Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • w14 1/3 uku. 12-15
  • Kujulisha Neno la Mungu Katika Inchi ya Hispania ya Zamani

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Kujulisha Neno la Mungu Katika Inchi ya Hispania ya Zamani
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • BIBLIA ZA KILATINI ZILITOSHELEZA UHITAJI HUO
  • BIBLIA KWENYE MABAMBA YA MAWE
  • BIBLIA KATIKA KIARABU
  • KUTOKEA KWA TAFSIRI ZA KIHISPANIA
  • Jina la Mungu na Jitihada za Alfonso de Zamora za Kutokeza Maandishi Sahihi
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Biblia—Sababu Gani Ni Nyingi?
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Watu Wote)—2017
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
w14 1/3 uku. 12-15
Biblia ya Alba yenye kufunguliwa

Kujulisha Neno la Mungu Katika Inchi ya Hispania ya Zamani

‘Wakati nitakapokuwa nimeenda Hispania, natumaini, zaidi ya yote, nitakapokuwa katika safari kuenda huko, niwaangalie ninyi kidogo nanyi munisindikize kidogo kuenda huko baada ya mimi kutosheka kwa kiasi fulani.’​—Waroma 15:24.

MUTUME Paulo aliwaandikia maneno hayo Wakristo wenzake waliokuwa katika muji wa Roma mwaka wa 56 hivi kisha kuzaliwa kwa Yesu. Biblia haiseme ikiwa Paulo alisafiri kuenda Hispania ao ikiwa hakuenda huko. Kwa vyovyote, kupitia bidii ya mutume Paulo ao ya Wakristo wengine wamishonari, habari njema kutoka katika Neno la Mungu, Biblia, ilifika Hispania kati ya mwaka wa 101 na 200 kisha kuzaliwa kwa Yesu.

Bila kukawia, vikundi vya Kikristo vikaanza kujitokeza na kuenea kotekote katika Hispania. Kwa sababu ya ongezeko hilo, watu wa Hispania walihitaji kuwa na Biblia iliyotafsiriwa katika luga ya Kilatini. Ilikuwa hivyo kwa sababu kufikia kati ya mwaka wa 101 na 200, inchi ya Hispania ilikuwa imetawaliwa na Waroma kwa muda murefu na luga ya Kilatini ndiyo ilikuwa luga iliyozungumuzwa na watu wengi katika Utawala wote wa Roma.

BIBLIA ZA KILATINI ZILITOSHELEZA UHITAJI HUO

Wakristo wa zamani wa Hispania walitafsiri Biblia nyingi za Kilatini, na zote zilijulikana kwa jina la Vetus Latina Hispana. Biblia hizo za Kilatini zilienea kotekote katika Hispania mupaka wakati Jerome alimaliza tafsiri yake ya Kilatini iliyojulikana sana kwa jina la Vulgate kati ya mwaka wa 401 na 500 kisha kuzaliwa kwa Yesu.

Tafsiri hiyo ya Jerome ambayo alimaliza akiwa Bethlehemu, katika inchi ya Palestina, ilifika Hispania haraka sana. Lusinio, mwanafunzi wa Biblia mwenye bidii, alipojua kwamba Jerome alikuwa akitafsiri Biblia ya Kilatini, alitaka apate kopi ya tafsiri hiyo haraka kabisa. Kwa hiyo, alituma waandishi sita katika muji wa Bethlehemu ili wamuandikie kopi ya tafsiri hiyo na wailete Hispania. Mamia ya miaka kisha hapo, tafsiri ya Vulgate ilichukua pole kwa pole nafasi ya tafsiri ya Vetus Latina Hispana. Tafsiri hizo za Kilatini zilisaidia watu wa Hispania kuisoma Biblia na kuelewa ujumbe wake. Lakini, Utawala wa Roma ulipofikia mwisho wake, tafsiri za luga zingine zilihitajiwa.

BIBLIA KWENYE MABAMBA YA MAWE

Kati ya mwaka wa 401 na 500, Wagoti na makabila mengine ya Ujerumani walivamia Hispania, na hivyo luga mupya ya Kigoti ikaenea katika inchi hiyo ya Hispania inayoingia ndani ya bahari. Makabila hayo yaliyovamia Hispania yalikuwa na aina fulani ya Ukristo unaojulikana kuwa mafundisho ya Ariasi, ambayo hayakukubali fundisho la utatu. Wavamizi hao walikuja pia na tafsiri yao ya Biblia iliyotafsiriwa katika luga yao ya Kigoti, Biblia hiyo inaitwa Biblia ya Ulfilas’. Biblia hiyo ilisomwa katika inchi ya Hispania kufikia mwisho wa miaka kati ya 501 na 600, wakati ambapo Reccared, mufalme wa Wagoti, aliacha dini ya Ariasi na kuwa Mukatoliki. Aliagiza vitabu vyote vya Ariasi vikusanywe na kuharibiwa, kutia ndani Biblia ya Ulfilas’. Kwa sababu hiyo, maandishi yote ya Wagoti yalipotea katika inchi ya Hispania.

Bamba la jiwe lenye kuwa na maandishi ya Biblia ya Kilatini

Maandishi ya Biblia kwenye bamba la jiwe katika luga ya Kilatini, kati ya mwaka wa 501 na 600 kisha kuzaliwa kwa Yesu

Lakini, Neno la Mungu liliendelea kuenea katika inchi ya Hispania katika kipindi hicho. Zaidi ya luga ya Kigoti, kulikuwa pia luga ya Kilatini iliyozungumuzwa na watu wengi katika inchi ya Hispania, ambayo baadaye ilitokeza luga za Kiroma zinazozungumuzwa katika inchi zinazounda Rasi ya Iberia.a Maandishi ya zamani sana katika luga hiyo ya Kilatini yanajulikana kuwa mabamba ya Wagoti, kwa sababu yaliandikwa kwenye mabamba ya mawe. Mabamba hayo ni ya tangu kati ya mwaka wa 501 na 700, na kwenye mabamba fulani kati ya hayo kuna maandiko fulani ya Zaburi na ya Injili. Bamba moja lina andiko lote la Zaburi 16.

Kupatikana kwa Maandishi hayo ya Biblia kwenye mabamba ya kawaida kunaonyesha kwamba wakati huo watu wa hali ya chini walisoma Neno la Mungu na wakaliandika. Inaonekana kwamba, walimu walitumia maandishi hayo ya Biblia kama mazoezi ya kuwafundisha watoto kusoma na kuandika. Mabamba yalikuwa ya bei chini, yakilinganishwa na ngozi za kuandikia ambazo zilikuwa za bei kali na ambazo zilitumiwa katika nyumba za watu wa dini ili kutokeza Biblia zao zenye picha zilizochorwa.

Ukurasa moja wa Biblia ya Leon

Ukurasa moja wa Biblia ya León yenye kupambwa sana. Hata ikiwa Biblia hizo zilikuwaza bei kali, hazikusaidia sana kueneza ujumbe wa Neno la Mungu kati ya watu

Biblia moja ya bei kali iliyo na picha zilizochorwa inapatikana katika kanisa la San Isidoro katika muji wa León, Hispania. Iliandikwa katika mwaka wa 960 kisha kuzaliwa kwa Yesu, juu ya vipande vya ngozi 516, ina urefu wa sentimeta 47, upana wa sentimeta 34, na ina uzito wa kilo 18. Biblia ingine ni Biblia ya Ripoll, inayopatikana katika maktaba ya Vatikani, na iliyoandikwa mwaka wa 1020 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Ni moja kati ya Biblia za zamani zilizopambwa sana. Ili kufanya kazi hizo za ufundi, inawezekana mutawa mwanaume alitumika kwa muda wa siku nzima ili kuunda herufi moja ya kwanza ya neno ao alitumia juma nzima ili kutayarisha tungo ya ukurasa. Lakini, hata ikiwa Biblia hizo zilikuwa za bei kali, hazikusaidia sana kueneza ujumbe wa Neno la Mungu kati ya watu.

BIBLIA KATIKA KIARABU

Kuanzia kati ya mwaka wa 701 na 800, luga ingine ilianza kuzungumuzwa katika Hispania, luga hiyo ilitokana na uvamizi wa Waislamu katika inchi hiyo. Katika maeneo ambayo Waislamu walitawala, luga ya Kiarabu ilichukua nafasi ya Kilatini na hivyo kukakuwa ulazima wa kutafsiri Biblia katika luga hiyo mupya.

Kuanzia mwaka wa 401 mupaka mwaka wa 800 kisha kuzaliwa kwa Yesu, Biblia ya Kilatini na ya Kiarabu, zote mbili ziliwezesha watu wa Hispania wasome Neno la Mungu

Tafsiri nyingi za Biblia za luga ya Kiarabu, zaidi sana vitabu vya Injili, zilisambazwa katika Hispania ya zamani. Inaonekana kwamba kati ya mwaka wa 701 na 800, John, askofu wa Seville, alitafsiri Biblia nzima katika luga ya Kiarabu. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, tafsiri nyingi za luga hiyo ya Kiarabu zimepotea. Tafsiri moja ya Kiarabu ya vitabu vya Injili iliyoandikwa katika mwaka wa 950 hivi inalindwa ndani ya kanisa la León, katika inchi ya Hispania.

Tafsiri ya Kiarabu ya vitabu vya Injili yenye kufunguliwa

Tafsiri ya Injili katika Kiarabu, kati ya mwaka wa 901 na 1000

KUTOKEA KWA TAFSIRI ZA KIHISPANIA

Katika mwisho wa kipindi kinachoitwa Enzi ya Kati (500-1500 kisha kuzaliwa kwa Yesu), Kikastilia, ao Kihispania, kilianza kuzungumuzwa katika inchi zinazounda Rasi ya Iberia. Luga hiyo mupya ilikusudiwa kuwa ya maana ili kueneza Neno la Mungu.b Tafsiri ya kwanza kabisa ya Biblia katika Kihispania iliitwa La Fazienda de Ultra Mar (Maandishi Kutoka Katika Bahari Mbalimbali), iliandikwa mwanzoni mwa miaka kati ya 1201 na 1300. Tafsiri hiyo ina maelezo juu ya safari iliyofanywa na watafsiri kuenda Israeli, na ina habari za vitabu vitano vya kwanza vya Biblia na vitabu vingine vya Maandishi ya Kiebrania na pia vitabu vya Injili na Barua za Mitume.

Mufalme Alfonso wa 10

Mufalme Alfonso wa 10 alitegemeza kutafsiriwa kwa Biblia katika Kihispania

Viongozi wa dini hawakufurahia tafsiri hiyo. Katika mwaka wa 1234, Baraza la Tarragona liliamua kwamba vitabu vyote vya Biblia katika luga za asili vipewe viongozi wa dini ili waviunguze. Jambo la kufurahisha ni kwamba agizo hilo halikuzuia Biblia iendelee kutafsiriwa. Mufalme Alfonso wa 10 (1252-1284), anayesemwa kuwa ndiye mwanzilishi wa maandishi ya Kihispania, alipenda kupata tafsiri ya Maandiko katika luga mupya na aliunga mukono kazi hiyo. Tafsiri za Kihispania za tangu wakati huo zinatia ndani Biblia iliyotangulia tafsiri ya Biblia ya Alfonso na tafsiri ya Biblia ya Alfonso iliyotokea muda mufupi kisha hapo na iliyokuwa kubwa zaidi kwa wakati huo.

Ukurasa wa Biblia iliyotangulia tafsiri ya Biblia ya Alfonso na ukurasa wa tafsiri ya Biblia ya Alfonso

Ukurasa wa Biblia iliyotangulia tafsiri ya Biblia ya Alfonso ya kati ya mwaka wa 1201 na 1300 (kushoto) na ukurasa wa tafsiri ya Biblia ya Alfonso (kuume)

Tafsiri hizo mbili zilisaidia kuanzisha maandishi ya luga mupya ya Kihispania na kuiendeleza. Thomas Montgomery, mutu mwenye elimu, anasema hivi juu ya Biblia iliyotangulia tafsiri ya Biblia ya Alfonso: “Mutu aliyetafsiri Biblia hiyo alifanya kazi nzuri isiyokuwa na makosa na alitumia luga nzuri. . . . Luga hiyo ni nyepesi na wazi, na Biblia iliyotayarishwa kwa ajili ya watu ambao hawakujua Kilatini kigumu ilipaswa kuwa hivyo.”

Lakini, tafsiri hizo za kwanza za Biblia katika Kihispania zilizotafsiriwa kutoka katika Kilatini cha Vulgate, hazikutafsiriwa kutoka katika luga za kwanza. Kuanzia kati ya mwaka wa 1301 na 1400, Wayahudi wenye elimu walitokeza tafsiri nyingi za Biblia za Kihispania za Maandiko ya Kiebrania kutoka moja kwa moja katika luga ya Kiebrania. Wakati huo, inchi ya Hispania ndiyo ilikuwa na Wayahudi wengi katika Ulaya yote, na watafsiri Wayahudi walipata kwa vyepesi maandishi mazuri ya Kiebrania ili kufanya kazi yao ya kutafsiri.c

Mufano mumoja wa pekee ni Biblia ya Alba, iliyotafsiriwa kati ya mwaka wa 1401 na 1500. Luis de Guzmán, tajiri Muhispania mwenye kujulikana sana, alimuomba Rabbi Moisés Arragel atafsiri Biblia katika castizo, ni kusema, Kihispania (safi). Alitoa sababu mbili zilizomusukuma aombe tafsiri hiyo mupya. Kwanza, alisema hivi: “Biblia zinazopatikana leo katika luga zilizotokana na Kilatini zina makosa,” na pili, “Watu kama sisi wanahitaji sana maelezo ya pembeni ili kuelewa maandiko yaliyo magumu kueleweka.” Ombi lake linaonyesha kwamba watu wa wakati wake walipenda sana kusoma Biblia na kuielewa. Ombi hilo linaonyesha pia kwamba Maandiko katika luga ya asili yalikuwa tayari yameenezwa sana katika inchi ya Hispania.

Kwa sababu ya watafsiri na waandikaji wa zamani, watu wenye elimu katika Hispania waliweza kusoma Biblia katika luga yao bila kizuizi kikubwa. Kwa hiyo, mwanahistoria Juan Orts González alisema kwamba “watu wa Hispania walijua Biblia vizuri kuliko watu wa Ujerumani ao watu wa Uingereza mbele ya wakati wa Luther.”

“Watu wa Hispania walijua Biblia vizuri kuliko watu wa Ujerumani ao watu wa Uingereza mbele ya wakati wa Luther.”​—Mwanahistoria Juan Orts González

Lakini, mwishoni mwa miaka kati ya 1401 na 1500, Baraza la Hispania la Kuhukumu Waasi wa Dini lilikataza kutafsiri na kuwa na Maandiko katika luga zote za asili. Biblia ilikatazwa kwa muda murefu katika inchi ya Hispania. Kisha miaka mia tatu, watu waliruhusiwa tena kuwa na Biblia. Katika kipindi hicho kigumu, watafsiri wachache wenye uhodari walitokeza tafsiri mupya mbalimbali katika Kihispania wakiwa katika inchi zingine na wakaziingiza kisiri katika inchi ya Hispania.d

Kama historia hii juu ya Biblia katika Hispania ya zamani inavyoonyesha, wapinzani walijikaza sana wakitumia njia nyingi ili kufanya Neno la Mungu lipotee kabisa. Hata hivyo, hawakuweza kunyamazisha maneno ya Mweza​-Yote.​—Zaburi 83:1; 94:20.

Kazi ya bidii ya watu wengi wenye elimu ilifanya Biblia itafsiriwe na ienezwe katika Hispania yote ya zamani. Watafsiri wa leo wamefuata mufano wa watafsiri hao wa kwanza waliotafsiri Maandiko katika Kilatini, Kigoti, Kiarabu, na Kihispania. Matokeo ni kwamba mamilioni ya watu wanaozungumuza Kihispania leo wanaweza kusoma Neno la Mungu katika luga inayogusa moyo wao.

a Luga hizo zinatia ndani luga ya Kikastilia, Kikatalani, Kigalisiani, na Kireno.

b Leo, Kihispania ndiyo luga ya asili ya watu milioni 540 hivi.

c Soma habari “Jina la Mungu na Jitihada za Alfonso de Zamora za Kutokeza Maandishi Sahihi,” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 1, Mwezi wa 12, 2011.

d Soma habari “Pambano la Casiodoro de Reina kwa Ajili ya Biblia ya Kihispania,” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 6, 1996.

Biblia Katika Luga Zingine za Asili za Hispania

Kikatalani: Biblia ilitafsiriwa katika Kikatalani kati ya mwaka wa 1201 na 1300. Tafsiri moja, inayoitwa, Biblia ya Mashairi (maandishi yanayopangwa kwa utaratibu fulani), ilikuwa tafsiri ya maandishi fulani ya Biblia yaliyopangwa kwa mashairi ili kumusaidia musomaji aweke maandishi akilini. Katika miaka hiyo hiyo, ni kusema, kati ya mwaka wa 1287 na 1290, Jaume de Montjuich alitafsiri Biblia nzima ya kwanza katika Kikatalani kwa agizo la Mufalme Alfonso wa 2 aliyetawala Katalonia na Aragoni.

Kivalensia: Mwanzoni mwa miaka kati ya 1401 na 1500, Bonifacio Ferrer alitafsiri Biblia katika Kivalensia, na Biblia hiyo ilichapishwa katika mwaka wa 1478. Tafsiri hiyo ya Kivalensia ndiyo ilikuwa Biblia ya kwanza kuchapishwa katika inchi ya Hispania. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, Baraza la Kuhukumu Waasi wa Dini liliharibu kila kopi ya tafsiri hiyo, na ukurasa wake wa mwisho ndio tu uliokoka. Ukurasa huo unalindwa katika maktaba ya Shirika la Hispania Lililo Amerika katika muji wa New York.

Kibaske: Katika mwaka wa 1571, Jean de Liçarrague alitafsiri Maandiko ya Kigiriki katika luga ya Kibaske, akiungwa mukono na malkia wa Navarre. Kazi ya Liçarrague ilisaidia kuunda sarufi moja tu kwa ajili ya luga ya Kibaske. Watu wamesema kwamba mambo Liçarrague alifanya juu ya Kibaske ndiyo Jerome alifanya juu ya Kilatini na ndiyo Luther alifanya juu ya Kijerumani.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine