Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Sehemu 7: Kutoa Sala Kwenye Funzo
1 Ili wanafunzi wa Biblia wafanye maendeleo ya kiroho, baraka ya Yehova inahitajiwa. (1 Kor. 3:6) Kwa hiyo, ni jambo lenye kufaa kuanza na kumaliza funzo kwa sala. Mara kwa mara tunaweza kufanya hivyo kwenye funzo la kwanza kabisa pamoja na watu walio na mwelekeo wa kidini. Kwa wanafunzi wengine, huenda tukahitaji kuwa na utambuzi ili kujua ni wakati gani unaofaa ili kuanza funzo kwa sala. Unaweza kutumia Zaburi 25:4, 5 na 1 Yohana 5:14 ili kusaidia mwanafunzi aelewe kwa nini sala inapaswa kutolewa na unaweza pia kutumia Yohana 15:16 ili kueleza umaana wa kusali kwa Yehova kupitia Kristo.
2 Ni nani anayepaswa kutoa sala kwenye funzo la Biblia? Ikiwa ndugu aliyebatizwa anaandamana na dada kwenye funzo, ndugu ndiye atatoa sala, na dada ataongoza funzo lake akiwa mwenye kuvaa kitu cha kufunika kichwani. (1 Kor. 11:5, 10) Kwa upande mwingine, ikiwa mhubiri wa Ufalme asiyebatizwa ni wa kiume, naye anaandamana na dada kwenye funzo, dada ndiye atatoa sala. Katika hali hiyo, dada anapaswa kuvaa kitu cha kufunika kichwani anaposali na anapoongoza funzo.
3 Mambo ya Kutia Katika Sala: Sala kwenye funzo la Biblia si lazima ziwe ndefu, lakini zinapaswa kuwa kamili. Zaidi ya kumwomba Mungu abariki funzo na kutoa shukrani kwa ajili ya kweli tunazojifunza, ni jambo lenye kufaa kutoa sifa kwa Yehova akiwa Chanzo cha mafundisho. (Isa. 54:13) Tunaweza pia kutia ndani maneno yanayoonyesha kwamba tunapendezwa kikweli na mwanafunzi na maneno yanayoonyesha kwamba tunathamini tengenezo ambalo Yehova anatumia. (1 The. 1:2, 3; 2:7, 8) Kumwomba Yehova abariki jitihada za mwanafunzi ili kutumia katika maisha yale anayojifunza kunaweza kumsaidia atambue umaana wa kuwa ‘mtendaji wa neno.’—Yak. 1:22.
4 Kuna baraka nyingi zinazotokana na sala. Inaleta baraka ya Mungu. (Luka 11:13) Inatilia mkazo ili kwamba kujifunza Neno la Mungu kuchukuliwe kwa uzito. Mwanafunzi anaposikiliza sala zetu, anajifunza jinsi ya kusali. (Luka 6:40) Zaidi ya hiyo, sala ambazo zinazotoka katika moyo unaojaa upendo kwa Mungu na shukrani kwa sifa zake zisizo na kifani zinaweza kusaidia mwanafunzi kukuza uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova.
[Maulizo ya Funzo]
1. (a) Kwa nini ni jambo lenye kufaa kuanza na kumaliza funzo la Biblia kwa sala? (b) Namna gani tunaweza kutambua wakati unaofaa ili kuanza funzo la Biblia kwa sala?
2. Ikiwa ndugu aliyebatizwa au mhubiri asiyebatizwa wa kiume anaandamana na dada kwenye funzo la Biblia, ni nani atatoa sala?
3. Ni mambo gani yanayofaa yanayoweza kutiwa katika sala zinazotolewa kwenye funzo la Biblia?
4. Kuanza na kumaliza funzo kwa sala kunaleta baraka gani?