Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • bhs uku. 207-223
  • Mafasirio Ingine

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Mafasirio Ingine
  • Biblia Inatufundisha Nini?
  • Habari za Kufanana na Zile
  • Saidia Mwanafunzi Wako wa Biblia Apendezwe na Sifa za Yehova za Pekee
    Huduma Yetu ya Ufalme—2006
  • Tumia Nguvu za Neno la Mungu Katika Mahubiri
    Huduma Yetu ya Ufalme—2015
  • Namna Nabii Danieli Alivyotabiri Kutokea Kwa Masiya
    Biblia Inafundisha Kabisa Nini?
Biblia Inatufundisha Nini?
bhs uku. 207-223

MAFASIRIO INGINE

1 YEHOVA

Jina la Mungu ni Yehova, maana yake “Yeye Anafanya Kuwa.” Yehova ni Mungu mweza-yote, na ni yeye aliumba vitu vyote. Iko na uwezo wa kufanya mambo yote yenye anaamua kufanya.

Mu Kiebrania, jina la Mungu lilikuwa linaandikwa na herufi ine. Mu Kiswahili herufi hizo ni YHWH ao YHVH. Jina la Mungu linapatikana mara 7 000 hivi mu maandishi ya Biblia ya kwanza-kwanza ya Kiebrania. Watu mu dunia yote wanaandika jina Yehova kwa njia mbalimbali na wanalisema kulingana na luga yao.

▸ Sura ya 1, fu. 15

2 BIBLIA ‘ILIONGOZWA NA ROHO YA MUNGU’

Biblia ni kitabu cha Mungu, lakini alitumia watu ili kuiandika. Ni kama vile tate (nkambo) anaambia mujukuu (munkana) wake amuandikie barua, barua hiyo itakuwa na mawazo ya tate huyo. Mungu alitumia roho yake takatifu ili kuongoza wale wenye waliandika Biblia ili waandike mawazo yake. Roho ya Mungu iliwaongoza mu njia mbalimbali, wakati fulani iliwafanya waone maono ao kulota ndoto na kisha waliandika maono ao ndoto hizo.

▸ Sura ya 2, fu. 5

3 KANUNI

Kanuni ni mafundisho ya Biblia yenye kufasiria kweli fulani ya musingi. Kwa mufano, kanuni moja inasema hivi: “Mashirika ya mubaya yanaharibu tabia za muzuri.” Kanuni hiyo inatufundisha kama watu wenye tunapitisha wakati pamoja nao wanaweza kutuchochea ao kutusukuma kufanya mambo ya muzuri ao ya mubaya. (1 Wakorinto 15:33) Na kanuni yenye kusema “kitu chochote chenye mutu anapanda, ni kile atavuna pia” inatufundisha kama hatuwezi kuepuka matokeo ya matendo yetu.​—Wagalatia 6:7.

▸ Sura ya 2, fu. 12

4 UNABII

Unabii ni ujumbe kutoka kwa Mungu. Ujumbe huo unaweza kuwa mafasirio juu ya mapenzi ya Mungu, fundisho fulani juu ya mwenendo muzuri, amri, ao hukumu. Unaweza pia kuwa ujumbe juu ya jambo fulani lenye litatokea wakati wenye kuja. Mu Biblia, kuko unabii mbalimbali wenye umekwisha kutimia.

▸ Sura ya 2, fu. 13

5 UNABII MBALIMBALI JUU YA MASIYA

Yesu njo alitimiza unabii mbalimbali wenye kuwa mu Biblia wenye kuzungumuzia Masiya. Ona kisanduku chenye kichwa “Unabii Mbalimbali Juu ya Masiya.”

▸ Sura ya 2, fu. 17, maelezo ya chini.

UNABII MBALIMBALI JUU YA MASIYA

TUKIO

UNABII

UTIMIZO

Anazaliwa mu kabila la Yuda

Mwanzo 49:10

Luka 3:23-33

Anazaliwa na bikira

Isaya 7:14

Matayo 1:18-25

Wa kizazi cha Mufalme Daudi

Isaya 9:7

Matayo 1:1, 6-17

Yehova anamutangaza Yesu kuwa Mwana wake

Zaburi 2:7

Matayo 3:17

Watu wengi hawaamini kama Yesu ni Masiya

Isaya 53:1

Yohana 12:37, 38

Anaingia Yerusalemu juu ya mwana-punda

Zekaria 9:9

Matayo 21:1-9

Anasalitiwa na rafiki wa sana

Zaburi 41:9

Yohana 13:18, 21-30

Anasalitiwa kwa vipande 30 vya feza

Zekaria 11:12

Matayo 26:14-16

Anabakia kimya wakati anashitakiwa

Isaya 53:7

Matayo 27:11-14

Nguo zake zinapigiwa kura

Zaburi 22:18

Matayo 27:35

Anachekelewa wakatiiko kwenye muti

Zaburi 22:7, 8

Matayo 27:39-43

Hakuna mufupa wake wenye unavunjwa

Zaburi 34:20

Yohana 19:33, 36

Anazikwa pamoja na matajiri

Isaya 53:9

Matayo 27:57-60

Ufufuo wake

Zaburi 16:10

Matendo 2:24, 27

Anafufuliwa na kuenda mbinguni ili akae kwenye mukono wakuume wa Mungu

Zaburi 110:1

Matendo 7:55, 56

6 JUU YA NINI YEHOVA ALIUMBA DUNIA?

Yehova aliumba dunia ili ikuwe paradiso na watu wenye kumupenda waishi ndani. Kusudi lake halijabadilika. Hivi karibuni, Mungu atatosha mambo yote ya mubaya na kupatia watu wake uzima wa milele.

▸ Sura ya 3, fu. 1

7 SHETANI IBILISI

Shetani njo malaika mwenye alianzisha upinzani juu ya Mungu. Anaitwa Shetani, maana yake “Mupinzani,” kwa sababu anamupinga Yehova. Anaitwa pia Ibilisi, maana yake “Musingiziaji.” Alipewa jina hilo juu anasema mambo ya uongo juu ya Mungu na anadanganya watu.

▸ Sura ya 3, fu. 4

8 MALAIKA

Yehova aliumba malaika miaka mingi mbele ya kuumba dunia. Waliumbwa ili waishi mbinguni. Kuko malaika zaidi ya milioni mia moja. (Danieli 7:10) Kila malaika iko na jina lake na utu wake ao namna yake ya kuwa, na malaika washikamanifu wako wanyenyekevu, wanakataa watu wasiwaabudu. Malaika wako na vyeo mbalimbali na wanapewa kazi mbalimbali za kufanya. Wanafanya kazi kama vile kutumika mbele ya kiti cha ufalme cha Yehova, kutoa ujumbe mbalimbali wa Mungu, kulinda na kuongoza watumishi wake mu dunia, kutimiza hukumu zake, na kuunga mukono kazi ya kuhubiri. (Zaburi 34:7; Ufunuo 14:6; 22:8, 9) Wakati wenye kuja, watamusaidia Yesu kupigana vita ya Armagedoni.​—Ufunuo 16:14, 16; 19:14, 15.

▸ Sura ya 3, fu. 5; Sura ya 10, fu. 1

9 ZAMBI

Zambi ni kuwaza ao kufanya jambo lenye kumuchukiza Yehova ao lenye kupingana na mapenzi yake. Zambi inaharibu urafiki wetu pamoja na Yehova. Kwa hiyo, ametupatia sheria na kanuni mbalimbali ili kutusaidia tuepuke kufanya zambi kwa makusudi. Ku mwanzo, vitu vyote vyenye Yehova aliumba vilikuwa vikamilifu. Lakini wakati Adamu na Eva walikosa kumutii ao kumusikia Yehova, walifanya zambi na hawakukuwa tena wakamilifu. Walizeeka na wakakufa, na tuliriti zambi kutoka kwa Adamu, njo maana na sisi tunazeeka na tunakufa.

▸ Sura ya 3, fu. 7; Sura ya 5, fu. 3

10 ARMAGEDONI

Armagedoni ni vita ya Mungu. Ku vita hiyo ataharibu ulimwengu wa Shetani na kumaliza mambo yote ya mubaya.

▸ Sura ya 3, fu. 13; Sura ya 8, fu. 18

11 UFALME WA MUNGU

Ufalme wa Mungu ni serikali ao guvernema yenye Yehova amesimamisha mbinguni. Mufalme wa serikali hiyo ni Yesu Kristo. Wakati wenye kuja, Yehova atatumia Ufalme huo juu ya kumaliza mambo yote ya mubaya. Ufalme wa Mungu utatawala dunia yote.

▸ Sura ya 3, fu. 14

12 YESU KRISTO

Mungu alimuumba Yesu mbele ya kuumba vitu vingine vyote. Yehova alimutuma Yesu mu dunia ili akufe kwa ajili ya wanadamu wote. Yesu aliuawa, na kisha Yehova alimufufua. Sasa Yesu anatawala mbinguni; yeye ni Mufalme wa Ufalme wa Mungu.

▸ Sura ya 4, fu. 2

13 UNABII JUU YA MAJUMA 70

Biblia ilitabiri wakati wenye Masiya angetokea. Angetokea kwenye mwisho wa kipindi cha majuma 69. Kipindi hicho kilianza mu mwaka wa 455 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu (M.K.Y.) na kikaisha mu mwaka wa 29 kisha kuzaliwa kwa Yesu (K.K.Y.).

Namna gani tunajua kama kiliisha mwaka wa 29 kisha kuzaliwa kwa Yesu? Majuma hayo 69 yalianza mu mwaka wa 455 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, wakati Nehemia alifika Yerusalemu na kuanza kazi ya kujenga upya muji huo. (Danieli 9:25; Nehemia 2:1, 5-8) Juma moja liko na siku 7. Mu unabii huu, majuma hayana urefu wa siku 7, lakini ni majuma yenye kuwa na miaka saba-saba. Hilo linapatana na kanuni fulani yenye kuhusu unabii yenye kusema hivi: “Siku moja kwa mwaka mumoja.” (Hesabu 14:34; Ezekieli 4:6) Kwa hiyo, kila juma liko na miaka 7. Na majuma 69 yako na miaka 483 (69 x 7). Kama tunahesabia miaka 483 kuanzia mwaka wa 455 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, tutafika kwenye mwaka wa 29 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Yesu alibatizwa na kuwa Masiya mu mwaka huo!​—Luka 3:1, 2, 21, 22.

Unabii uleule ulitabiri kama kutakuwa juma lingine moja, ni kusema miaka ingine 7. Katika kipindi hicho, mu mwaka wa 33, Masiya angeuawa, na kuanzia mwaka wa 36, watu wa mataifa yote wangehubiriwa habari njema ya Ufalme wa Mungu, haiko tu Wayahudi.​—Danieli 9:24-27.

▸ Sura ya 4, fu. 7

Muchoro: Unabii juu ya majuma 70 mu Danieli 9 unatabiri kutokea kwa Masiya

14 UTATU NI FUNDISHO LA UONGO

Biblia inafundisha kama Yehova Mungu ni Muumbaji na kama alimuumba Yesu mbele ya kuumba vitu vingine vyote. (Wakolosai 1:15, 16) Yesu haiko Mungu Mweza-Yote. Hakuna siku alisema kama iko sawa na Mungu. Alisema hivi: “Baba ni mukubwa kuliko mimi.” (Yohana 14:28; 1 Wakorinto 15:28) Lakini dini fulani zinafundisha Utatu, ni kusema, watu watatu katika Mungu mumoja: Baba, Mwana, na roho takatifu. Neno “Utatu” halipatikane mu Biblia. Hilo ni fundisho la uongo.

Roho takatifu ni nguvu ya utendaji ya Mungu, nguvu yake yenye haionekane yenye anatumia ili atimize mapenzi yake. Roho takatifu haiko mutu. Kwa mufano, Wakristo wa kwanza-kwanza, ‘walijazwa roho takatifu,’ na Yehova alisema hivi: “Nitamwanga sehemu ya roho yangu juu ya kila namna ya mwili.”​—Matendo 2:1-4, 17.

▸ Sura ya 4, fu. 12; Sura ya 15, fu. 17

15 MUSALABA

Wakati Wakristo wa kweli wanamuabudu Mungu, hawatumie musalaba. Juu ya nini?

  1.  Musalaba umetumiwa mu dini za uongo tangu zamani. Wakati wa zamani, ulitumiwa mu ibada ya vitu vyenye Mungu aliumba na mu desturi za wapagani za ngono. Kwa miaka 300 kisha kifo cha Yesu, Wakristo hawakutumia musalaba katika ibada yao. Kisha wakati fulani, Constantin, Mutawala wa Roma, alifanya musalaba kuwa alama ya Ukristo. Alama hiyo ilitumiwa ili kujaribu kufanya watu wengi wafurahie Ukristo. Lakini musalaba hauna upatano wowote na Yesu Kristo. Kitabu kimoja (New Catholic Encyclopedia) kinasema hivi: “Musalaba ulitumiwa mu desturi zenye zilikuwa mbele Yesu azaliwe na mu desturi zenye haziko za Kikristo.”

  2. Yesu hakukufa kwenye musalaba. Maneno ya Kigiriki yenye kutafsiriwa “musalaba” yako na maana ya “muti wenye kunyoroka,” “nguzo,” ao “mbao.” Kitabu kimoja (The Companion Bible) kinasema hivi: “Hakuna mahali katika Maandiko ya Kigiriki ya [Agano Jipya] kwenye kunatajwa vipande mbili vya mbao.” Yesu alikufa kwenye muti wenye kunyoroka.

  3.  Yehova hapendi tutumie sanamu ao alama fulani katika ibada yetu.​—Kutoka 20:4, 5; 1 Wakorinto 10:14.

▸ Sura ya 5, fu. 12

16 UKUMBUSHO

Yesu aliamuru wanafunzi wake wafanye Ukumbusho wa kifo chake. Wanafanyaka vile kila mwaka tarehe 14 ya Mwezi wa Nisani, siku ileile yenye Waisraeli walikuwa wanafanya Sikukuu ya Pasaka. Mukate wenye kufananisha mwili wa Yesu na divai yenye kufananisha damu yake, vinapitishwa mbele ya watu wote ku Ukumbusho. Wale wenye watatawala pamoja na Yesu mbinguni wanakula mukate na kunywa divai. Wale wenye kuwa na tumaini la kuishi milele katika dunia wanaonyesha heshima kwa kufika ku Ukumbusho lakini hawakule mukate ao kunywa divai.

▸ Sura ya 5, fu. 21

17 NAFSI

Katika Biblia​—Tafsiri ya Ulimwengu Mupya, neno “nafsi” linatumiwa juu ya kuzungumuzia (1) mutu, (2) munyama, ao (3) uzima wa mutu ao wa munyama. Ona mifano fulani:

  • Mutu. “Katika siku za Noa . . . watu kidogo, ni kusema, nafsi munane (8), walichukuliwa salama kupitia maji.” (1 Petro 3:20) Katika andiko hili neno “nafsi” linazungumuzia watu, ni kusema, Noa na bibi yake, watoto wao wanaume tatu na bibi zao.

  • Munyama. “Mungu akasema: ‘Maji yajae viumbe vyenye [ao, “nafsi zenye,” maelezo ya chini] uzima na viumbe vyenye kuruka viruke juu ya dunia kwenye anga la mbingu.’ Kisha Mungu akasema: ‘Dunia itokeze viumbe vyenye [ao, “nafsi zenye,” maelezo ya chini] uzima kulingana na aina yavyo, wanyama wa kufugwa na wanyama wenye kutambaa na wanyama wa pori kulingana na aina yao.’ Na ikakuwa vile.”​—Mwanzo 1:20, 24.

  • Uzima wa mutu ao wa munyama. Yehova alimuambia Musa hivi: “Watu wote wenye walikuwa wanatafuta kukuua [ao, “wanatafuta nafsi yako,” maelezo ya chini] wamekufa.” (Kutoka 4:19) Wakati Yesu alikuwa katika dunia, alisema hivi: “Mimi ndiye muchungaji mwema; muchungaji mwema anatoa uzima wake [ao, “nafsi yake,” maelezo ya chini] kwa ajili ya kondoo.”​—Yohana 10:11.

    Tena, wakati mutu anafanya jambo fulani kwa “nafsi yake yote,” maana yake, anafanya jambo hilo kwa kujipendea na kwa uwezo wake wote. (Matayo 22:37; Kumbukumbu la Torati 6:5) Neno “nafsi” linaweza pia kutumiwa ili kuzungumuzia tamaa ao hamu ya kiumbe chenye kuwa na uzima. Mutu mwenye kufa ao kiumbe chenye kufa vinaweza kuzungumuziwa kuwa nafsi yenye kufa.​—Hesabu 6:6; Mezali 23:2; Isaya 56:11; Hagai 2:13.

▸ Sura ya 6, fu. 5; Sura ya 15, fu. 17

18 ROHO

Maneno ya Kiebrania na ya Kigiriki yenye kutafsiriwa “roho” katika Biblia​—Tafsiri ya Ulimwengu Mupya yanaweza kumaanisha mambo mbalimbali. Lakini kila mara yanazungumuzia kitu chenye watu hawawezi kuona, kama vile upepo ao pumuzi ya watu na ya wanyama. Maneno hayo yanaweza pia kuzungumuzia malaika, ao roho takatifu, ni kusema, nguvu ya utendaji ya Mungu. Biblia haifundishe kama kuko sehemu fulani katika mwili wa mutu yenye inaendelea kuishi kisha mutu kufa.​—Kutoka 35:21; Zaburi 104:29; Matayo 12:43; Luka 11:13.

▸ Sura ya 6, fu. 5; Sura ya 15, fu. 17

19 GEHENA

Gehena ni jina la bonde moja lenye lilikuwa karibu na muji wa Yerusalemu; uchafu ulikuwa unaunguzwa na kuharibiwa mu bonde hilo. Hakuna hata ushuhuda wenye kuonyesha kama wakati wa Yesu, watu ao wanyama walikuwa wanateswa ao kuunguzwa wakiwa wazima katika bonde hilo. Kwa hiyo, Gehena haifananishe mahali fulani kwenye hakuonekane kwenye watu wenye wamekufa wanateswa na kuunguzwa milele. Wakati Yesu alizungumuzia wale wenye wanatupwa katika Gehena, alikuwa anazungumuzia kuharibiwa kabisa-kabisa.​—Matayo 5:22; 10:28.

▸ Sura ya 7, fu. 20

20 SALA YA BWANA

Ni sala yenye Yesu alifundisha wanafunzi wake wakati aliwaonyesha namna ya kusali. Inaitwa pia sala ya Baba Yetu ao sala ya mufano. Katika sala hiyo, Yesu alitufundisha tusali hivi:

  • “Jina lako litakaswe”

    Tunamuomba Yehova asafishe jina lake, ao sifa yake kwa kutosha mambo yote ya uongo yenye yamesemwa juu ya jina hilo. Kwa hiyo, kila mutu mbinguni na duniani atatukuza na kuheshimia jina la Mungu.

  • “Ufalme wako ukuje”

    Tunasali serikali ya Mungu iharibu ulimwengu mubaya wa Shetani, itawale dunia, na kuifanya kuwa paradiso.

  • “Mapenzi yako yafanyike duniani”

    Tunasali kusudi la Mungu juu ya dunia litimizwe ili watu wenye kutii ao kumusikia Mungu na wenye kuwa wakamilifu waishi milele mu Paradiso, kama vile Yehova alikusudia wakati aliumba watu.

▸ Sura ya 8, fu. 2

21 BEI YA UKOMBOZI

Yehova alitoa bei ya ukombozi ili aokoe wanadamu kutoka katika zambi na kifo. Bei ya ukombozi ni bei yenye iliombwa ili kulipia uzima mukamilifu wa kibinadamu wenye Adamu, mutu wa kwanza, alipoteza. Tena, ingewezesha wanadamu wakuwe tena na urafiki muzuri pamoja na Mungu. Mungu alimutuma Yesu katika dunia ili akufe kwa ajili ya watenda-zambi wote. Kwa sababu ya kifo cha Yesu, wanadamu wote wako na nafasi ya kuishi milele na kuwa wakamilifu.

▸ Sura ya 8, fu. 21; Sura ya 9, fu. 13

22 JUU YA NINI MWAKA WA 1914 NI WA MAANA SANA?

Unabii wenye kuwa katika Danieli sura ya 4 unatufundisha kama Mungu angesimamisha Ufalme wake katika mwaka wa 1914.

Unabii: Yehova alimufanya Mufalme Nebukadneza alote ndoto ya unabii kuhusu muti mukubwa wenye ulikatwa. Katika ndoto hiyo, pingu ya chuma na ya shaba viliwekwa kuzunguka shina ao kisiki cha muti huo ili kuuzuia kuota kwa kipindi cha “nyakati saba (7).” Kisha pale muti huo ungeota tena.​—Danieli 4:1, 10-16.

Maana ya unabii huo: Muti unafananisha utawala wa Mungu. Kwa miaka mingi Yehova alitumia wafalme katika Yerusalemu ili watawale taifa la Israeli. (1 Mambo ya Nyakati 29:23) Lakini wafalme hao walikosa kuwa waaminifu, na utawala wao ukafikia mwisho. Yerusalemu iliharibiwa mu mwaka wa 607 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu (M.K.Y.). Huo ulikuwa mwanzo wa zile “nyakati saba (7).” (2 Wafalme 25:1, 8-10; Ezekieli 21:25-27) Wakati Yesu alisema, “Yerusalemu itakanyangwa-kanyangwa na mataifa, mupaka nyakati zenye ziliwekwa za mataifa zitimie,” alikuwa anazungumuzia zile “nyakati saba (7).” (Luka 21:24) Kwa hiyo, zile “nyakati saba (7)” hazikuisha wakati Yesu alikuwa mu dunia. Yehova aliahidi kumuweka Mufalme kwenye mwisho wa zile “nyakati saba (7).” Utawala wa Yesu, Mufalme huyo mupya, ungeletea watu wa Mungu baraka za mingi za milele mu dunia yote.​—Luka 1:30-33.

Urefu wa zile “nyakati saba (7)”: Zile “nyakati saba (7)” zilikuwa na urefu wa miaka 2 520. Kama tunahesabia miaka 2 520 kuanzia mwaka wa 607 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, tunafika mu mwaka wa 1914. Huo njo wakati Yehova alimufanya Yesu, Masiya, kuwa Mufalme wa Ufalme wa Mungu mbinguni.

Namna gani tunapata miaka 2 520? Biblia inasema kama nyakati tatu na nusu ni siku 1 260. (Ufunuo 12:6, 14) Kwa hiyo, “nyakati saba (7)” ni hesabu hiyo mara mbili, ni kusema, siku 2 520. Kanuni moja yenye kuhusu unabii inasema hivi: “Siku moja kwa mwaka mumoja.” Kwa hiyo, siku 2 520 ni miaka 2 520.​—Hesabu 14:34; Ezekieli 4:6.

▸ Sura ya 8, fu. 23

Muchoro wa tarehe na matukio yenye kuhusu ndoto ya Nebukadneza

23 MIKAELI, MALAIKA MUKUBWA

Neno “malaika mukubwa” maana yake “mukubwa wa malaika.” Biblia inataja malaika mukubwa mumoja tu, na jina lake ni Mikaeli.​—Danieli 12:1; Yuda 9.

Mikaeli ni Kiongozi wa jeshi la malaika waaminifu wa Mungu. Andiko la Ufunuo 12:7 linasema hivi: “Mikaeli na malaika wake wakapigana na ule nyoka mukubwa . . . na malaika wake.” Kitabu cha Ufunuo kinasema kama Kiongozi wa jeshi la Mungu ni Yesu, kwa hiyo, Mikaeli ni jina lingine la Yesu.​—Ufunuo 19:14-16.

▸ Sura ya 9, fu. 4

24 SIKU ZA MWISHO

Maneno hayo yanazungumuzia kipindi chenye matukio makubwa mu dunia mbele tu Ufalme wa Mungu uharibu ulimwengu wa Shetani. Maneno ingine kama vile “umalizio wa mupangilio wa mambo” na “kuwapo kwa Mwana wa binadamu,” yanatumiwa katika unabii wa Biblia ili kuzungumuzia kipindi hicho. (Matayo 24:3, 27, 37) “Siku za mwisho” zilianza wakati Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mbinguni mu mwaka wa 1914 na zitamalizika wakati ulimwengu wa Shetani utaharibiwa ku vita ya Armagedoni.​—2 Timoteo 3:1; 2 Petro 3:3.

▸ Sura ya 9, fu. 5

25 UFUFUO

Wakati Mungu anapatia tena uzima mutu mwenye amekufa, tendo hilo linaitwa ufufuo. Biblia inataja ufufuo kenda. Eliya, Elisha, Yesu, Petro, na Paulo, wote walifufua watu. Waliweza kufanya miujiza hiyo kwa sababu Mungu aliwapatia nguvu. Yehova anaahidi kufufua “wenye haki na wenye hawako wenye haki” ili waishi tena mu dunia. (Matendo 24:15) Biblia inazungumuzia pia ufufuo wa wale wenye wataenda mbinguni. Wanadamu fulani wenye Mungu anachagua wanafufuliwa ili waishi mbinguni pamoja na Yesu.​—Yohana 5:28, 29; 11:25; Wafilipi 3:11; Ufunuo 20:5, 6.

▸ Sura ya 9, fu. 13

26 KUPASHANA HABARI NA PEPO WACHAFU

Kupashana habari na pepo wachafu ni zoea la mubaya la kujaribu kuzungumuza na pepo, moja kwa moja ao kupitia mufumu, mulozi, ao muchawi. Watu wenye kupashana habari na pepo wachafu wanaamini fundisho la uongo lenye kuonyesha kama kisha kifo, roho za wanadamu zinaendelea kuishi na zinakuwa mizimu. Pepo wachafu wanajaribu pia kufanya wanadamu waache kumutii ao kumusikia Mungu. Elimu ya nyota, uaguzi, uchawi, na ulozi ni njia zingine za kupashana habari na pepo wachafu. Vitabu mingi, magazeti, kusoma nyota, filme, picha na hata nyimbo, vinafanya ionekane kuwa haiko hatari ao inafurahisha kupashana habari na pepo wachafu. Desturi za mingi zenye kufanywa wakati wa maziko, kama vile kukumbuka kila mwaka siku yenye mutu fulani alikufa, kutolea zabihu watu wenye wamekufa, desturi zenye kufanywa juu ya wajane, ao desturi fulani za kukesha wakati wa kilio, ni njia zingine za kupashana habari na pepo wachafu. Mara mingi watu wanatumia dawa za kulewesha wakati wanajaribu kutumia nguvu za pepo wachafu.​—Wagalatia 5:20; Ufunuo 21:8.

▸ Sura ya 10, fu. 10; Sura ya 16, fu. 4

27 MAMLAKA MAKUBWA YA YEHOVA

Yehova ni Mungu Mweza-Yote. Aliumba ulimwengu wote muzima. (Ufunuo 15:3) Njo maana vitu vyote ni vyake na iko na mamlaka makubwa ao mamlaka yote ya kutawala viumbe vyake vyote. (Zaburi 24:1; Isaya 40:21-23; Ufunuo 4:11) Ameweka sheria kwa ajili ya vitu vyote vyenye aliumba. Yehova iko pia na mamlaka ya kufanya wengine wakuwe watawala. Tunaunga mukono mamlaka makubwa ya Mungu wakati tunamupenda na kumutii ao kumusikia.​—1 Mambo ya Nyakati 29:11.

▸ Sura ya 11, fu. 10

28 KUTOSHA MIMBA

Mwanamuke mwenye anatosha mimba anaua kwa makusudi mutoto mwenye angali mu tumbo. Haiko jambo lenye kutokea lenyewe ao jambo lenye kutokea kwa sababu ya hali fulani ya kawaida mu mwili wa mutu. Kuanzia wakati mimba inaanza mu tumbo la uzazi, mutoto haiko tu sehemu ya mwili wa mama yake. Mutoto ni mutu mwingine.

▸ Sura ya 13, fu. 5

29 KUTIWA DAMU MU MISHIPA

Ni aina ya matunzo ya kutia mu mwili wa mutu damu ao sehemu moja kati ya sehemu ine kubwa za damu. Inaweza kuwa damu yake mwenyewe yenye ilikuwa imechungwa ao damu ya mutu mwingine. Sehemu ine kubwa za damu ni plasma, chembe nyekundu za damu, chembe nyeupe za damu, na vigandisha-damu (plaquettes).

▸ Sura ya 13, fu. 13

30 NIZAMU

Katika Biblia, neno “nizamu” halina tu maana ya malipizi. Wakati tunapewa nizamu, tunafundishwa, tunazoezwa, na kurekebishwa. Yehova hatendee kwa ukali ao bila huruma watu wenye anapatia nizamu. (Mezali 4:1, 2) Yehova anaonyesha wazazi mufano muzuri sana. Nizamu yenye anatoa inaleta matokeo ya muzuri kabisa mupaka inafanya mutu apende nizamu. (Mezali 12:1) Yehova anapenda watu wake, na anawazoeza. Anawapatia mazoezi yenye inawasaidia kubadilisha mawazo ya mubaya na inawasaidia kujifunza namna ya kuwaza na kutenda katika njia yenye kumupendeza. Kwa wazazi, kupatia watoto wao nizamu ni kuwasaidia waelewe sababu gani wanapaswa kutii. Tena ni kuwafundisha kumupenda Yehova, na kupenda Neno lake, Biblia, na kuelewa kanuni zake.

▸ Sura ya 14, fu. 13

31 PEPO WACHAFU

Ni viumbe wabaya wenye hawaonekane wenye kuwa na nguvu nyingi kupita watu. Pepo wachafu ni malaika wabaya. Walijifanya kuwa wabaya wakati walikosa kumutii Mungu, kwa hiyo wakakuwa maadui wake. (Mwanzo 6:2; Yuda 6) Walijiunga na Shetani katika kumupinga Yehova.​—Kumbukumbu la Torati 32:17; Luka 8:30; Matendo 16:16; Yakobo 2:19.

▸ Sura ya 16, fu. 4

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine