sana kwamba safari itakayofuata tutaangalia namna tunavyoweza kujipatia silaha za kupigana na roho waovu hawa.

Je! Wewe Unaweza Kujibu Maulizo Haya?

□ Kusudi la Ibilisi ni nini anapowakaribia watu wa Yehova?

◻ Kwa sababu gani Ibilisi anatumia hila?

◻ Ni hila gani mbalimbali anazotumia Shetani?

◻ Ni nini kitakachotusaidia tuepuke kupatwa na hila hizo?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mwendo wa mashua inayosonga-songa polepole unakuwa ni kama usioonekana. Hivyo ndivyo kunavyoweza kuwa kupeperuka kwa Mkristo anapoendelea kumwacha Mungu na tengenezo Lake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki