Je! Wewe Waona Tu Sura ya Nje?
1 Kadiri tunavyoendesha huduma yetu ya peupe, mawazo yetu ya kwanza juu ya watu fulani yanaweza kutufanya tusite kushiriki habari njema pamoja nao. Kwa mfano, ungeitikiaje ikiwa mwanamume anayeonekana kuwa mkatili angekuangalia vibaya sikuzote unapotembelea jirani yake aliyeonyesha kupendezwa na kweli? Dada mmoja painia aliyeona jambo hilo aliamua kumkaribia mwanamume huyo na kuongea naye. Mwanamume huyo alimsalimu bila adabu. Lakini, kwa kushangaza, yeye alisikiliza ujumbe wa Biblia na kwa msisimuko fulani alikubali funzo. Kama tokeo la jambo la kwamba dada hakuamua mambo kwa kuangalia sura ya nje, njia ilifunguliwa kwa mume huyo na mke wake ili wajifunze kweli.
2 Dada mwingine aliogopeshwa kwanza na sura ya nje ya mwanamume kijana mwenye nywele ndefu, lakini aliendelea kumtolea ushahidi kwa kifupi wakati wote alipokuja katika duka ambamo dada huyo alikuwa akitumika. Jitihada zake zilizaa matunda, na mwanamume huyo kijana sasa ni Shahidi mwenye kubatizwa. Ni jambo gani litakalotuzuia tusikate maneno haraka kwamba watu fulani hawataitikia?
3 Kuiga Kielelezo cha Yesu: Yesu alijua kwamba angetoa uhai wake kwa ajili ya kila mtu. Hivyo, yeye hakuvunjwa moyo na sura ya nje ya wengine. Alitambua kwamba hata wale waliokuwa na sifa yenye kukata tamaa wangeweza kuwa tayari kubadilika ikiwa wangetolewa msaada na kichocheo vyenye kufaa. (Mt. 9:9-13) Alijaribu kusaidia matajiri na maskini pia. (Mt. 11:5; Mk. 10:17-22) Acheni tusihukumu watu tunaowakuta katika eneo kwa kuangalia sura zao za nje, huku tukifunga macho juu ya ile inayoweza kuwa hali njema ya moyo. (Mt. 7:1; Yn. 7:24) Ni nini kinachoweza kutusaidia tuige kielelezo chenye kutokeza cha Yesu?
4 Kupitia funzo letu la Biblia, tumekuja kutambua kwamba Neno la Mungu lina uwezo wa kubadilisha mafikiri ya mtu, mwenendo na utu wake. (Efe. 4:22-24; Ebr. 4:12) Kwa hiyo, tungepaswa kudumisha mtazamo wenye kufaa na kuacha mambo mengine katika mikono ya Yehova, ambaye husoma mioyo ya wanadamu. —1 Sam. 16:7; Mdo. 10:34, 35.
5 Acheni kushiriki kwetu kusiko na upendeleo habari njema pamoja na watu wa aina zote, bila kujali sura zao za nje, kuchangie katika kazi kubwa ya mavuno katika hizi siku za mwisho. —1 Tim. 2:3, 4.