Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • lv sura 4 uku. 36-49
  • Sababu Gani Tunapaswa Kuheshimu Mamlaka?

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Sababu Gani Tunapaswa Kuheshimu Mamlaka?
  • Mubaki “Katika Upendo wa Mungu”
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • INAWEZA KUWA VIGUMU KUHESHIMU WENYE MAMLAKA
  • SABABU GANI TUNAPASWA KUHESHIMU MAMLAKA?
  • KUHESHIMU MAMLAKA KATIKA FAMILIA
  • KUHESHIMU MAMLAKA KATIKA KUTANIKO
  • KUHESHIMU MAMLAKA YA WATAWALA WA ULIMWENGU
  • Juu ya Nini Tuheshimie Mamlaka?
    Namna ya Kubakia Katika Upendo wa Mungu
  • Heshimia Bengine
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2025
  • Ukichwa mu Kutaniko
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2021
  • Heshima Imeenda Wapi?
    Amuka!—2024
Mubaki “Katika Upendo wa Mungu”
lv sura 4 uku. 36-49
Baba anafundisha familia yake

SURA YA 4

Sababu Gani Tunapaswa Kuheshimu Mamlaka?

‘Muwaheshimu watu wa namna zote.’—1 PETRO 2:17.

1, 2. (a) Sisi wote tuna tatizo gani kuhusu mamlaka? (b) Tutazungumuzia maulizo gani?

UMEKWISHA kuona namna uso wa mutoto mudogo ulivyo anapoambiwa kufanya jambo fulani ambalo hataki kufanya? Uso wake unaweza kuonyesha wazi kama hataki. Anajua kama yule anayemutuma ni muzazi wake, na anajua kama anapaswa kuheshimu mamlaka yake. Lakini, anakataa, hataki tu kutii. Hali yetu inafanana na ya mutoto huyo.

2 Wakati fulani si vyepesi kwetu kuheshimu mamlaka. Je, wewe pia kuna wakati inakuwa vigumu kwako kuwaheshimu wale walio na mamlaka fulani juu yako? Ikiwa ni hivyo, jua kama watu wengi wana tatizo hilo. Tunaishi wakati ambao watu wengi hawaheshimu tena mamlaka. Lakini, Biblia inasema kama ni lazima tuwaheshimu wale walio na mamlaka juu yetu. (Methali 24:21) Kwa kweli, kufanya hivyo ni kwa lazima ikiwa tunataka kubaki katika upendo wa Mungu. Lakini tunaweza kujiuliza: Sababu gani inaweza kuwa vigumu sana kwetu kuheshimu wenye mamlaka? Sababu gani Yehova anatuomba tuheshimu mamlaka, na ni jambo gani litatusaidia kufanya hivyo? Basi, ni katika njia gani mbalimbali tunaweza kuonyesha kama tunaheshimu mamlaka?

INAWEZA KUWA VIGUMU KUHESHIMU WENYE MAMLAKA

3, 4. Zambi na kukosa kukamilika vilianza namna gani, na sababu gani hali yetu ya kukosa kukamilika inafanya iwe vigumu kwetu kuheshimu mamlaka?

3 Acha tuone kwa kifupi sababu mbili zinazoweza kufanya iwe vigumu kwetu kuheshimu wale walio na mamlaka. Ya kwanza, sisi ni watu wasio wakamilifu. Ya pili, hata wale walio na mamlaka juu yetu ni watu wasio wakamilifu. Zambi ya wanadamu na kukosa ukamilifu kwao vilianzia katika bustani ya Edeni, wakati Adamu na Eva waliasi mamlaka ya Mungu. Kwa hiyo, zambi ya kwanza ilikuwa ni uasi. Mupaka leo tunazaliwa na mawazo ya kuasi.—Mwanzo 2:15-17; 3:1-7; Zaburi 51:5; Waroma 5:12.

4 Kwa sababu sisi ni watu wasio wakamilifu, ni vyepesi kuwa na kiburi na majivuno. Kwa hiyo, inaomba mutu ajikaze ili awe na sifa ya unyenyekevu na aendelee kuonyesha sifa hiyo. Hata kisha kutumikia Mungu kwa uaminifu miaka mingi, tunaweza kugeuka na kuwa watu wenye kiburi na majivuno. Kwa mufano, Kora alishikamana na watu wa Yehova kwa uaminifu hata katika taabu nyingi. Hata hivyo, alitamani sana mamlaka na akaanza kuasi na kuwachochea Waisraeli wengine wamutombokee Musa, ambaye alikuwa mupole zaidi kuliko watu wote walioishi wakati ule. (Hesabu 12:3; 16:1-3) Kumbuka pia, kwa sababu ya kiburi, Mufalme Uzia aliingia katika hekalu la Yehova na kufanya kazi takatifu ambayo ilipaswa kufanywa na makuhani tu. (2 Mambo ya Nyakati 26:16-21) Wanaume hao waliazibiwa na Mungu. Mifano hiyo mibaya ni onyo kwetu sisi wote. Ni lazima tuondoe kabisa kiburi kwa sababu kinafanya iwe vigumu kwetu kuheshimu mamlaka.

5. Namna gani wanadamu wasio wakamilifu wametumia mamlaka yao vibaya?

5 Kwa upande mwengine, wanadamu wasio wakamilifu walio na mamlaka wanafanya mambo fulani yanayowasukuma watu wasiheshimu tena mamlaka. Wengi wao hawana huruma, wanatawala kwa kinguvu na wanatesa watu. Kwa kweli, historia ya wanadamu ina mambo mengi yanayoonyesha namna watu wametumia mamlaka yao vibaya. (Mhubiri 8:9) Kwa mufano, Sauli alikuwa mwanaume mwema na munyenyekevu wakati Yehova alimuchagua kuwa mufalme. Lakini, aligeuka na kuwa mutu wa kiburi na wivu; na kisha akaanza kumutesa mwanaume mwaminifu Daudi. (1 Samweli 9:20, 21; 10:20-22; 18:7-11) Kisha Daudi akawa mufalme wa Israeli; mufalme muzuri kuliko wafalme wote waliotawala Israeli. Lakini yeye pia alitumia vibaya mamlaka yake; alikamata bibi ya Uria Muhiti na akaamuru Uria atiwe kwenye mustari wa mbele katika vita ili auawe, ijapokuwa Uria hakuwa na kosa lolote. (2 Samweli 11:1-17) Kwa kweli, ni vigumu kwa wanadamu wasio wakamilifu kutumia mamlaka yao vizuri; ni vigumu tena zaidi kwa wale wasiomuheshimu Yehova. Kiongozi mumoja wa serikali ya Angleterre alizungumuzia namna mapapa fulani wa dini ya Kikatoliki walivyoanzisha mateso mengi, kisha aliandika hivi: “Mamlaka inaharibu watu na mamlaka kamili inawaharibu zaidi.” Kisha kuona namna wanadamu wanavyotumia mamlaka vibaya, tuchunguze sasa ulizo hili: Sababu gani tunapaswa kuheshimu mamlaka?

SABABU GANI TUNAPASWA KUHESHIMU MAMLAKA?

6, 7. (a) Upendo wetu kwa Yehova unatusukuma kufanya nini, na sababu gani? (b) Namna gani tunaweza kuonyesha kama tuna sifa ya utii?

6 Kuna sababu ya maana zaidi inayotusukuma tuheshimu mamlaka. Sababu hiyo ni upendo: upendo wetu kwa Yehova, upendo kwa wanadamu wenzetu, na hata kwetu sisi wenyewe. Kwa kuwa tunamupenda Yehova zaidi ya mambo yote, tunapenda kufurahisha moyo wake. (Methali 27:11; Marko 12:29, 30) Tunajua kama utawala wake ulimwenguni pote, ni kusema, haki yake ya kutawala ilipingwa duniani tangu uasi ulipoanza katika Edeni. Tunajua pia kama watu wengi wamemuunga Shetani mukono kwa kukataa kabisa utawala ao uongozi wa Yehova. Lakini sisi tunategemeza ao kuunga mukono utawala wa Yehova kwa furaha. Wakati tunasoma maneno mazuri yaliyoandikwa katika Ufunuo 4:11, moyo wetu unachochewa kabisa. Hatuna shaka lolote, ni Yehova aliye na haki ya kutawala ulimwengu wote muzima! Tunaonyesha kama tunaunga mukono utawala wa Yehova kwa kukubali aongoze maisha yetu ya kila siku.

7 Heshima kama hiyo inamaanisha kumutii Mungu, lakini pia inaomba zaidi. Tuko tayari kumutii Yehova kwa sababu tunamupenda. Hata hivyo, wakati fulani inaweza kuwa vigumu zaidi kwetu kutii. Wakati kama huo, kama yule mutoto mudogo tuliyezungumuzia katika fungu la 1, tutakuwa na lazima ya kutii tu. Tunakumbuka kama Yesu alimutii Baba yake hata wakati ilionekana kuwa vigumu sana kufanya hivyo. Alimuambia Baba yake hivi: “Si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.”—Luka 22:42.

8. (a) Namna gani leo tunaweza kuonyesha kama tunatii mamlaka ya Yehova, na mawazo ya Yehova ni nini juu ya jambo hilo? (b) Ni nini itatusaidia kusikia shauri na kukubali karipio? (Soma kisanduku, “‘Sikiliza Mashauri na Ukubali Nizamu’.”)

8 Ni kweli kwamba, leo Yehova hazungumuze na kila mumoja wetu kipekee; anatumia Neno lake na wanadamu ambao alichagua hapa duniani. Hivyo basi, tunaonyesha kama tunamutii Yehova kwa kuheshimu wanadamu hao ambao ameweka, au wale ambao ameruhusu wawe na mamlaka juu yetu. Tukiasi mamlaka yao, ni kusema, tukikataa shauri na karipio ambalo wanatutolea kupitia Biblia, tutaonyesha kama tunamuasi Mungu wetu. Wakati Waisraeli walinungunikia Musa na kumuasi, Yehova aliona kama ni Yeye ndiye waliasi na kunungunikia.—Hesabu 14:26, 27.

9. Sababu gani upendo wetu kwa wanadamu wenzetu unatusukuma kuheshimu mamlaka? Toa mufano unaoonyesha jambo hilo.

9 Pia, tunaheshimu mamlaka kwa sababu tunapenda wanadamu wenzetu. Namna gani? Wazia kwamba wewe ni askari katika jeshi fulani. Ili muweze kushinda ao kupona katika vita, inaomba kuungana mukono na wengine, kutii na kuheshimu maagizo ya viongozi mbalimbali wa jeshi. Ukikataa kufanya mambo hayo, unaweza kuhatarisha maisha ya wenzako. Ni kweli kwamba leo duniani, maaskari wengi wanafanya mambo mengi mabaya. Lakini, Yehova yeye ana majeshi yanayotenda tu mambo mazuri kwa faida ya wanadamu. Mahali pengi katika Biblia, Mungu anaitwa “Yehova wa majeshi.” (1 Samweli 1:3) Yeye anaongoza majeshi ya malaika wenye nguvu na wenye kupangwa vizuri. Wakati fulani, Yehova anafananisha watumishi wake duniani na jeshi fulani. (Zaburi 68:11; Ezekieli 37:1-10) Kwa hiyo, tukiasi watu ambao Yehova ameweka kwenye mamlaka juu yetu, hauone kama tunaweza kutia ndugu zetu wa kiroho katika hatari? Wakati Mukristo fulani anaasi wazee waliowekwa, wengine katika kutaniko wanaweza kuteseka vilevile. (1 Wakorintho 12:14, 25, 26) Wakati mutoto katika familia anaasi, familia nzima inaweza kuteseka, sivyo? Kwa hivyo, tunaonyesha upendo wetu kwa Wakristo wenzetu kwa kuendelea kuheshimu mamlaka na kuwa na nia ya kutumika pamoja ao kushirikiana.

10, 11. Kujua kwamba kutii mamlaka ni kwa faida yetu, namna gani kunaweza kutusukuma kutii mamlaka?

10 Tunaheshimu pia mamlaka kwa sababu jambo hilo linatuletea sisi wenyewe faida. Wakati Yehova anatuomba kuheshimu mamlaka, mara nyingi anatuonyesha pia faida ambazo tutapata kwa kufanya hivyo. Kwa mufano, Yehova anawaagiza watoto watii wazazi wao ili waishi siku nyingi na wawe na maisha yenye furaha. (Kumbukumbu la Torati 5:16; Waefeso 6:2, 3) Anatuagiza kuwaheshimu wazee wa kutaniko, kwa sababu tusipofanya hivyo tunaweza kupatwa na matatizo ya kiroho. (Waebrania 13:7, 17) Pia, anatuambia tuwatii wakubwa wenye mamlaka ya ulimwengu kwa sababu wako hapo kwa faida yetu.—Waroma 13:4.

11 Je, hauone kwamba kujua sababu gani Yehova anataka tutii kunatusukuma kuheshimu mamlaka? Sasa, acha tuone namna gani tunaweza kuheshimu mamlaka katika sehemu tatu za maisha yetu.

KUHESHIMU MAMLAKA KATIKA FAMILIA

12. Yehova alimupatia baba ao bwana mamlaka gani katika familia, na namna gani anaweza kutumia mamlaka yake?

12 Ni Yehova mwenyewe ndiye alianzisha mupango wa familia. Kwa kuwa yeye ni Mungu wa utaratibu, aliweka utaratibu fulani katika familia ili kusiwe na muvurugo. (1 Wakorintho 14:33) Yehova alimupatia baba ao bwana mamlaka ya kuwa kichwa katika familia. Baba ataonyesha kama yeye pia anaheshimu kichwa chake, ni kusema, Yesu Kristo, kwa kuiga namna Yesu alivyotumia mamlaka yake juu ya kutaniko. (Waefeso 5:23) Kwa hiyo, baba ao bwana hapaswe kupuuza daraka lake, anapaswa kulitimiza kwa bidii. Hapaswe kuwa mukali ao mwenye kukandamiza familia yake, anapaswa kuwa mwenye upendo, asiyengangania mawazo yake, na mwema. Siku zote, anapaswa kukumbuka kama mamlaka yake ni ya kadiri fulani tu, ni kusema, mamlaka yake haipite mamlaka ya Yehova.

Baba Mukristo anaiga namna Kristo anaonyesha ukichwa

13. Namna gani bibi ao mama anaweza kutimiza daraka lake katika familia kwa njia inayomupendeza Yehova?

13 Bibi ao mama anapaswa kutenda kama musaidizi wa bwana yake. Yeye pia alipewa mamlaka fulani katika familia, kwa sababu Biblia inazungumuzia “sheria ya mama yako.” (Methali 1:8) Lakini, mamlaka yake haipite mamlaka ya bwana yake. Mwanamuke Mukristo anaonyesha kwamba anaheshimu mamlaka ya bwana yake kwa kumusaidia kutimiza daraka lake la kichwa katika familia. Hamuzarau ao kumushushia bwana yake heshima, hatumie njia za ujanja ili bwana yake afanye yale anayopenda, wala hamunyanganye bwana yake ukichwa. Kuliko kufanya hivyo, anamuunga mukono na kumusaidia. Wakati uamuzi wa bwana yake haumufurahishe, anaweza kutoa mawazo yake kwa heshima, na anaendelea tu kuwa mutiifu. Ikiwa bwana yake si Shahidi, mwanamuke anaweza kupambana na hali ngumu, lakini ikiwa anaendelea kutii, hilo linaweza kumuchochea bwana yake ajifunze juu ya Yehova.​—1 Petro 3:1.

Baba anamushauria kwa upendo mutoto wake mwanaume mwenye aliingiza matope katika nyumba

14. Namna gani watoto wanaweza kufurahisha wazazi wao, na Yehova?

14 Watoto wanapotii wazazi wao, jambo hilo linamufurahisha Yehova sana. Pia, kufanya hivyo kunawaheshimisha wazazi wao na kuwafurahisha. (Methali 10:1) Katika familia za muzazi mumoja, watoto wanapaswa pia kutii baba yao ao mama yao. Wanapaswa kukumbuka kama kwa kuwa baba ao mama iko yeye mwenyewe, ana lazima sana watoto wamuunge mukono na wamusaidie. Katika familia ambazo kila mutu anatimiza daraka lake alilopewa na Mungu, muna amani sana na furaha. Jambo hilo linamuletea Yehova Mungu sifa, Yeye aliyeanzisha familia zote.—Waefeso 3:14, 15.

KUHESHIMU MAMLAKA KATIKA KUTANIKO

15. (a) Katika kutaniko, namna gani tunaweza kuonyesha kama tunaheshimu mamlaka ya Yehova? (b) Ni kanuni gani zinazoweza kutusaidia tuwatii wale wanaotuongoza? (Soma kisanduku, “‘Muwatii Wale Wanaoongoza’.”)

15 Yehova ameweka Mwana wake kuwa Mutawala wa kutaniko la Kikristo. (Wakolosai 1:13) Yesu pia ameweka ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara,’ ili awatimizie watu wa Mungu duniani pote mahitaji yao ya kiroho. (Mathayo 24:45-47) Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linawakilisha mutumwa mwaminifu na mwenye busara. Kama vile ilivyokuwa wakati wa mitume, leo wazee katika makutaniko wanapokea maagizo na mashauri moja kwa moja kutoka kwa Baraza Linaloongoza ao kupitia waangalizi wanaotumwa na Baraza hilo. Wakati tunaheshimu mamlaka ya wazee katika kutaniko, tunaonyesha kama tunamutii Yehova.​—Waebrania 13:17.

16. Wazee wanawekwa na roho takatifu namna gani?

16 Wazee na watumishi wa huduma ni wanadamu wasio wakamilifu. Wao pia wanaweza kukosea kama sisi. Hata hivyo, wazee ni “zawadi katika wanadamu,” na kutaniko limepewa zawadi hiyo ili lisaidiwe kuwa na uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova. (Waefeso 4:8) Wazee wanawekwa na roho takatifu. (Matendo 20:28) Namna gani? Kwanza, wanaume hao wanapaswa kutimiza sifa zinazotajwa katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake takatifu. (1 Timotheo 3:1-7, 12; Tito 1:5-9) Pili, wazee wanaochunguza sifa za ndugu anayependekezwa, wanasali kwa bidii ili wapate muongozo wa roho takatifu ya Yehova.

17. Sababu gani wakati fulani wanawake Wakristo wanafunika vichwa vyao wanapotimiza kazi fulani katika kutaniko?

17 Ikiwa katika kutaniko hakuna wazee wala watumishi wa huduma wanaopaswa kufanya kazi ambayo ni daraka lao, kwa mufano kuongoza mukutano kwa ajili ya mahubiri, ndugu wengine waliobatizwa wanaweza kufanya kazi hiyo. Ikiwa hakuna hata ndugu aliyebatizwa, dada Mukristo anayestahili anaweza kufanya hivyo. Hata hivyo, katika kutaniko, wakati mwanamuke anatimiza kazi ambayo ilipaswa kufanywa na mwanaume aliyebatizwa, anapaswa kufunika kichwa.a (1 Wakorintho 11:3-10) Kuwaomba wafanye hivyo hakuwashushe wanawake. Lakini, kunawapatia nafasi ya kuonyesha kama wanaheshimu mupango wa Yehova kuhusu mamlaka, katika familia na katika kutaniko.

KUHESHIMU MAMLAKA YA WATAWALA WA ULIMWENGU

18, 19. (a) Namna gani unaweza kufasiria kanuni zinazoonyeshwa katika andiko la Waroma 13:1-7? (b) Namna gani tunaonyesha kama tunaheshimu mamlaka ya watawala wa ulimwengu?

18 Wakristo wa kweli wanajikaza kufuata kabisa kanuni zinazopatikana katika andiko la Waroma 13:1-7. Ukisoma andiko hilo, utaona kama “mamlaka zilizo kubwa” ni serikali ao guvernema za wanadamu. Yehova anaziachilia serikali hizo za wanadamu ziendelee kuwa, nazo pia wakati huo zinatimiza kazi za lazima sana. Kwa mufano, kwa kadiri fulani zinasaidia kusiwe na muvurugo na pia zinasaidia watu katika mambo mbalimbali. Tunaonyesha kama tunaheshimu mamlaka hizo kwa kutii sheria zao. Tunafanya yetu yote ili kulipa kodi wanayotuomba, kujaza vikaratasi vya serikali wanavyotuomba tujaze, na tunatii yale ambayo sheria inaomba kuhusu sisi wenyewe, familia yetu, mambo yetu ya biashara, ao mali yetu. Lakini, hatuwezi kutii mamlaka ya watawala wa ulimwengu ikiwa wanatukataza kumutii Mungu. Wakitukataza, tunajibu kama vile mitume walivyosema: ‘Lazima tumutii Mungu kuwa mutawala kuliko wanadamu.’—Matendo 5:28, 29; soma habari “Ninapaswa Kutii Mamlaka ya Nani?”

NINAPASWA KUTII MAMLAKA YA NANI?

Kanuni: ‘Yehova ni Muamuzi wetu, Yehova ni Mupaji-sheria wetu, Yehova ni Mufalme wetu.’—Isaya 33:22.

Ujiulize

  • Nitafanya nini wakiniomba nivunje kanuni za Yehova?—Mathayo 22:37-39; 26:52; Yohana 18:36.

  • Nitafanya nini nikipewa agizo la kuacha kutii amri za Yehova?—Matendo 5:27-29; Waebrania 10:24, 25.

  • Ni nini kinachoweza kunisaidia niwe na nia ya kutii wale walio na mamlaka juu yangu?—Waroma 13:1-4; 1 Wakorintho 11:3; Waefeso 6:1-3.

19 Tunaonyesha pia kama tunaheshimu mamlaka ya watawala wa ulimwengu kupitia mwenendo wetu. Wakati fulani, tunaweza kukutana na wakubwa wa serikali. Mutume Paulo alikutana na Mufalme Herode Agripa na Guvernere Festo. Ni kweli kwamba wakubwa hao walijulikana kuwa na mwenendo mubaya sana, hata hivyo, mutume Paulo alizungumuza nao kwa heshima. (Matendo 26:2, 25) Tunaiga mufano wa mutume Paulo, iwe mukubwa huyo ni mutu mwenye mamlaka sana katika serikali ao ni polisi tu. Kwenye masomo, vijana Wakristo wanajikaza kuwaheshimu walimu wao, viongozi wao wa masomo na wafanyakazi wengine. Kwa kweli, hatutaheshimu tu wale wanaopendezwa na imani yetu; lakini hata wale wanaopinga Mashahidi wa Yehova, tutawaheshimu. Wale wasio Mashahidi wanapaswa kuona kama sisi ni watu wenye kuheshimu wengine.​—Waroma 12:17, 18; 1 Petro 3:15.

20, 21. Taja faida fulani tunazopata kwa sababu tunaheshimu mamlaka kama inavyostahili?

20 Tusisite kuwaonyesha wengine heshima. Mutume Petro aliandika hivi: ‘Muwaheshimu watu wa namna zote.’ (1 Petro 2:17) Watu wanapoona kama tunawatendea kwa heshima ya kweli, wanaweza kuguswa moyo sana. Kumbuka, leo ni watu wachache tu ndio wanaoonyesha heshima. Kuonyesha heshima ni njia moja inayoonyesha kama tunatii amri ya Yesu inayosema: ‘Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumupa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.’—Mathayo 5:16.

21 Katika ulimwengu huu wenye giza, watu wazuri wanavutiwa na nuru ya kiroho. Kwa hiyo, heshima tunayoonyesha katika familia, katika kutaniko, na kwa wenye mamlaka wa ulimwengu huu, inaweza kuvutia watu fulani na kuwafanya watembee katika nuru pamoja na sisi. Hilo ni jambo nzuri kabisa! Hata ikiwa hilo halifanyike, tuko hakika na jambo hili: Kuwaheshimu wanadamu kunamufurahisha Yehova na kunatusaidia tubaki katika upendo wake. Hiyo ni baraka inayoshinda baraka zote, sivyo?

a Nyongeza “Kufunika Kichwa: Wakati Gani na Sababu Gani?” inazungumuzia namna kanuni hiyo inavyotumika katika njia mbalimbali.

‘SIKILIZA MASHAURI NA UKUBALI NIZAMU’

Leo roho ya Shetani, ni kusema, mawazo yake ya kuasi na kushindana yanajaa katika dunia. Ndio sababu, Biblia inamuita Shetani ‘mutawala wa mamlaka ya hewa.’ Kazi yake imeleta ‘roho ambayo sasa inatenda katika wana wa kutokutii.’ (Waefeso 2:2) Watu wengi leo hawatake kuwa chini ya mamlaka ya mutu yeyote. Jambo la kusikitisha ni kwamba, hata katika kutaniko, roho hiyo imekwisha kuwaambukia wengine. Kwa mufano, muzee katika kutaniko anaweza kutoa mashauri fulani kwa upole; mashauri yanayoonyesha hatari za kujifurahisha kutokana na mambo machafu ao mambo ya jeuri, lakini ndugu na dada fulani wanaweza kupuuza mashauri hayo ao hata labda kuchukizwa. Sisi wote tunapaswa kutii shauri la Methali 19:20: ‘Sikiliza shauri na kukubali nizamu, ili upate kuwa na hekima katika wakati wako ujao.’

Ni nini inayoweza kutusaidia tukubali shauri hilo? Tuone sababu tatu zinazofanya wengine wasikubali mashauri, na kisha ulinganishe mawazo yao na yale ambayo Biblia inasema.

  • “Mimi ninawaza shauri hilo halinihusu.” Tunaweza kuwaza kwamba shauri tunalopewa halipatane kabisa na hali yetu ao kwamba yule aliyetupatia shauri haelewe vizuri jambo hilo. Kwa hiyo, wazo letu la kwanza linaweza kuwa la kupuuza mara moja shauri hilo. (Waebrania 12:5) Kwa kuwa sisi wote ni watu wasio wakamilifu, inawezekana kuwa ni sisi ndio tunapaswa kubadilisha mawazo yetu, sivyo? (Methali 19:3) Je, shauri hilo lilitokea bure tu ao kulikuwa na sababu fulani ya lazima? Hivyo basi, tunapaswa kufikiria sana sababu hiyo iliyomuchochea muzee kututolea shauri. Neno la Mungu linatushauria hivi : ‘Shika nizamu; usiiache. Uilinde, kwa maana hiyo ndiyo uzima wako.’—Methali 4:13.

  • “Mimi sifurahie namna shauri hilo lilivyotolewa.” Ni kweli, neno la Mungu linaonyesha namna gani shauri linapaswa kutolewa. (Wagalatia 6:1) Hata hivyo, Biblia inasema pia kwamba, ‘wote wamefanya zambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.’ (Waroma 3:23) Ikiwa basi tunataka siku fulani tupewe shauri lenye kukamilika na litolewe kwa njia inayofaa kabisa, itatuomba tungojee mutu mwenye kukamilika. (Yakobo 3:2) Tusisahau kwamba Yehova anatumia wanadamu wasio wakamilifu ili watushauri. Kwa hiyo, si jambo la hekima kukazia fikira namna ambavyo shauri linatolewa. Kazia fikira juu ya mawazo mazuri yanayopatikana katika shauri hilo na usali ili kujua namna ya kutumia mawazo hayo.

  • “Hastahili kunipatia mimi shauri!” Ikiwa tunawaza kama mutu fulani hastahili kutushauri kwa sababu yeye pia ana uzaifu fulani, ni vizuri tukumbuke mashauri ambayo tumetoka kuzungumuzia hapo juu. Vilevile, ikiwa tunawaza kama hatuna lazima ya shauri kwa sababu ya umri wetu, kwa sababu ya miaka tumepitisha katika kweli, ao kwa sababu ya madaraka tuliyo nayo katika kutaniko, basi, ni lazima kabisa tubadilishe mawazo yetu. Fikiria madaraka makubwa ambayo mufalme alikuwa nayo hapo zamani katika taifa la Israeli, hata hivyo, alipaswa kukubali mashauri aliyotolewa na manabii, makuhani, na watu wengine kati ya raia wake. (2 Samweli 12:1-13; 2 Mambo ya Nyakati 26:16-20) Leo, tengenezo la Yehova linawapatia wanaume wasio wakamilifu daraka la kutoa mashauri, na ndugu na dada wenye kukomaa wanakubali bila kusita mashauri hayo na wanayatumia. Ikiwa tuna madaraka makubwa ao tumekwisha kupitisha miaka mingi katika kweli, tunapaswa kujua kwamba sisi ndio tunapaswa hata zaidi kuonyesha mufano muzuri kwa wengine kuhusu usawaziko na unyenyekevu kwa kukubali mashauri na kuyatumia.—1 Timotheo 3:2, 3; Tito 3:2.

Bila shaka, sisi wote tuna lazima ya kupewa mashauri. Kwa hiyo, acheni tukubali mashauri na tuyatumie bila kusita, na tumushukuru Yehova kwa moyo wetu wote, kwa sababu ya mashauri hayo yanayoweza kuokoa uzima wetu. Kwa kweli, mashauri ni alama inayoonyesha kama Yehova anatupenda, na tusisahau kama tunataka kubaki katika upendo wa Mungu.—Waebrania 12:6-11.

‘MUWATII WALE WANAOONGOZA’

Wakati wa zamani mipango ilichukuliwa ili taifa la Israeli lisimamiwe vizuri. Musa peke yake hangeweza kusimamia mamilioni ya watu aliokuwa akiongoza kupitia jangwa lenye hatari. Basi Musa alifanya nini? ‘Alichagua wanaume wenye uwezo katika Israeli na kuwapa vyeo vya kuwa vichwa juu ya watu; kuwa wakubwa wa maelfu, wakubwa wa mamia, wakubwa wa 50 na wakubwa wa makumi.’—Kutoka 18:25.

Leo pia, kutaniko la Kikristo lina lazima ya usimamizi. Hiyo ndio sababu kila kikundi cha mahubiri katika kutaniko kina mwangalizi wa kikundi, kila kutaniko lina wazee, kila muzunguko una mwangalizi wa muzunguko, kila wilaya, ina mwangalizi wa wilaya, na kila inchi ina Halmashauri ya Inchi ao Halmashauri ya Tawi. Kwa sababu ya mupango huo, kila mwanaume ambaye ni muchungaji anaweza kutunza kwa uangalifu kondoo wa Yehova ambao alipewa achunge. Wachungaji hao watatoa hesabu mbele ya Yehova na Kristo.—Matendo 20:28.

Ili mupango huo ufanye kazi vizuri, inaomba kila mumoja wetu atii na kunyenyekea. Hatupaswe hata kidogo kuwa kama Diotrefe, ambaye hakuwa hata na heshima kuelekea ndugu waliokuwa wakiongoza kazi katika siku zake. (3 Yohana 9, 10) Kuliko kufanya hivyo, tunapaswa kutii maneno ya mutume Paulo, aliyeandika hivi: ‘Muwatii wale wanaoongoza katikati yenu na munyenyekee, kwa kuwa wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa kuwa kufanya hivyo kungewazuru ninyi.’ (Waebrania 13:17) Ndugu na dada fulani wanatii wakati wanakubaliana na maagizo ya wale wanaoongoza, lakini wakati hawakubaliane na maagizo hayo ao wakati hawaelewe sababu gani maagizo hayo yametolewa, wanakataa kujinyenyekeza. Lakini tusisahau kama kujinyenyekeza kunaweza pia kumaanisha kutii hata wakati mutu hatake kufanya hivyo. Kwa hiyo, kila mumoja wetu anapaswa kujiuliza hivi, ‘Je, mimi ninatii na kujinyenyekeza kwa wale wanaoongoza?’

Ni kweli, Neno la Mungu halionyeshe kila jambo ao kila mupango unaopaswa kufuatwa ili kutaniko litembee vizuri. Lakini, Biblia inasema hivi: ‘Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mupango.’ (1 Wakorintho 14:40) Baraza Linaloongoza linatii agizo hilo; linatolea makutaniko miongozo na maagizo mbalimbali yanayosaidia kuendesha mambo kwa utaratibu na amani. Wazee na watumishi wa huduma wanaonyesha kama wao ni mufano muzuri wa kutii wakati wanafuata bila kusita maagizo hayo. Wanaonyesha pia kwamba wana ‘usawaziko,’ na wako ‘tayari kutii’ wale wanaoongoza. (Yakobo 3:17) Hiyo ndiyo sababu, katika kila kikundi, kila kutaniko, kila muzunguko, kila wilaya, na kila inchi, tuna furaha ya kumutumikia Yehova kwa umoja na kwa utaratibu, na hilo linamuheshimisha Mungu mwenye furaha.—1 Wakorintho 14:33; 1 Timotheo 1:11.

Kwa upande mwengine, maneno ya mutume Paulo katika Waebrania 13:17 yanaonyesha pia hatari ya kuwa na roho ya kutokutii. Roho hiyo inaweza kufanya ndugu walio na madaraka watumike “kwa kuugua” ao kwa huzuni. Utumishi mutakatifu ambao ndugu angepaswa kuona kuwa pendeleo, unaweza kuwa muzigo kabisa, ikiwa katika kutaniko wengine wanakuwa na roho ya kuasi ao kutokushirikiana. Na hali hiyo inaweza kuwa hatari kwa nani? Mutume Paulo anatumia neno “ninyi,” ni kusema, kutaniko muzima. Kwa kweli, kuna matatizo mengine yanayoweza kutokea wakati mutu anakataa kutii mipango ya kiteokrasi. Ikiwa mutu ana kiburi sana, hivi kwamba anakataa kutii, hali yake ya kiroho itaharibika: ataharibisha uhusiano wake pamoja na Baba yake wa mbinguni. (Zaburi 138:6) Kwa hiyo basi, sisi wote na tuazimie kuendelea kutii na kujinyenyekeza.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine