Tujulishe Watu Jina la Mungu
1 Uliitikiaje ulipojua jina la Mungu kwa mara ya kwanza? Itikio la wengi linafanana na lile la mwanamke mmoja aliyesema: “Nilipoona jina la Mungu kwa mara ya kwanza katika Biblia, nililia machozi. Niliguswa sana kujua kwamba ningeweza kujua na kutumia jina la kibinafsi la Mungu.” Kwa mwanamke huyo, kujua jina la Mungu kulikuwa hatua ya maana ya kupata kujua Yehova kama mtu na kuweza kusitawisha uhusiano pamoja naye.
2 Kwa Nini Kulijulisha Watu? Jina la Mungu linahusianishwa na sifa zake, makusudi yake, na matendo yake. Linahusianishwa pia na wokovu. “Kila mtu aitiaye jina la Yehova ataokolewa,” aliandika mtume Paulo. Lakini watu “watamwitiaje,” Paulo anatafakari, isipokuwa wajifunze kwanza kuhusu Yehova na kutenda kwa namna yenye kuonyesha kwamba wanamwamini? Kwa hiyo, ni jambo la haraka kwa Wakristo kujulisha wengine jina la Mungu na yote ambayo jina hilo linamaanisha. (Rom. 10:13, 14) Lakini, kuna hata sababu kubwa zaidi inayopaswa kutuchochea tujulishe watu jina la Mungu.
3 Mnamo miaka ya 1920, watu wa Mungu walitambua kupitia Maandiko suala la ulimwenguni pote linalohusisha kutetewa kwa enzi kuu ya Mungu na kutakaswa kwa jina lake. Kabla ya Yehova kuharibu waovu ili kuondoa suto ambalo limewekwa juu ya jina lake, kweli kuhusu yeye inapaswa kufanywa ‘ijulikane katika dunia yote.’ (Isa. 12:4, 5; Ezek. 38:23) Kwa hiyo, sababu yetu ya kwanza kabisa ya kuhubiri ni kumsifu Yehova peupe na kutakasa jina lake mbele ya watu wote. (Ebr. 13:15) Kupenda Mungu na jirani kutatuchochea tushiriki kikamili katika kazi hiyo tuliyoamuriwa na Mungu tuifanye.
4 “Watu kwa Ajili ya Jina Lake”: Katika mwaka wa 1931 tulikubali jina Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10) Tangu hapo, watu wa Mungu wamejulisha watu wengine jina la Mungu hivi kwamba kitabu Wapiga-Mbiu, kwenye ukurasa wa 124, kinasema: “Kimataifa, yeyote ambaye hutumia sana jina la Yehova anatambuliwa haraka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.” Je, unatambuliwa hivyo? Shukrani kwa wema wa Yehova inapaswa kutuchochea ‘kubariki jina lake,’ tukisema kuhusu yeye kila wakati nafasi inayofaa inapojitokeza.—Zab. 20:7; 145:1, 2, 7.
5 Tukiwa “watu kwa ajili ya jina lake,” tunapaswa kutegemeza viwango vyake. (Mdo. 15:14; 2 Tim. 2:19) Mara nyingi jambo ambalo watu wanatambua kwanza kuhusu Mashahidi wa Yehova ni mwenendo wao bora. (1 Pet. 2:12) Hatutataka kamwe kuchafua jina lake kwa kudharau kanuni za kimungu au kwa kutia ibada yake pa nafasi ya pili maishani mwetu. (Law. 22:31, 32; Mal. 1:6-8, 12-14) Badala yake, njia yetu ya maisha na ionyeshe kwamba tunathamini sana pendeleo la kuchukua jina la Mungu.
6 Leo, tunaona tangazo hili la Yehova likitimizwa: “Tangu kucha kwa jua hata kushuka kwake jina langu ni kubwa katikati ya Mataifa.” (Mal. 1:11) Acheni tuendelee kujulisha watu kweli kuhusu Yehova na ‘kubariki jina lake takatifu milele na milele.’—Zab. 145:21.
[Study Questions]
1. Kujua jina la kibinafsi la Mungu kunaweza kuwa na uvutano gani juu ya watu?
2. Kwa nini ni jambo la haraka kwetu kufundisha wengine kuhusu Yehova?
3. Ni nini iliyo sababu yetu ya kwanza kabisa ya kuhubiri?
4. Mashahidi wa Yehova wamekuja kutambulikanaje kuhusiana na jina la Mungu?
5. Mwenendo wetu unahusikaje katika kuchukua jina la Mungu?
6. Ni pendeleo gani tunaloweza kufurahia sasa na milele?