Kisanduku cha maulizo
◼ Ni nani anayepaswa kutoa sala kwenye mikutano ya kutaniko?
Sala katika kutaniko ni sehemu ya maana ya ibada yetu. Kuwakilisha wengine mbele ya Yehova ni pendeleo la thamani na ni daraka zito. Kwa sababu ya umaana wa hilo, wazee wanahitaji kutumia utambuzi mzuri wakati wa kuamua ni akina ndugu gani walio na sifa za kuwastahilisha kutoa sala kwenye mikutano. Ndugu wenye kubatizwa ambao huwakilisha kutaniko wanapaswa kuwa wahudumu Wakristo wenye kukomaa ambao wanajulikana kuwa mifano mizuri na ambao wanaheshimiwa na kutaniko. Sala zao zenye heshima na adabu zinapaswa kuonyesha uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu. Makala “Kusali Mbele ya Wengine kwa Moyo Mnyenyekevu” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1986, inaonyesha kanuni za maana ambazo ni zenye kusaidia hasa wale wanaosali peupe kwa ajili ya kutaniko.
Wazee hawapaswi kuomba ndugu atoe sala ikiwa anajulikana kwa sababu ya mwenendo wenye kushakiwa au mlegevu. Ndugu aliye na mwelekeo wa kuwa mwenye hasira au anayeelekea kutumia sala ya peupe kuwa njia ya kujulisha wengine tofauti za kibinafsi hapaswi kuchaguliwa. (1 Tim. 2:8) Hata ikiwa tineja huenda akawa mwenye kubatizwa, wazee watalazimika kuamua ikiwa yeye ni mwenye kukomaa kiroho ili kusali kwa ajili ya kutaniko.—Matendo 16:1, 2.
Pindi kwa pindi kwenye mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani, huenda ikawa lazima dada mwenye kubatizwa atoe sala ikiwa hakuna ndugu mwenye sifa za kumstahilisha kuwakilisha kikundi. Dada huyo atahitaji kuvaa kitambaa cha kichwani chenye kufaa. Ikiwa inaelekea kwamba ndugu mwenye sifa za kumstahilisha hatakuwako kwenye mkutano fulani kwa ajili ya utumishi, wazee wanapaswa kutoa mgawo kwa dada mwenye sifa za kumstahilisha aongoze.
Ni kawaida kwa msimamizi wa Mkutano wa Watu Wote kutoa sala ya kwanza. Hata hivyo, kwenye mikutano mingine ya kutaniko, wakati kunapatikana zaidi ya ndugu wachache wenye sifa za kuwastahilisha, ndugu mwingine, tofauti na yule mwenye kufungua mkutano au yule aliyetolewa mgawo wa sehemu ya mwisho, anaweza kuombwa atoe sala ya kwanza au ile ya kumalizia. Kwa vyovyote, ndugu yule anayepaswa kuombwa kusali kwenye mkutano wa kutaniko anapaswa kujulishwa mbele ya wakati kusudi aweze kufikiria yale atakayosema. Ndipo anaweza kutoa sala yenye kushikamana, na yenye unyofu ambayo ni yenye kufaa kwa mkutano huo hasa.
Sala kama hizo hazihitaji kuwa ndefu. Wakati ndugu anapotoa sala ya peupe, yeye kwa kawaida atasikiwa vizuri ikiwa anasimama, ikiwa anasema kwa sauti ya kutosha, na ikiwa anasema wazi. Hilo litawezesha wale wote wenye kukusanyika wasikie sala na kusema mwishoni “Ameni!” yenye kutoka moyoni.—1 Nyak. 16:36; 1 Kor. 14:16.