JE, ULIJUA?
Udi uliotumiwa katika nyakati za Biblia ni nini?
Udi ulitokana na muti wa Agarwood
Biblia inasema kwamba udi (manukato) ulitumiwa ili kutia harufu nzuri ya marashi kwenye nguo na kwenye vitanda. (Zaburi 45:8; Methali 7:17; Wimbo wa Sulemani 4:14) Udi unaozungumuziwa katika Biblia ulitengenezwa na muti ulioitwa Agarwood (aina ya Aquilaria). Muti huo ulipooza, ulitoa mafuta yenye harufu nzuri ya marashi na umajimaji mwengine. Pia ulisagwa na kugeuzwa unga, ambao uliuzishwa kuwa “udi.”
Biblia inafananisha mahema ya Israeli na “mimea ya udi ambayo Yehova amepanda.” (Hesabu 24:5, 6) Inawezekana Biblia inasema hivyo kwa sababu ya ukubwa wa muti wa Agarwood. Muti huo unaweza kufikia urefu wa meta 30 na matawi yake yanasambaa sana. Hata ikiwa muti huo haupatikane tena katika inchi ya Israeli ya sasa, kitabu kimoja kinasema kwamba “hakuna kitu kinachoweza kutuzuia kufikiri kwamba muti huo na miti mingine ambayo haijulikane leo katika [eneo hilo] ilipandwa katika Bonde la Yordani, ambalo wakati huo lilikuwa na watu wengi na utajiri mwingi.” (A Dictionary of the Bible)
Ni matoleo gani yaliyokubaliwa kwenye hekalu la Yerusalemu?
Muhuri huu wa udongo uliopatikana katika hekalu la Yerusalemu una miaka 2 000 hivi
Sheria ya Mungu ilisema kwamba zabihu zote zilizotolewa kwenye hekalu zilipaswa kuwa za hali nzuri sana. Mungu hangekubali zabihu zenye kasoro. (Kutoka 23:19; Mambo ya Walawi 22:21-24) Kulingana na Philo, muandikaji Muyahudi wa wakati wa mitume, wakati huo makuhani walichunguza wanyama “kuanzia kwenye kichwa mupaka kwenye miguu” ili kuhakikisha kwamba wanyama hao walikuwa sawa katika hali zote na “bila doa wala kasoro yoyote.”
Ed Parish Sanders, mutu mwenye elimu, anasema kwamba inawezekana wakubwa wa hekalu “waliruhusu wachuuzi wenye kutegemeka wa wanyama wa zabihu wauzishe tu wanyama na ndege ambazo makuhani walikuwa wamekwisha kuchunguza. Kwa njia hiyo, muchuuzi angepaswa kumupatia mutu anayenunua kipande cha karatasi ao risiti, iliyoonyesha kwamba munyama hana kasoro.”
Katika mwaka wa 2011, wachimbuaji wa vitu vya zamani walipata kipande cha karatasi cha namna hiyo kandokando ya hekalu, ni kusema, muhuri wa udongo wenye ukubwa wa faranga ya kichele uliotengenezwa kati ya miaka 100 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu na mwaka wa 70 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Maneno yake mawili ya Kiaramu yametafsiriwa “Safi kwa Ajili ya Mungu.” Inawaziwa kwamba wakubwa wa hekalu walibandika vipande vya karatasi vya namna hiyo kwenye vitu vilivyotumiwa katika mambo ya dini ao kwenye wanyama waliotolewa zabihu.