Ni Vizuri Kwetu Kuwako Sikuzote!
1 Muda wa makumi mengi ya miaka, haikuwezekana kwa ndugu zetu wengi wa Ulaya ya Mashariki kukusanyika peupe. Fikiria furaha yao siku ilipowezekana kufanya hivyo katika uhuru wote, marufuku yalipoondolewa!
2 Mwangalizi mmoja wa mzunguko aliandika hivi kuhusu kutaniko moja alilozuru: “Siku ya Pili jioni, baada ya mimi tu kufika, chombo cha kupasha moto kiliharibika. Nje kulikuwa theluji, na katika jumba hali-joto ilikuwa yenye digrii za Selsio 5. Ndugu walivaa makoti, shali (écharpe), mifuko ya mikono, kofia na viatu vikubwa. Hakuna mtu ambaye angaliweza kufuata katika Biblia, kwa kuwa haikuwezekana kufungua kurasa. Jukwani, nikiwa katika koti langu, nilikauka kwa baridi hadi mifupani na niliona pumzi yangu kila wakati niliposema. Lakini jambo lililonigusa moyoni ni kwamba sikusikia hata neno moja la nung’uniko. Wote walisema kwamba walikuwa wenye furaha kuwako!” Kukosa mkutano hakukuja hata akilini mwa ndugu hao!
3 Je! Sisi Tunafikiri Kama Wao? Je! tunapenda furaha ya kukutana pamoja kwa uhuru kila juma? Au tunahudhuria mikutano tu hali zinapokuwa zenye kufaa? Linaweza kuwa jambo gumu kuhudhuria kikawaida na inaweza kuwa kwamba hatukuhudhuria kwa sababu nzuri. Hata hivyo, tufikiri juu ya wale ambao, kati yetu, wanajua umaana wa mikutano na ambao huwako karibu sikuzote, ujapokuwa umri wao, matatizo makubwa ya afya, ulemavu wa kimwili, saa za kazi zenye kuchosha na madaraka makubwa. Tuige mifano hiyo myema!—Ona Luka 2:37.
4 Tufanye yawe mazoea yetu kutegemeza ibada ya kweli kwa kuhudhuria mikutano yote, tangu funzo la kitabu dogo hadi makusanyiko ya wilaya makubwa. Kwa nini tuchukue mikutano hiyo kwa uzito? Kwa kuwa kukusanyika ni amri ya kimungu. Lakini kuna sababu zingine za maana. Sote tunahitaji faida za kufunzwa na Mungu, na pia msaada wa roho takatifu. Na hayo ndiyo mambo tunayopokea kwenye mikutano. (Mt. 18:20) Zaidi ya hayo, tunajengwa kupitia vitia-moyo tunavyobadilishana na ndugu na dada zetu.—Ebr. 10:24, 25.
5 Wakati wa mgeuko-sura, Petro alisema: “Mfunzi, ni vizuri kwetu kuwa hapa.” (Lk. 9:33) Tungepaswa kuwa na hisia iyohiyo kuhusiana na mikutano yetu ya Kikristo. Ndiyo, ni vizuri kwetu kuwako sikuzote!