Ni nini kinachoweza kutusaidia kusimama imara katika imani?
1 Tangu tulipoanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, maendeleo yetu ya kiroho yameonekana sikuzote kuwa chanzo cha furaha kwetu! Hata hivyo, ili kudumu katika kuwa ‘wenye kutia mizizi, wenye kujengwa, na wenye kuimarishwa katika imani,’ ukuzi wa kiroho wenye kuendelea unahitajiwa. (Kol. 2:6, 7) Ingawa wengi walisitawi kiroho, wengine wamepeperushwa mbali kwa sababu ya kushindwa ‘kusimama imara katika imani.’ (1 Kor. 16:13) Tunaweza kuzuia hilo lisitupate. Jinsi gani?
2 Utendaji wa kiroho wa kawaida: Sitawisha programu nzuri ya kiroho katika tengenezo la Yehova. Humo mahitaji yetu ya kiroho hutoshelezwa kwa wingi. Mikutano ya kutaniko, mikusanyiko, na makusanyiko hutuchochea kuelekea ukuzi mkubwa zaidi wa kiroho na kuimarishwa, ikiwa tu sisi twahudhuria kikawaida ili kuvuna faida hizo. (Ebr. 10:24, 25) Programu ya kawaida ya kusoma Biblia, magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, na vitabu vinavyozungumzia chakula kigumu cha Neno la Mungu vitafanya mizizi yetu ya kiroho ikomae kwa kina kirefu na kwa nguvu. (Ebr. 5:14) Kujiwekea miradi ya kiroho na kujitahidi kwa bidii kuifikia pia kutaleta baraka zenye kudumu.—Flp. 3:16.
3 Msaada kutoka kwa wale wenye kukomaa: Tafuta kupanuka katika kushirikiana na wale wenye kukomaa kiroho katika kutaniko. Pata kujua wazee, kwa kuwa hao ndio wa kwanza wanaoweza kututia nguvu. (1 Thes. 2:11, 12) Kubali shauri lolote au madokezo wanayoweza kutoa. (Efe. 4:11-16) Watumishi wa huduma pia ni wenye kupendezwa na kusaidia wengine wafanywe imara katika imani; kwa hiyo, waendee ndugu hao kwa ajili ya kitia-moyo.
4 Je, unahitaji msaada katika huduma? Zungumza na wazee, na uombe msaada. Labda unaweza kushirikishwa katika programu Mapainia Husaidia Wengine. Je, ulibatizwa juzijuzi? Kujifunza kitabu Huduma Yetu na kutumia mambo yaliyo ndani ya hicho kutachochea maendeleo kuelekea ukomavu wa kiroho. Je, wewe ni mzazi? Endelea kujenga hali ya kiroho ya watoto wako. —Efe. 6:4.
5 Kwa kuwa wenye kutia mizizi na wenye kuimarishwa katika imani, tunafurahia uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, na ushirika wenye shauku pamoja na ndugu zetu. Hilo hutuwezesha kuzuia mashambulio ya Shetani, na hutia nguvu tumaini letu la wakati ujao wa milele. —1 Pet. 5:9, 10.