MAKALA YA 51
Unaweza Kupata Amani Unapokabili Hali Ngumu
“Mioyo yenu isitaabike wala kuogopa.”—YOH. 14:27.
WIMBO 112 Yehova, Mungu wa Amani
MUHTASARIa
1. “Amani ya Mungu” ni nini, na tunanufaikaje tunapokuwa nayo? (Wafilipi 4:6, 7)
KUNA amani ambayo watu katika ulimwengu huu hawaifahamu. Ni “amani ya Mungu,” utulivu unaotokana na kuwa na uhusiano wenye thamani pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Tunapokuwa na amani ya Mungu, tunajihisi salama. (Soma Wafilipi 4:6, 7.) Tunafurahia urafiki wa karibu pamoja na wengine wanaompenda. Na tunafurahia uhusiano wa karibu na wa kibinafsi pamoja na “Mungu wa amani.” (1 The. 5:23) Tunapomjua, kumtumaini, na kumtii Baba yetu, amani ya Mungu inaweza kuutuliza moyo wetu wenye mahangaiko tunapokabili hali ngumu.
2. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba inawezekana kupata amani ya Mungu?
2 Je, kweli tunaweza kupata amani ya Mungu tunapokabili hali ngumu, kama vile milipuko ya magonjwa, misiba ya asili, misukosuko ya kijamii, au mateso? Matatizo hayo yote yanaweza kufanya tuwe na hofu. Ingawa hivyo, Yesu aliwashauri hivi wafuasi wake: “Mioyo yenu isitaabike wala kuogopa.” (Yoh. 14:27) Inafurahisha kwamba ndugu na dada zetu wamefuata ushauri wa Yesu. Kwa msaada wa Yehova, wamefaulu kupata amani wanapokabili hali ngumu.
KUPATA AMANI WAKATI WA MILIPUKO YA MAGONJWA
3. Mlipuko au janga la ugonjwa linapotokea linawezaje kuathiri amani yetu?
3 Kunapokuwa na mlipuko au janga la ugonjwa fulani, hilo linaweza kuathiri kwa njia kubwa karibu kila sehemu ya maisha yetu. Wazia jinsi ugonjwa wa COVID-19 ulivyowaathiri wengi. Katika utafiti mmoja uliofanywa, zaidi ya nusu ya watu waliohojiwa walisema kwamba walikosa usingizi wakati wa janga hilo. Janga hilo lilichangia kuongezeka sana kwa visa vya tatizo la kuwa na wasiwasi kupita kiasi, kushuka moyo, kunywa pombe kupita kiasi, matumizi ya dawa za kulevya, visa vya ukatili nyumbani, na majaribio ya kujiua. Ikiwa kuna mlipuko wa ugonjwa katika sehemu unayoishi unawezaje kudhibiti hisia za wasiwasi na kufurahia amani ya Mungu?
4. Kwa nini kujua unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho kunatupatia amani?
4 Yesu alitabiri kwamba katika siku za mwisho kungekuwa na magonjwa yanayoenea upesi, “katika sehemu mbalimbali.” (Luka 21:11) Kujua jambo hilo kunatusaidiaje kuwa na amani? Hatushangazwi na milipuko ya magonjwa. Tunatambua kwamba mambo yanatokea kama Yesu alivyosema yangetokea. Basi, tuna sababu nzuri ya kufuata ushauri ambao Yesu aliwapa wale ambao wangeishi siku za mwisho: “Msishtuke.”—Mt. 24:6.
Kusikiliza rekodi za usomaji wa Biblia kunaweza kukusaidia upate amani ya akili wakati wa mlipuko wa ugonjwa (Tazama fungu la 5)
5. (a) Kulingana na Wafilipi 4:8, 9, tunapaswa kusali kuhusu nini tunapokabiliana na mlipuko wa ugonjwa? (b) Kusikiliza rekodi za usomaji wa Biblia kunawezaje kukunufaisha?
5 Kunapokuwa na mlipuko wa ugonjwa tunaweza kuwa na wasiwasi na kuogopa. Ilikuwa hivyo kwa dada anayeitwa Desi.b Baada ya mjomba, binamu, na daktari wake kufa kwa sababu ya ugonjwa wa COVID-19, alikuwa na wasiwasi kwamba angepata virusi hivyo na kumwambukiza mama yake aliyezeeka. Kwa sababu ya janga hilo, pia alikuwa na wasiwasi kwamba angepoteza kazi yake na hivyo hakujua jinsi ambavyo angegharamia chakula na nyumba. Mambo hayo yalimhangaisha sana hivi kwamba alikosa usingizi. Lakini Desi alipata tena amani. Jinsi gani? Alisali kihususa kwamba Yehova amsaidie awe mtulivu na afikirie mambo yanayofaa. (Soma Wafilipi 4:8, 9.) Alimsikiliza Yehova “akizungumza” naye kupitia rekodi za usomaji wa Biblia. Anasema hivi: “Sauti tulivu za wasomaji zilipunguza mahangaiko yangu na kunikumbusha kuhusu rehema ya Yehova.”—Zab. 94:19.
6. Funzo la kibinafsi na mikutano itakusaidiaje?
6 Bila shaka, mlipuko wa ugonjwa unaweza kuvuruga baadhi ya mambo katika ratiba yako. Lakini usiruhusu uvuruge ratiba yako ya funzo la kibinafsi na kuhudhuria mikutano. Masimulizi halisi ya maisha yanayopatikana katika machapisho na video zetu yatakukumbusha kwamba ndugu na dada zako wanaendelea kudumisha utimilifu licha ya kukabili changamoto kama hizo. (1 Pet. 5:9) Mikutano itakusaidia kujaza akili yako mawazo ya Kimaandiko yenye kujenga. Pia, utapata fursa ya kuwatia moyo wengine na kutiwa moyo. (Rom. 1:11, 12) Unapotafakari jinsi ambavyo Yehova amewategemeza waabudu wake walipokuwa wagonjwa, walipokuwa na woga, au kuhisi upweke imani yako itaimarishwa na utasadikishwa kwamba atakutegemeza pia.
7. Unajifunza somo gani kutokana na mtume Yohana?
7 Jitahidi kuwasiliana na ndugu na dada zako. Kunapokuwa na mlipuko wa ugonjwa huenda tukahitaji kudumisha umbali unaofaa kutoka kwa wengine hata tunapokuwa na waabudu wenzetu. Katika pindi kama hizo, huenda ukahisi kama alivyohisi mtume Yohana. Alitamani kumwona rafiki yake Gayo uso kwa uso. (3 Yoh. 13, 14) Hata hivyo, Yohana alitambua kwamba kwa muda fulani hangeweza kumwona Gayo. Basi, Yohana alifanya jambo aliloweza, alimwandikia Gayo barua. Ikiwa haiwezekani sikuzote kwako kuwatembelea ndugu na dada zako uso kwa uso, jitahidi kuwasiliana nao kupitia simu, kwa njia ya video, au ujumbe wa kielektroni. Ukidumisha mawasiliano mazuri pamoja na Wakristo wenzako utahisi ukiwa salama zaidi na mwenye amani. Wasiliana na wazee hasa ikiwa una mahangaiko, na ukubali msaada wao wanapokutia moyo kwa upendo.—Isa. 32:1, 2.
KUPATA AMANI WAKATI WA MISIBA YA ASILI
8. Msiba unawezaje kuvuruga amani yako?
8 Ikiwa umewahi kukabiliana na mafuriko, tetemeko la ardhi, au moto, huenda uliendelea kuwa na hisia nyingi za wasiwasi muda mrefu baada ya msiba huo. Ikiwa uliwapoteza wapendwa wako, au mali zako ziliharibiwa, huenda ulihisi majonzi, kukata tamaa, au hata hasira. Hilo halimaanishi kwamba unapenda vitu vya kimwili au huna imani. Ulipitia hali ngumu, na huenda wengine wakatarajia kwamba utatenda kwa njia isiyofaa. (Ayu. 1:11) Lakini licha ya hali hizo ngumu unaweza kupata amani. Jinsi gani?
9. Yesu alisema nini ili kututayarisha kukabiliana na misiba?
9 Kumbuka unabii ambao Yesu alitoa. Tofauti na watu fulani ulimwenguni ambao hawawazii kwamba watawahi kukabiliana na msiba wa asili kibinafsi, sisi tunatarajia kwamba misiba ya asili itaongezeka, na baadhi ya misiba hiyo inaweza kutuathiri. Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba kungekuwa na “matetemeko makubwa ya ardhi” na misiba mingine ambayo ingetokea kabla ya mwisho kuja. (Luka 21:11) Pia, alitoa unabii kwamba kungekuwa na “kuongezeka kwa uasi sheria,” jambo linaloonekana kupitia uhalifu, ukatili, na mashambulizi ya kigaidi. (Mt. 24:12) Yesu hakusema kamwe kwamba misiba hiyo ingewapata tu wale ambao hawana kibali cha Yehova. Kwa kweli, watumishi wengi waaminifu wa Yehova wamepatwa na misiba. (Isa. 57:1; 2 Kor. 11:25) Huenda Yehova asitulinde kimuujiza ili tusipatwe na misiba, lakini atatupatia chochote tunachohitaji ili tuendelee kuwa watulivu na wenye amani.
10. Kwa nini kujitayarisha sasa kwa ajili ya misiba ya asili kunaonyesha kwamba tuna imani? (Methali 22:3)
10 Itakuwa rahisi kwetu kuendelea kuwa watulivu hali ya dharura inapotokea ikiwa tumefanya mipango mapema ya jinsi tutakavyotenda. Lakini, je, kujitayarisha kunaonyesha kwamba hatuna imani katika Yehova? Hapana. Kwa kweli, kujitayarisha kwa ajili ya misiba ya asili kunaonyesha kwamba tuna imani katika uwezo wake wa kututunza. Jinsi gani? Neno la Mungu linatushauri tujitayarishe kwa ajili ya misiba inayoweza kutokea. (Soma Methali 22:3.) Na kupitia makala katika magazeti yetu, mikutano ya kutaniko, na matangazo yanayotolewa kwa wakati unaofaa, tengenezo la Mungu limetuhimiza tena na tena tujitayarishe kwa ajili ya hali za dharura.c Je, tunamtumaini Yehova? Ikiwa tunamtumaini, tutafuata ushauri huo sasa—kabla ya msiba kutokea.
Matayarisho ya mapema yanaweza kukusaidia uokoke msiba wa asili (Tazama fungu la 11)d
11. Unajifunza nini kutokana na mfano wa Margaret?
11 Fikiria jambo ambalo dada anayeitwa Margaret alijionea. Aliagizwa aondoke baada ya moto kutokea kwenye kichaka karibu na eneo alilokuwa anaishi. Kwa kuwa watu wengi walikuwa wakikimbia, barabara zilikuwa na msongamano mkubwa wa magari na hayakuwa yakisonga. Hewa ilijaa moshi mweusi, na Margaret alilazimika kukaa ndani ya gari lake kwa muda fulani. Hata hivyo, aliokoka kwa sababu alikuwa amejitayarisha. Alikuwa amebeba ramani kwenye mkoba wake na hivyo alipata barabara nyingine ya kutokea. Hata alikuwa ameendesha gari katika barabara hiyo mapema ili aweze kuifuata kwa urahisi wakati wa dharura. Kwa sababu ya matayarisho aliyofanya, Margaret aliokoka tukio hilo.
12. Kwa nini tunafuata miongozo ya usalama tunayopewa?
12 Ili kutulinda na kudumisha utaratibu, huenda wenye mamlaka wakatuomba tutii amri ya kubaki ndani, kuondoka, au kuchukua hatua nyingine hususa. Baadhi ya watu husita kutii au huahirisha kuondoka kwa sababu hawataki kuacha mali zao. Wakristo hutendaje? Biblia inatuambia hivi: “Kwa ajili ya Bwana jitiisheni wenyewe kwa kila kitu kilichofanywa na binadamu, iwe ni kwa mfalme akiwa mkubwa au kwa magavana wakiwa kama wametumwa naye.” (1 Pet. 2:13, 14) Pia, tengenezo la Mungu hutupatia mwongozo ili kutulinda. Tunakumbushwa kwa ukawaida tuwapatie wazee habari zetu za mawasiliano za karibuni ili waweze kuwasiliana nasi wakati wa dharura. Je, wewe umefanya hivyo? Huenda pia tukapata mwongozo kuhusu kubaki nyumbani, kuondoka, jinsi ya kupokea misaada, au jinsi na wakati wa kuwasaidia wengine. Ikiwa tutakosa kutii, tunaweza kuhatarisha uhai wetu na uhai wa wazee. Kumbuka kwamba wanaume hao waaminifu wanaendelea kutulinda. (Ebr. 13:17) Margaret alisema hivi: “Ninaamini kabisa kwamba kufuata mwongozo wa wazee na tengenezo kuliokoa uhai wangu.”
13. Ni nini ambacho kimewaletea shangwe na amani Wakristo wengi ambao wamelazimika kuhama?
13 Ndugu na dada wengi ambao wamelazimika kuhama kwa sababu ya misiba ya asili au vita au misukosuko ya kijamii wamejitahidi kuzoea hali zao mpya na wameanza mara moja kushiriki katika utendaji wa kitheokrasi. Kama Wakristo wa mapema ambao walitawanyika kwa sababu ya mateso, wanaendelea “[kutangaza] habari njema ya lile neno.” (Mdo. 8:4) Kuhubiri huwasaidia kukazia fikira Ufalme badala ya hali zao ngumu. Matokeo ni kwamba wamedumisha shangwe na amani yao.
KUPATA AMANI TUNAPOTESWA
14. Mateso yanawezaje kuvuruga amani yetu?
14 Mateso yanaweza kufanya tupoteze mambo mengi yanayotuletea amani. Tunafurahi na kuridhika tunapokutana kwa uhuru, tunapohubiri hadharani, na kuendelea na shughuli zetu za kila siku bila kuogopa kwamba tutakamatwa. Ikiwa tutapoteza uhuru huo, huenda tukawa na wasiwasi tukiogopa jambo litakalotupata. Ni jambo la kawaida kuhisi hivyo. Ingawa hivyo, ni lazima tuwe waangalifu. Yesu alisema kwamba mateso yangeweza kufanya wafuasi wake wakwazike. (Yoh. 16:1, 2) Basi, tunawezaje kudumisha amani yetu tunapoteswa?
15. Kwa nini hatupaswi kuogopa mateso? (Yohana 15:20; 16:33)
15 Neno la Mungu linatuambia hivi: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Tim. 3:12) Ilikuwa vigumu kwa ndugu anayeitwa Andrei kukubaliana na hilo baada ya kazi yetu kupigwa marufuku katika nchi anayoishi. Alijiambia hivi: ‘Kuna Mashahidi wengi sana huku. Wenye mamlaka wanawezaje kutukamata sisi sote?’ Lakini badala ya kupata amani, njia hiyo ya kufikiri ilimletea Andrei mahangaiko muda wote. Ndugu wengine waliacha mambo mikononi mwa Yehova, na hawakujaribu kujisadikishia kwamba wangeweza kuepuka kukamatwa. Walijua kwamba huenda wangekamatwa, lakini hawakuwa na wasiwasi mwingi kama Andrei. Basi, Andrei aliamua kuwa na mtazamo kama wao na akamtegemea kabisa Mungu. Baada ya muda alipata amani, na sasa anapata shangwe licha ya kukabili changamoto. Inaweza kuwa hivyo pia kwetu. Ingawa Yesu alituambia kwamba tutarajie mateso, pia alituhakikishia kwamba tunaweza kuendelea kuwa waaminifu.—Soma Yohana 15:20; 16:33.
16. Tunahitaji kutii mwongozo gani tunapokabili mateso?
16 Kazi yetu inapopigwa marufuku au kuwekewa vizuizi vikubwa, huenda tukapata maagizo kutoka ofisi ya tawi au wazee wa kutaniko. Maagizo hayo yamekusudiwa kutulinda, kuhakikisha kwamba tunaendelea kupokea chakula cha kiroho, na kutusaidia tuendelee kuhubiri kwa kadiri inayowezekana. Jitahidi kabisa kutii mwongozo unaopokea, hata kama huelewi kikamili kwa nini unatolewa. (Yak. 3:17) Pia, usifunue habari kuhusu akina ndugu na dada au kuhusu utendaji wa kutaniko kwa wale ambao hawastahili kuzipata.—Mhu. 3:7.
Ni nini kitakachokusaidia uwe na amani hata unapokabili hali ngumu? (Tazama fungu la 17)e
17. Kama mitume katika karne ya kwanza, tumeazimia kufanya nini?
17 Mojawapo ya sababu kuu inayofanya Shetani apigane vita dhidi ya watu wa Mungu ni kwamba wana “kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufu. 12:17) Usiruhusu Shetani na ulimwengu wake ukuogopeshe. Kuhubiri na kufundisha licha ya upinzani, hutuletea shangwe na amani. Katika karne ya kwanza wakati Wayahudi wenye mamlaka walipowaamuru mitume waache kuhubiri, wanaume hao waaminifu walichagua kumtii Mungu. Waliendelea kuhubiri, na kazi hiyo iliwaletea furaha. (Mdo. 5:27-29, 41, 42) Bila shaka, kazi yetu inapowekewa vizuizi, tunapaswa kuhubiri kwa tahadhari. (Mt. 10:16) Lakini ikiwa tutafanya yote tunayoweza, tutapata amani inayotokana na kumfurahisha Yehova na kushiriki kutangaza ujumbe unaookoa uhai.
“MUNGU WA AMANI ATAKUWA PAMOJA NANYI”
18. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu Chanzo cha amani ya kweli?
18 Uwe na hakika kwamba hata unapokabili hali ngumu sana, unaweza kuwa na amani. Katika pindi kama hizo, tunapaswa kukumbuka kwamba amani tunayohitaji ni amani ya Mungu, yaani, amani ambayo ni Yehova peke yake anayeweza kutoa. Mtegemee unapokabiliana na mlipuko wa ugonjwa, misiba ya asili, au mateso. Kaa karibu na tengenezo lake, kazia fikira hali nzuri ajabu za wakati ujao unazotazamia. Ukifanya hivyo, “Mungu wa amani atakuwa pamoja [nawe].” (Flp. 4:9) Katika makala inayofuata, tutachunguza jinsi tunavyoweza kuwasaidia Wakristo wenzetu ambao wanakabiliana na dhiki wapate amani ya Mungu.
WIMBO 38 Atakupa Nguvu
a Yehova anaahidi kuwapatia amani wale wanaompenda. Ni amani gani ambayo Mungu anatupatia, na tunawezaje kuipata? Kuwa na “amani ya Mungu” kunatusaidiaje tunapokabili milipuko ya magonjwa, misiba ya asili, au mateso? Makala hii itajibu maswali hayo.
b Baadhi ya majina yamebadilishwa.
c Tazama makala “Majanga Yanapotokea—Unachoweza Kufanya Ili Uokoke” katika gazeti la Amkeni! Na. 5 2017.
d MAELEZO YA PICHA: Dada alijitayarisha mapema kuondoka nyumbani kwake.
e MAELEZO YA PICHA: Ndugu anayeishi mahali ambapo kazi yetu imewekewa vizuizi anaendelea kuhubiri kwa tahadhari.