Sisi twahubiri habari njema
1 Ni pendeleo kama nini tulilo nalo kuwa wachukuaji wa “habari njema ya mambo mema!” (Rom. 10:15) Tuna ujumbe wenye kuburudisha ambao tunapaswa kushiriki na watu wanaozungukwa na msukosuko na ukosefu wa tumaini. Tunaweza kuwasaidiaje watambue kwamba sisi tunatoa “habari njema ya maneno mazuri”? (Italiki ni zetu.)—Isa. 52:7.
2 Tayarisheni ujumbe wenye kujenga: Mazungumzo yetu katika huduma yatakuwa na matokeo yenye kufaa ikiwa tunakaza fikira juu ya mambo yenye kujenga. Kwa hiyo, wakati tunapotayarisha utoaji wetu na kurudilia kichapo tutakachotolea watu, tunahitaji kukazia pande zenye kujenga za ujumbe. Kwa kutoa tumaini letu lenye msingi juu ya Biblia tukiwa na usadikisho na shauku, tunaweza kutazamia matokeo yenye kutia moyo.—Mez. 25:11.
3 Ingawa sisi ni wenye kusikitika wakati watu wanapoonyesha jinsi hali za ulimwengu zenye kuwa mbaya zaidi na zaidi zilivyokuwa na uvutano juu yao, tunapaswa kuwaonyesha suluhisho la kweli kwa matatizo ya wanadamu, Ufalme wa Mungu. Hata wakati tunapozungumzia “siku ya kisasi” ya Yehova inayokuja, tunataka kuonyesha jinsi hiyo humaanisha kwelikweli ‘habari njema kwa wanyenyekevu.’ (Isa. 61:1, 2) Tunaweza kuhakikishia wasikilizaji wetu kwamba jambo lolote analofanya Yehova litaleta hatimaye furaha kubwa zaidi na matokeo mazuri zaidi iwezekanavyo.
4 Toeni kweli kwa furaha ya kweli: Wakati watu wanapoona sura yetu yenye furaha na sauti yetu yenye usadikisho, wao huwa na mwelekeo zaidi wa kusikiliza. Ikiwa tunaonyesha maoni yenye kutazamia mema, wasikilizaji wetu watatambua kwamba sisi ‘tunashangilia katika tumaini.’ (Rom. 12:12) Hivyo, huenda wakaelekea zaidi kuitikia habari njema. Bila shaka, tunayo sababu nzuri ya kuonyesha sikuzote mtazamo wenye kufaa na wenye furaha katika pande zote za huduma yetu.
5 Tukiwa wahudumu wa habari njema, tunatimiza mengi zaidi sana kuliko kupasha habari tu. Kuhubiri kwetu kunatoa tumaini hakika la maisha bora sasa na wakati ujao. (1 Tim. 4:8) Kadiri tunavyomkaribia kila mtu, hali yetu ya akili yenye kutazamia mema itaonekana katika yale tunayosema na itasaidia watu wakubali habari njema. Kwa kuwa waangalifu kwa yale tunayosema na jinsi tunavyoyasema, acheni tuchochee wale wenye mioyo minyofu wakubali habari njema yenye kusisimua tunayohubiri!