Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • g 11/15 uku. 7-9
  • Kuishi Bila Kuona

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Kuishi Bila Kuona
  • Amuka!—2015
  • Habari za Kufanana na Zile
  • Tuwasaidie Vipofu Wajifunze Juu ya Yehova
    Huduma Yetu ya Ufalme—2015
  • Tukomalishe Ufundi Wetu wa Kuhubiri​—Kuhubiria Vipofu
    Buku ya Mukutano Utumishi na Maisha ya Mukristo—2020
  • Jibu ya Sala za Mwanamuke Moja Kipofu
    Ushuhuda wa Mashahidi wa Yehova
  • Walijionea Kabisa Upendo wa Ndugu na Dada
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2023
Ona Habari Zaidi
Amuka!—2015
g 11/15 uku. 7-9
Paqui na bwana yake

Kuishi Bila Kuona

“Nilipoteza karibu uwezo wangu wote wa kuona wakati nilizaliwa kwa sababu nilitiwa matone ya dawa kali katika macho. Nilifikia kuwa kipofu kabisa wakati nilikuwa kijana na nilivunjika moyo sana.”—Paqui, mwanamuke mwenye miaka kati ya 40 na 60 mwenye bwana yake ni kipofu pia.

KUWA kipofu ao kuwa na magumu makubwa ya kuona kunaweza kuletwa na mambo mengi, kama vile kuumia ao ugonjwa. Mambo hayo yanaweza kuwa na matokeo mabaya juu macho, juu ya mishipa ya macho yenye kupeleka habari kwenye ubongo, ao juu ya ubongo. Watu wenye kuwa na magumu makubwa ya kuona, ao wenye kuwa vipofu, wanakataa kuitika hali yao, wanakuwa na huzuni sana, na wanakuwa na woga. Lakini, watu wengi wenye kuwa katika hali hiyo wanajifunza kupambana muzuri na hali yao na wanaendelea kuwa na maisha ya furaha.

Kwa kawaida, macho ndiyo yanatusaidia sana kupata habari juu ya mambo yenye kutuzunguka. Kwa hiyo, wakati mutu anapoteza uwezo wake wa kuona, anafikia kutegemea sana uwezo mwengine mbalimbali, ni kusema, uwezo wa kusikia, kunusa, kugusa, na kuonja.

Kulingana na gazeti moja, uchunguzi juu ya namna ubongo unajipanga upya unaonyesha kama ubongo uko na uwezo wa “kubadilika kulingana na hali zenye kutokea.” (Scientific American) Habari hiyo inaongeza hivi: “Kuko mambo mengi yenye kuhakikisha kama wakati ubongo haupate habari kutoka kwenye kiungo chetu kimoja, uko na uwezo wa kujipanga upya ili kutegemeza na kuongeza uwezo wa viungo vingine.” Fikiria mambo yenye kufuata.

Uwezo wa kusikia: Sauti ao vishindo vya miguu vinaweza kuleta picha fulani katika akili. Mwanaume kipofu mwenye kuitwa Fernando anasema hivi: “Nilijifunza kukumbuka na kutambua watu kupitia sauti zao ao hata namna yao ya kutembea.” Juan, mwenye kuwa kipofu pia, anasema hivi: “Kwa mutu mwenye kuwa kipofu, sauti ya mutu mwengine ndiyo inamutambulisha yeye ni nani.” Na kama sisi wote, kipofu anasikiliza kwa uangalifu sauti, yenye inaweza kumusaidia ajue kama mutu anafurahi, anakasirika, na mambo mengine.

Kupitia masikio ya kipofu yenye kuzoezwa muzuri, sauti inamusaidia pia kutambua mambo yenye kumuzunguka, kama vile mahali motokari zinaelekea, ukubwa wa chumba ao mahali penye kuwa vizuizi fulani.

Uwezo wa kunusa: Uwezo wa kunusa unaweza pia kumusaidia kipofu apate habari nyingi, haiko tu juu ya mahali kwenye kuko harufu ya muzuri. Kwa mufano, wakati kipofu anatembea kwenye barabara fulani, uwezo huo unaweza kumusaidia ajifanyie karte ya eneo katika akili yake. Karte hiyo inaweza kuwa na mambo kama vile mahali penye kuuzishwa kahawa (café), restora, soko, na mahali pengine. Kwa kweli, sauti zenye anajua zinaongezeka kwenye karte hiyo na pia habari zingine zenye anapata kupitia uwezo wake wa kugusa.

Uwezo wa kugusa: Francisco anasema hivi: “Vidole vyangu ndiyo macho yangu.” Fimbo yenye kipofu anatumia inaweza pia kuwa “macho” yake. Manasés, mwenye alizaliwa kipofu na alijifunza kutumia fimbo wakati alikuwa mutoto, anasema hivi: “Ninajua mahali ninapatikana kupitia uwezo wangu mwengine mbalimbali, uwezo wa kukumbuka, na vitu vyenye kuwa kwenye njia; fimbo yangu inanisaidia kutambua vitu hivyo.”

Mutu mwenye kusoma gazeti Munara wa Mulinzi katika Maandishi ya Vipofu

Mutu mwenye kusoma gazeti Munara wa Mulinzi katika Maandishi ya Vipofu

Uwezo wa kugusa unawezesha pia vipofu wengi kusoma kupitia vichapo vyenye kuchapishwa katika Maandishi ya Vipofu. Leo, ni jambo la kawaida kwa kipofu kupata mambo mengi ya kumusaidia kufanya afya yake ya akili na ya kiroho ikuwe muzuri. Zaidi ya vichapo katika Maandishi ya Vipofu, mambo hayo ni kama vile rekodi za kusikiliza na teknolojia yenye kutumia ordinatere. Kwa musaada wa mambo hayo, vipofu wanaweza kusoma Biblia na vichapo vingi vya kusaidia watu kujifunza Biblia.a

Paqui, mwenye tumekwisha kutaja, pamoja na bwana yake, wametiwa moyo sana na wamepata tumaini kupitia mambo hayo ya kiroho. Tena, wamepata musaada kupitia familia kubwa ya kiroho, ni kusema, kutaniko la Mashahidi wa Yehova la eneo lao. Paqui anasema hivi: “Sasa katika maisha tuko na mambo mengi ya kufanya na tunajitegemea kwa kiasi fulani.”

Kwa kweli, kuwa kipofu kunaleta magumu ya pekee. Lakini wakati watu wanapambana na matatizo hayo na kuendelea kuwa na furaha katika maisha, hilo linaonyesha kama mwanadamu ana uwezo wa kuvumilia na kubadilika kulingana na hali!

a Mashahidi wa Yehova wanachapisha vichapo vya kusaidia watu kujifunza Biblia katika Maandishi ya Vipofu katika luga zaidi ya 25.

Hata Kama Niko Kipofu, Niko na Maisha ya Furaha

Marco Antonio na imbwa wake mwenye kumuongoza anayeitwa Dante

Marco Antonio ni bwana, baba, na anasimamia kazi fulani pamoja na mutu mwengine. Tena, ni kipofu wa kizalikio. Alizungumuza na gazeti Amuka! juu ya furaha na magumu yake fulani.

Unasimamia kazi fulani. Namna gani unatimiza jambo hilo?

Katika kazi yangu, ninajibu maulizo ya watu kwenye telefone, ninakutana na watu wenye tunatumikia na pia watu wenye kututolea vitu, na ninaangalia mambo ya benki.

Unafanya nini ili kujifurahisha?

Ninapenda muziki. Unanifanya nijisikie muzuri. Na ninacheza piano, hata kama ni vigumu kwa sababu siwezi kusoma muziki katika Maandishi ya Vipofu na wakati uleule kuucheza kwa mikono yangu miwili. Wakati ninapiga muziki kwa mara ya kwanza, ninausoma na mukono wa kuume na ninapiga piano na mukono wa kushoto. Kisha ninarudilia tena jambo hilo, lakini mikono yangu inabadilishana kazi. Wakati ninaweka muziki katika akili, ninapiga piano kwa mikono yangu miwili.

Umekwisha kupata magumu fulani ya pekee?

Wakati nilikuwa ninakomaa, wazazi wangu pamoja na ndugu zangu walikuwa wananihangaikia sana na kunitendea kama vile siko kipofu. Kwa kweli, nilipata magumu ya kawaida kwa watoto kama vile kuanguka na kuumia, lakini nilifikia kuzoea kufanya mambo mengi yenye mutu mwenye kuona anaweza kufanya. Wakati nilikomaa, jambo lenye lilikuwa linaniumiza sana ni kwamba singeweza kutembeza motokari.

Sasa niko bwana na baba, na niko na familia yenye upendo yenye ninategemeza na ambayo inanitegemeza pia. Mutoto wangu mupendwa, David, ameriti ugonjwa wangu wa macho, yeye pia ana tatizo la kuharibika kwa mishipa ya kuona yenye kupeleka habari kwenye ubongo. Lakini ninajikaza kumuwekea mufano wa muzuri. Ninapenda ajue kama ikiwa anavumilia na hakate tamaa, anaweza kufanya mambo mengi.

Sasa uko na imbwa wa kukuongoza. Sababu gani uliamua kuwa naye?

Dante, imbwa wangu, ananisaidia kutembea mbio na kwa usalama zaidi. Wakati ninaenda nafasi fulani kwa mara ya kwanza, Loli, bibi yangu, mwenye haiko kipofu, anatusindikiza ili mimi na Dante tujue njia. Kusema kweli, mwanzoni sikutumainia kama imbwa anaweza kuniongoza salama. Lakini nilisha kutumainia Dante sana. Hata kutokee nini pembeni yetu, imbwa huyo haache kazi yake ya kuniongoza. Lakini, wakati ninamutosha mushipi, anatenda kama imbwa wengine.

Kwa sababu uko Shahidi wa Yehova, namna gani unajifunza Biblia wewe mwenyewe?

Wakati teknolojia kwa ajili ya vipofu ilikuwa haijaendelea, Loli alikuwa ananisomea Biblia na vichapo vyenye kusaidia kujifunza Biblia. Alinisaidia sana. Kupitia musaada wake, niliweza hata kutoa hotuba nyingi kwenye mikutano ya kutaniko. Lakini leo, ninaweza kujisomea kwa sababu niko na Biblia na vichapo vya kusaidia kujifunza Biblia katika Maandishi ya Vipofu. Ninaweza pia kufungua adresi ya Internete ya Mashahidi wa Yehova, ni kusema, jw.org, kwenye ninachukua rekodi za kusikiliza. Pia, niko na chombo fulani cha Maandishi ya Vipofu chenye kunisaidia kusoma maandishi kwenye ordinatere yangu. Chombo hicho kiko na nukta ndogo-ndogo zenye zinajiunga pamoja ili kufanyiza Maandishi ya Vipofu. Ni jambo la kushangaza sana!

Pendeleo nimefurahia zaidi ni kusaidia kugeuza maandishi ya kawaida yakuwe Maandishi ya Vipofu, kwenye Beteli ya Hispania ya Mashahidi wa Yehova yenye kuwa katika muji wa Madrid. Ili vichapo vya Maandishi ya Vipofu vikuwe muzuri zaidi, wale wenye kuvitayarisha wanafurahia mawazo yenye vipofu wanawatolea. Kwa hiyo, ninaweza kusema kabisa kama ninajisikia kuwa ndugu na dada zangu wa kiroho wananipenda na wananiona kuwa wa maana.

Unafurahia kufanya mambo pamoja na watu wengine?

Ndiyo, zaidi sana pamoja na watu wa familia yangu na Mashahidi wenzangu, wenye ninahubiri pia pamoja nao nyumba kwa nyumba. Ndugu na dada zangu wa kiroho wananitendea namna wanatendea mutu mwengine yeyote. Kwa kweli, wakati fulani wanasahau kama niko kipofu!

Ninaweza pia kusema kama kazi ya kuhubiri inaniwezesha kujulisha wengine tumaini la muzuri sana lenye kupatikana katika Biblia. Kwa mufano, andiko la Isaya 35:5 linasema kama chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, “macho ya vipofu yatafunguliwa.” Wakati Yesu Kristo alikuwa hapa duniani, aliponyesha vipofu; kwa kufanya hivyo alituonyesha kimbele mambo atafanya wakati huo unaokuja. (Mathayo 15:30, 31) Kwa hiyo, kuwa kipofu ni tatizo la muda tu, kama vile ulemavu mwengine wote. Katika dunia Paradiso inayokuja, hakuna mutu atasema, ‘Mimi ni mugonjwa ao mulemavu.’—Isaya 33:24; Luka 23:43.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine