Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w23 Novemba kur. 2-7
  • Jinsi Yehova Anavyotupatia Uhakikisho wa Ahadi Yake ya Paradiso

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Yehova Anavyotupatia Uhakikisho wa Ahadi Yake ya Paradiso
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YEHOVA AMETUAHIDI NINI?
  • YEHOVA ANATUHAKIKISHIA KWAMBA AHADI YAKE ITATIMIA
  • “TAZAMA! NINAFANYA VITU VYOTE KUWA VIPYA”
  • “MANENO HAYA NI YA UAMINIFU NA YA KWELI. . . . YAMETIMIA!”
  • “MIMI NDIYE ALFA NA OMEGA”
  • JINSI TUNAVYOIMARISHA UHAKIKA WETU KATIKA AHADI YA YEHOVA YA PARADISO
  • “Alfa na Omega” Ni Nani au Ni Nini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Alpha na Omega
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Mbingu Mpya na Dunia Mpya
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Kusudi la Mungu kwa Wanadamu Ni Nini?
    Biblia Inatufundisha Nini?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
w23 Novemba kur. 2-7

MAKALA YA 46

Jinsi Yehova Anavyotupatia Uhakikisho wa Ahadi Yake ya Paradiso

“Kila mtu anayejitafutia baraka duniani abarikiwe na Mungu wa kweli.”—ISA. 65:16.

WIMBO 3 Tumaini, Nguvu, na Uhakika Wetu

MUHTASARIa

1. Ni ujumbe gani ambao nabii Isaya aliwapatia Waisraeli wenzake?

NABII Isaya anamfafanua Yehova kuwa “Mungu wa kweli.” Neno linalotafsiri “kweli” kihalisi linamaanisha “amina.” (Isa. 65:​16, maelezo ya chini) Neno “amina” linamaanisha “na iwe hivyo,” au “bila shaka.” Neno “amina” linapotumiwa katika Biblia kumhusu Yehova au Yesu, ni uhakikisho wa kwamba jambo fulani ni la kweli. Hivyo, ujumbe wa Isaya kwa Waisraeli wenzake ulikuwa wazi: Jambo ambalo Yehova anatabiri sikuzote linatumainika. Yehova amethibitisha jambo hilo kwa kutimiza ahadi zake zote.

2. Kwa nini tunaweza kutumaini ahadi za Yehova kuhusu wakati wetu ujao, na tutachunguza maswali gani?

2 Je, sisi pia tunaweza kutumaini kwamba ahadi za Yehova za wakati ujao zitatimia? Karibu miaka 800 baada ya wakati wa Isaya, mtume Paulo alifafanua kwa nini ahadi za Yehova sikuzote zinatumainika. Paulo alisema: “Mungu hawezi kamwe kusema uwongo.” (Ebr. 6:18) Kama tu ambavyo chemchemi haiwezi kutoa maji matamu na maji ya chumvi kwa wakati mmoja, ndivyo ambavyo Yehova, Chanzo cha kweli, hawezi kusema uwongo. Hivyo, tunaweza kutumaini kabisa kila kitu ambacho Yehova anasema, kutia ndani ahadi zake za wakati ujao. Katika makala hii, tutachunguza maswali yafuatayo: Yehova ameahidi kutupatia nini wakati ujao? Na Yehova ametupatia uhakikisho gani kwamba ahadi yake itatimia?

YEHOVA AMETUAHIDI NINI?

3. (a) Ni ahadi gani inayowavutia watumishi wa Mungu? (Ufunuo 21:​3, 4) (b) Baadhi ya watu huitikiaje tunapowaambia kuhusu ahadi hiyo?

3 Ahadi tutakayozungumzia inawavutia watumishi wa Mungu ulimwenguni pote. (Soma Ufunuo 21:​3, 4.) Yehova ameahidi wakati ambapo “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” Sisi hutumia ujumbe huo wa Biblia unaogusa moyo, tunapowahubiria wengine kuhusu maisha katika Paradiso. Baadhi ya watu huitikiaje tunapowaambia kuhusu ahadi hiyo? Huenda wakasema, “Ahadi hii haiwezi kutimia.”

4. (a) Ni jambo gani ambalo Yehova alijua lingetokea wakati wetu, na alitabiri nini? (b) Mbali na kutoa tu ahadi hiyo, Yehova alifanya nini kingine?

4 Bila shaka, Yehova alipomwongoza mtume Yohana kuandika ahadi hii kuhusu maisha katika Paradiso, alijua kwamba leo tungeshiriki tumaini hilo tunapowahubiria wengine kuhusu ujumbe wa Ufalme. Pia, Yehova alitabiri kwamba ingekuwa vigumu kwa wengi kuamini ahadi hiyo ya “mambo mapya.” (Isa. 42:9; 60:2; 2 Kor. 4:​3, 4) Hivyo, tunawezaje kuwahakikishia wengine—na sisi wenyewe—kwamba baraka zinazotajwa katika Ufunuo 21:​3, 4 zitatimia? Yehova hakutoa tu ahadi hiyo inayogusa moyo, bali pia alitoa sababu zinazotuhakikishia kwamba atatimiza ahadi hiyo. Alitoa sababu gani?

YEHOVA ANATUHAKIKISHIA KWAMBA AHADI YAKE ITATIMIA

5. Tuna sababu gani za kutumaini ahadi ya Mungu ya Paradiso, na tunaweza kuzipata wapi sababu hizo?

5 Mistari inayofuata katika Ufunuo sura ya 21 inaonyesha sababu za kutumaini ahadi ya Yehova ya Paradiso. Mistari hiyo inasema hivi: “Yule aliyeketi kwenye kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’ Pia anasema: ‘Andika, kwa maana maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’ Naye akaniambia: ‘Yametimia! Mimi ndiye Alfa na Omega, mwanzo na mwisho.’”—Ufu. 21:​5, 6a.

6. Kwa nini uhakikisho ulio kwenye Ufunuo 21:​5, 6 unaimarisha tumaini letu katika ahadi ya Mungu?

6 Kwa nini mistari hiyo ya Biblia inaimarisha tumaini letu katika ahadi ya Mungu? Kitabu Upeo wa Ufunuo kinasema hivi kuhusu mistari hiyo: “Ni kana kwamba Yehova mwenyewe alikuwa akitia saini ya dhamana au [hati-miliki] kwenye baraka hizi za wakati ujao kwa ajili ya aina ya binadamu yenye uaminifu.”b Ahadi ya Mungu inapatikana kwenye Ufunuo 21:​3, 4. Hata hivyo, kwenye mstari wa 5 na 6, tunaona saini ya Yehova kwa njia ya mfano, inayotuhakikishia kwamba ahadi hiyo itatimia. Sasa tutachunguza kwa undani maneno aliyotumia Yehova alipotoa uhakikisho huo. 

7. Kwa nini maneno ya mwanzoni mwa mstari wa 5 ni ya pekee, na kwa nini jambo hilo ni muhimu?

7 Mstari wa 5 unaanza kwa kusema hivi: “Yule aliyeketi kwenye kiti cha ufalme akasema.” (Ufu. 21:5a) Maneno hayo ni ya pekee kwa sababu ni mojawapo ya sehemu tatu katika kitabu cha Ufunuo ambapo Yehova mwenyewe anazungumza. Kwa hiyo, uhakikisho huo unatolewa, si na malaika mwenye nguvu, au hata Yesu aliyefufuliwa, bali na Yehova mwenyewe! Jambo hilo linathibitisha kwamba tunaweza kutumaini maneno ya Yehova yanayofuata. Kwa nini? Kwa sababu Yehova ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Hivyo, maneno tunayosoma kwenye Ufunuo 21:​5, 6 hakika yatatimia.

“TAZAMA! NINAFANYA VITU VYOTE KUWA VIPYA”

8. Yehova anasema nini ili kukazia kwamba ahadi yake itatimia? (Isaya 46:10)

8 Sasa, tuchunguze neno “Tazama!” (Ufu. 21:5) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “tazama!” limetumiwa mara kwa mara katika kitabu cha Ufunuo. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba alama ya mshangao inatumiwa kama “njia ya kumfanya msomaji akazie fikira maneno yanayofuata.” Ni maneno gani yanayofuata baada ya alama ya mshangao? Mungu anasema: “Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” Ni kweli kwamba Yehova anazungumza kuhusu mabadiliko ya wakati ujao, lakini kwake, ahadi hiyo ni hakika na itatimia, hivi kwamba anayazungumzia mabadiliko hayo kana kwamba tayari yanatukia.—Soma Isaya 46:10.

9. (a) Maneno “ninafanya vitu vyote kuwa vipya” yanarejelea mambo gani mawili ambayo Yehova atafanya? (b) Ni nini kitakachoipata “mbingu” na “dunia” ya sasa?

9 Sasa tuchunguze maneno yanayofuata kwenye Ufunuo 21:5: “Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” Katika sura hii ya Biblia, maneno hayo yanarejelea mambo mawili ambayo Yehova atafanya—atabadili na kurudisha upya. Kwanza, Yehova atabadili nini? Kwenye Ufunuo 21:​1, tunasoma hivi: “Mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali.” “Mbingu ya kwanza” inarejelea serikali za kisiasa zinazoongozwa na Shetani na roho wake waovu. (Mt. 4:​8, 9; 1 Yoh. 5:19) Katika Biblia, neno “dunia” linaweza kurejelea watu wanaoishi duniani. (Mwa. 11:1; Zab. 96:1) Hivyo, “dunia ya kwanza” inarejelea jamii ya wanadamu waovu leo. Si kwamba Yehova atarekebisha au kuboresha “mbingu” na “dunia” ya kwanza; badala yake, ataziondoa kabisa kwa kuzibadili. Ataondoa mbingu na dunia ya sasa na kuleta “mbingu mpya na dunia mpya”—yaani, serikali mpya na jamii mpya ya wanadamu.

10. Yehova atafanya vitu gani viwe vipya?

10 Ni katika njia gani nyingine Yehova atafanya vitu vyote kuwa vipya? (Ufu. 21:5) Yehova ataifanya dunia kuwa mpya na atawafanya wanadamu kuwa wapya kwa kuwarudishia hali yao ya ukamilifu. Kama Isaya alivyotabiri, dunia nzima itafanywa kuwa bustani maridadi—kama ilivyokuwa bustani ya Edeni. Kila mmoja wetu atafanywa kuwa mpya, kwa kuponywa kikamili. Vilema, vipofu, na viziwi wataponywa, na hata waliokufa watarudishiwa uhai.—Isa. 25:8; 35:​1-7.

“MANENO HAYA NI YA UAMINIFU NA YA KWELI. . . . YAMETIMIA!”

11. Yehova alimpa Yohana amri gani, na alitoa sababu gani?

11 Mungu ametoa uhakikisho gani mwingine? Yehova alimwambia Yohana hivi: “Andika, kwa maana maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.” (Ufu. 21:5) Yehova hakutoa tu amri ya ‘kuandika.’ Lakini pia alitoa sababu ya kufanya hivyo. Alisema: “Kwa maana maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli”—yaani, maneno ya Mungu ni sahihi na yanategemeka. Tunashukuru kwamba Yohana alitii amri hiyo ya ‘kuandika.’ Hivyo, tunaweza kusoma kuhusu ahadi ya Mungu ya Paradiso na kutafakari baraka nyingi nzuri tunazotarajia.

12. Kwa nini Yehova ana haki ya kusema: “Yametimia!”

12 Mungu anasema jambo gani lingine? “Yametimia!” (Ufu. 21:6) Sasa, Yehova anazungumza kana kwamba mambo aliyotaja kuhusu Paradiso aliyoahidi, tayari yametokea. Na ana haki ya kuzungumza hivyo kwa sababu hakuna kinachoweza kumzuia kutimiza kusudi lake. Kisha, Yehova anasema jambo lingine ambalo linatuhakikishia kwamba ahadi yake hakika itatimia. Ni jambo gani hilo?

“MIMI NDIYE ALFA NA OMEGA”

13. Kwa nini Yehova alisema: “Mimi ndiye Alfa na Omega”?

13 Kama ilivyotajwa mwanzoni, Yehova mwenyewe alizungumza mara tatu katika maono aliyopata Yohana. (Ufu. 1:8; 21:​5, 6; 22:13) Na kila alipofanya hivyo, Yehova alisema maneno haya: “Mimi ndiye Alfa na Omega.” Herufi alfa ndiyo ya kwanza katika alfabeti ya Kigiriki, na herufi omega ndiyo ya mwisho. Kwa kusema kwamba yeye ndiye “Alfa na Omega,” Yehova anatusaidia kuelewa kwamba anapoanza kufanya jambo fulani, lazima alikamilishe kwa mafanikio.

Mkusanyo wa picha: Kusudi la Yehova linavyotimizwa. 1. “Alfa.” Adamu na Hawa wakiwa katika bustani ya Edeni. 2. Madhara ya uasi, yanaonyeshwa kupitia Shetani akiwa malaika mwovu, Adamu na Hawa wakiwa wazee, mnara wa Babeli, makaburi, wanajeshi, kifaru, ndege za vita, uchafuzi unaotokana na viwanda, na waandamanaji. Wakati huohuo, picha mbili zinaonyesha kusudi la Yehova likiendelea kutimia: Yesu akiwa katika mti wa mateso, kuonyesha mpango wa fidia, na watumishi wa zamani wa Yehova na wa siku zetu, kuonyesha wazao waadilifu wa Adamu na Hawa. 3. “Omega.” Watu wakifanya kazi pamoja na kufurahia katika Paradiso.

Yehova anapoanza kufanya jambo fulani, yeye hulikamilisha (Tazama fungu la 14, 17)

14. (a) Toa mfano wa wakati ambapo ni kana kwamba Yehova alisema “Alfa” na wakati atakaposema “Omega.” (b) Ni uhakikisho gani unaopatikana kwenye Mwanzo 2:​1-3?

14 Baada ya kuwaumba Adamu na Hawa, Yehova aliwaeleza kusudi lake kwa ajili ya wanadamu na dunia. Biblia inasema hivi: “Mungu akawabariki, na Mungu akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, muijaze dunia na kuitiisha.’” (Mwa. 1:28) Wakati huo ni kama Yehova alikuwa akisema “Alfa.” Alieleza waziwazi kusudi lake kwamba wakati utafika ambapo dunia itajaa wazao wa Adamu na Hawa walio wakamilifu na watiifu, ambao wataigeuza dunia kuwa paradiso. Wakati huo ujao, kusudi lake litakapotimia, ni kana kwamba atasema “Omega.” Baada ya kukamilisha uumbaji wa “mbingu na dunia na kila kitu kilichomo,” Yehova alitoa uhakikisho huu. Unapatikana kwenye Mwanzo 2:​1-3. (Soma.) Yehova aliitangaza siku ya saba kuwa takatifu kwake. Hilo linamaanisha nini? Yehova alitoa uhakikisho kwamba atatimiza kusudi lake kwa ajili ya wanadamu na dunia. Lingetimizwa kikamili mwishoni mwa ile siku ya saba.

15. Kwa nini ilionekana ni kana kwamba Shetani alizuia kutimizwa kwa kusudi la Mungu kwa wanadamu?

15 Adamu na Hawa walipoasi, wakawa watenda dhambi na wakapitisha dhambi na kifo kwa wazao wao. (Rom. 5:12) Hivyo, huenda ilionekana kwamba Shetani alizuia kusudi la Mungu la kuijaza dunia wanadamu wakamilifu na watiifu. Ilionekana kana kwamba Shetani amefanya isiwezekane kamwe kwa Yehova kusema “Omega.” Huenda Shetani alifikiri kwamba Yehova amebaki na njia chache za kushughulikia jambo hilo. Njia moja ilikuwa kuwaua Adamu na Hawa na kuwaumba wenzi wa ndoa wengine wakamilifu ili watimize kusudi Lake kwa ajili ya wanadamu. Lakini ikiwa Mungu angefanya hivyo, Ibilisi angedai kwamba Mungu ni mwongo. Kwa nini? Kwa sababu, kama ilivyoandikwa kwenye Mwanzo 1:​28, Yehova aliwaambia Adamu na Hawa kwamba wazao wao wangeijaza dunia.

16. Kwa nini huenda Shetani angefikiri kuwa angeweza kudai kwamba Yehova ameshindwa?

16 Ni njia gani nyingine ambayo huenda Shetani alifikiri Yehova angechagua? Inawezekana Shetani alifikiri kwamba Yehova angewaruhusu Adamu na Hawa wazae watoto wasio wakamilifu ambao hawangeweza kamwe kuufikia ukamilifu. (Mhu. 7:20; Rom. 3:23) Ikiwa ingekuwa hivyo, bila shaka Ibilisi angedai kwamba Yehova ameshindwa. Kwa nini? Kwa sababu njia hiyo haingetimiza kusudi la Mungu, yaani, kuijaza dunia paradiso wazao wa Adamu na Hawa walio wakamilifu na watiifu.

17. Yehova alisuluhishaje uasi wa Shetani na wanadamu wa kwanza, na matokeo ya mwisho yatakuwaje? (Tazama pia picha.)

17 Yehova alisuluhisha uasi wa Shetani na wanadamu wa kwanza kwa njia ambayo Shetani hangeweza kuiwazia kamwe. (Zab. 92:5) Badala ya kuonekana kuwa mwongo, Yehova alithibitika kuwa msema kweli kwa kuwaruhusu Adamu na Hawa wapate watoto. Na badala ya kuonekana kuwa ameshindwa, Yehova alithibitika kuwa mshindi. Alihakikisha kusudi lake lingetimia kwa kuandaa “uzao” ambao ungewaokoa wazao watiifu wa Adamu na Hawa. (Mwa. 3:15; 22:18) Ni lazima Shetani alipigwa na butwaa alipotambua mpango wa fidia wa Yehova! Kwa nini? Kwa sababu ni mpango unaotegemea upendo usio na ubinafsi. (Mt. 20:28; Yoh. 3:16) Shetani hana sifa hiyo. Yeye ni mbinafsi. Hivyo, mpango wa fidia utafanya jambo gani liwezekane? Mwishoni mwa ile Miaka Elfu Moja ya Utawala wa Kristo, wazao watiifu wa Adamu na Hawa walio wakamilifu wataishi katika dunia paradiso—kama Yehova alivyokusudia mwanzoni. Wakati huo, ni kana kwamba Yehova atasema, “Omega.”

JINSI TUNAVYOIMARISHA UHAKIKA WETU KATIKA AHADI YA YEHOVA YA PARADISO

18. Mungu anatupatia uhakikisho kupitia mambo gani matatu? (Tazama pia sanduku “Sababu Tatu za Kutumaini Ahadi ya Yehova.”)

18 Kulingana na mambo tuliyojifunza, ni uhakikisho gani tunaoweza kushiriki na wale ambao wana shaka kwamba ahadi ya Mungu ya Paradiso itatimia? Kwanza, Yehova mwenyewe ndiye anayetoa ahadi hiyo. Kitabu cha Ufunuo kinasema: “Yule aliyeketi kwenye kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’” Yeye ana hekima, nguvu, na tamaa ya kutimiza ahadi yake. Pili, utimizo wa ahadi hiyo ni hakika kabisa, hivi kwamba kwa maoni ya Yehova tayari mambo hayo yametukia. Ndiyo sababu anasema: “Maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli. . . . Yametimia!” Tatu, Yehova anapoanza kufanya jambo, anahakikisha linakamilika kwa mafanikio, kama inavyothibitishwa na maneno haya: “Mimi ndiye Alfa na Omega.” Yehova atathibitisha kwamba Shetani ni mwongo na ameshindwa.

Sababu Tatu za Kutumaini Ahadi ya Yehova

Kiti cha ufalme kinachotoa mwangaza kinachomfananisha Yehova.
  • “Yule aliyeketi kwenye kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’”—Ufu. 21:5

Mtume Yohana akiandika kwenye kitabu cha kukunjwa.
  • “Pia anasema: ‘Andika, kwa maana maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli. . . . Yametimia!’”—Ufu. 21:​5, 6

Herufi za Kigiriki alfa na omega.
  • “Mimi ndiye Alfa na Omega.”—Ufu. 21:6

19. Unaweza kufanya nini watu wanapotilia shaka ahadi ya Mungu ya Paradiso?

19 Kumbuka, kila mara unapowahubiria watu mambo ambayo Yehova ametuambia ili kutuhakikishia kwamba ahadi yake itatimia, unaimarisha uhakika wako kwake. Hivyo, wakati mwingine utakapomsomea mtu ahadi yenye kugusa moyo kuhusu Paradiso, inayopatikana kwenye Ufunuo 21:​4, naye aseme, “Ahadi hii haiwezi kutimia,” unaweza kumwambia nini? Unaweza kusoma na kufafanua mstari wa 5 na wa 6. Mwonyeshe jinsi ambavyo Yehova ametoa uhakikisho wa ahadi yake, kwa kuitia saini yake mwenyewe kwa njia ya mfano.—Isa. 65:16.

UNGEJIBUJE?

  • Kwa nini ni jambo la muhimu kwamba Yehova mwenyewe ndiye aliyetoa ahadi ya Paradiso?

  • Mungu amesema maneno gani ili kutuhakikishia kwamba ahadi yake itatimia?

  • Tunawezaje kuimarisha uhakika wetu katika ahadi ya Mungu?

WIMBO 145 Ahadi ya Mungu ya Paradiso

a Katika makala hii, tutachunguza uhakikisho ambao Yehova anatupatia kwamba ahadi yake ya Paradiso itatimia. Kila mara tunapowahubiria wengine kuhusu uhakikisho huo, tunaimarisha uhakika wetu katika ahadi za Yehova.

b Tazama Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! uku. 303-304, fu. 8-9.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki