Tumieni matukio ya sasa ili kuamsha kupendezwa
1 Je, ungetaka kuwa na kiasi chenye kuendelea cha mawazo mazuri ambayo yatafanya huduma yako iendelee kuwa mpya na kuamsha kupendezwa kwa watu katika ujumbe wa Biblia? Basi tumia yale yanayotukia ulimwenguni na katika eneo lenu ili kuanzisha mazungumzo. Mambo hayo ni yenye kubadilika-badilika. (1 Kor. 7:31) Fikiria mifano ifuatayo.
2 Matatizo ya kiuchumi na gharama ya maisha ni mambo yenye kuhangaisha watu kwelikweli. Hivyo, unaweza kusema:
◼ “Je, umesikia katika vyombo vya habari kwamba bei za [taja bidhaa] zinapanda tena?” Au unaweza kusema kuhusu ukosefu wa kazi ikiwa shirika kubwa limefukuza wafanyakazi wengi. Kulingana na jinsi unavyotaka kufanya mazungumzo, unaweza kuendelea kwa kuuliza, “Je, umepata kujiuliza wakati wowote kwa nini ni vigumu kupata mahitaji ya maisha?” au “Je, unafikiri kwamba itakuwa vigumu sikuzote kupata mahitaji ya maisha?”
3 Ripoti kuhusu jeuri, kama vile mambo ya kuhuzunisha katika familia au kati ya wanafunzi wa shule, hutoa msingi wa mazungumzo mengine. Unaweza kuuliza:
◼ “Je, umesoma katika magazeti kwamba [taja jambo la kuhuzunisha lililotukia katika eneo lenu]?” Kisha uliza, “Unafikiri ni nini iliyo sababu ya jeuri nyingi sana hivyo ulimwenguni?” au “Je, unafikiri kwamba wakati utakuja ambapo tutajisikia salama?”
4 Habari kuhusu mafuriko ya maji yenye kuharibu, matetemeko ya dunia, au vita vya wenyewe kwa wenyewe katika sehemu mbalimbali za dunia pia ni jambo linaloamsha kupendezwa. Kwa mfano, unaweza kuuliza:
◼ “Je, ni Mungu ndiye amesababisha [taja msiba wa kiasili]?” Au unaweza kusema juu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyotukia juzijuzi, na useme: “Ikiwa kila mtu anataka amani, kwa nini hiyo ni ngumu sana kufikia?”
5 Endeleeni kuwa macho ili kujua matukio ya sasa ambayo mnaweza kutumia katika utangulizi wenu. Madokezo yenye kusaidia yanapatikana chini ya “Matukio ya Sasa,” kwenye ukurasa 12, katika kitabu Kutoa Sababu. Hata hivyo, epukeni kujiweka upande mmoja au mwingine katika mambo ya kisiasa au ya kijamii. Badala yake, ongozeni uangalifu kwenye Maandiko na kwenye Ufalme wa Mungu kuwa suluhisho moja pekee la kudumu la matatizo ya wanadamu.