“Acheni mambo yote yatukie kwa ajili ya kujenga”
1 Katika kushughulika na ndugu zetu, tunapaswa kufanya lililo zuri kwa ajili ya kuwajenga. Hilo linamaanisha kuhangaikia kulinda faida zao za kiroho. Ikiwa tunajitoa katika aina fulani ya kazi ya kimwili inayohusisha kuendeleza biashara fulani au huduma, tunapaswa kuwa waangalifu kusudi tusifanye jambo lolote litakalokwaza ndugu zetu.—2 Kor. 6:3; Flp. 1:9, l0.
2 Wengine wamejihusisha katika miradi mbalimbali ya biashara, wakiona Wakristo wenzao kuwa wanaoweza kuwa wanunuzi wao. Mashirika fulani yenye kuuzisha biashara hutia moyo mawakili wao waone kila mtu kuwa anayeweza kuwa mnunuzi—kutia ndani wale walio wa dini moja nao. Ndugu wengine wamepanga mikusanyiko mikubwa ya Mashahidi kwa kusudi la kuwatia moyo wajihusishe katika shirika la kibiashara. Wengine wanaanzisha miradi yao kwa kuelekeza uangalifu wa waamini wenzao kwenye makala, broshua, habari kwenye Internet, au kaseti zisizotakiwa. Je, lingekuwa jambo lenye kufaa kwa Mkristo kutumia uhusiano wake wa kitheokrasi ili kuchuma faida kutoka kwa ndugu zake wa kiroho? Hapana!—1 Kor. 10:23, 24, 31-33.
3 Akina ndugu wanapaswa kufanya angalisho: Hilo halimaanishi kwamba Mkristo hawezi kufanya biashara pamoja na ndugu. Hilo ni jambo la kibinafsi. Hata hivyo, wengine huanzisha mipango ya kibiashara inayochochea pupa, nao huchochea waamini wenzao kushirikiana nao au kuwapa fedha kwa ajili ya mipango hiyo huku wakitazamia kupata faida. Mingi ya miradi hiyo haifaulu, nayo hugharimu washiriki wayo kiasi kikubwa cha fedha. Ingawa wale wanaojiunga katika shirika huenda wakawa walichochewa na tamaa ya kupata fedha haraka, yule aliyelisimamia hapaswi kufikiri kwamba hana kosa ikiwa hilo halifaulu. Angepaswa kimbele kufikiria kwa uangalifu matokeo ambayo kutofaulu kwa mradi huo kungekuwa nayo juu ya hali njema ya kiroho na ya kimwili ya ndugu zake. Wale walio na madaraka ya kitheokrasi wanapaswa hasa kuwa waangalifu kuhusu kazi zao za kimwili kwa kuwa wengine wanaweza kuwategemea kwa heshima na kuwaaminia sana. Lingekuwa kosa kutumia vibaya kuaminiwa huko. Mapendeleo ya utumishi mtakatifu yanaweza kupotezwa ikiwa ndugu anapoteza heshima ya wengine.
4 Mradi wetu ungepaswa kuwa ‘kuacha mambo yote yatukie kwa ajili ya kujenga.’ (1 Kor. 14:26) Tunapaswa kuepuka kufanya jambo lolote linaloingiza au linalotia moyo utendaji wa kibiashara katika kutaniko. Mambo kama hayo hayana uhusiano wowote na sababu zetu za Kimaandiko za kukusanyika pamoja.—Ebr. 10:24, 25.