Jinsi ya kupata furaha nyingi zaidi kutokana na mikutano
1 Mikutano ni ya lazima kwa ajili ya hali yetu njema ya kiroho. Furaha tunayopata kutokana na hiyo ni yenye kuhusiana moja kwa moja na kile tunachofanya kabla ya mikutano, wakati hiyo inapoendeshwa, na baada ya mikutano hiyo. Tunawezaje kujisaidia wenyewe na kusaidia wengine kudumisha furaha ya hali ya juu katika kuhudhuria mikutano?
2 Kabla ya mikutano: Matayarisho yana uvutano wa moja kwa moja juu ya furaha tunayopata kutokana na mikutano. Wakati tunapokuwa wenye kujitayarisha vizuri, tunaelekea zaidi kusikiliza kwa uangalifu na kushiriki. Kwa kuongezea, mgawo wowote kwenye mikutano ambao tunapokea ungepaswa kutayarishwa vizuri, huku tukiwa na mradi wa kutoa habari kwa usahihi kulingana na maagizo, na kufanya wasikilizaji wapendezwe na habari hiyo. Tungepaswa kujizoeza kikamili. Wakati tunapochangia kwenye mikutano yenye kuchochea na yenye kujenga ambayo hufaidi kila mmoja, maendeleo yetu binafsi yanakuwa wazi na tunapata furaha kubwa zaidi.—1 Tim. 4:15, 16.
3 Wakati wa mikutano: Kutoa maelezo kwenye mikutano kunaweza kutusaidia tuifurahie zaidi. Migawo inayoomba ushiriki wa wasikilizaji ingepaswa kuonwa kama migawo ya kila mtu binafsi katika kutaniko. Mara nyingi, maelezo mafupi na ya moja kwa moja huwa yenye matokeo zaidi. Kueleza kwa kifupi mambo yaliyoonwa kunaweza kuwa kwenye kutia moyo sana na kwenye kutia nguvu, na tungepaswa kuwa tayari kutia hayo ndani ya maelezo wakati wowote hilo linapofaa. (Mez. 15:23; Mdo. 15:3) Wakati tunapotoa sehemu kwenye mikutano, tungepaswa kusema kwa shauku na usadikisho, tukiifanya iwe yenye kupendeza, ya kweli, na yenye mafaa.
4 Baada ya mikutano: Kushiriki pamoja na wengine neno lenye wema, salamu ya kirafiki, na mambo makuu machache yaliyozungumziwa kwenye mikutano kutatufaidi sote. Kuonyesha furaha yetu kwa kuona vijana, wazee, na wapya wakishiriki kunafanya upendo wetu kwa udugu uwe wenye kina kirefu. Badala ya kusema isivyofaa kuhusu wale ambao huenda walikosa mikutano, tungepaswa kushiriki pamoja nao furaha yetu ya kuhudhuria, tukiwatia moyo kwa njia hiyo wahudhurie.—Ebr. 10:24, 25.
5 Acheni tusijinyime wenyewe uandalizi huo muhimu wa kuwa na badilishano la kitia-moyo. (Rom. 1:11, 12) Kwa kuchangia katika kila jitihada yenye bidii, huku tukiwa wenye kusukumwa na dhamiri, tunaweza sote kudumisha furaha katika kuhudhuria mikutano ya Kikristo.