Tuwe Waangalifu Tunapokuwa Katika Mahubiri
1. Sababu gani ni jambo la lazima tuwe waangalifu tunapokuwa katika mahubiri?
1 “Kama kondoo katikati ya mbwa-mwitu,” watumishi wa Mungu wanahubiri “katikati ya kizazi kilicho kombo na kilichopotoka.” (Mt. 10:16; Flp. 2:15) Habari zenye kuogopesha kuhusu watu wenye kukasirika na wenye kufanya jeuri, na watu wenye kuchukua wengine kwa nguvu ili kuwaua ao kuwaficha zimekua za kawaida; hilo linaonyesha wazi kama watu wanaendelea ‘kutoka ubaya mupaka ubaya zaidi.’ (2 Tim. 3:13) Ni kanuni gani za biblia zinazoweza kutusaidia ‘tujionyeshe wenyewe kuwa waangalifu’ katika mahubiri?—Mt. 10:16.
2. Ni hali gani zinazoweza kufanya iwe jambo la hekima kuondoka katika eneo fulani na kuenda hubiri mahali pengine?
2 Tenda kwa Uangalifu: Methali 22:3 inakazia hekima ya ‘kujificha’ unapoona musiba. Uwe mwangalifu! Hali katika eneo lenye usalama inaweza kubadilika gafula. Unapoona wapolisi wengi katika eneo ao vikundivikundi vya watu barabarani, hilo linaweza kuonyesha kama hali si nzuri. Nyakati fulani, mutu unayehubiri anaweza kukuambia kama hali si nzuri. Kuliko kutafuta kujua ni nini inayopitikana, ni jambo la hekima kuondoka haraka katika eneo hilo na kuenda hubiri mahali pengine.—Met. 17:14; Yoh. 8:59; 1 Tes. 4:11.
3. Namna gani kanuni iliyo katika Mhubiri 4:9 inahusu mahubiri?
3 Tumika na Wengine: Mhubiri 4:9 inasema: ‘Wawili ni afazali kuliko mumoja.’ Hata kama umezoea kuhubiri peke yako bila tatizo, je, unawaza hakuna hatari kufanya hivyo? Katika maeneo fulani hakuna hatari yoyote. Lakini katika maeneo mengine kuna hatari ikiwa dada ao kijana anahubiri nyumba kwa nyumba akiwa peke yake, hasa wakati wa mangaribi sana. Katika maeneo hayo, ni jambo la lazima sana kuwa wawili. (Mhu. 4:10, 12) Kila mutu katika kikundi cha mahubiri anapaswa kuwa mwangalifu kwa ajili ya wengine pia. Kila mara unapoondoka katika eneo, uwajulishe wengine.
4. Tunaweza kufanya nini ili kutumika kwa ajili ya usalama wa ndugu na dada katika kutaniko?
4 Kwa kuwa wazee ‘wanalinda nafsi zetu,’ wao wana daraka la kutoa uongozi wenye kufaa kulingana na hali za eneo letu. (Ebr. 13:17) Tuko hakika kama Yehova atatubariki tukiepuka kujitegemea na tukiwaunga kabisa wazee mukono. (Mika 6:8; 1 Kor. 10:12) Acheni basi kila mutumishi wa Mungu ashiriki katika kazi ya kutoa ushahidi wenye matokeo katika eneo letu, lakini siku zote tuwe waangalifu.