Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • w13 15/8 uku. 10-14
  • Usimukasirikie Yehova Hata Kidogo

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Usimukasirikie Yehova Hata Kidogo
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • NI MAMBO GANI YANAYOWEZA KUTUFANYA ‘TUMUKASIRIKIE’ YEHOVA?
  • NAMNA TUNAVYOWEZA KUEPUKA ‘KUMUKASIRIKIA’ YEHOVA
  • LINDA UHUSIANO WAKO WA MAANA SANA PAMOJA NA YEHOVA
  • Yehova Anakupenda Sana!
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2021
  • Unatumainia Njia ya Yehova ya Kufanya Mambo?
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2022
  • Mungu Ni Nani?
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • ‘Umutegemee Yehova na Ufanye Mema’
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2017
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
w13 15/8 uku. 10-14
[Picha katika ukurasa wa 10]

Usimukasirikie Yehova Hata Kidogo

“Upumbafu wa mutu unapotosha njia yake, na moyo wake unakasirika juu ya [Yehova].”​—MET. 19:3, La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo

UNGEJIBU NAMNA GANI?

  • Ni mambo gani yanayoweza kutufanya tuanze ‘kumukasirikia’ Yehova?

  • Ni mambo matano gani yanayoweza kutusaidia tuepuke kumukasirikia Mungu?

  • Tunapaswa kukumbuka nini tunapopambana na matatizo makali?

1, 2. Kwa nini hatupaswe kumulaumu Yehova kwa sababu ya matatizo yetu? Toa mufano.

TUSEME kwamba wewe ni mwanaume ambaye amefanya miaka mingi katika ndoa yenye furaha. Lakini siku moja unaporudi nyumbani, unakuta muvurugo katika nyumba yako. Kabati, meza na viti vyote vimevunjika, sahani, vikombe, na vyungu vimepondekana. Nyumba yako nzuri si mahali pazuri tena pa kuishi. Unapoingia katika nyumba yako, je, utauliza kwa hasira, “Sababu gani bibi yangu alifanya hivi?” Ao labda utauliza, “Ni nani aliyefanya hivi?” Bila shaka, utafikiria mara moja ulizo la pili. Sababu gani? Kwa sababu unajua kwamba bibi yako mupendwa hawezi kufanya matendo hayo mabaya ya kuharibu vitu kimakusudi.

2 Leo, makao ya wanadamu yamejaa uhalifu, mwenendo muchafu na uchafuzi wa vitu kama vile maji na hewa. Sisi wanafunzi wa Biblia, tunajua kwamba si Yehova anayeleta matatizo hayo yote. Yehova aliumba dunia ili iwe paradiso nzuri. (Mwa. 2:8, 15) Yehova ni Mungu mwenye upendo. (1 Yoh. 4:8) Kujifunza Biblia kumetusaidia tujue yule anayeleta mengi ya matatizo ya wanadamu. Si mwingine, isipokuwa tu Shetani Ibilisi, ‘mutawala wa ulimwengu.’​—Yoh. 14:30; 2 Kor. 4:4.

3. Namna gani mawazo yetu yanaweza kuanza kupotoka?

3 Hata hivyo, hatuwezi kumulaumu Shetani kwa sababu ya matatizo yetu yote. Sababu gani? Kwa sababu matatizo fulani yanayotupata yanatokana na makosa yetu wenyewe. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:4-6.) Hata ikiwa tunaweza kukubali ukweli huo, kutokamilika kwetu kunaweza kupotosha mawazo yetu na kutufanya tufuate njia ambayo inaweza kutuongoza kwenye musiba. (Met. 14:12) Namna gani? Kuliko kujilaumu sisi wenyewe ao kumulaumu Shetani kwa sababu ya tatizo fulani, tunaweza kuanza kumulaumu Yehova. Tunaweza hata kuanza ‘kumukasirikia’ Yehova.​—Met. 19:3.

4, 5. Namna gani Mukristo anaweza kuanza ‘kumukasirikia’ Yehova?

4 Je, inawezekana kabisa tuanze ‘kumukasirikia’ Yehova? Kufanya hivyo ni upumbavu kabisa. (Isa. 41:11) Hilo halitatuletea faida yoyote. Mwandishi mumoja alisema hivi: “Mukono wako ni mufupi sana hivi kwamba hauwezi kupigana na Mungu.” Labda hatutafikia hatua ya kusema waziwazi maneno ya kumulaumu Yehova. Lakini Methali 19:3 inasema kwamba upumbavu wa mutu ‘unapotosha njia yake, na moyo wake unakasirika juu ya [Yehova].’ (La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo) Ndiyo, mutu anaweza kuanza kumukasirikia Yehova katika moyo wake. Labda hilo halitaonekana wazi wazi. Lakini mutu anaweza kuanza kumuwekea Yehova kinyongo. Hilo linaweza kumufanya ajiondoe katika kutaniko ao asitegemeze tena mipango ya ibada ya Yehova kwa moyo wote.

5 Ni mambo gani yanayoweza kutufanya ‘tumukasirikie’ Yehova? Namna gani tunaweza kuepuka mutego huo? Ni jambo la maana sana tupate majibu ya maulizo hayo. Kwa sababu, jambo hilo linaweza kuharibu ao kutia nguvu urafiki wetu pamoja na Yehova Mungu!

NI MAMBO GANI YANAYOWEZA KUTUFANYA ‘TUMUKASIRIKIE’ YEHOVA?

6, 7. Sababu gani Waisraeli katika siku za Musa walianza kumulaumu Yehova?

6 Ni nini kinachoweza kufanya moyo wa mutumishi mwaminifu wa Yehova uanze kumulaumu Mungu? Tuzungumuzie mambo matano na tuchunguze mifano ya Biblia inayoonyesha namna watu fulani zamani walivyonaswa katika mutego huo.​—1 Kor. 10:11, 12.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kusikiliza mawazo yenye kuvunja moyo kunaweza kutufanya tumukasirikie Yehova (Ona fungu la 7)

7 Maneno yenye kuvunja moyo ya wengine yanaweza kutufanya tumukasirikie Mungu. (Soma Kumbukumbu la Torati 1:26-28.) Waisraeli walikuwa wametoka tu kukombolewa katika utumwa huko Misri. Yehova alikuwa ameleta kimuujiza mapigo kumi juu ya taifa la Wamisri lililokuwa likigandamiza watu wake na kisha hapo alimuharibu Farao na jeshi lake katika Bahari Nyekundu. (Kut. 12:29-32, 51; 14:29-31; Zab. 136:15) Watu wa Mungu walikuwa karibu kuingia katika Inchi ya Ahadi. Huo ulikuwa wakati wa maana sana kwao; hata hivyo, Waisraeli walianza kumulaumu Yehova. Ni nini kilichowafanya wakose imani hivyo? Mioyo yao iliyeyuka kwa sababu ya ripoti yenye kuvunja moyo ya Waisraeli fulani waliotumwa kupeleleza inchi ya Kanaani. (Hes. 14:1-4) Matokeo yalikuwa nini? Kizazi hicho chote hakikuruhusiwa kuingia katika ‘inchi nzuri.’ (Kum. 1:34, 35) Je, wakati fulani tunaacha maneno yenye kuvunja moyo ya wengine yaregeze imani yetu na kutufanya tuanze kulaumu mambo ambayo Yehova anatutendea?

8. Ni nini kilichowafanya watu wa Mungu katika siku za Isaya waanze kumulaumu Yehova?

8 Taabu na matatizo yanaweza kutuvunja moyo. (Soma Isaya 8:21, 22.) Katika siku za Isaya, taifa la Yuda lilijikuta katika shida. Taifa hilo lilizungukwa na maadui. Chakula kilikosekana na wengi walikuwa na njaa. Zaidi ya hilo, kulikuwa na njaa ya kiroho. (Amo. 8:11) Kuliko kutafuta musaada wa Yehova ili kupambana na shida hizo, Wayahudi walianza ‘kulaani’ mufalme wao na Mungu wao. Bila shaka, walimulaumu Yehova kwa sababu ya matatizo yao. Ikiwa tunapatwa na musiba ao matatizo fulani, sisi pia tunaweza kuanza kujiuliza hivi katika moyo wetu, ‘Kwa nini Yehova hakunisaidia nilipohitaji musaada wake?’

9. Sababu gani Waisraeli katika siku za Ezekieli walianza kuwa na maoni mabaya?

9 Hatujui mambo yote kuhusu hali fulani. Kwa kuwa hawakujua habari zote, Waisraeli katika siku za Ezekieli walifikiri kwamba njia za Yehova ‘hazikuwa sawa.’ (Eze. 18:29) Ni kama vile walipenda kumuhukumu Mungu, wakitia viwango vyao vya mema na mabaya juu kuliko viwango vya Yehova na kumuhukumu kulingana na ujuzi wao mudogo. Ikiwa wakati fulani hatuelewe vizuri simulizi fulani la Biblia ao mambo fulani ambayo yametupata katika maisha, labda sisi pia tunaweza kuanza kuwaza katika moyo wetu kwamba njia za Yehova ‘haziko sawa.’​—Ayu. 35:2.

10. Namna gani mutu anaweza kuiga mufano mubaya wa Adamu?

10 Sisi ndio wa kulaumiwa kwa sababu ya zambi na makosa yetu. Mwanzoni tu mwa historia ya wanadamu, Adamu alimulaumu Mungu kwa sababu ya zambi aliyofanya. (Mwa. 3:12) Adamu alitenda zambi kimakusudi na alijua vizuri matokeo ya kuvunja sheria ya Mungu, lakini alimulaumu Yehova. Alisema kwamba Yehova alimupatia mwanamuke mubaya. Tangu wakati huo, wengine wamefuata mufano wa Adamu, wamemulaumu Mungu kwa sababu ya makosa yao wenyewe. Ni vizuri kila mumoja wetu ajiulize hivi: ‘Je, kuvunjika moyo na kusumbuliwa kwa sababu ya makosa yangu mwenyewe kunanifanya ninungunike kuhusu viwango vya Yehova?’

11. Habari ya Yona inaweza kutufundisha nini?

11 Kujifikiria sana. Nabii Yona alikasirikia uamuzi wa Yehova wa kuwasikilia huruma wakaaji wa Ninawi. (Yona 4:1-3) Sababu gani? Labda alifikiri tu kwamba ataonekana kuwa muongo ikiwa watu hawaharibiwe kama alivyowatangazia. Kwa sababu ya kuhangaikia sana sifa yake, Yona hakusikilia Waninawi waliotubu huruma yoyote. Je, sisi pia tunaweza kuanza kujifikiria sana ao kuhangaikia tu sifa yetu hivi kwamba tunafikia ‘kumukasirikia’ Yehova kwa sababu halete mwisho haraka? Ikiwa tumekuwa tukihubiri kwa miaka mingi kwamba siku ya Yehova inakaribia, je, tutaanza kufikiri kwamba Yehova amechelewa wakati wengine wanatuchambua kwa sababu tunawatangazia yale ambayo Biblia inasema?​—2 Pet. 3:3, 4, 9.

NAMNA TUNAVYOWEZA KUEPUKA ‘KUMUKASIRIKIA’ YEHOVA

12, 13. Ikiwa tunaanza kulaumu matendo fulani ya Yehova katika moyo wetu, tunapaswa kufanya nini?

12 Tunaweza kufanya nini ikiwa mioyo yetu yenye zambi inaanza kulaumu matendo ya Yehova? Tukumbuke kwamba kufanya hivyo ni upumbavu. Tafsiri La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo inatafsiri andiko la Methali 19:3 hivi: “Upumbavu wa mutu unapotosha njia yake, na moyo wake unakasirika juu ya [Yehova].” Tukiwa na mawazo hayo katika akili, tufikirie sasa mambo matano yatakayotusaidia tusiache hata kidogo matatizo ya maisha yatufanye tumulaumu Yehova.

13 Endelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Tunaweza kuepuka muelekeo wa kutokamilika wa kumukasirikia Yehova kwa kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. (Soma Methali 3:5, 6.) Tunapaswa kumutegemea Yehova. Pia tunapaswa kuepuka kuwa wenye hekima machoni petu wenyewe ao kujifikiria sana. (Met. 3:7; Mhu. 7:16) Tukifanya hivyo, hatutamulaumu Yehova kwa sababu ya mambo mabaya.

14, 15. Nini itatusaidia tusivunjwe moyo na maneno yasiyofaa ya wengine?

14 Usiruhusu maneno yasiyofaa yakuvunje moyo. Waisraeli wa siku za Musa walikuwa na sababu nyingi za kuamini kwamba Yehova atawaingiza katika Inchi ya Ahadi. (Zab. 78:43-53) Lakini walipopata ripoti yenye kuvunja moyo ya wale wapelelezi kumi wasio waaminifu, ‘hawakukumbuka mukono wake [Yehova].’ (Zab. 78:42) Ikiwa tunatafakari juu ya matendo ya Yehova na kukumbuka mambo yote mazuri ambayo ametufanyia, tutakuwa na uhusiano wenye nguvu pamoja naye. Na hilo litatusaidia tusiruhusu mawazo mabaya ya wengine yatutenganishe na Yehova.​—Zab. 77:11, 12.

15 Namna gani ikiwa tuna maoni mabaya kuhusu waabudu wenzetu? Hilo linaweza kuharibu uhusiano wetu na Yehova. (1 Yoh. 4:20) Waisraeli waliponungunika kuhusu madaraka ya Haruni, Yehova aliona kwamba ni kama vile walimunungunikia Yeye. (Hes. 17:10) Vivyo hivyo, ikiwa tunaanza kulaumu na kunungunikia wale ambao Yehova anatumia ili kuongoza sehemu inayoonekana ya tengenezo lake hapa duniani, itakuwa kama vile tunamunungunikia Yehova.​—Ebr. 13:7, 17.

16, 17. Tunapaswa kukumbuka nini tunapopatwa na matatizo?

16 Kumbuka kwamba si Yehova anayetuletea matatizo. Hata ikiwa Waisraeli wa siku za Isaya walimukataa Yehova, yeye aliendelea kuonyesha kwamba iko tayari kuwasaidia. (Isa. 1:16-19) Hata tupatwe na matatizo gani, inafariji kujua kwamba Yehova anatuhangaikia na iko tayari kutusaidia. (1 Pet. 5:7) Zaidi ya hayo, anaahidi kututolea nguvu tunayohitaji ili tuendelee kuvumilia.​—1 Kor. 10:13.

17 Ikiwa tunatendewa isivyo haki katika njia fulani, kama vile mwanaume mwaminifu Ayubu, tunapaswa kukumbuka kwamba si Yehova anayetuletea matatizo hayo. Yehova anapenda haki; na anachukia ukosefu wa haki. (Zab. 33:5) Kama vile Elihu rafiki ya Ayubu, tunapaswa kujua kwamba, ‘Mungu wa kweli hatende kwa uovu, na Mweza-Yote hatende isivyo haki!’ (Ayu. 34:10) Kuliko kutuletea matatizo, Yehova anatutolea “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.”​—Yak. 1:13, 17.

18, 19. Sababu gani hatupaswe kumulaumu Yehova hata kidogo? Toa mufano.

18 Usimulaumu Yehova hata kidogo. Mungu ni mukamilifu, na mawazo yake yako juu sana kuliko yetu. (Isa. 55:8, 9) Kwa hiyo, unyenyekevu na kiasi vinapaswa kutusaidia tukubali kwamba hatuwezi kuelewa kila jambo. (Rom. 9:20) Kila mara hatuna habari zote kuhusu jambo fulani. Bila shaka umejionea ukweli wa methali hii: “Mwenye kujitetea kwanza anaonekana kuwa na haki, lakini jirani yake anakuja na kutafuta maneno yake.”​—Met. 18:17, La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo.

19 Ikiwa rafiki yetu tunayetumainia anafanya jambo ambalo hatuelewe mwanzoni ao ambalo tunaona kuwa si la kawaida, je, tutamulaumu mara moja kwamba amekosea? Bila shaka, tutamuaminia rafiki yetu, zaidi sana ikiwa tumemujua tangu zamani. Ikiwa tunawaaminia hivyo marafiki zetu wasio wakamilifu, je, hatupaswi kumutumainia hata zaidi Baba yetu wa mbinguni, Yehova, ambaye njia na mawazo yake yako juu sana kuliko yetu?

20, 21. Sababu gani ni jambo la maana kutambua chanzo cha matatizo yetu?

20 Tutambue chanzo cha matatizo yetu. Sababu gani tunapaswa kufanya hivyo? Kwa kweli, tunaweza sisi wenyewe kujiletea matatizo fulani. Ikiwa ni hivyo, tunapaswa kuchukua muzigo wetu. (Gal. 6:7) Usijaribu kumulaumu Yehova kwa sababu ya matatizo ambayo wewe mwenyewe ulijiletea. Sababu gani kufanya hivyo si jambo la hekima? Fikiria mufano huu: Labda motokari fulani una uwezo wa kutembea kwa mwendo wa haraka. Wazia kwamba yule anayeendesha motokari hiyo anafanya hivyo mbio sana anapofika mahali ambapo anapaswa kugeukia upande mwengine na kisha anafanya aksidenti. Je, yule aliyetengeneza motokari anapaswa kulaumiwa kwa sababu ya aksidenti hiyo? Hapana kabisa! Vivyo hivyo, Yehova ametuumba tukiwa na uhuru wa kuchagua. Lakini ametutolea pia maagizo kuhusu namna ya kuchukua maamuzi mazuri. Kwa hiyo basi, sababu gani tumulaumu Muumbaji wetu kwa sababu ya makosa yetu wenyewe?

21 Bila shaka, matatizo yetu yote hayatokane na makosa yetu na matendo yetu mabaya. Mambo mengine yanatupata kwa sababu ya “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhu. 9:11) Hata hivyo, tusisahau hata kidogo kwamba Shetani Ibilisi ndiye chanzo kikubwa cha mambo mabaya. (1 Yoh. 5:19; Ufu. 12:9) Shetani ndiye adui yetu, wala si Yehova!​—1 Pet. 5:8.

LINDA UHUSIANO WAKO WA MAANA SANA PAMOJA NA YEHOVA

[Picha katika ukurasa wa 14]

Yoshua na Kalebu walibarikiwa kwa sababu walimutegemea Yehova (Ona fungu la 22)

22, 23. Tunapaswa kukumbuka nini ikiwa tunaanza kuvunjika moyo kwa sababu ya matatizo yetu?

22 Unapopambana na matatizo, kumbuka mufano wa Yoshua na Kalebu. Tofauti na wale wapelelezi kumi, wanaume hao waaminifu walileta ripoti nzuri. (Hes. 14:6-9) Walionyesha kwamba walikuwa na imani kabisa katika Yehova. Hata hivyo, walipaswa kutangatanga katika jangwa kwa miaka 40 pamoja na Waisraeli wengine. Je, Yoshua na Kalebu walinungunika, na kusikia uchungu, wakifikiri kwamba huo ulikuwa ukosefu wa haki? Hapana. Walimutegemea Yehova. Je, walibarikiwa? Bila shaka! Ijapokuwa kizazi chote hicho kilikufa katika jangwa, wanaume hao wawili waliingia mwishowe katika Inchi ya Ahadi. (Hes. 14:30) Vivyo hivyo, Yehova atatubariki ikiwa ‘hatuchoke kabisa’ kufanya mapenzi yake.​—Gal. 6:9; Ebr. 6:10.

23 Ikiwa umevunjika moyo kwa sababu ya matatizo, kwa sababu ya makosa ya wengine, ao kwa sababu ya makosa yako mwenyewe, unapaswa kufanya nini? Fikiria sana sifa nzuri za Yehova. Wazia namna maisha yako yatakavyokuwa wakati ahadi ya Yehova itatimizwa. Jiulize hivi: ‘Bila Yehova, ningekuwa wapi leo?’ Baki siku zote karibu na Yehova, na usiruhusu hata kidogo moyo wako uanze kumukasirikia Yehova!

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine