MASIMULIZI KUHUSU MAISHA YA WATU
Nimefanya Kumutumikia Yehova Iwe Kazi Yangu ya Maisha
Kisha kumaliza masomo ya sekondari Mwezi wa 1, 1937, nilijiandikisha kwenye masomo ya juu katika Jimbo la Iowa, karibu na mahali ambapo tuliishi huko mangaribi ya kati ya Inchi ya Amerika. Kuenda kwenye masomo na kufanya kazi ili kulipia garama za masomo kuliniachia wakati kidogo tu ili kufanya mambo mengine. Tangu ujana wangu, nilipenda sana kujifunza namna ya kujenga majengo marefu na madaraja (vilalo) yenye kuninginia.
Mwanzoni mwa mwaka wa 1942, muda mufupi tu kisha Amerika kuingia katika Vita ya Pili ya Ulimwengu, nilikuwa katika mwaka wangu wa tano wa masomo ya juu na ilibaki miezi michache tu mbele nipate cheti cha fundi wa ujenzi. Nilikuwa ninaishi katika nyumba pamoja na wenzangu wawili. Mumoja wao aliniomba nizungumuze na mutu ambaye “anatembelea vijana waliokuwa katika vyumba vya chini.” Huko nilikutana na Shahidi mumoja wa Yehova anayeitwa John (Johnny) Brehmer. Nilishangazwa na namna alivyopata jibu la Biblia kwa ulizo lolote ambalo aliulizwa. Nikiwa mwenye kufurahishwa, nilianza kujifunza Biblia na Johnny kwa ukawaida na mwishowe nikaanza kumusindikiza katika mahubiri wakati wowote ambao niliweza kufanya hivyo.
Otto, baba yake na Johnny aliamini na kuwa Shahidi wa Yehova alipokuwa Musimamizi wa benki huko Walnut, Iowa. Otto aliacha cheo hicho ili kuanza utumishi wa wakati wote. Baada ya muda, mufano wake na mufano wa familia yake, ulinitia moyo nifanye uamuzi wa maana.
WAKATI WA KUFANYA UAMUZI
Siku moja, musimamizi wa masomo ya juu aliniambia kwamba alama zangu zilikuwa zinashuka na kwamba singepata cheti cha mwaka wangu wa mwisho. Ninakumbuka kwamba nilisali Yehova kwa bidii, nikimuomba muongozo. Muda mufupi kisha hapo, niliitwa kwenye mukutano pamoja na mwalimu wangu wa somo la ufundi wa ujenzi. Aliniambia kwamba alikuwa amepata ombi la kutafuta mutu ambaye ni fundi wa ujenzi na kwamba alikubali ombi hilo bila kuniuliza ikiwa nilikuwa tayari. Nilimushukuru mwalimu huyo lakini nikamuelezea sababu gani nilikusudia kufanya kumutumikia Yehova kuwa kazi yangu ya maisha. Tarehe 17 Mwezi wa 6, 1942, nilibatizwa na mara moja nikakubaliwa kuwa painia, kama vile watumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa.
Mwishowe katika mwaka wa 1942, nilipata barua ya kuniomba nijiandikishe katika jeshi na nikaenda mbele ya halmashauri ya kuandikisha watu katika jeshi, nikaeleza sababu gani zamiri yangu haikuniruhusu kushiriki katika vita. Nilionyesha karatasi zilizotiwa sahihi na walimu wa masomo ya juu ambao waliandika kuhusu tabia yangu nzuri na uwezo wangu wa pekee nikiwa fundi wa ujenzi. Hata hivyo, ijapokuwa ushahidi huo muzuri ambao walitoa juu yangu, mwishowe niliombwa kulipa dola 10 000 za Kiamerika na nikahukumiwa miaka tano ya kifungo katika gereza la Leavenworth, Kansas, Amerika.
MAISHA YANGU KATIKA GEREZA
Gereza la Leavenworth, Amerika, leo. Watu 230 hivi kati yetu walifungwa ndani ya gezeza hili
Zaidi ya vijana Mashahidi wa Yehova 230 walikuwa wamehukumiwa kifungo katika gereza lililokuwa kwenye shamba la Leavenworth ambako wafungwa walifanya kazi ya kulima, jengo la Leavenworth lilikuwa ndilo gereza kubwa katika eneo hilo. Katika shamba hilo tulipewa kazi mbalimbali chini ya uongozi wa walinzi wengi. Wamoja kati yao walijua musimamo wa Wakristo wa kutounga mukono mambo ya siasa na vita na hawakupinga maoni yetu.
Walinzi wachache walitusaidia tuendelee kufanya mikutano yetu ya kujifunza Biblia. Walitusaidia pia kupata vichapo vinavyotegemea Biblia katika gereza. Musimamizi wa gereza hata alijiandikisha ili awe anapokea kila mwezi gazeti Consolation (ambalo linaitwa leo Amuka!)!
KUFUNGULIWA KWANGU, NA KAZI YA UMISHONARI
Kisha kutumika miaka tatu kati ya miaka tano ambayo nilihukumiwa, nilifunguliwa tarehe 16 Mwezi wa 2, 1946, miezi michache kisha Vita ya Pili ya Ulimwengu kumalizika. Mara moja, nilianza utumishi wa wakati wote nikiwa painia. Nilipewa mugawo wa kurudia tena katika muji wa Leavenworth, Kansas. Niliogopa sana kuenda huko kwa sababu kulikuwa ubaguzi mwingi juu ya Mashahidi wa Yehova. Ilikuwa vigumu kwangu kupata kazi ya kujitegemeza, na pia ilikuwa vigumu hata zaidi kupata mahali pa kuishi.
Ninakumbuka mulinzi mumoja ambaye nilikutana naye aliyenifokea kwa kusema, “Toka hapa kwangu!” Wakati niliona fimbo ya kuchezea mupira wa besiboli aliyokuwa nayo mukononi, niliogopa sana na nikatoka haraka. Kwenye nyumba nyingine, mwanamuke mumoja alisema, “Ngojea kidogo,” na akafunga mulango. Nilingojea na kwa gafula dirisha la juu likafunguliwa na maji mengi machafu kutoka juu yakamwangika juu yangu. Hata hivyo, kazi yangu ya kuhubiri iliniletea baraka. Kisha hapo, nilisikia kwamba watu fulani waliochukua vichapo vinavyotegemea Biblia ambavyo niliwapatia waliamini na kuwa Mashahidi wa Yehova.
Katika mwaka wa 1943, masomo mapya kwa ajili ya wamishonari yalianzishwa katika eneo la kaskazini mwa muji wa New York. Nilialikwa kuhuzuria masomo hayo, na nikamaliza katika darasa la kumi tarehe 8 Mwezi wa 2, 1948. Masomo hayo yalikuja kuitwa baadaye Masomo ya Biblia ya Gileadi. Kisha kumaliza masomo, nilipewa mugawo wa kutumikia katika inchi ya Gold Coast, inayoitwa leo Ghana.
Wakati nilifika katika inchi ya Ghana, nilipewa mugawo wa kuhubiria wakubwa wa serikali na Wazungu. Siku za mwisho za juma, nilitumika na kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova na nilisaidia washiriki wa kutaniko kuhubiri nyumba kwa nyumba. Pia, nilitembelea maeneo ya mbali ambako kulikuwa Mashahidi wa Yehova wachache na kuwazoeza katika kazi ya kuhubiri. Zaidi ya hayo, nilitumika nikiwa mwangalizi anayesafiri karibu na inchi ya Ivory Coast, ambayo inaitwa leo Côte d’Ivoire.
Wakati nilitumikia katika maeneo hayo, nilijifunza kuishi kama wazaliwa wa Afrika wanavyoishi, ni kusema, kulala katika nyumba za matope, kula na mikono, na kuchutama katika choo za ‘inje’ kama vile Waisraeli walivyofanya wakati walikuwa katika jangwa. (Kumbukumbu la Torati 23:12-14) Kufanya hivyo kulinisaidia mimi na wamishonari wenzangu tuwe na maoni mazuri. Mabibi wa wakubwa wa serikali wa eneo hilo walianza kujifunza Biblia na sisi. Kwa hiyo, wakati wapinzani wetu walituletea matatizo na kuunda sheria kwamba viza zetu zisitumike tena, mabibi wa wakubwa hao waliwakaza bwana zao wapinge sheria hiyo na sheria hiyo ikaondolewa!
Kama wamishonari wengi katika Afrika, mwishowe mimi pia nilipata ugonjwa wa malaria. Nilisumbuliwa na baridi na homa ambayo ilinifanya nivurugike akili. Wakati mwingine, nilishikilia hata kidevu changu ili kisitikisike. Ijapokuwa mambo hayo, kazi yangu iliendelea kuniletea furaha na kutosheka.
Katika miaka yangu ine ya kwanza Afrika, tuliandikiana barua na Eva Hallquist, ambaye nilikutana naye mbele ya kuondoka katika inchi ya Amerika. Nilisikia kwamba alikuwa amemaliza darasa la 21 la Masomo ya Biblia ya Gileadi tarehe 19 Mwezi wa 7, 1953, kwenye mukusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova uliofanywa katika Uwanja wa Michezo wa Yankee, New York. Nilipatana na kapteni wa mashua nitumike katika mashua yake ili nifike Amerika bila kulipa.
Kisha siku 22 ya safari katika bahari yenye zoruba, nilifika na nikaenda moja kwa moja kumuona Eva kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika muji wa Brooklyn. Huko, tukiwa na Eva juu ya gorofa ambako tungeweza kuona vizuri muji wote wa New York na bandari yake, nilimueleza kwamba nilitaka kufunga ndoa naye. Mwishowe, Eva alikuja Ghana ili kutumika pamoja na mimi.
KUSHUGULIKIA MADARAKA YA FAMILIA
Kisha kutumika pamoja na Eva kwa miaka mingi katika Afrika, nilipata barua kutoka kwa mama yangu, katika barua hiyo mama alinielezea kwamba baba alikaribia kufa na ugonjwa wa kansa. Kisha kupata ruhusa ya kuacha mugawo wetu, mimi na Eva tulirudia Amerika. Afya ya baba iliharibika sana, na hakukawia kufa.
Baadaye, kulipopita miaka ine hivi kisha kurudia Ghana, tulisikia kwamba afya ya mama pia haikuwa nzuri. Marafiki wetu fulani walitushauria mimi na Eva turudie nyumbani ili kumuchunga mama. Huo ndio ulikuwa uamuzi mugumu sana katika maisha yetu. Kisha miaka 15 katika kazi ya umishonari, miaka 11 kati ya miaka hiyo nikiwa pamoja na Eva, tulirudia Amerika.
Ninakutana na mukubwa wa kijiji fulani katika inchi ya Gold Coast, inayoitwa leo Ghana
Kwa miaka mingi, kila mutu alikuwa na wakati wake wa kumuchunga Mama, na kumusaidia afike kwenye mikutano wakati aliweza kufanya hivyo. Tarehe 17 Mwezi wa 1, 1976, mama alikufa akiwa na miaka 86. Lakini pigo kubwa zaidi lilikuja miaka munane kisha hapo. Eva alipatikana na ugonjwa wa kansa. Tulipiganisha ugonjwa huo katika njia zote, lakini mwishowe alikufa tarehe 4 Mwezi wa 6, 1985, akiwa na miaka 70.
MABADILIKO ZAIDI KATIKA KAZI YENYE KUTOSHELEZA
Katika mwaka wa 1988, nilialikwa kwenye muzinduo wa ofisi mupya ya tawi iliyopanuliwa ya inchi ya Ghana. Hilo lilikuwa tukio lisiloweza kusahauliwa kabisa! Wakati nilifika Ghana kisha kumaliza masomo ya Biblia ya Gileadi miaka 40 hivi iliyopita, kulikuwa mamia tu ya Mashahidi wa Yehova. Kuanzia mwaka wa 1988, kulikuwa Mashahidi wa Yehova zaidi ya 34 000, na sasa wanakaribia 114 000!
Miaka miwili kisha kutembelea Ghana, nilioa Betty Miller tarehe 6 Mwezi wa 8, 1990, Betty alikuwa rafiki yake na Eva wa nguvu sana. Mimi naye tumeendelea kufanya kumutumikia Yehova iwe kazi yetu ya maisha. Tunangojea kwa hamu siku ambayo tutawaona tena wazazi wa wazazi wetu, wazazi wetu, na Eva hapa duniani watakapofufuliwa katika Paradiso.—Matendo 24:15.
Ninalia machozi wakati ninafikiri juu ya pendeleo nzuri sana ambalo nimepata la kutumiwa na Yehova kwa miaka zaidi ya 70 katika kazi yake. Ninamushukuru mara nyingi kwa sababu aliniongoza nifanye kumutumikia iwe kazi yangu ya maisha. Ijapokuwa sasa nina miaka 90 na kitu, Yehova, fundi wa ujenzi mukubwa zaidi katika ulimwengu, ameendelea kunipatia nguvu na bidii ili niendelee kumutumikia.