Thamini sana jina zuri la Yehova
1 Shetani alichafua jina la Mungu wakati aliposhawishi wazazi wetu wa kwanza wafanye dhambi. Ibilisi alitokeza wazo la kwamba Yehova alikuwa amemwambia Adamu uwongo. (Mwa. 3:1-5) Kwa kuwa jina la Mungu linahusiana na uwezo wake wa kutimiza neno lake, maneno ya Shetani yalikuwa ndio uchongezi mbaya zaidi. Kwa kutimiza kusudi lake la kimungu hatua kwa hatua, Yehova amesafisha jina lake kwa kuliondolea laumu na amelifanya kuwa zuri.—Isa. 63:12-14.
2 Sisi ndio watu ambao Yehova ameita ‘kwa jina lake.’ (Mdo 15:14, 17) Hilo latutolea nafasi ya kuonyesha jinsi tunavyojisikia kuhusu utakaso wa jina hilo. Tunaona jina la Yehova kuwa zuri kwelikweli, kwa kuwa hilo lawakilisha kila kitu kizuri, chema, chenye upendo, chenye rehema, na chenye haki. Ukubwa wa jina tukufu la Mungu watutia hofu. (Zab. 8:1; 99:3; 148:13) Hilo lingepaswa kutuchochea kufanya nini?
3 Takasa jina la mungu: Jina la Mungu haliwezi kufanywa kuwa takatifu zaidi kuliko lilivyo. Lakini kwa mwenendo wetu safi na kuhubiri kwetu Ufalme, tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini zaidi sana jina la Mungu. Acheni tuseme: “Mshukuru BWANA [Yehova, NW], mwitie jina lake; mutangaze matendo yake katikati ya mataifa, mufanye ukumbusho ya kwamba jina lake limetukuka.” (Isa. 12:4) Tunawezaje kufanya hivyo?
4 Tunaweza kuchukua kila nafasi ili kutangaza jina la Yehova na yale yote ambayo hilo lawakilisha. Iwe kwamba ni kwa namna iliyotayarishwa au kivivi hivi, kutoka nyumba hadi nyumba au kutoka duka hadi duka, iwe kwamba ni barabarani au kwa njia ya simu, utendaji wetu wa kuhubiri humtukuza Yehova. Tunapokuta watu wenye kupendezwa ambao husikiliza, tungepaswa kufanya mipango kamili ili kuwarudilia na kuwafundisha mengi zaidi juu ya Yehova. Hilo lamaanisha kwamba tunapaswa kufanya mipango hiyo ifanikiwe na kudumu katika jitihada zetu za kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani. Kwa kufurahisha, kila mwaka mamia ya maelfu ni wenye kuja ili kujua, kuheshimu, na kutukuza jina zuri la Yehova.
5 Kushiriki kwetu kwa moyo wote katika kazi ya kutakasa jina la Mungu kunaonyesha wazi msimamo wetu kuhusiana na swali ambalo Shetani alitokeza katika Edeni. Hiyo ndiyo kazi yenye kusifika na yenye kuheshimika zaidi ambayo tunaweza kufanya. Acheni tuthamini sana na kutukuza kwa bidii jina zuri la Yehova!—1 Siku 29:13.