Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w12 1/15 kur. 16-20
  • Jifunze Kutokana na ‘Ile Picha ya Kweli’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jifunze Kutokana na ‘Ile Picha ya Kweli’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAMBO YALIYOKUWA KIVULI CHA DHABIHU YA YESU
  • MTAZAMO UNAOFAA KUHUSU DHABIHU
  • MAONYO KUHUSU DHABIHU
  • ONYESHA IMANI KATIKA DHABIHU YA YESU!
  • Dhabihu za Sifa Zinazompendeza Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kutoa Dhabihu Ambazo Zinampendeza Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Je, Utatoa Dhabihu kwa Ajili ya Ufalme?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Dhabihu Zilizompendeza Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
w12 1/15 kur. 16-20

Jifunze Kutokana na ‘Ile Picha ya Kweli’

“[Una] picha ya ujuzi na ya ile kweli katika Sheria.” ​—ROM. 2:20.

TAFUTA MAJIBU YA MASWALI HAYA:

  • Dhabihu zilizoagizwa na Sheria ya Musa zilifananisha nini?

  • Kuna ulinganifu gani kati ya dhabihu fulani zilizotolewa na Waisraeli na zile zinazotolewa na Wakristo leo?

  • Ni mambo gani yanayoamua ikiwa Yehova atakubali au hatakubali dhabihu fulani?

1. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuelewa umuhimu wa Sheria ya Musa?

KAMA hatungekuwa na maandishi ya mtume Paulo yaliyoongozwa na roho takatifu, ingekuwa vigumu kwetu kuelewa maana ya mambo mengi katika Sheria ya Musa. Kwa mfano, katika barua yake kwa Waebrania, anaeleza jinsi ambavyo Yesu akiwa ‘kuhani mkuu mwaminifu’ angeweza kutoa “dhabihu ya upatanisho” mara moja kwa wakati wote na hivyo kuwawezesha wale ambao wanaonyesha imani katika dhabihu hiyo kupata “ukombozi wa milele.” (Ebr. 2:17; 9:11, 12) Paulo alieleza kwamba maskani yalikuwa tu “kivuli cha vitu vya mbinguni” na kwamba Yesu alikuwa Mpatanishi wa “agano bora” kuliko lile ambalo Musa alikuwa mpatanishi wake. (Ebr. 7:22; 8:1-5) Katika siku za Paulo, maelezo kama hayo kuhusu Sheria yalikuwa muhimu sana kwa Wakristo, na bado ni muhimu leo. Yanatusaidia kuelewa kikamili zaidi thamani ya maandalizi ambayo Mungu ametupatia.

2. Wakristo Wayahudi walikuwa na pendeleo gani ambalo watu wa Mataifa hawakuwa nalo?

2 Paulo alipowaandikia Wakristo huko Roma, alielekeza baadhi ya maelezo yake kwa washiriki wa kutaniko ambao walikuwa wa asili ya Kiyahudi na ambao walikuwa wamefundishwa Sheria ya Musa. Alikiri kwamba kwa sababu ya kuifahamu Sheria hiyo ya Mungu, watu hao walikuwa na pendeleo la kuwa na “picha ya ujuzi na ya ile kweli” kumhusu Yehova na kanuni zake za uadilifu. Kuelewa ‘picha hiyo ya kweli’ na kuiheshimu kutoka moyoni kuliwawezesha Wayahudi Wakristo, kama Wayahudi waaminifu waliowatangulia, kuweza kuongoza, kufundisha, na kuwaelimisha wale ambao hawakujua Sheria ambayo Yehova alikuwa amewapa watu wake.​—Soma Waroma 2:17-20.

MAMBO YALIYOKUWA KIVULI CHA DHABIHU YA YESU

3. Tunafaidika jinsi gani kwa kujifunza kuhusu dhabihu ambazo Wayahudi walitoa zamani?

3 Picha ya ile kweli ambayo Paulo alirejelea bado ni muhimu kwetu ili tuelewe makusudi ya Yehova. Kanuni zinazotokana na Sheria ya Musa hazijapoteza umuhimu au thamani yake. Tukiwa na hilo akilini, acheni tuchunguze jambo moja tu katika hiyo Sheria—jinsi dhabihu na matoleo mbalimbali yalivyowaongoza Wayahudi wanyenyekevu kwa Kristo na kuwasaidia kuelewa mambo ambayo Mungu alitaka watimize. Na kwa kuwa mambo ya msingi ambayo Yehova anataka watumishi wake watimize hayabadiliki kamwe, tutaona pia kwamba sheria ambazo Mungu aliwapa Waisraeli kuhusu dhabihu na matoleo zinaweza kutusaidia kuchanganua ubora wa utumishi wetu mtakatifu.​—Mal. 3:6.

4, 5. (a) Sheria ya Musa iliwakumbusha nini watu wa Mungu? (b) Sheria ya Mungu kuhusu dhabihu ilionyesha nini?

4 Mambo mengi yaliyo katika Sheria ya Musa yaliwakumbusha Wayahudi wa zamani kwamba walikuwa watenda-dhambi. Kwa mfano, mtu yeyote aliyegusa maiti ya mwanadamu alipaswa kujitakasa. Kwa hiyo, ng’ombe mwekundu asiye na kasoro yoyote alichinjwa na kuteketezwa. Majivu yake yaliwekwa ili kutengeneza “maji ya kutakasa,” ambayo alinyunyiziwa mtu aliyekuwa akitakaswa siku ya tatu na ya saba baada ya kutiwa unajisi. (Hes. 19:1-13) Wayahudi walikumbushwa pia kwamba wanadamu wote wanazaliwa wakiwa na dhambi na hali ya kutokamilika kwa sababu mwanamke alipozaa alionwa kuwa asiye safi kwa muda, na baada ya hapo alihitaji kutoa dhabihu ya upatanisho.​—Law. 12:1-8.

5 Dhabihu za wanyama zilihitajiwa katika hali nyingine nyingi za maisha ya kila siku ili kufunika dhambi. Iwe mwabudu alijua au hakujua, dhabihu hizo na zile ambazo zilitolewa baadaye katika hekalu la Yehova, zilikuwa “kivuli” cha dhabihu kamilifu ya Yesu.​—Ebr. 10:1-10.

MTAZAMO UNAOFAA KUHUSU DHABIHU

6, 7. (a) Waisraeli walipaswa kukumbuka nini walipochagua matoleo ya dhabihu, na hilo lilikuwa kivuli cha nini? (b) Tunaweza kujiuliza maswali gani?

6 Takwa la msingi kuhusu mnyama yeyote ambaye angetolewa dhabihu kwa Yehova ni kwamba alipaswa kuwa “asiye na kasoro” yoyote, hakupaswa kuwa kipofu, mwenye jeraha, mlemavu, au mgonjwa. (Law. 22:20-22) Waisraeli walipomtolea Yehova matunda au nafaka, walipaswa kutoa ‘matunda ya kwanza,’ yaliyo “bora zaidi” ya mavuno yao. (Hes. 18:12, 29) Yehova hakukubali matoleo yasiyo bora. Takwa muhimu kuhusu dhabihu za wanyama lilionyesha kwamba dhabihu ya Yesu haingekuwa na doa wala dosari yoyote na kwamba Yehova angetoa dhabihu iliyo bora na yenye thamani kabisa kwake ili kuwakomboa wanadamu.​—1 Pet. 1:18, 19.

7 Ikiwa mtu aliyetoa dhabihu alithamini kikweli wema wote wa Yehova, bila shaka angefurahi kuchagua kitu bora zaidi alichokuwa nacho. Kila mtu alikuwa na uhuru wa kuchagua angemtolea Yehova dhabihu bora kadiri gani. Hata hivyo, mtu huyo alijua kwamba Mungu hangefurahia toleo lenye kasoro kwa sababu hilo lingeonyesha kwamba mtu huyo aliiona dhabihu hiyo kuwa ya kidesturi tu au hata mzigo. (Soma Malaki 1:6-8, 13.) Jambo hilo linapaswa kutufanya tutafakari kuhusu utumishi tunaomtolea Mungu: ‘Ninamtumikia Yehova nikiwa na mtazamo gani? Je, itafaa nichunguze ubora wa utumishi wangu na nia yangu ya kumtumikia Mungu?’

8, 9. Kwa nini tunapaswa kufikiria mtazamo ambao Waisraeli walionyesha walipokuwa wakitoa dhabihu zao?

8 Ikiwa Mwisraeli alitoa dhabihu yake kwa hiari ili kuonyesha shukrani kwa Yehova au alitoa toleo la kuteketezwa ili kupata kibali chake, basi inaelekea kwamba hangekuwa na tatizo la kuchagua mnyama anayefaa. Mwabudu huyo angefurahi kumpa Yehova kitu chake kilicho bora zaidi. Wakristo leo hawatoi dhabihu halisi ambazo ziliagizwa na Sheria ya Musa; hata hivyo, wanatoa dhabihu katika maana ya kwamba wanatumia wakati, nguvu, na mali zao ili kumtumikia Yehova. Mtume Paulo alisema kwamba “tangazo la hadharani” la tumaini la Kikristo na “kushiriki vitu pamoja na wengine” ni dhabihu ambazo zinampendeza Mungu. (Ebr. 13:15, 16) Mtazamo ambao watu wa Yehova wanaonyesha wanaposhiriki katika utendaji huo unafunua jinsi wanavyoshukuru na kuthamini vitu vyote ambavyo Mungu amewapa. Kwa hiyo, mitazamo na nia ya wale ambao wanashiriki katika utumishi wa Kikristo leo inalingana na ya wale ambao walitoa dhabihu za hiari katika nyakati za kale.

9 Hata hivyo, tunaweza kusema nini kuhusu agizo la Sheria ya Musa la kumtaka mtu atoe toleo la dhambi au toleo la hatia kwa sababu ya kosa fulani alilofanya? Je, unafikiri kwamba kwa kuwa watu walipaswa kutoa dhabihu hizo ingekuwa vigumu kwa Mwisraeli kuzitoa kwa hiari na kwa utayari? Je, huenda dhabihu kama hizo zilitolewa kwa kulazimishwa? (Law. 4:27, 28) Hazingetolewa kwa njia hiyo ikiwa mtu alitoa dhabihu hizo kwa unyoofu akitaka kudumisha uhusiano mzuri pamoja na Yehova.

10. Wakristo wanaweza kutoa “dhabihu” gani ili kurekebisha mahusiano yaliyoharibika?

10 Vivyo hivyo leo, huenda ukagundua kwamba umemkosea ndugu fulani kwa sababu ya kusema maneno bila kufikiri, bila kujua, au bila kujali. Au labda dhamiri yako inakusumbua kwa sababu umetenda jambo lisilofaa. Mtu yeyote ambaye anachukua kwa uzito utumishi wake kwa Yehova atafanya yote anayoweza ili kurekebisha kosa lake, sivyo? Hilo linaweza kumaanisha kumwomba msamaha kwa unyoofu mtu uliyemkosea au, inapohusu makosa mazito, kutafuta msaada wa waangalizi Wakristo wenye upendo. (Mt. 5:23, 24; Yak. 5:14, 15) Ni lazima tuchukue hatua fulani ili kurekebisha dhambi ambayo tumemtendea ndugu au Mungu. Hata hivyo, tunapotoa “dhabihu” kama hizo, tunakuwa tena na uhusiano mzuri pamoja na Yehova na ndugu yetu na tunapata dhamiri safi. Na hilo linatuhakikishia kwamba njia ya Yehova ndiyo njia bora.

11, 12. (a) Dhabihu za ushirika zilitia ndani nini? (b) Dhabihu za ushirika zinahusianaje na ibada safi leo?

11 Dhabihu fulani ambazo ziliagizwa chini ya Sheria ya Musa zilionwa kuwa matoleo ya ushirika. Dhabihu hizo zilionyesha kwamba mtu alikuwa na amani pamoja na Yehova. Mtu aliyetoa toleo kama hilo pamoja na familia yake wangekula nyama ya mnyama aliyetolewa dhabihu, labda katika moja ya vyumba vya kulia chakula katika hekalu. Kuhani aliyeshughulikia dhabihu hiyo alipokea sehemu ya nyama, pamoja na makuhani wengine waliotumika katika hekalu. (Law. 3:1; 7:31-33) Mwabudu alitoa dhabihu kwa sababu tu alitamani kufurahia uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Ilikuwa ni kana kwamba mwabudu huyo, familia yake, makuhani, na Yehova mwenyewe walikula pamoja mlo huo kwa shangwe na amani.

12 Je, kuna pendeleo kubwa zaidi kuliko pendeleo la kumwalika Yehova kwa njia ya mfano kwenye mlo na yeye kukubali mwaliko huo? Kwa kawaida, yule aliyemwalika mgeni alijitahidi kumpa mgeni mheshimiwa chakula kilicho bora zaidi. Mpango wa dhabihu za ushirika, ambao ni sehemu ya picha ya kweli katika Sheria, ulionyesha uhakika wa kwamba kupitia dhabihu bora zaidi ya Yesu, wanadamu wote wanaotamani kuwa na uhusiano wa karibu na wenye amani pamoja na Muumba wao wanaweza kuwa nao. Leo, tunaweza kufurahia ushirika na urafiki pamoja na Yehova tunapodhabihu kwa hiari mali na nguvu zetu katika utumishi wake.

MAONYO KUHUSU DHABIHU

13, 14. Kwa nini Yehova hakukubali dhabihu ambayo Mfalme Sauli alitaka kutoa?

13 Kwa kawaida, ili Yehova akubali dhabihu zilizoagizwa na Sheria ya Musa mtu alipaswa kuzitoa akiwa na hali nzuri ya moyo na mtazamo unaofaa. Hata hivyo, Biblia ina mifano mingi ya kuonya kuhusu dhabihu ambazo hazikukubaliwa na Mungu. Kwa nini alikataa dhabihu hizo? Acheni tuone mifano miwili.

14 Nabii Samweli alimwambia Mfalme Sauli kwamba wakati ulikuwa umefika wa Yehova kutekeleza hukumu juu ya Waamaleki. Kwa hiyo, Sauli alipaswa kuliangamiza taifa hilo adui pamoja na wanyama wa kufugwa. Hata hivyo, baada ya Sauli kushinda aliwaruhusu askari-jeshi wake wamhifadhi hai Agagi, mfalme wa Waamaleki. Pia, Sauli alihifadhi wanyama wazuri zaidi ili kumtolea Yehova dhabihu. (1 Sam. 15:2, 3, 21) Yehova alitendaje? Alimkataa Sauli kwa sababu alikosa kutii. (Soma 1 Samweli 15:22, 23.) Tunajifunza nini kutokana na hilo? Tunajifunza kwamba ili dhabihu ikubaliwe na Mungu, ni lazima mtu anayeitoa atii amri za Mungu.

15. Mwenendo mbaya wa Waisraeli fulani ambao walitoa dhabihu katika siku za Isaya ulionyesha nini?

15 Kitabu cha Isaya kina mfano mwingine kama huo. Katika siku za Isaya, Waisraeli walikuwa wakimtolea Yehova dhabihu kidesturi tu. Hata hivyo, tabia yao mbaya ilifanya dhabihu zao ziwe za bure. Yehova aliuliza hivi: “Dhabihu zenu nyingi zina faida gani kwangu? Nimetosheka na matoleo mazima ya kuteketezwa ya kondoo-dume na mafuta ya wanyama waliolishwa vizuri; nami sikupendezwa na damu ya ng’ombe-dume wachanga na wana-kondoo na mbuzi-dume. . . . Acheni kuleta ndani matoleo zaidi ya nafaka yasiyo na thamani. Uvumba—ni chukizo kwangu.” Tatizo lilikuwa nini? Mungu aliwaambia hivi: “Hata mjapotoa sala nyingi, mimi sisikilizi; mikono yenu imejaa umwagaji wa damu. Jiosheni; jisafisheni; ondoeni ubaya wa matendo yenu mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya.”​—Isa. 1:11-16.

16. Ni nini kinachoamua ikiwa Mungu atakubali dhabihu fulani?

16 Yehova hakupendezwa na dhabihu ambazo zilitolewa na watenda-dhambi wasiotubu. Hata hivyo, Mungu alikubali sala na matoleo ya watu waliojitahidi kwa moyo wote kuishi kupatana na amri zake. Picha ya Sheria iliwafundisha watu kama hao kwamba walikuwa watenda-dhambi na walihitaji msamaha. (Gal. 3:19) Kwa kufaa, kutambua jambo hilo kuliwachochea watu kujuta moyoni. Vivyo hivyo leo, tunapaswa kutambua kwamba tunahitaji dhabihu ya Kristo, ambayo kwa kweli inaweza kufunika dhambi zetu. Tukielewa na kuthamini jambo hilo, basi Yehova ‘atapendezwa’ na yote tunayomtolea katika utumishi wetu ulio wakfu.​—Soma Zaburi 51:17, 19.

ONYESHA IMANI KATIKA DHABIHU YA YESU!

17-19. (a) Ni njia gani inayofaa ya kumshukuru Yehova kwa sababu ya dhabihu ya fidia ya Yesu? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

17 Waisraeli waliona tu “kivuli” cha makusudi ya Mungu, lakini sisi tuna mambo halisi. (Ebr. 10:1) Sheria kuhusu dhabihu ziliwatia moyo Wayahudi wasitawishe mitazamo inayofaa ili kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu, yaani, kumwonyesha uthamini wa kutoka moyoni, kuwa na tamaa ya kutoa dhabihu iliyo bora zaidi, na kutambua uhitaji wa ukombozi. Maelezo yaliyo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yametusaidia kuelewa kwamba kupitia fidia, Yehova ataondoa madhara ya dhambi milele na kwamba hata sasa anaturuhusu kuwa na dhamiri njema mbele zake. Dhabihu ya fidia ya Yesu ni uandalizi mzuri ajabu!—Gal. 3:13; Ebr. 9:9, 14.

18 Bila shaka, ili tufaidike kutokana na dhabihu ya fidia haitoshi tu kuelewa mambo ya msingi kuhusu dhabihu hiyo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Sheria imekuwa mtunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo, ili tutangazwe kuwa waadilifu kutokana na imani.” (Gal. 3:24) Na imani hiyo haiwezi kuwa bila matendo. (Yak. 2:26) Hivyo, Paulo aliwatia moyo Wakristo wa karne ya kwanza ambao walikuwa na picha ya ujuzi iliyotegemea Sheria ya Musa watende kupatana na ujuzi huo. Kwa kufanya hivyo, mwenendo wao ungepatana na kanuni za Mungu ambazo walifundisha.​—Soma Waroma 2:21-23.

19 Ingawa Wakristo leo hawatakiwi kushika Sheria ya Musa, ni lazima watoe pia dhabihu ambazo Yehova anakubali. Katika makala inayofuata tutazungumzia jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

[Blabu katika ukurasa wa 17]

Mambo ya msingi ambayo Yehova anataka watumishi wake watimize hayabadiliki kamwe

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ni mnyama gani ambaye ungemtolea Yehova?

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wale wanaomtolea Yehova dhabihu zinazokubalika wanafurahia kibali chake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki