“Wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika bwana”
1 Kwa maneno hayo yaliyo juu, Paulo alitoa habari kuhusu Trifaina na Trifosa, dada wawili waliofanya kazi ngumu katika kutaniko la Roma. Alisema kuhusu mwingine, Persisi: “Alifanya kazi nyingi za jasho katika Bwana.” Vivyo hivyo, alitaja ifaavyo Fibi kuwa “mtetezi wa wengi.” (Rom. 16:2, 12) Katika Maandiko, Dorkasi peke yake anasemwa kuwa mmoja ambaye “alizidi katika vitendo vyema na zawadi za rehema.” (Mdo. 9:36) Wanawake wa kiroho ni baraka kama nini kwa kutaniko!
2 Je! sisi tunathamini akina dada wanaofanya kazi kwa bidii katika kutaniko letu? Wao hufanya sehemu kubwa zaidi ya kazi ya kuhubiri, wao huongoza mengi ya mafunzo ya Biblia, na wao husaidia wengi kati ya wapya. Wao hupitisha pia wakati mwingi wakisaidia watoto wafanye maendeleo ya kiroho. Wanawake Wakristo hutimiza fungu lao katika kujenga roho ya upendo, shangwe, amani, na bidii katika kutaniko. Wao ni wenye kutoa utegemezo katika njia nyingi hivi kwamba waume wao na washiriki wengine wa familia wanaweza kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova.
3 Akina dada katika utumishi wa wakati wote: Kati ya wale wanaofanya kazi ya jasho kwa bidii katika Bwana kuna akina dada wamishonari; wengi wao wameshiriki katika kusitawisha kazi katika nchi za kigeni. Katika makutaniko yanayohudumiwa na waume wao, wake wa waangalizi wasafiri huwa wenye shughuli katika huduma ya shambani, wakitia moyo akina dada wengi. Hatupaswi kusahau akina dada kwenye Betheli, ambao hutimiza kwa bidii utumishi mtakatifu ili kutegemeza tengenezo la Yehova. Dada zetu mapainia wa kawaida pia, kupitia jitihada zao za kusifu Mungu, ni wenye kusaidia maelfu wajifunze kweli.
4 Akina dada hao waaminifu hupata kutosheka kwingi katika njia yao ya maisha yenye kujinyima. (1 Tim. 6:6, 8) Wanastahili pongezi na kitia-moyo chochote na utegemezo tunaoweza kuwatolea.
5 Wanawake Wakristo ni watu wenye thamani kwa tengenezo la Yehova; hao hutimiza utumishi mwaminifu ambao ni baraka kwa wote. Acheni tuendelee kuthamini wanawake kama hao na kuomba baraka ya Yehova iwe juu yao huku wakiendelea ‘kufanya kazi kwa bidii katika Bwana.’